|
![]() |
SAFARI
YA MALEZI
ya Utawa wa
Ndugu Wadogo wa Afrika
YALIYOMO
0.1.
AINA ZA UFUASI
Yesu, Mwana wa Baba, ndiye ukombozi na ukamilifu
wetu.
Kadiri ya matakwa ya Baba na kwa msukumo ya Roho
Mtakatifu, kila wakati wanapatikana waamini ambao wanamfuata Yesu na kushuhudia
fumbo lake kwa namna mbalimbali, hasa: walei kwa kuratibu malimwengu, wenye
daraja kwa kutoa huduma walizokabidhiwa mitume, na wanaoshika mashauri ya
Kiinjili kwa kufanana zaidi na Yesu safi, fukara na mtiifu ili wote watambue
kuwa kweli yu pamoja nasi hata mwisho wa dunia.
0.2.
KARAMA YETU
Mungu Baba ametujalia tuanzishe chama cha
kimisionari chenye jamaa mbalimbali ndani yake, ambamo tufuate nyayo za Mwanae
katika kujishusha mfululizo ili kutumikia kwa upendo hata kufa msalabani.
Sisi sote wanachama tuishi kati ya watu wa nyakati
zetu tukiwa na msimamo huohuo aliokuwanao yeye, ingawa kila mmojawetu kadiri ya
hali maalumu aliyonayo ndani ya Kanisa, kama mlei, kleri au mshikamashauri ya
Kiinjili.
Tarajio la chama ni kujaliwa kwa wingi mashahidi wa
imani ambao wamelishwa sana Injili hata waweze kuishi kama ndugu wadogo wa wote,
tena kwa namna bora zaidi na zaidi, katika mazingira mbalimbali watakayopangiwa.
0.3.
SAFARI HII
Kwa ajili hiyo yanahitajika malezi ambayo yafuate
maelekezo ya Kanisa na kulingana na karama yetu maalumu, tusiisawazishe na miito
mingine tusije tukamzimisha Roho Mtakatifu na kulidhoofisha taifa la Mungu.
Malezi hayana mwisho kamwe: ingawa kuna hatua za
kupigwa, ni mtiririko mmoja tu wa ustawishaji wa maadili n.k.
Ulinganifu wa malezi ya Kiroho, ya kitume, ya
kielimu na ya kiufundi utusaidie tangu tunuie kukomaa ndani ya Kristo mpaka
tukutane naye moja kwa moja kwa kupokea ndugu kifo.
0.4.
MIONGOZO MAALUMU
Mpango huu unakusudiwa kuonyesha wazi namna ya
kuchochea karama yetu.
Upande mmoja utuonyeshe namna ya kuitekeleza katika
hatua mbalimbali za maisha hadi kufikia utakatifu.
Upande mwingine utuonyeshe namna ya kuishirikisha
kikamilifu kwa vizazi vijavyo viweze kuitimiza katika utamaduni wowote, kwa kuwa
Ufransisko unafaa kuutakasa na kuuboresha kila utamaduni kwa chumvi na chachu ya
Injili, bila ya kukwama katika wowote ule.
Lakini malezi hayawezi kupangwa jumla tu, pasipo
kuzingatia wahusika ni wepi na wanaishi wapi: kwa hiyo mpango huu utimilizwe na
halmashauri kuu kwa kila jamaa, hatua na nyumba.
Miongozo yake hiyo iwe sahili, mifupi na wazi,
ilingane na mpango huu halafu ipitiwe kwa marekebisho kila baada ya miaka mitatu.
1.1.
UTATU NA UTAWA
Karama yoyote ya kitawa inaongoza kwa Baba, ikitia
hamu ya kutimiza matakwa yake yote: humo utiifu unazaa uhuru wa kweli, useja
mtakatifu unatokeza jinsi moyo usivyoweza kutosheka na upendo wa viumbe, na
ufukara unachochea njaa ya haki aliyoahidi kuishibisha.
