Tuujue Mtaguso Mkuu

Morogoro: Un momento di formazione - Morogoro: Kipindi cha malezi - Morogoro: A moment of formation

Home Tuujue Mtaguso Mkuu Hystoria ya utawa Historia ya Wafransisko MASWALI JUU YA MASHAURI YA KIINJILI NANI MWABUDU SANAMU rosary HATUA TATU ZA MAISHA YA KIROHO Sala ya Moyo MATAKASO KABLA YA KUAHIDI MASHAURI YA KIINJILI

TUUJUE MTAGUSO MKUU

UTANGULIZI

Yesu Kristo aliwakabidhi mitume kumi na wawili uongozi wa Kanisa wakiwa kundi moja lenye mkuu wake, yaani Petro. Vilevile waandamizi wao, yaani maaskofu wote, ni kundi moja na papa wa Roma ndiye mkuu wao. Huyo peke yake, na kundi la maaskofu likiwa pamoja naye na chini yake, ndio wenye mamlaka ya juu katika Kanisa lote. Mamlaka hiyo inatumika kwa namna ya pekee unapofanyika mtaguso mkuu, yaani mkutano maalumu wa maaskofu uliokubaliwa na papa kuwa unawakilisha kundi hilo lote.

 

 

ORODHA YA MITAGUSO MIKUU

 

KATIKA MILENIA YA KWANZA ILIFANYIKA MASHARIKI (UTURUKI):

1.       Nisea I (mwaka 325)

2.       Kostantinopoli I (381)

3.       Efeso (431)

4.       Kalsedonia (451)

5.       Kostantinopoli II (553)

6.       Kostantinopoli III (680-681)

7.       Nisea II (787)

8.       Kostantinopoli IV (869-870)

 

KATIKA MILENIA YA PILI ILIFANYIKA MAGHARIBI (ITALIA, UFARANSA, UJERUMANI):

9.       Laterano I (1123)

10.   Laterano II (1139)

11.   Laterano III (1179)

12.   Laterano IV (1215)

13.   Lyon I (1245)

14.   Lyon II (1274)

15.   Vienne (1311-1312)

16.   Kostansa (1414-1418)

17.   Firenze (1439-1445)

18.   Laterano V (1512-1517)

19.   Trento (1545-1563)

20.   Vatikano I (1869-1870)

21.   Vatikano II (1962-1965)

 

 

MTAKATIFU FRANSISKO NA MTAGUSO

Mitaguso mikuu ya kwanza ilifanyika hasa ili kubainisha katika mafundisho yaliyogongana yapi yanalingana na imani sahihi. Mwisho wake ulikuwa kutangaza dogma fulani na kutenga na Kanisa watakaokataa kuiamini na watakaofundisha tofauti.

Mitaguso iliyofanyika baada ya farakano la mwaka 1054 kati ya Kanisa la Mashariki na la Magharibi, pamoja na kulenga umoja uliovunjika na kufundisha dogma mpya, ilishughulikia zaidi urekebisho wa Kanisa katika ngazi na nyanja zote. Kwa namna ya pekee mtaguso wa pili wa Vatikano tangu uitishwe ulijulikana kuwa wa kichungaji, yaani usio na lengo la kufundisha dogma mpya wala kulaani mafundisho mengine.

 

Mzee wetu Fransisko anasifika kwa ukatoliki wake: alishikamana kabisa na Kanisa akiwatii viongozi wake na kuwa rafiki yao. Tangu mwanzo alitaka kuweka utawa wake chini ya Mama Kanisa Takatifu la Roma akakubaliwa kwa moyo. Kinyume cha uzushi mwingi wa wakati wake, karama ya Fransisko ilionyesha wazi kuwa Injili imekabidhiwa kwa Kanisa, hivyo ishikwe kikamilifu ndani ya Kanisa na kwa msaada wake.

Tukiangalia zaidi uhusiano huo tunaona kuwa Fransisko aliingia kabisa katika juhudi za urekebisho wa liturujia na maadili ambazo kilele chake ni mtaguso wa nne wa Laterano (1215). Wengi wanadhani kuwa mwenyewe aliuhudhuria akiwa ni mkuu wa utawa; kwa vyovyote ni hakika kuwa baadaye alionekana kujua sana malengo na maamuzi ya mtaguso huo, na kutaka kuyatekeleza pamoja na wafuasi wake na waamini wote.

Kwa mfano, barua zake zinahimiza heshima kwa ekaristi na kwa yale yote yanayohusu liturujia: katika kuziandika alitumia hata maneno yenyewe ya hati za mtaguso na za papa. Zaidi tena, Fransisko alipokea kwa moyo mpango wa Inosenti III wa kufanya Kanisa lote (hasa makleri) liongoke kwa kusulubisha mwili na tamaa zake, likitumia ile tau inayoongelewa na Ezekieli 9 kuwa ni muhuri waliotiwa wateule wa Mungu waliokubali msalaba katika maisha yao. Hivyo tau ikawa kwa Fransisko pia ishara ya toba aliyojitahidi kuieneza kati ya waamini. Kwa kuungana kabisa na Msulubiwa na kuongozwa na Roho Mtakatifu katika yote, akawa chombo cha kurekebishia Kanisa si kwa kulilaumu wala kwa kulipinga, bali kwa njia ya utakatifu.

 

Kwa namna fulani Kanisa linajikuta leo katika nafasi inayofanana na ile ya zamani za Fransisko na linahitaji watu ambao wamefanywa wapya kwa kushiriki mateso ya Kristo, na ambao Roho aweze kuwatumia bila ya pingamizi kwa ujenzi wa ufalme wa Mungu. Mtaguso wa pili wa Vatikano umepanga kwa upana wote kazi ya kutengeneza upya maisha ya Kikristo, lakini kazi hiyo haiwezi kufanyika bila ya mwanga na nguvu ya Roho Mtakatifu, naye anafanya kazi hasa katika watu waliokubali kujazwa naye hata kuwashirikisha ndugu zao.

Basi, mfano wa Fransisko unawahimiza Wakristo washikamane na Kanisa kwa nguvu zao zote; ndani yake mfumo au muundo wowote usikubali kuwa na mpango wake wenyewe, bali utumie kwa unyenyekevu karama yake katika kutimiza mpango uliofanyika katika mtaguso kwa ushirikiano wa Roho na maaskofu wote. La sivyo miongozo na maagizo yake bora yatabaki maandishi matupu ambayo hayazai matunda yale yote yaliyotarajiwa. Hasa Kanisa linatazamia kuwa wafuasi wote wa Fransisko watatoa mchango wa utakatifu wao ambao kwa namna fulani umfufue kwa ulimwengu wa leo.

 

 

MALENGO YA MTAGUSO WA PILI WA VATIKANO

 

Muda mfupi baada ya kuchaguliwa papa mwenye heri Yohane XXIII alitangaza uamuzi wake wa kuitisha mtaguso mkuu akiamini kwamba utaweza kuandaa na kusababisha ustawi mpya wa maisha ya Kanisa. Lengo kuu la mtaguso lilikuwa kuliamsha Kanisa likumbuke wito wake na kwa kujifanya upya kwa ndani lipate msukumo mpya wa kimisionari ili kuwatangazia watu wote ujumbe wa milele wa wokovu, amani na umoja.

Tangazo hilo lilitolewa tarehe 25-1-1959. Baada ya maandalizi mtaguso wa pili wa Vatikano ulifunguliwa tarehe 11-10-1962. Vikao vinne vikafanyika mpaka ulipofungwa tarehe 8-12-1965. Kila kikao kilianza Oktoba na kumalizika Desemba ya miaka hiyo.

Kwa kuwa Yohane XXIII alifariki tarehe 2-6-1963, vikao vitatu vya mwisho viliongozwa na mwandamizi wake, Paulo VI, na hati zote kumi na sita zikatolewa chini yake pia kwa kupigiwa kura ya ndiyo karibu kwa kauli moja. Maaskofu na wakuu wa mashirika kadhaa wenye haki ya kupiga kura walikuwa kama elfu tatu, wakiwakilisha karibu Kanisa lote duniani, isipokuwa nchi zile zenye kuwadhulumu Wakristo.

 

 

ORODHA YA HATI 16 ZA MTAGUSO

 

HADHI

JINA LA KILATINI

KIFUPISHO

YAHUSUYO

TAREHE

KATIBA

1.        Sacrosanctum Concilium

SC

Liturujia takatifu

4-12-1963

2.        Lumen Gentium

LG

Kanisa

21-11-1964

3.        Dei Verbum

DV

Ufunuo wa Kimungu

18-11-1965

4.        Gaudium et Spes

GS

Kanisa katika ulimwengu wa kisasa

7-12-1965

MAAGIZO

1.        Inter Mirifica

IM

Vyombo vya upashanaji habari

4-12-1963

2.        Orientalium Ecclesiarum

OE

Makanisa katoliki ya Mashariki

21-11-1964

3.        Unitatis Redintegratio

UR

Ekumeni

21-11-1964

4.        Christus Dominus

CD

Huduma ya kichungaji ya maaskofu

28-10-1965

5.        Perfectae Caritatis

PC

Kurekebisha upya maisha ya kitawa

28-10-1965

6.        Optatam Totius

OT

Malezi ya kipadri

28-10-1965

7.        Apostolicam Actuositatem

AA

Utume wa walei

18-11-1965

8.        Ad Gentes

AG

Utendaji wa kimisheni wa Kanisa

7-12-1965

9.        Presbyterorum Ordinis

PO

Huduma na maisha ya kipadri

7-12-1965

MATAMKO

1.        Gravissimum Educationis

GE

Malezi ya Kikristo

28-10-1965

2.        Nostra Aetate

NA

Uhusiano wa Kanisa na dini zisizo za Kikristo

28-10-1965

3.        Dignitatis Humanae

DH

Uhuru wa dini

7-12-1965

 

 

MAPOKEZI YA MTAGUSO

 

Kwa kuwa Roho Mtakatifu alitaka hivyo, Wakristo walio wengi walipokea kazi ya mtaguso kwa mikono miwili, na wengi nje ya Kanisa pia waliridhika sana. Kutokana nao yamepatikana matunda mengi, lakini zimejitokeza hata kasoro na shida kwa sababu mbalimbali, hasa kwa kutoelewa wala kutotekeleza sawasawa maagizo yake. Kwa vyovyote hatuwezi kusema yote yaliyotokea baada ya mtaguso yamesababishwa nao, k.mf. maovu yaliyofanywa na baadhi ya mapadri hayamo kabisa.