Halafu inaongoza kwa Mwana, ikirahisisha ushirika
wa ndani naye, katika kuwatumikia kwa bidii Mungu na watu, na katika kusali na
kuteseka ili kueneza ufalme.
Hatimaye inaongoza kwa Roho Mtakatifu, ikiandaa
kujiachia kwake na kutegemezwa naye katika maisha ya Kiroho, ushirika wa kidugu
na utume.
1.2.
KARAMA ZA KITAWA
Namna mbalimbali za kuishi kitawa zinatokana na
karama maalumu ambazo waanzilishi walijaliwa na ambazo wafuasi wao
wakashirikishwa ili wazitekeleze, wazitunze, wazichimbe na kuziendeleza
mfululizo kulingana na ustawi wa Mwili wote wa Kristo.
Kanisa linataka kila utawa ustawi kadiri ya karama
hai na bunifu ya mwanzilishi, kufuatana na mapokeo yake maalumu ya Kiroho, ya
kijumuia na ya kitume.
Hivyo sio tu kwamba tuna historia tukufu ya
kuikumbuka na kuisimulia, bali pia tunayo nyingine ya kuitimiza bado ili katika
milenia mpya ulimwengu uliokabidhiwa mikononi mwetu binadamu uwe na imani na
upendo, haki na amani zaidi, uwe kama utangulizi wa ulimwengu ujao.
Roho anatusukuma tukafanye makuu, hivyo tuitazame
kesho kwa tumaini.
1.3.
UTAWA NA NYAKATI ZETU
Tumeitwa tutambue na kuhudumia mpango wa Mungu kwa
ajili ya watu, ambao unatangazwa na Maandiko Matakatifu na kujitokeza katika
maisha yao.
Kwa hiyo tuwe tayari kuchochewa na Neno la Mungu na
ishara za nyakati, tukiunganisha daima upya wa Kiroho na ari ya kitume, ambavyo
cha kwanza kinawezesha cha pili.
Tumshiriki Mungu ili kukabili changamoto za nyakati
zetu, tukiamini ya kuwa Roho anaweza kutoa majibu ya kufaa hata kwa zile ngumu
zaidi.
Mbele ya changamoto kuu tatu za ulimwengu tuonyeshe
jinsi mashauri ya Kiinjili yanavyotustawisha kwa kutuelekeza moja kwa moja kwa
Mungu aliye Wema mkuu, badala ya kufuata mielekeo ya kibinadamu iliyoathiriwa na
dhambi.
Hasa siku hizi wanahitajika watakatifu ambao
watumainishe wale waliokata tamaa kuhusu maisha na maana yake: ubora wa utawa
unaweza kuwatuliza wale wanaoona kiu ya tunu halisi.
1.4.
USEJA MTAKATIFU NA UTAMADUNI WA ANASA
Changamoto ya kwanza ni utamaduni wa anasa unaoona
jinsia ni mchezo tu usio na masharti: matokeo ni maovu ya kila aina yanayoathiri
kinafsi na kiuchumi jamii, familia na watu mmojammoja, kuanzia watoto.
Itikio la maisha ya wakfu ni kuishi useja mtakatifu
kwa furaha, na hivyo kushuhudia uwezo wa Mungu unaofanya kazi katika udhaifu wa
binadamu hata akampenda yeye kuliko yote na kumpenda yeyote kwa uhuru wa wanae.
Ushuhuda huo unahitajiwa na wote kadiri
wanavyoshindwa kuuelewa, ili wajifunze kuwa wa kweli katika mafungamano.
Mapendo yao ya kibinadamu yanapewa kielelezo cha
yale safi ya mtawa ambaye anachota katika Mungu-Upendo: kwa kuzama katika fumbo
la Utatu anajisikia apende wote pasipo mipaka na kwa kujitawala.
Hakika, usafi unaukomboa moyo kwa namna ya pekee na
kuzidi kuuwasha upendo kwa Mungu na kwa watu wote.
Mchango mmojawapo mkubwa wa mtawa ni kuonyesha kwa
maisha yake uwezekano wa kujitoa kwa wengine na kushiriki furaha na huzuni zao
kwa uaminifu na udumifu, pasipo vitendo vya jinsia wala misimamo ya utawala na
ubaguzi.
Pia utawa unamaanisha na kuelekea moja kwa moja
uzima wa milele, hasa kwa njia ya useja unaotugeuza tayari kwa ajili ya
ulimwengu ule ambapo watu hawaoi wala hawaolewi.
1.5.
KUZINGATIA TUNU NA GHARAMA YAKE
Kwa kuwa useja huo unadai usafi kamili na kuyahusu
sana maelekeo yetu ya dhati, wanazoezi wasiuahidi wala wasikubalike kabla ya
kujaribu vya kutosha na kufikia ukomavu wa kufaa upande wa nafsi na wa hisi za
moyo.
Watambue kwamba elekeo la umimi tulilonalo linataka
tutie maanani mno mapendo ya kibinadamu, na kumtumia mwenzetu kama njia ya
kujipata heri fulani.
Lakini wasiangalishwe tu kuhusu hatari
zinazowakabili, bali walelewe kukumbatia useja kwa ajili ya ufalme wa Mungu,
kama tunu kwa ustawi wao na wa Kanisa.
1.6.
MALEZI YA USEJA
Malezi ya useja mtakatifu yajitahidi:
- kuchochea furaha na shukrani kwa upendo ule ambao
kila mmoja ametazamwa na kuteuliwa na Yesu;
- kuangazia matunda ya moyo usiogawanyika, yaani
uzazi mwingi wa Kiroho hasa katika utume;
- kuhimiza adhimisho la upatanisho, uongozi wa
Kiroho na upendo halisi katika jumuia;
- kujenga hali ya kuaminiana kati ya walelewa na
mlezi, ambaye awe tayari kusikiliza yoyote kwa upendo ili aangaze na kutegemeza;
- kumsaidia kila mmoja akubali mang'amuzi yake
mabaya ya zamani kwa kutambua udhaifu, kujinyenyekeza na kukesha;
- kumshukuru Mungu tu na kuzuia kiburi cha
kujipongeza kwa usafi, usije ukazua ugumu wa moyo;
- kufundisha juu ya jinsia mbili upande wa mwili,
nafsi na roho;
- kueleza maana ya mwili na namna ya kutunza afya
yake;
- kuelekeza kujitawala upande wa ashiki na wa moyo,
na vilevile upande wa ulafi na ulevi;
- kuwa waangalifu katika kutumia vyombo vya
upashanaji habari na katika mafungamano na watu (busara inawadai watumishi,
walinzi na walezi pia wachukue hatua za kufaa).
1.7.
UFUKARA NA UTAMADUNI WA FEDHA
Changamoto ya pili inatokana na ulimwengu kuabudu
pesa na mali, kwa kutoelewa maana yake kwa maisha, wala kufuata kiasi kinachofaa,
wala kujali mahitaji na mateso ya wanyonge, wala kuhifadhi mazingira kwa ajili
ya wajukuu wetu.
Hivyo leo ufukara unatawala maisha ya watu wengi na
ya nchi nyingi kwa sababu ulimwengu unaendeshwa namna inayozidisha hali ya njaa,
ujinga, maradhi, kukosa kazi, kunyimwa haki za msingi, ukoloni mamboleo, rushwa
n.k.
Itikio la maisha ya wakfu ni ufukara wa Kiinjili
ambao upendo unahimiza kupokea mlio wa wenye mashaka katika matatizo, mateso na
matarajio yao ili kuwasaidia wakabili maisha kwa mshikamano wa wote.
1.8.