Pamoja na upinzani wa wazi wa mifumo kadhaa ya kisiasa (ukomunisti na ubepari) na matapo mengine (Wamasoni n.k.) dhidi ya Kanisa, hali ya jumla ya ulimwengu inazidi kuelekea anasa na kuabudu utajiri hata kuzima maisha ya Kiroho. Hivyo ni vigumu kufanikisha mtaguso.

Hata ndani ya Kanisa wengi wamesoma hati zake kijuujuu, wakishikilia upande mmoja na kutojali wa pili. Wengine wamevunjika moyo kuona utekelezaji wa mtaguso unavyokwenda polepole. Wengine wameshughulikia miundo tu ya Kanisa, bila ya kujali fumbo la Kimungu lililomo ndani yake. Pengine umekosekana upambanuzi, k.mf. wengi walipofuata mitazamo ya ulimwengu uliomuasi Mungu badala ya kujadiliana nao ili kuuokoa.

Matatizo yaliyojitokeza baada ya mtaguso yanaonyesha haja ya kuupokea vizuri zaidi, kwa kupiga hatua nne zifuatazo:

1.       Hati za mtaguso zijulikane na watu wengi zaidi na kwa dhati zaidi.

2.       Zipokewe kwa moyo.

3.       Zizingatiwe kwa upendo.

4.       Zitekelezwe maishani.

 

 

NAMNA YA KUELEWA MTAGUSO

 

Tukitaka kuelewa vizuri hati za mtaguso, ni lazima tuzizingatie zote 16 zilivyo na zinavyofungamana. Ni lazima pia tutie maanani hasa katiba zake 4, kwa kuwa ndizo hati kuu zinazotuwezesha kuelewa maagizo 9 na matamko 3. Tena hatutakiwi kutenganisha mtazamo wa kichungaji na msingi wa imani wa hati hizo, wala kutenganisha roho ya mtaguso na hati zenyewe. Mwishowe mtaguso ueleweke katika mapokeo ya Kanisa kwa kuwa katika mitaguso yote Kanisa ni lilelile. Hivyo tu tutapata mwanga tunaouhitaji kwa wakati huu.

Tahadhari hizo zote zinahitajika kwa sababu katika kutekeleza mtaguso yamejitokeza maelekeo mawili ambayo yanapingana na kuvuruga hali ya Kanisa. La kwanza linadai mabadiliko yasiyolingana na mtaguso, ingawa wenyewe wanasema ni maendeleo yanayotakiwa na roho ya mtaguso. Maendeleo ya namna hiyo hayakubaliki kwa sababu hayajali mapokeo ya mitume yanayodai imani idumu kuwa ileile. La pili linaambatana na mambo ya zamani, bila ya kujali ishara za nyakati zetu zinazodai mambo mapya pia kwa wokovu wa watu wa leo na wa kesho.

Ni wajibu wa maaskofu chini ya papa kutambua yapi yanajenga na yapi yanazuia ujenzi au pengine yanabomoa Kanisa. Ndiyo kazi inayofanyika hasa katika sinodi (= pamoja-njia, yaani kusafiri pamoja). Kati ya sinodi za ngazi mbalimbali kuanzia ile ya jimbo, muhimu zaidi ni zile za kimataifa zinazofanyika mara kwa mara huko Roma (mtaa wa Vatikano), zikikusanya maaskofu wawakilishi wa nchi zote na baadhi ya wakuu wa mashirika ya kitawa.

 

 

JUHUDI ZA KUTEKELEZA MTAGUSO

 

Kama vile mitaguso mikuu iliyotangulia kupanga urekebisho wa hali ya Kanisa, mtaguso wa pili wa Vatikano pia ujumbe wake hautaweza kuzaa matunda isipokuwa kwa juhudi za muda mrefu. Miaka ishirini baada ya mtaguso kumalizika, sinodi maalumu iliyoitishwa ili kutathmini matokeo yake ilisema wazi kuwa kazi bado sana, kwa namna ya pekee kuhusu kulenga utakatifu kwa waamini wote. Ndiyo maana ilihamasisha tufanye juu chini ili ujumbe wa mtaguso usikilizwe upya katika kila jimbo. Ni lazima tushike jembe kwa kazi hiyo bila ya kuangalia nyuma tukipatwa na matatizo yasiyoepukika.

SACROSANCTUM CONCILIUM

 

Kikao cha pili cha mtaguso kilipitisha hati mbili za kwanza. Ya kwanza kabisa inahusu liturujia ambayo ni moyo wa Kanisa kwa kuwa ndipo linapoungana na Mungu wake na kuonekana katika sura yake takatifu. Lengo la hati hiyo ni kufanya kwanza mapadri, halafu Wakristo wengine pia waelewe na kutimiza liturujia ili kwa njia yake wamtukuze kweli Mungu na kufaidika Kiroho.

Karne ya XX iliiandaa kwa kuwa wataalamu walijitahidi kwa muda mrefu kuchambua maana ya liturujia kwa jumla na ya ibada zake mbalimbali. Mapapa wote walipokea na kuagiza marekebisho kadhaa yalitopendekezwa na wataalamu hao. Lakini kazi kubwa zaidi ilikuwa bado.

Kikwazo kikuu kilikuwa ni lugha ya Kilatini iliyokwishakufa tangu miaka elfu hivi. Muda huo wote wasomi tu waliweza kuelewa masomo na mengineyo ya liturujia. Hivyo watu wa kawaida wakawa watazamaji tu wa matendo ya ibada. Bila ya kupata mafundisho wala sakramenti ya ekaristi, Wakristo wa Magharibi walijitungia ibada zao badala ya kutegemea liturujia ya Kanisa.

Huko Mashariki hali ilikuwa tofauti kabisa: ndiyo sababu hati hiyo inahusu liturujia ya Roma tu, isipokuwa misingi ya liturujia yoyote na mengineyo yanayofaa hata Mashariki.

 

Sura ya kwanza inahusu kanuni za jumla kwa urekebisho na ustawishaji wa liturujia. Kwanza inaeleza undani na umuhimu wake, halafu inasisitiza haja ya malezi ya kiliturujia kuanzia seminari na nyumba za kitawa ambapo maisha yote yafuate roho ya liturujia na masomo yote yafundishwe kwa kuonyesha uhusiano wake na liturujia ambayo ihesabiwe kati ya masomo muhimu zaidi na kufundishwa na wataalamu. Hivyo waamini wote watasaidiwa kuchota roho halisi ya Kikristo katika chemchemi hiyo ya kwanza na ya lazima; pia wataweza kushiriki ibada kwa jinsi iliyo haki na wajibu wao.

Baadaye tu yanaagizwa marekebisho ya jumla ya liturujia na vitabu vyake vyote; msingi wake ni kwamba liturujia, mbali ya mambo yaliyoagizwa na Bwana, ina mengi yaliyopangwa na Kanisa lenyewe katika historia yake kulingana na mahali na nyakati mbalimbali. Kwa hiyo mara kwa mara linaweza na kupaswa kuyapanga upya kwa manufaa ya waamini.

Kwa kuwa liturujia ni kazi ya Kanisa lote, inaratibiwa na uongozi wake tu: wengine wasithubutu kubadilisha lolote wanapofanya ibada zake. Hata uongozi wa Kanisa usirekebishe vitabu harakaharaka na pasipo lazima, bali uhakikishe kwamba mapya yanalingana na ya zamani.

Kwa namna ya pekee ni lazima neno la Mungu katika liturujia liheshimiwe linavyostahili, tena lionjwe kama ilivyokuwa mwanzoni mwa Kanisa.

Maagizo mengine yanatokana na hali ya kijumuia ya liturujia, yaani kwamba ibada zake si za binafsi, bali ni za Kanisa lote, na kila mmoja anahusika namna yake kama mwamini wa kawaida au kama mwenye daraja au huduma fulani. Hivyo ipendelewe ibada ya pamoja ambapo kila mmoja ashike nafasi yake na kulingana vizuri na wengine wanaoshika nafasi zao.

Maagizo mengine yanazingatia faida ya waamini upande wa imani ikiwa ni pamoja na kujifunza undani wa imani yenyewe. Kwa ajili hiyo mtaguso umeamua ibada zieleweke kwa urahisi, mapadri watoe hotuba na mawaidha mbalimbali wakati wa ibada, pia ziruhusiwe lugha hai za watu ingawa Kilatini kinabaki lugha rasmi ya madhehebu ya Kanisa la Magharibi na waamini wake wote wanatarajiwa kujua kuitikia na kuimba kwa Kilatini wakati wa Misa.

Mbali ya lugha, mtaguso umekubali yafanyike marekebisho mengine ili kupokea katika liturujia ya Roma utamaduni wa makabila yoyote mradi usipingane na imani. Utamadunisho huo ufanyike chini ya Baraza la Maaskofu na kukubaliwa na Roma.

Mwisho wa sura hiyo unasisitiza umuhimu wa watu kushiriki liturujia ya askofu katika Kanisa kuu na ile ya parokia ili waamini wajisikie kweli Kanisa moja.

Ili kustawisha liturujia mtaguso umeagiza ziwepo kamati maalumu kitaifa na kijimbo.

 

Ili kutekeleza yaliyosemwa hapo juu, sura ya pili inaagiza namna ya kurekebisha madhehebu ya Misa, sura ya tatu inafanya vilevile kuhusu sakramenti nyingine na visakramenti, na sura ya nne kuhusu Sala ya Kanisa. Vitabu vyote vinavyohusika tunavyo tayari vimerekebishwa: katika kuvitumia ni muhimu kujisomea utangulizi wake.