YESU NA UFUKARA
Asili ya ufukara huo wa Kiinjili ni kutafakari
alivyoishi Yesu fukara msulubiwa; udhihirisho wake ni kushika maisha ya kawaida
ya watu wadogo kuhusu chakula, mavazi na nyumba, na kukwepa uwezo wowote wa
kutawala wengine kisiasa, kijamii, kiuchumi, kielimu na kidini.
Moyo wa maskini tu ulioamua kumfuata Yesu hivyo
unaweza kushikamana na watu usiambatane na vitu.
Jumuia ndogo za kitawa katika mazingira duni
zinatokeza ule upendeleo wa Kiinjili kwa fukara, unaotufanya sio tu
tuwashughulikie, bali tuishi pamoja nao, tena sawa nao kadiri inavyofaa
kulingana na hali halisi na mahitaji ya kila mmojawetu, hasa akiwa bado katika
hatua za kuingizwa.
Upendeleo huo unatokana na upendo ambao Yesu
aliuishi, hivi kwamba kila mfuasi wake anapaswa kuwa nao, hasa sisi tunaomfuata
kwa karibu zaidi katika maisha ya wakfu, ambayo ni ya kifukara na ya kuwatetea
fukara.
Mshikamano nao ndio msimamo unaotufanya ndugu
wadogo, ni mhuri wa Ukristo halisi, kichocheo cha wongofu, tendo la kitume na
thibitisho la ujio wa ufalme wa Mungu, ambapo fukara wanahubiriwa na kuhubiri
Injili.
Zaidi ya hayo ufukara wenyewe ni tunu iliyotangazwa
na maisha yote ya Yesu kama heri ya kwanza na ushuhuda wa kuwa Mungu ndio
utajiri pekee wa moyo.
1.9.
MALEZI YA UFUKARA
Malezi ya ufukara yakazie maisha ya Yesu
aliyejifanya maskini kwa ajili yetu.
Halafu yahimize:
- kuwa na unyenyekevu;
- kuishi kwa imani kama wana wa Baba wa mbinguni
anayejua mahitaji yetu na kututunza siku kwa siku;
- kuwajibika katika kazi;
- kujali vitu vinavyopatikana jumuiani;
- kutaka vyote viwe kweli vya wote ili kila mmoja
apate anavyohitaji;
- kutumia fedha na vitu kwa usimamizi wa viongozi;
- kubana matumizi iwezekanavyo, bila ya kufuata
uwezo uliopo wala ruhusa tu;
- kuwa tayari kukosa vitu mbalimbali;
- kujiepusha na vitu ambavyo watu wadogo hawawezi
kujipatia, ili kuishi ufukara kwa ukweli zaidi;
- kujinyima kwa hiari hata vitu halali.
Pia yazingatie:
- historia ya kila ndugu kabla ya kupata wito (wengine
walijitegemea na kupata vingi, kumbe wengine walikuwa na hali ngumu kuliko ile
ya jumuia);
- hali ya sasa ya familia yake na matarajio
iliyonayo juu ya mwanae;
- mafundisho ya Kanisa kuhusu jamii, kwa kuwa
ufukara wetu haulengi maendeleo ya roho tu.
1.10.
UTIIFU NA UTAMADUNI WA UHURU USIO NA MASHARTI
Changamoto ya tatu inatokana na mtazamo ambao
unadai hiari ya mtu isibanwe sana na maadili, na hivyo unasababisha kwa wingi
ubinafsi, dhuluma, ukatili n.k.
Itikio la kufaa ni utiifu wa kitawa unaoonyesha
kwamba kutimiza matakwa ya Mungu kunatukamilisha kwa kukuza ukweli wetu kama
viumbe tunaomtegemea kabisa Muumba, na kama watoto wapenzi tunaotafuta na
kutekeleza kwa pamoja yale yote yanayompendeza Baba.
Umoja huo wa jumuia ni ishara kubwa ya jinsi ya
kushinda ugomvi na utengano, na ni hakika ya kufuata njia tuliyopangiwa.