Sura ya tano inarekebisha mwaka wa Kanisa kusudi mpango wake ueleweke zaidi bila ya kujaa mno sikukuu za watakatifu: hasa siku ya Bwana na vipindi maalumu vya mwaka vipate nafasi vinavyostahili.

Sura mbili za mwisho zinahusu muziki na sanaa takatifu ili liturujia ipendeze kwa uzuri wake, iinue roho kwa Mungu na kuwa kielelezo cha ile ya mbinguni. Hivyo vipawa mbalimbali vya binadamu vitumike kumtukuza Mungu. Hayo yameelezwa baada ya vitabu kwa sababu hivyo vina neno la Mungu na maitikio yetu kwa neno hilo lenye kututakasa. Vilevile muziki unaelezwa kabla ya sanaa nyingine kwa sababu unaambatana na maneno matakatifu. Mtaguso umesisitiza umuhimu wa kuimba katika liturujia, ukiagiza malezi kwa ajili hiyo, uundaji wa kwaya, utungaji wa nyimbo ambazo zichote hasa katika vitabu vya Biblia na liturujia. Kuhusu aina za muziki mtaguso umekubali aina yoyote inayoweza kulingana na utakatifu wa ibada; vilevile umeruhusu ala mbalimbali za kufaa. Hata hivyo liturujia ya Roma inapendelea muziki wa Kigregori na kinanda cha mabomba. Sanaa nyingine pia zinaheshimiwa na kutumiwa na Kanisa kwa ujenzi, mapambo, vifaa na picha takatifu. Kadiri ya mahali na nyakati limekubali mitindo mbalimbali mradi ilingane na imani, maadili na ibada ya Kikristo. Mtaguso umeagiza maaskofu hasa wajitahidi kudumisha msimamo huo na uzuri wa yote yanayohusu liturujia, kwa kuelimisha wanasanaa na makleri.

 

 

LUMEN GENTIUM

 

Hati hiyo juu ya Kanisa ndiyo muhimu kuliko nyingine zote za mtaguso. Inajibu swali la PauloVI, “Kanisa, unasemaje juu yako?”.

Sura ya kwanza inafafanua fumbo la Kanisa ambalo, kama sakramenti, lina mawili yasiyotenganika: kwa nje linaonekana kwa namna fulani, na kwa ndani mwa neema isiyoonekana inayoletwa na yale yanayoonekana. Ndani ya Kanisa la watu Mungu anaishi na kufanya kazi.

Kwa hiyo hati inaanza kwa kueleza jinsi Baba, Mwana na Roho Mtakatifu wanavyohusika na Kanisa. Halafu unaonyesha kuwa Kanisa ni mwanzo wa ufalme wa Mungu, nalo linafananishwa na kundi la kondoo, shamba, jengo na hekalu la Mungu au bibiarusi anayeungana na Bwanaarusi wake kuwa mwili mmoja, yaani mwili wa Kristo: ndio ukweli wenyewe wa Kanisa.

 

Baada ya kuona ukweli huo wa ndani, sura ya pili inaelekea kutazama watu wanavyohusika na fumbo la Kanisa. Kuanzia Agano la Kale Mungu hakupenda kuokoa watu mmojammoja bali aliwaunganisha wawe taifa lake lenye kujua ukweli na kumtumikia kitakatifu. Katika taifa hilo wote wamejaliwa ukuhani ambao unatumika katika adhimisho la sakramenti, na unabii wenye karama mbalimbali.

Katika taifa hilo watu wote wanapaswa kuingia bila ya ubaguzi ili wawe kitu kimoja. Ndiyo maana ya jina “Katoliki”: la mahali pote na nyakati zote. Wote wanahusiana na Kanisa ila kwa namna mbalimbali. Kwanza wapo Wakatoliki, yaani waliojiunga nalo kikamilifu kwa kumkubali Roho Mtakatifu na miundo yake yote. Halafu wapo Wakristo wengine waliokwishabatizwa na hivyo wameungana nalo ingawa si kikamilifu, kwa sababu hawakubali baadhi ya mafundisho na miundo yake. Hatimaye wapo watu wengine pia, wenye dini mbalimbali au wasio na dini, ambao wote wanaitwa na Mungu wajiunge na Kanisa kwa kuwa linahitajika kwa wokovu, ingawa Mungu anaweza kuwaokoa wenye nia njema wasiopata habari njema.

Bila ya shaka hali ya Wakatoliki ni bora zaidi, nao wanapaswa kuwashirikisha wengine wote ili kuwaokoa kutoka udanganyifu wa shetani na ulimwengu. Ndiyo maana ya kazi ya kimisionari ambayo imeagizwa na Yesu na ni wajibu wa kila Mkristo.

 

Sura ya tatu inatoa mafundisho muhimu tena mapya kuhusu muundo wa uongozi wa Kanisa, hasa uaskofu. Ni kwamba mtaguso wa I wa Vatikano ulifundisha sana kuhusu papa lakini haukupata nafasi ya kutoa hati iliyopangwa juu ya maaskofu, kwa sababu ulisambaratika jeshi la Italia lilipoteka Roma. Hivyo mtaguso wa PILI wa Vatikano ulikusudia kukamilisha kazi hiyo.

Hasa umefundisha kwamba kama vile mitume walivyokuwa kundi moja na Petro na chini yake, maaskofu wote ni kundi moja na papa wa Roma na chini yake. Kwa mpango wa Mungu kundi hilo ni la kudumu, maaskofu wakiwa waandamizi halisi wa mitume, na papa mwandamizi halisi wa Petro, mkuu wao.

Kwa namna ya pekee mtaguso umefundisha kuwa ibada ya kumweka wakfu askofu ni ngazi ya juu kabisa ya sakramenti ya daraja, si baraka fulani kwa padri anayepewa kazi ya juu kama wengine walivyodhani awali. Hivyo uaskofu unatia alama isiyofutika milele. Kutokana na fundisho hilo, mtaguso umesisitiza kila mara umuhimu wa maaskofu katika maisha yote ya Kanisa.

Lakini mtaguso umesisitiza pia umoja wa maaskofu, ukidai kila mmoja wao afanye kazi yake akishirikiana na kundi lote na achangie ustawi wa Kanisa zima, si jimbo lake tu. Katika hilo askofu ndiye nguzo ya umoja wa waamini wake wao kwa wao tena kati yao na waamini wote duniani: hivyo linafanya listahili kuitwa Kanisa, kwa kuwa ndani yake Kanisa lote limo kweli. Kwa msingi huo askofu anawakilisha Kanisa lake maalumu katika Kanisa Katoliki, na kulifundisha, kulitakasa na kuliongoza kwa msaada wa mapadri wake na wa mashemasi, ambao wote wanashiriki ukuhani wake mkuu.

Mwishoni mwa sura hiyo Kanisa la Magharibi linaruhusu ushemasi wa kudumu urudishwe na kutolewa kwa wanaume wenye ndoa pia.

 

Mara baada ya sura inayohusu wale wachache waliopata daraja takatifu (wanaoitwa makleri), inafuata sura ya nne juu ya Wakristo wa kawaida (wanaoitwa walei). Kwa karne nyingi hao walibaki kama wasikilizaji na watazamaji tu katika ibada na katika maisha yote ya Kanisa, lakini kuanzia karne ya XIX utume wao ulianza kuamka upya. Mtaguso umesisitiza kwa nguvu wajibu na haki yao ya kutumia neema na vipaji walivyojaliwa na Mungu kwa ujenzi wa taifa lake na kwa wokovu wa ulimwengu. Msingi wake ni ubatizo uliowafanya manabii, makuhani na wafalme; hivyo wamejaliwa huduma na karama mbalimbali ambazo wachungaji wanapaswa kuziheshimu wakiwaachia uhuru na nafasi katika utendaji. Kwa namna ya pekee ni juu yao kulenga utawala wa Mungu kwa kushughulikia malimwengu.

 

Baada ya kuona hayo makundi mawili ya waamini, wanaotofautiana kwa alama walizotiwa rohoni na ubatizo na kipaimara tu, au na daraja takatifu pia, sura ya tano inahusu wito unaowaunganisha wote, yaani kupata utakatifu. Karne za nyuma wengi walidhani hiyo ni kazi ya watawa tu, waliojichagulia “hali ya ukamilifu”, au sanasana mapadri. Kumbe sivyo: Wakristo wote wanapaswa kulenga utakatifu, kila mmoja kadiri ya wito wake maalumu na hali yake maishani. Hati inaorodhesha aina mbalimbali za waamini na jinsi kila moja ilivyo na njia yake; halafu inakumbusha njia mbili bora, yaani kifodini na mashauri ya Kiinjili: kwa maisha na kifo chao mashahidi na watawa wanahimiza Wakristo wote kutafuta ukamilifu wa upendo.

 

Hivyo ni rahisi kuelewa kwa nini sura ya sita inazungumzia watawa. Hao hawahusiki na uongozi wa Kanisa (isipokuwa kama wamepata pia daraja takatifu), ili wanahusika moja kwa moja na utakatifu na uhai wake. Si kundi la tatu kati ya makleri na walei, bali ni walei au makleri waliojifunga kulenga utakatifu kwa kushika mashauri ya Kiinjili, yaani useja mtakatifu, ufukara na utiifu. Mtaguso umesisitiza umuhimu wa mtindo huo wa maisha na asili yake katika maneno na mifano ya Yesu: utawa hautokani na historia ya Kanisa tu, bali upo na lazima uwepo kwa mpango wa Mungu. Hivyo uongozi wa Kanisa unapaswa kuuratibu na kuudumisha katika mitindo yake mingi. Mtawa amewekwa wakfu kwa ubatizo, halafu anaimarisha hali hiyo kwa nadhiri ili achume kwa wingi zaidi matunda ya neema kwa kuondoa mapingamizi yoyote yanayoweza kumzuia maishani.

 

Baada ya kuwaongelea watawa, wanaoshuhudia kwa namna ya pekee ulimwengu mpya ambapo hapana ndoa, sura ya saba inakuja kufundisha kuwa Kanisa lote hapa duniani liko safarini kuelekea mbinguni, huku likiwa na umoja na watakatifu. Sura hiyo inasisitiza tena imani yetu kuhusu mambo ya mwisho ikituhimiza tutazame juu na pia tuzingatie mifano bora ya wale waliokwishafikia heri ya milele. Hao wanastahili tuwaheshimu na kuwaomba watuombee, mradi tuepuke makosa mbalimbali yaliyojitokeza huku na huku. Daima ionekane wazi kuwa tunamuabudu Mungu tu na kwamba tukiwaheshimu watakatifu ni kwa sababu ni marafiki wa Mungu na wafuasi hodari wa Mwanae. Tunawaheshimu sio tu ili kupata msaada fulani, bali hasa kwa kufuata mifano yao ili tuwafikie katika liturujia ya mbinguni kuwaabudu Mungu na Mwanakondoo.

 

Mwishoni mwa hati hii yanapatikana mafundisho kuhusu Bikira Maria, akiwa ni mkuu wa watakatifu na mfano wa Kanisa lote. Baada ya mabishano makali kati ya washiriki wa mtaguso, wingi wa kura ulikataa kutoa hati maalumu juu ya Maria peke yake, kwa kuwa hawezi kueleweka nje ya fumbo la Kristo na la Kanisa. Hivyo mafundisho hayo yamepangwa katika sura ya nane ya hati hii, si kwa nia ya kuamua mabishano kati ya wanateolojia, wala kufundisha mapya, bali kupanga upya mafundisho ya Maandiko na ya Mapokeo. Baada ya kumsifu sana Bikira, mtaguso umesisitiza juu yake pia kuwa Kristo ndiye mshenga pekee kati ya Mungu na watu, hivyo hatuwezi kumlinganisha Maria na yeye kama walivyowahi kufanya baadhi ya waamini. Mchango wake kwa ukombozi wetu ulitokana na ukombozi ulioletwa na Yesu, ni kushiriki kazi yake tu. Hivyo Maria azidi kuigwa na kuheshimiwa kwa namna ya pekee, hasa kwa njia ya liturujia, lakini kwa kukwepa neno lolote ambalo linapita kiasi au kumweka pembeni Kristo.

 

Wazo kuu la hati hii kuhusu Kanisa ni kwamba lenyewe hasa ni ushirika wa Mungu nafsi tatu na watu, ni ushirika wa watakatifu wa duniani, toharani na mbinguni, ni ushirika wa waamini wa aina mbalimbali, kama vile wenye daraja na walei, au watawa na wenzao wote. Ushirika huo unatakiwa kuonekana wazi katika maisha ya Kanisa katika ngazi zote; hivyo litaonekana lilivyo, yaani ishara na chombo cha kuwaunganisha watu wote katika umoja wa Utatu mtakatifu.

 

 

DEI VERBUM

 

Katika Kanisa Katoliki tangu zamani sana zilisisitizwa liturujia na sakramenti, ingawa lugha ya kawaida ilikuwa haitumiki katika ibada hizo. Hivyo waamini walikuwa hawaelewi masomo ya Biblia wala matini mengine. Kwa jumla walikuwa hawaelewi Neno la Mungu kwa kukosa tafsiri za vitabu vyake hata nyumbani. Kuanzia karne ya kumi na mbili tafsiri hizo zilianza kupatikana kwa juhudi za wazushi waliozitumia kupinga ualimu wa Kanisa. Baadaye watu walipobuni uchapishaji, kitabu cha kwanza kutolewa kikawa ni Biblia huko Ujerumani. Mara ukaanza Uprotestanti pia ambao katika madhehebu yake yote ulisisitiza Maandiko kwa kukataa Mapokeo na Ualimu wa Kanisa. Ndiyo sababu yenyewe yalifanya kazi kubwa ya kutafsiri na kueneza Biblia ulimwenguni kote. Upande wake Kanisa Katoliki likaogopa kwa kuona nchi ngapi zimeliasi, hivyo likachukua msimamo wa kinyume kwa kusisitiza tena Mapokeo na Ualimu wake. Basi, Biblia ikazidi kubaki pembeni mwa maisha ya Wakatoliki wengi. Hata mwanzoni mwa karne ya XX walipojitokeza wataalamu wa Biblia walikatazwa wasifundishe baadhi ya mambo mapya kuhusu utungaji na maana ya Maandiko. Hivyo kabla ya mtaguso Wakatoliki kwa jumla walikuwa wakiogopa Biblia badala ya kuipenda.

Kumbe hati hiyo kuhusu ufunuo wa Kimungu ilipotolewa baada ya majadiliano na marekebisho mengi imelirudishia Kanisa lote Maandiko Matakatifu. Hapo Wakatoliki wataalamu wa Biblia wamefanya kazi kubwa sawa na wenzao Waprotestanti. Waseminari na watawa wengi wamefundishwa sana Neno la Mungu, na hata walei wameanza kulifurahia. Matunda yake yamepatikana tayari katika uzima mpya unaoonekana katika mifumo ya Kiroho, vyama na jumuia mbalimbali.

 

Baada ya dibaji, inayotamka nia ya kufuata nyayo za mitaguso iliyotangulia, sura ya kwanza inahusu ufunuo wa Mungu. Ni kwamba hatuwezi kuelewa Biblia mbali na historia ya wokovu, kwa sababu si kitabu kilichoandikwa leo kwa ajili yangu mimi, bali kilipatikana zamani Mungu alipojifunua hatua kwa hatua.

Sura ya pili inafundisha jinsi ufunuo huo uliokamilika zamani za Yesu unavyotufikia sisi watu wa leo, yaani kwa njia ya Mapokeo ya Mitume yakiwa na Maandiko Matakatifu ambayo kwa pamoja ni hazina takatifu ya Neno la Mungu, si chemchemi mbili tofauti. Hazina hiyo imekabidhiwa kwa Kanisa ambalo linaweza kuifafanua rasmi kwa njia ya Ualimu wake. Basi, Mapokeo Matakatifu, Maandiko Matakatifu na Ualimu wa Kanisa yameshikamana na kuunganika kiasi kwamba moja haliwezi kusimama bila ya mengine.

Baada tu ya kuelewa hayo tunaweza kukabili Biblia yenyewe (sura ya tatu) kwa kuzingatia jinsi Roho Mtakatifu alivyovuviwa juu ya waandishi wake. Hao walifanya kazi kama waandishi wowote, lakini vitabu vilivyopatikana vinafundisha tu kwa hakika na bila ya kosa ule ukweli ambao Mungu alitaka uandikwe kwa wokovu wetu. Si ukweli wowote (k.mf. wa sayansi) bali ule unaohusu wokovu. Hivyo Biblia mwandishi wake hasa ni Mungu, lakini yeye alijieleza kwa njia ya watu tena kwa namna ya kibinadamu. Basi, tukitaka kumuelewa tunapaswa kuelewa kwanza waandishi walitaka kusema nini tukizingatia pia mitindo waliyoitumia. Utaalamu huo ni muhimu ingawa hautoshi, kwa sababu tunapaswa bado kuzingatia umoja wa Biblia nzima, Mapokeo ya Kanisa na kweli za imani.

Baada ya kuona habari za Biblia kwa jumla, sura ya nne inaeleza umuhimu wa Agano la Kale kwa Wakristo pia, kwa kuwa linashikamana na Agano Jipya kama kitabu kimoja ambacho pande zake mbili zinahitajiana.

Sura ya tano inaeleza juu ya Agano Jipya: kwanza ubora wake unaozidi vitabu vya kale; halafu asili ya Kitume ya Injili nne ambazo tena zinapita hata Maandiko mengine ya Agano Jipya; mwishowe hakika ya kihistoria ya Injili hizo. Hati hii imepokea pia mtazamo mpya uliosema Wainjili waliandika historia ya Yesu kwa kuchagua baadhi ya habari, kufupisha nyingine na kueleza upya nyingine kadiri ya mazingira, wakidumisha namna ya kuhubiri kwa lengo la kufanya watu waamini. Habari zenyewe ziliwaelea kwa mwanga wa Roho Mtakatifu aliyelifikia Kanisa baada ya Kristo kufufuka ili kuliongoza kwenye ukweli wote.

Hatimaye sura ya sita inatoa maagizo kuhusu Maandiko Matakatifu katika maisha ya Kanisa. Kwanza ziwepo juhudi mpya ili wote wapate lishe katika meza ya Neno la Mungu ambalo ni hai na lina nguvu. Pia juhudi zifanyike ili waamini wapate Maandiko hayo katika lugha zao. Wataalamu pamoja na kuyatafsiri wayafafanue na kuelimisha wengine. Wale wote wanaotoa mafundisho ya imani katika ngazi zozote washikamane na Maandiko kwa kuyasoma pamoja na kusali ili Biblia iwe kiini cha mafundisho yao. Waamini wote, hasa watawa, wanahimizwa kuisoma sana kwa sababu kutoijua ni sawa na kutomfahamu Kristo.

 

 

GAUDIUM ET SPES

 

Hati hiyo, ndefu kuliko zote za mtaguso, inaitwa ya kichungaji kwa sababu inataka kutazama mambo kwa lengo la kuongoza maisha ya watu. Sehemu yake ya kwanza inaweka misingi juu ya imani, na sehemu ya pili inaonyesha msimamo wa Kanisa kuhusu ulimwengu wa leo. Kichwa kinasema wazi kuwa hati inahusu Kanisa katika ulimwengu “wa kisasa”, kwa kuwa tunapaswa daima kuishi na kutenda “leo”, huku tukijua vizuri mambo yalivyo, tukitambua ishara za nyakati zijazo ili tuone njia za kufaa kwa wokovu wa ulimwengu.

Bila ya shaka imepita miaka mingi tangu hati iandikwe, hivyo yameshatokea mabadiliko mengi, yaliyochunguzwa na mapapa na sinodi mbalimbali. Ingawa baadhi ya mambo leo yanaonekana tofauti kidogo, hati hiyo inabaki muhimu: kwanza kwa mtazamo wake wa jumla, pili kwa mtindo wa kuwaelekeza watu katika mambo ya kawaida yanayowahusu maishani, tatu kwa mafundisho ya msingi yasiyoweza kubadilika, nne kwa kuwa misimamo mbalimbali inafaa mpaka leo.