Katika malezi na maisha ya kila siku, chama
kinatusaidia tupate msimamo wa kudumu, kwa mafundisho ya hakika kuhusu kufikia
ukamilifu, kwa ushirika wa kidugu katika kumfuata Yesu na kwa utiifu
unaoimarisha hiari yetu katika kuitikia wito.
1.11.
KUSHIRIKI UTIIFU WA YESU
Shauri hilo, tunalolipokea kwa upendo ili kumfuata
Yesu aliyetii hata kufa msalabani, linatuelekeza tuweke matakwa yetu chini ya
yale ya wakili wa Mungu, yaani mlinzi, mtumishi, askofu na hasa Baba Mtakatifu.
Utiifu huo hautudhalilishi bali unastawisha uhuru
wetu kama wana wa Mungu wanaoendeleza ule wa Yesu kwa wokovu wa ulimwengu.
Nidhamu utawani isishikwe tu ili kulinda maisha ya
kijumuia na upendo, bali kama sharti la kujijengea tabia ya kujitawala, kukomaa
n.k.
Hivyo itekelezwe namna inayostawisha utayari wa
kutii si kwa hofu, bali kwa kufuata dhamiri na maadili.
Polepole ndugu wazoee kutumia vema hiari yao katika
kujifanyia mipango na kutenda kwa uelewano na watu wa ndani na wa nje ya jumuia,
hasa viongozi.
Mtumishi au mlinzi anayejadiliana na ndugu zake
anawasaidia kutii kwa uwajibikaji, mradi hatimaye awe tayari kutoa uamuzi na
kuagiza la kufanya kwa niaba ya Mungu.
Katika majadiliano hayo tuzuie mawazo ya kibinadamu
mno yasijiingize upande wa kiongozi wala wa ndugu wala kati yao, bali wote
tulenge tu matakwa ya Mungu yafanyike.
1.12.
MALEZI YA UTIIFU
Katika malezi ya utiifu tukumbuke kwamba:
- ni lazima kwanza tutambue na kutambuliwa hadhi
yetu kama watu na watoto wa Mungu ili tutii kibinadamu, si kwa unyonge;
- tunapaswa kuvuka toka yale yanayotupendeza sisi
hadi yale yanayompendeza Mungu, ambayo yanajitokeza kwa namna ya pekee kwa njia
ya wachungaji wa Kanisa na ya kanuni na katiba walizotuthibitishia;
- ushuhuda wetu kama watawa watiifu una uzito
kuliko nadharia tunayowafundisha walelewa, ingawa hao wanatakiwa kufuata njia
nyofu bila ya kukwazwa na mifano yetu mibaya.
1.13.
USHUHUDA WA JUMUIA
Kwa kuwa tendo la kuweka ahadi linatuingiza katika
chama kwa haki na wajibu vinavyoelezwa na katiba, tunapaswa kuishi kidugu katika
jumuia yake mojawapo kama mahali ambapo upendo, ukichota nguvu katika sala,
uongoze maisha yote na kuzaa heri.
Hivyo uanachama unatuwezesha kumpatia Yesu ushuhuda
wa hadhara na wa pamoja, mradi maisha yetu yawe ishara ya ufalme wa Mungu na
tangazo hai la Injili.
Kwa ushuhuda huo wa jumuia zilizojaa furaha na Roho
Mtakatifu, ambapo ubinafsi unashindwa na uwajibikaji kwa ajili ya wengine,
ambapo madonda yanaponywa na msamaha, na ambapo karama inaongoza uaminifu wa
wote katika wito na utume, ndivyo Kanisa linavyojitambulisha kama sakramenti ya
umoja na Mungu na kati ya watu, na kuonyesha matunda ya amri mpya aliyotuachia
Bwana.
Pamoja na hayo, Kanisa linataka kuonekana wazi
ulimwenguni hata kwa njia ya kanzu zetu.