Kanisa halijioni tena mbali na ulimwengu, wala dhidi ya ulimwengu, bali ndani ya ulimwengu. Wakristo wanasafiri duniani pamoja na binadamu wenzao, wakishirikiana nao katika yale yote yasiyopingana na imani na maadili ya Kikristo. Hasa walei, ambao idadi yao ni karibu sawa na idadi ya wanakanisa wote, wanapaswa kuishi ulimwenguni kama chachu mpaka donge lote liumuke. Basi, Kanisa linajisikia kuhusika kabisa na maisha ya watu wote, hasa fukara. Ndiyo maana maneno ya kwanza ya hati hiyo yanasema kuwa “furaha na matumaini, huzuni na mafadhaiko ya watu ni pia ya wanafunzi ya Kristo”.

Hati hiyo ni ujumbe wa Kanisa kwa watu wote unaotaka kuwasaidia waelewe mambo yanayotukia siku hizi, kwa kuwa katika hayo binadamu anaweza kujipatia maisha bora kweli na halafu uzima wa milele, au kinyume chake anaweza kudanganyika na kupotoka. Siku hizi ugumu wa pekee kwa binadamu ni kwamba mabadiliko ya kila aina yanatokea haraka ajabu, tofauti na zamani. Mtu wa kawaida hapati nafasi ya kuyafikiria kwa dhati na kuyachambua. Hivyo hatari yake ni kufuata mkondo au kuongozwa na matukio badala ya kujifanyia mpango wa kumfaa, hata anaweza akafikia hatua ya kushindwa kujielewa ni nani, pamoja na kukosa msimamo maishani na raha moyoni mwake. Basi, anahitaji kuchungwa na kuelekezwa kwa imani na upendo: ndiyo kazi ya Kanisa ambalo lina nafasi nzuri ya kuwatangazia watu majibu ya Injili kwa maswali yanayowakera.

Kwa ajili hiyo hati inamuongoza msomaji hatua kwa hatua kufikiria utatanishi wa kisasa katika nadharia, jamii, uchumi na siasa unaomfanya afadhaike, hasa akiona maendeleo hayafaidishi wote na pengine yanatumika dhidi ya binadamu. Hivyo anaweza kutambua kuwa shida zinaanza moyoni mwake, ambamo mna mashindano makali na maswali ya msingi kama vile, “Mtu ni nani? Mateso na kifo vinavyodumu hata wakati huu wa maendeleo makubwa maana yake nini? Mtu ailetee nini jamii na atarajie kupata nini toka kwake? Baada ya maisha haya kutakuwa na nini?”. Jibu ni Kristo, mwokozi pekee, kiini na lengo la historia yote, msingi hasa usiobadilika. Katika mwanga wake mtaguso umechunguza fumbo la binadamu na wito wake.

 

Katika sehemu ya kwanza, sura ya kwanza inaeleza hadhi ya binadamu yeyote. Ingawa karibu wote wanakubali kuwa mtu ni kiumbe bora duniani, Kanisa linasisitiza ukweli huo kwa kumuona na kumuita “sura ya Mungu” hata baada ya kuathiriwa na dhambi. Ndio msingi wa heshima anayostahili katika mwili na zaidi katika roho ambayo kwa akili inaweza kujipatia ukweli na hekima, kwa dhamiri inasikia wito wa Mungu, na kwa hiari inaweza kuuitikia. Lakini Kanisa, pamoja na kusisitiza hiari kama wanavyofanya wengi siku hizi, linahimiza pia kuitumia vizuri, kwa kuwa mwishoni kila mtu atahukumiwa juu ya matumizi ya vipawa vyake.

Baada ya kukabili swala la kifo kwa kutangaza habari njema ya ufufuko, hati inakabili janga mojawapo la siku hizi, yaani kwamba wengi wanakanusha uwepo wa Mungu au wanaishi bila ya kumjali. Mtaguso ulifikiria hasa ukomunisti na misimamo mingine ya kupinga na kuzuia dini zote, lakini badala ya kuilaani tu, umetuhimiza kujadiliana na kushirikiana nayo, pamoja na kutoa ushuhuda wa maisha bora ya Kikristo, ukikiri kuwa pengine mifano yetu mibaya ndiyo iliyosababisha wengi wakose imani. Mwisho inachorwa taswira ya Kristo, mtu mpya, ambaye pekee yake anaangaza fumbo la binadamu pamoja na uchungu na kifo.

 

Sura ya pili inatupatia mafundisho kuhusu jamii yanayozingatia mpango wa Mungu wa kuwa watu waishi kwa ushirikiano. Kuukamilisha ushirikiano huo kwa msingi wa haki ni muhimu kuliko maendeleo ya ufundi tu. Kwa ajili hiyo kila mtu awajibike kuhusu wenzake wote bila ya kumsahau hata mmoja, akijifanya jirani wa wenye shida na kujitahidi kustawisha usawa kwa kutumia nafasi yoyote aliyonayo katika jamii. Maadili ya kibinafsi hayakubaliki, bali wajibu mkuu mmojawapo ni kujihusisha na ustawi wa jamii na mshikamano ili wote kwa neema ya Kristo waishi kijamaa.

 

Sura ya tatu inatoa msimamo kuhusu utendaji wa binadamu ulimwenguni. Hasa leo ambapo maendeleo ni ya haraka tunajiuliza kuhusu maana ya juhudi zetu na namna ya kuziendeleza. Ni hakika kuwa Mungu ametuagiza tufanye kazi na kutawala ulimwengu ili wote wapate hali ya maisha wanayostahili walio sura yake. Wakristo wanapaswa kuwa mstari wa mbele bila ya kudhani eti, Mungu anauonea kijicho ushindi wowote wa binadamu juu ya maadui wake (ujinga, maradhi na ufukara). Kinyume chake ushindi huo unatangaza ukuu wa Mungu aliyemuumba mtu akiwa na akili nyingi.

Lakini binadamu asisahau kuwa ubora wake hautokani na wingi wa vitu anavyojipatia, bali unategemea tuni za kiadili anazostawisha kwa kazi yake, hasa haki na udugu. Shida ni kwamba mara nyingi akishindwa na dhambi anafuata ubinafsi au utaifa na kuanzisha miundo ya dhuluma na vita hata kutengeneza silaha za kutosha kuangamizia uhai wowote duniani. Mbele ya hali hiyo Wakristo wanapaswa kutofuata mitindo ya ulimwengu bali njia ya upendo nyuma ya Kristo, wakiwa tayari kubeba msalaba wanaotwishwa wale wanaotafuta haki na amani. Tumaini la uzima wa milele lisipunguze bidii yetu kwa maisha ya binadamu wa leo, kwa kuwa huyo anaandaliwa hapa duniani kuingia katika ufalme wa mbinguni.

Katika utendaji wake mtu ana haki ya kufuata taratibu za elimudunia , siasa n.k. Imani haiogopi kumuachia nafasi hiyo, kwa kuwa Mungu yuleyule aliyejifunua kwetu kwa imani ameumba pia vitu vyote na kutujalia akili na uvumbuzi. Mtaguso umelaumu mawazo finyu yanayogonganisha imani na sayansi.

 

Sura ya nne inaeleza yatokanayo na zile zilizotangulia, yaani uhusiano wa Kanisa na ulimwengu. Kanisa likiwa na lengo la milele, linaishi duniani na wanae ni pia raia wa nchi hii. Hivyo linachangia ustawi wa binadamu pamoja na kupokea kwa shukrani misaada mbalimbali ya walimwengu. Lina ujumbe kwa watu wote kuhusu wokovu, lakini pia kuhusu maisha haya, hasa hadhi na haki za kila mtu. Kwa hiyo, ingawa utume wa Kanisa ni wa kidini hasa, linashughulikia pia ustawi wa jamii na umoja wa mataifa. Wakristo wasisahau tena majukumu yao ya kidunia, wala wasiyaone hayahusiki na imani. Mojawapo kati ya makwazo makubwa zaidi ya nyakati zetu ni utengano huo kati ya imani na maisha ya Wakristo wengi. Kwa namna ya pekee, walei wanapaswa kushughulikia malimwengu yote kwa mfano wa Yesu huko Nazareti. Wasisubiri kuagizwa na wachungaji wao, kwa kuwa kuratibu hayo ni kazi yao hasa. Mtaguso umekiri tena ukosefu wa wanakanisa na kuwahimiza kujirekebisha wasije wakazuie uenezaji wa Injili. Vilevile umeshukuru kwa juhudi za watu wowote kwa ajili ya ustawi wa familia, utamaduni, uchumi, jamii, amani na mshikamano wa kimataifa, hata ukakiri Kanisa limefaidika sana na upinzani na dhuluma za maadui wake.

 

Baada ya kumaliza kueleza kwa jumla jinsi Kanisa linavyohusika na wito wa binadamu, hati hii katika sehemu ya pili inakabili maswala kadhaa yaliyo muhimu zaidi kwa watu wa leo.

Kati ya hayo sura ya kwanza inafafanua kwanza hadhi ya ndoa na familia na namna ya kuzipa nafasi za kufaa, kwa sababu mengine mengi yanategemea hali ya familia. Baada ya kueleza utakatifu wa ndoa, kwa kuifananisha na hali ya kuwekwa wakfu kwa njia ya sakramenti za kudumu, mtaguso umeonyesha ubora wa upendo kati ya mume na mke na namna ya kuutekeleza, ukisisitiza unavyoelekea uzazi. Hivyo watu wa ndoa wanapaswa kupanga kwa pamoja mbele ya Mungu na kwa kuzingatia mafundisho ya Kanisa ili wazae kwa busara na ukarimu. Kwa namna ya pekee inasisitizwa kuwa ni lazima uhai wa binadamu kisha kuanza ulindwe kwa bidii zote: kuua mimba au mtoto ni maovu ya kutisha. Katika magumu yanayohusu uzazi wa mpango, wanandoa wajitahidi kufuata usafi wa moyo unaowafaa. Hata jamii nzima inatakiwa kuchangia ustawi wa familia: viongozi watunge sheria na kufanya mipango kwa ajili hiyo; wanasayansi waendelee kutafuta njia halali za kupanga uzazi; mapadri wafanye juu chini familia ziishe kwa utulivu.

 

Sura ya pili inafikiria namna za kustawisha utamaduni, yaani zile namna maalumu ambazo binadamu anakabili maisha katika mazingira na nyakati mbalimbali kulingana na orodha ya tunu anazothamini. Tofauti na wanyama, yeye hawezi kufikia hali ya maisha ya kumfaa kweli asipoyafanyia kazi mema yaliyoumbwa na Mungu ndani mwake na kandokando yake. Kila kabila na kundi la watu lina utajiri wake ambamo binadamu achote ili kujiendeleza na kuwaendeleza wenzake.

Lakini huu wa leo ni wakati mpya wa historia kwa sababu ya mabadiliko ya haraka mno. Upande mmoja zimefunguliwa njia mpya za kukuza na kueneza elimu na za kuunganisha aina tofauti za utamaduni. Upande mwingine kuna hatari za kufuta hekima na sura maalumu za kila jamii, kuvuruga mafungamano kati ya vizazi, kuacha elimu ya juu mikononi mwa wataalamu tu n.k.

Kufuatana na amri ya upendo Wakristo wanatakiwa kuchangia na wenzao ujenzi wa ulimwengu ili wote waone vizuri kazi ya Mungu na namna ya kuiendeleza. Kama vile yeye alivyotumia utamaduni wa watu ajifunue kwao, ndivyo Kanisa pia lilivyofanya na linavyopaswa kufanya katika kueneza habari njema. Lenyewe limetumwa kwa mataifa yote, hivyo halibanwi na utamaduni wowote, bali linautumia na kuuchangia, linausafisha na kuuinua lisiishie ndani yake. Ni wajibu wa wote kujitahidi kufuta ujinga kwa kueneza elimu hasa ya msingi ili kila mtu aweze kuchangia zaidi ustawi wa jamii. Vilevile kila mtu aelewe wajibu wa kujiendeleza kiutu na Kiroho bila ya kutawaliwa na kazi za mikono tu, akitumia vitabu na vyombo vingine vya upashanaji habari, muda huru ulio nje ya kazi n.k.

 

Sura ya tatu inafundisha kuhusu maisha ya kiuchumi na ya kijamii ya mtu wa nyakati zetu. Ni lazima huyo awekwe juu kabisa kuliko maendeleo ya vitu, kwa kuwa ndiye mtendaji, kiini na lengo la uchumi na la jamii. Kumbe wengi wanazingatia sheria za uchumi tu ili kutajirika iwezekanavyo. Matokeo ni kwamba mtengo kati ya mataifa, na kati ya matabaka ndani ya nchi, unazidi kuwa mkubwa. Anasa za wachache zinaleta ufukara wa kutisha wa umati hata kuhatarisha amani duniani.

Binadamu wa leo anaweza kurekebisha hali hiyo, lakini yanahitajika mageuzi mengi katika mitazamo, mazoea na miundo pia. Hapo tu ongezeko la uzalishaji litasaidia kweli, yaani litamsaidia mtu yeyote katika mahitaji yake yote (ya mwili, ya nafsi na ya roho). Kwa ajili hiyo ni lazima uchumi usiachwe uende zake wala usitawaliwe na wachache, bali wote waweze kuuchangia ustawi na uongozi wake bila ya ubaguzi, wakisaidiwa kushika nafasi yao hasa kwa njia ya ustadi. Kazi ya binadamu iheshimiwe kuliko mengine yanayohusu uchumi (k.mf. mtaji au malighafi). Wote wana wajibu na haki ya kufanya kazi na kujipatia hivyo riziki za kutosha. Vilevile wana haki ya kupata muda kwa maisha ya kifamilia, hasa akina mama. Wafanyakazi ni haki yao kuchangia uongozi wa kampuni, na vilevile kuunda vyama vya kutetea haki zao hata kwa migomo.

Mojawapo kati ya mambo yaliyozingatiwa zaidi na mtaguso ni njaa ya umati; kwa ajili hiyo umekumbusha kuwa Mungu ameumba vyote kwa ajili ya wote, basi ni lazima mali zigawiwe kwa haki na upendo. Ingawa mtu yeyote ana haki ya kumiliki vitu kadhaa, ni lazima kila mmoja awe na mali za kutosha, wasiwepo wenye kujipatia mali nyingi kiasi cha kuacha wengine wakose hata mahitaji. Matajiri wawajibike haraka kuwashirikisha wengine, la sivyo watakuwa wauaji wa wenye njaa. Hao wa mwisho ni haki yao kujipatia riziki kutoka utajiri wa wenzao. Kadiri ya mazingira tunaweza kuwa na njia mbalimbali za kuhakikisha wote wapate riziki zao (desturi za ukarimu, pensheni n.k.). Mashamba yagawiwe kwa wakulima wasiyonayo.Pesa zitumike ili kuandaa nafasi za kazi kwa watu wa leo na wa kesho wa nchi zote (vitegauchumi). Wakristo watafute ufalme wa Mungu hata katika uchumi na shughuli nyingine za kijamii.

 

Sura ya nne inafikiria siasa ambayo pia siku hizi inapitia mageuzi makubwa. Mchango wa Kanisa ni kutetea heshima ya kila mtu kwa kusisitiza kwamba lengo la siasa ni ustawi wa jamii nzima kuanzia watu na familia. Uongozi unahitajika ili kulinganisha kwa haki madai ya watu mbalimbali. Wananchi wote waelimishwe kuhusu siasa ili watoe mchango wao kwa kutumia nafasi wanazopewa (kura n.k.) na kwa kutetea haki zao bila ya kuwadai mno viongozi. Jamii na Kanisa vinawahudumia watu walewale lakini kwa namna tofauti, hivyo havichanganyikani bali ni vema vishirikiane. Hata hivyo Kanisa halifungamani na siasa yoyote, liweze kutangaza kwa uhuru maadili yanayotakiwa hata katika siasa, likipima mambo yote na kuhimiza yaliyo mema.

 

Hatimaye, sura ya tano inaongelea ujenzi wa amani na umoja kati ya mataifa. Wakati ilipoandikwa ulikuwa wa mafadhaiko makubwa kuhusu dunia nzima kuja kuangamizwa na wingi na ukali wa silaha zilizotengenezwa. Kwa msingi huo swala la vita linatakiwa tulifikirie upya kabisa, tusiridhike na msimamo wa zamani kuhusu masharti ya uhalali wake. Vilevile Wakristo wa madhehebu yoyote tuungane kati yetu, tena na wote wenye mapenzi mema, katika kujenga amani na haki. Kwa kuwa amani ya kweli sio tu kusimama kwa vita, labda kwa hofu tu ya silaha zilizolundikana; amani ni tunda la haki ambayo itafutwe mfululizo kwa bidii, tena ni tunda la upendo ule wenye msingi ndani ya Mungu. Kuhusu vita vinavyoendelea huku na huku, kwanza ukatili wake upunguzwe (kumbe siku hizi umezidi kwa sababu ya silaha mpya, mashambulizi ya raia, uangamizaji wa kabila zima n.k.). Utiifu kwa maagizo hauwezi kuwa kisingizio cha kutenda maovu, bali ni wajibu kuyakataa. Mapatano ya kimataifa kuhusu vita yaheshimiwe na wote. Ni wajibu wa viongozi wa nchi kuzilinda hata kijeshi, lakini wasitumie jeshi ili kugandamiza wengine. Pia waheshimu dhamiri ya wasiojisikia kutumia silaha. Vitendo vinavyowezekana leo vya kuangamiza miji mizima au maeneo mapana pamoja na wote waliopo ni makosa ya jinai yasiyovumilika. Wanaotengeneza au kununua silaha ili kujikinga na maadui wasije wakashambuliwa, wafikirie hatari ya silaha hizo kuja kutumika kweli, tena hasara ya maskini wanaokosa misaada wanayostahili kwa sababu tu pesa nyingi sana zinatumika kwa silaha. Tutafute mapema njia za upatanisho na muundo wa kimataifa wenye uwezo wa kudumisha amani na haki kwa wote. Hapo katikati akiba za silaha zipunguzwe kwa mpango wa pamoja. Viongozi na watu wao waache utaifa na misimamo yo yote inayotenganisha watu. Hasa malezi ya vijana na upashanaji habari vieneze mawazo ya amani na mitazamo mipana yenye faida kwa binadamu wote. La sivyo tutafikia tu ile amani ya kutisha itakayopatikana kwa kufa wote. Kanisa likisema hivi haliachi kutumaini na kuhimiza wongofu wa mioyo.

Kuhusu kujenga umoja kati ya mataifa, mara nyingi misingi ya kutoelewana ni hali tofauti mno za uchumi, nia ya kutawala, dharau ya wengine na vilema mbalimbali. Basi, ushirikiano mkubwa unaowezekana leo uwe njia ya kutatua matatizo hayo na kukidhi mahitaji ya watu, hasa maskini. Miundo ya kimataifa iliyopo iwajibike kuzingatia zaidi nchi zinazoendelea, wakimbizi na wengine wenye shida maalumu.

Ingawa miaka ileile ya mtaguso nchi nyingi zilipata uhuru wa kisiasa, hali ya uchumi inazirudisha chini ya ukoloni wa namna mpya. Basi, mshikamano uendeleze kweli nchi hizo. Lakini maendeleo yanategemea watu kuliko pesa, kwa hiyo kazi ya kwanza ni kuandaa raia wa nchi maskini kwa elimu na ufundi. Inahitajika misaada, mikopo na vitegauchumi tena kwa ukarimu, lakini pia kurekebisha sana sheria za uchumi wa kimataifa. Upande wao viongozi wa nchi maskini wapokee misaada hiyo kwa uaminifu, na raia wao wajitahidi kutumia vile vyote walivyo navyo. Maendeleo ya uchumi yasitusahaulishe roho ya binadamu, kwa kuwa huyo haishi kwa mkate tu.

Wengi leo wanafadhaishwa na kasi ya ongezeko la watu. Utatuzi wa kwanza ni kuleta usawa mkubwa zaidi kati ya watu na kueneza ujuzi kuhusu kilimo n.k. Halafu zitungwe sheria zinazosaidia familia, izuiwe kasi ya watu kuhamia mijini, watu waelimishwe kwa ukweli kuhusu hali ya nchi na uzazi wa mpango. Wote wajiepushe na njia za mkato zinazokwenda kinyume cha maadili na cha haki ya msingi ya wananchi kufunga ndoa na kuzaa wanavyoona vema wenyewe. Basi, wasaidiwe kuunda dhamiri na kujifunza njia halali za kupanga uzazi.

Wakristo wawe mstari wa mbele katika mshikamano wa kimataifa, wakijua Yesu katika maskini analia na kudai upendo. Mtaguso uliita kikwazo kuona nchi za Kikristo zikitapanya mali, wakati nyingine zinalemewa na njaa, maradhi n.k. Wakristo wajitolee kuhamia kwenye shida ili kusaidia kwa hali na mali wakishirikiana na miundo na watu wowote, kwa kuwa tunaye Baba mmoja na tunapaswa kuishi wote kidugu. Hapo watatambulikana kama wafuasi halisi wa Kristo. Tukikumbuka kuwa hatutaingia mbinguni kwa kusema tu, Bwana, Bwana, bali kwa kutimiza mapenzi ya Baba, tukabili kazi hiyo kubwa ambayo tutahukumiwa siku ya mwisho kwa jinsi tulivyoifanya.

 

 

INTER MIRIFICA

 

Hati hiyo ilitolewa na mtaguso mapema ili kukabili jambo ambalo siku hizi ni zito sana kwa jinsi linavyochangia maisha na utamaduni wa watu duniani kote, yaani vyombo vya upashanaji habari. Hivyo vimeendelea hasa katika karne ya XX na kuwafikia karibu watu wote vikieneza habari, mawazo, maadili n.k. Kanisa linavipokea kwa shukrani kwa Mungu aliyempa binadamu akili ya kuvumbua na kubuni njia hizo zinazoweza kumuinua hata kidini. Lakini kwa ubaya wa moyo wake anaweza pia kuzitumia kwa uharibifu wake na wa wengine wengi, hasa watoto na vijana wasio na kinga. Kwa hiyo Kanisa linapaswa kushughulika ili vyombo hivyo vyote vitumike vema kwa kueneza habari njema, maadili na taarifa za kweli ili watu wakabili maisha vizuri na kuokoka. Pia liwaelimishe wote kuhusu namna ya kuchuja na kutumia vilivyo magazeti, vitabu, filamu, redio, televisheni n.k., wakielewa urahisi wa kudanganywa na kupotoshwa na vyombo hivyo. Hiyo ni kazi ya wachungaji, wazazi na walezi, lakini serikali pia isaidie kutunza mazingira safi. Mtaguso umeagiza shughuli hizo ziratibiwe kijimbo, kitaifa hata kimataifa. Kwa kuwa shughuli hizo zina gharama kubwa, Wakristo wanahimizwa kujitolea kwa ukarimu hasa Jumapili maalumu moja kwa mwaka.

 

 

ORIENTALIUM ECCLESIARUM

 

Mtaguso ulizingatia hali duni ya Makanisa Katoliki ya Mashariki ukaamua kuirekebisha. Kwanza ulitamka kuwa yanastahili kuheshimiwa sana pamoja na mambo yote (liturujia, teolojia, sheria, miundo n.k.) kama sehemu ya hazina ya Kimungu iliyokabidhiwa kwa Kanisa. Liturujia zitunzwe kiaminifu na kurekebishwa kama zimeachana na mapokeo ya Mashariki, hasa sakramenti zirudi kufuata taratibu asili. Mashirika ya Kilatini yajitahidi kuanzisha jumuia za Mashariki. Madhehebu yoyote ya Kikatoliki yana haki na wajibu sawa hata kuhusu uenezaji Injili duniani kote. Wachungaji wa hayo yote wazoee kushirikiana, na wanaojiandaa kupata upadri waelimishwe juu ya uhusiano kati ya madhehebu hayo. Waamini wa Mashariki wapatiwe mapadri na maaskofu wao popote wanapohitaji. Waortodoksi wakijiunga na Kanisa Katoliki waendelee kufuata madhehebu yao, na wenye daraja kati yao waendelee kuitumia. Kutokana na umuhimu wa patriarki kwao, hadhi na haki zake zirudishwe kama kabla ya utengano na Waortodoksi, na Makanisa yasiyo naye yafikiriwe. Hatimaye hati hiyo inahimiza Wakatoliki wa Mashariki kushughulikia ekumeni hasa upande wa Waortodoksi, ikiruhusu kutoleana nao sakramenti kadhaa na mengineyo.

 

 

UNITATIS REDINTEGRATIO

 

Kurudisha umoja kati ya Wakristo wote ni lengo kuu mojawapo la mtaguso. Matengano yaliyokata vipandevipande mwili wa Kristo ni kinyume cha matakwa yake na yanakwaza ulimwengu usiweze kuamini. Siku hizi Mungu ametuhurumia na kututia hamu ya umoja hata ukatokea mfumo wa ekumeni. Kwa hati hiyo Kanisa Katoliki linawajibika kushirikiana na madhehebu yoyote ya Kikristo lisije likazuia kazi hiyo ya Roho Mtakatifu.

Sura ya kwanza inaeleza msimamo wa Kikatoliki kuhusu ekumeni. Imani yetu ni kwamba Kanisa ni moja tu, nalo limekabidhiwa kwa waandamizi wa mitume chini ya waandamizi wa Petro. Tunakiri kuwa mafarakano yaliyotokea kati ya Wakristo yalisababishwa na makosa ya pande zote. Waliolelewa Kikristo nje ya Kanisa Katoliki hawawezi kulaumiwa, tena ni Wakristo halisi na ndugu zetu, ingawa ushirika wetu si kamili. Tuwaheshimu pamoja na mema yao mengi ambayo yanatokana na Mungu na kuelekea ujenzi wa Kanisa. Makanisa yao au jumuia zao vinatumiwa na Mungu kama vyombo vya wokovu, ila katika Kanisa Katoliki tu unapatikana ukweli mzima na vifaa vyote vya wokovu. Hata hivyo tunakiri kwamba hatutumii vizuri neema hizo hata tunawakwaza wenzetu; basi, tunapaswa kulenga ukamilifu wa Kikristo ili Kanisa ling’ae mbele ya wote. Mbali ya matendo ya kupendana ni muhimu pia majadiliano ya kiteolojia na mikutano ya sala ya pamoja.

Sura ya pili inaeleza utekelezaji ikisisitiza kuwa unawapasa waamini wote, kwa njia ya kurekebisha Kanisa, kuongoka, kusali, kushirikishana sakramenti, kufahamiana, kueleza imani kwa usahihi na bila ya kudharau madhehebu mengine, kushirikiana katika kutetea haki na amani na kuleta maendeleo.

Sura ya tatu inaeleza kifupi historia ya mafarakano kwa kutofautiana sana yale yanayohusu Waortodoksi na yanayohusu Waprotestanti, hasa kutokana na makundi hayo mawili kuwa au kutokuwa na daraja halisi na hivyo kuwa au kutokuwa na ekaristi. Kwa msingi huo yanastahili kuitwa Makanisa au jumuia za Kikanisa tu. Uhusiano wetu na makundi hayo ni tofauti, na uwezekano wa kushirikiana katika sakramenti ni mkubwa kwa Waortodoksi bali ni mdogo kwa Waprotestanti.

Mwishoni hati hii inakiri kuwa ekumeni inapita uwezo wetu, kwa hiyo tegemeo lote ni katika sala ya Yesu kwa Kanisa, katika upendo wa Baba na katika uwezo wa Roho Mtakatifu.

 

 

CHRISTUS DOMINUS

 

Mtaguso, baada ya kufundisha wazi juu ya daraja ya maaskofu, ulitunga hati nyingine kuhusu utendaji wao katika ngazi tatu: Kanisa zima, Makanisa maalumu na ujirani mwema wa majimbo.

Kwanza askofu yeyote ni kiungo cha kundi la maaskofu ambalo linaongozwa na askofu wa Roma na kuwajibika kulichunga Kanisa zima. Wajibu huo unatimizwa kwa kushiriki mtaguso mkuu, ambako ni haki ya maaskofu wote, kuchangia muundo mpya wa sinodi ya maaskofu, kushughulikia kwa hali na mali misheni na majimbo yasiyo na mapadri au mali za kutosha, kuwaombea maaskofu wafungwa na wanaodhulumiwa, kuchangia katika ofisi za papa.

Pili, ni wajibu wa baadhi ya maaskofu kuchunga kwa jina la Bwana sehemu fulani ya taifa la Mungu wakitimiza kazi za kufundisha, kutakasa na kuongoza kama wachungaji halisi, ingawa wanapaswa kuheshimu mamlaka ya papa, patriarki na maaskofu wakuu. Chini ya askofu wake jimbo ni Kanisa maalumu ambamo Kanisa pekee linaishi na kutenda. Hati hiyo inaelekeza namna ya kutimiza wajibu huo (pamoja na kuagiza utungwe mwongozo maalumu ambao ufafanue zaidi), inaagiza mipaka ya majimbo irekebishwe yasiwe makubwa mno wala madogo mno, na inaratibu uhusiano na maaskofu waandamizi na wasaidizi, nafasi ya makamu na halmashauri za askofu, uhusiano na maparoko na mapadri wengine. Swala lingine gumu ni uhusiano na watawa hasa walio mapadri, ambao wamehimizwa sana kuishi kweli kama viungo vya jimbo na kujihusisha na maendeleo yake ya Kiroho na ya kitume kwa kushirikiana na askofu, mapadri na walei pamoja na watawa wengine. Pia maaskofu wazee au wenye shida nyingine wanahimizwa kujiuzulu.

Tatu, maaskofu wanahimizwa kuchangia ustawi wa Kanisa katika maeneo yao kupitia sinodi, mitaguso ya kanda au ya nchi, mabaraza ya maaskofu, ushirikiano katika kanda, pia na maaskofu waliopewa kazi tofauti na jimbo (k.mf. uchungaji wa askari wote wa nchi yao).

Maagizo yote ya hati hiyo yalikusudiwa kuongoza marekebisho ya sheria za Kanisa.

 

 

PERFECTAE CARITATIS

 

Siku hiyohiyo iliyotolewa hati kuhusu uchungaji wa maaskofu ilitolewa nyingine kuhusu kurekebisha upya maisha ya kitawa, nayo pia msingi wake ni hati Lumen Gentium juu ya Kanisa ambamo watawa wana nafasi yao (sura ya sita). Mtaguso ulitaja marekebisho makuu tu ya kufanywa, ukimuachia papa atunge sheria hapo baadaye. Hasa ulisisitiza hali mpya ya utawa inayotakiwa kutokana na mambo matano: kushika Injili kama kanuni kuu, kufuata kiaminifu karama ya mwanzilishi na mapokeo bora ya shirika, kujihusisha na maisha na malengo yote ya Kanisa, kupima hali na mazingira ya watu wa leo, kuweka mbele maisha ya Kiroho kuliko mipango mingine. Ili kuzingatia hayo yote, sheria za watawa zirekebishwe kwa kuwahusisha wanashirika wote.

Kabla ya kueleza juu ya aina mbalimbali za utawa, hati hiyo inasisitiza mambo kadhaa yaliyo sawa kwa zote: kushika mashauri ya Kiinjili, kujikatalia ulimwengu, kuwekwa wakfu kwa Mungu juu ya msingi wa ubatizo, kulitumikia Kanisa, kutekeleza maadili, kumfuata Kristo kwa bidii kama jambo pekee la lazima, kuunganisha sala hasa na moyo wa kitume. Nafasi ya kwanza inayo maisha ya Kiroho yaliyo chemchemi ya upendo unaohuisha hata utekelezaji wa mashauri ya Kiinjili. Watawa katika kulisha maisha ya sala wazingatie kila siku Maandiko matakatifu halafu liturujia.

 

Katika kutofautisha aina za utawa, kwanza yanatajwa mashirika yanayoshughulikia sala tu katika upweke na kimya; baadaye yanatajwa mashirika yale mengi yaliyoanzishwa waitimize huduma maalumu kwa niaba ya Kanisa na kama sehemu ya maisha yao ya kitawa; mwishoni yanatajwa mashirika yanayotakiwa kuunganisha kiaminifu ratiba ya sala na taratibu nyingine za kijumuia pamoja na utume fulani.

Halafu hati inaongelea maisha ya kitawa ya mabradha na masista, ikisisitiza kuwa ni muhimu yalivyo, bila ya kuhitaji yakamilishwe na daraja takatifu. Vilevile inasisitiza sura ya mashirika ya kilimwengu yanayopaswa kutafuta utakatifu kwa kuishi katika mazingira ya watu wa kawaida: kwa ajili hiyo yanahitajika malezi bora.

 

Baadaye hati inarudi kufafanua mambo yanayowahusu watawa wowote, hasa mashauri makuu matatu ya Kiinjili, ikitanguliza useja kwa kuwa ndio msingi hasa wa kubainisha waliowekwa wakfu kwa Mungu na kwa ufalme wake kwa namna ya pekee. Hati inaonyesha ubora wa useja na njia za kuushika sawasawa baada ya jaribio la kutosha. Halafu inasisitiza ufukara kama ushahidi unaothaminiwa sana siku hizi: basi, usiwe wa kiroho tu au wa binafsi tu, bali uonekane wazi katika maisha ya jumuia pia. Kuhusu utiifu umesisitizwa ukuu wa sadaka hiyo ambayo mtawa anaungana kwa hakika na matakwa ya Mungu kwa mfano wa Yesu. Pamoja na hayo ajitahidi kutoa mchango wake na kuwajibika chini ya viongozi kama mtu aliyekomaa. Upande wao viongozi wasitawale kwa mabavu bali waonyeshe upendo wa Mungu kwa mtawa, wakimheshimu na kumsikiliza na kumuachia nafasi ingawa wana haki na wajibu wa kumuagiza la kufanya. Pia mikutano na halmashauri vishiriki katika uongozi.

Sifa nyingine ya mashirika ya kitawa ni maisha ya pamoja ambayo yamesisitizwa upya kwa kutia maanani misingi yake na utekelezaji wa upendo kamili katika ushirika wa kidugu. Kwa lengo hilo tunakuta himizo la kufuta matabaka kati ya masista na la kushirikisha zaidi mabradha katika maisha ya jumuia, pamoja na kibali cha kuleta usawa kati ya wanashirika makleri na walei.

 

Katika kulinda utawa toka zamani unatumika ugo, ambao kwa baadhi ya watawa wa kike unafuata sheria za papa. Hati hii inadai hizo zirekebishwe, halafu zisibane wale wanaofanya utume fulani. Kinga nyingine ya watawa ni nguo maalumu. Kwa mara ya kwanza katika historia mtaguso uliongelea swala hilo na kulitia maanani kama alama ya kuwekwa wakfu, pamoja na kuagiza baadhi zibadilishwe.

Upande wa malezi hati hii imeyasisitiza sana kama msingi wa urekebisho, ikikataza watawa wasitumwe kufanya shughuli mara baada ya unovisi, bali waendelee kuundwa katika nyumba maalumu. Halafu malezi yaendelee maisha yote kwa ushirikiano wa watawa na viongozi wao, ambao wajitahidi hasa kuandaa walezi wa kufaa.

 

Zinafuata taratibu kuhusu kuunda mashirika mapya, halafu kuhusu kueneza aina mbalimbali za utawa katika Makanisa machanga kwa kuzingatia utambuzi na utamadunisho. Mashirika yaendelee kutimiza shughuli zake maalumu kulingana na karama na nyakati pamoja na kustawisha moyo wa kimisionari. Yale yasiyostawi yakatazwe yasipokee tena wanovisi au yaunganishwe na lingine la kufanana nayo. Tofauti na muungano, mtaguso umependekeza pia shirikisho la monasteri au mashirika ya familia moja ya kiroho, vyama vya mashirika yenye kazi ileile, mabaraza ya wakuu wa mashirika yote ya nchi au jimbo fulani ili kurahisisha ushirikiano kati ya watawa, tena kati yao na maaskofu.

Swala la mwisho ni namna ya kupata miito ya kitawa: hiyo ni kazi ya Kanisa lote, kuanzia mapadri, wazazi na walezi. Mashirika yenyewe yanaweza kujitafutia miito kwa kufuata taratibu za Kanisa, lakini njia bora ni kutoa mfano mzuri. Hatimaye watawa wote wanahimizwa kuitikia upya wito wao.

 

 

OPTATAM TOTIUS

 

Siku hiyohiyo ilitolewa hati nyingine tena inayohusu malezi ya kipadri: toka mwanzo hayo yanatiwa maanani sana kwa kusema urekebisho unaotumainiwa wa Kanisa lote unategemea kwa kiasi kikubwa upadri ukitimizwa kwa roho ya Kristo. Kuhusu jambo hilo mtaguso ulikusudia kulinganisha mang’amuzi ya karne zilizopita na mahitaji mapya. Kwa kuwa malezi yanapaswa kuwa tofauti kwa kila mtu na kila aina ya watu, basi maagizo ya hati hiyo yanayolenga kulinda umoja wa upadri, yatekelezwe kwa namna tofauti kadiri ya mazingira, madhehebu na aina ya upadri (watawa, wanajimbo waseja na wenye ndoa).

Kwanza jumuia nzima inapaswa kuwajibika kwa malezi ya vijana na ustawi wa miito hasa kwa njia ya sala. Wakurugenzi wa miito wasishindanie vijana, bali tujifunze wote kuwa na mtazamo wa Kikanisa na wa kimataifa. Njia ya kawaida ya kuotesha mbegu za miito ni seminari ndogo. Hizo si za lazima, kinyume na seminari kuu ambapo malezi yote yanalenga upadri moja kwa moja. Walezi wachaguliwe kati ya mapadri bora, kwa kuwa malezi yanawategemea hasa wao. Waseminari waendelee kuchambuliwa kwa imani ya kwamba Mungu hatakubali Kanisa likose wahudumu ikiwa wasiofaa wanaelekezwa kwingine. Namba nyingine zinahusu malezi ya kiroho, upendo kwa Kanisa, malezi ya kijinsia, ukomavu wa kibinadamu na uwezekano wa marekebisho ya sheria. Yanafuata maagizo kuhusu masomo yenyewe ambayo moyo wake uwe ni Biblia, na masomo ya juu. Pia inasisitizwa kuwa masomo na malezi hayo yote yanalenga uchungaji katika nyanja zote.

 

 

APOSTOLICAM ACTUOSITATEM

 

Mtaguso uliwaongelea walei katika hati mbalimbali ukionyesha nafasi yao katika maisha ya Kanisa (liturujia, upashanaji habari, ekumeni n.k.). hata hivyo uliona umuhimu wa kuwaandikia hati maalumu iwaongoze hasa katika utume ili watimize wajibu wao kwa wokovu wa ulimwengu. Karibu waamini wote ni walei, tena ndio wanaoshirikiana zaidi na watu wowote katika yote: hivyo wasipotoa mchango wao, utume wa Kanisa utakuwa mlemavu, hasa siku hizi. Si kwamba wanapaswa kufanya utume kutokana na upungufu wa mapadri na watawa, bali kutokana na wito walioupata katika ubatizo na kipaimara.

Sura ya kwanza inaeleza wito