1.14.
KATIKA USHIRIKA WA KANISA
Maisha ya Wakristo wa kwanza huko Yerusalemu ndiyo
kielelezo ambacho Kanisa lilikizingatia kila lilipojaribu kuchochea ari ya
mwanzoni na kuendelea Kiinjili safari yake.
Kwa mfano wao tuzidi kuchanga na waamini wote neema
na juhudi ili sura ya Kanisa ipendeze, nalo likabili kwa nguvu ya umoja
changamoto za nyakati zetu.
Basi, tusimbane Roho katika chama chetu, lakini
tusaidie wengine kufaidika na karama yetu.
Sisi watawa tunaitwa kuwa wataalamu wa ushirika,
mashahidi na wajenzi wa ule umoja ulio lengo la mpango wa Mungu: tuwe hivyo
kutokana na tamko letu la kushika mashauri ya Kiinjili ambayo yanakomboa ari ya
upendo isiwe na kizuio chochote; tena kutokana na mang'amuzi yetu ya kila siku
katika kuishi, kusali na kufanya kazi kama jumuia ya Kikanisa.
Kwa namna ya pekee ushirika wa Kanisa unatudai
utiifu wa akili na moyo kwa maaskofu, ambao utekelezwe mbele ya watu wote, hasa
tukishughulikia katekesi, ufundishaji, uandishi na upashanaji habari.
Msimamo wetu watawa kuhusu jambo hilo ni muhimu kwa
sababu tuna nafasi maalumu katika Kanisa na katika kushiriki utume wa maaskofu.
1.15.
WANDANI WA MUNGU
Ili tujaliwe kuwa kweli manabii, yaani kusema na
wote kwa niaba ya Mungu, kwanza ni lazima tuwe wandani wake, wasikivu kwa Neno
lake katika nafasi yoyote ya maisha, wenye utambuzi wa Kiroho na kupenda ukweli.
Basi, tuzidi kumuelekea Mungu, tukitafuta uso wake,
tukiachana na mitazamo isiyolingana na ufunuo wake, halafu kubadili mwenendo
wetu pia.
Tukiwa wanafunzi wa Neno linalotolewa na Kanisa,
tunakua kumuelekea Kristo katika yote hata tufikie kimo cha utimilifu wake,
tukizidi kujifunza fumbo la wokovu, kumuabudu Baba katika Roho na Ukweli, na
kutekeleza ukweli kwa upendo.
1.16.
TOBA YA KUDUMU
Ili tuwe mashahidi halisi wa Kristo duniani kote,
kwanza tunapaswa kuhakikisha tumeitwa na Mungu na kumtolea nafsi yetu pamoja na
yote tuliyonayo, hasa yale yanayotuzuia tusimuitikie kikamilifu.
Wito wetu wa toba ya kudumu unataka turekebishe
mfululizo uhusiano wetu na Mungu, na watu na ulimwengu ili Mungu atawale moja
kwa moja maisha yetu.
Kwa ajili hiyo tukiri kwa moyo udhaifu, ujinga na
uovu wetu, halafu tupambane navyo kwa roho na kwa mwili pia, tukifuata kwa
uaminifu kanuni, katiba, ratiba na mbinu za kufanya juhudi.
1.17.
MAISHA YA KIROHO
Daima maisha ya Kiroho yawe na nafasi ya kwanza
katika malezi yetu ili chama kiwe hasa shule ya Injili.
Ukarimu kwa fukara, uzazi wa kitume, mvutio kwa
miito na vinginevyo vinategemea ustawi huo wa ndugu mmojammoja na wa jumuia
nzima katika kuishi ndani ya Kristo kadiri ya Roho Mtakatifu kwa utukufu wa Baba.
Tunafanya safari hiyo ya uaminifu mkubwa zaidi na
zaidi kwa Mungu Baba tukiongozwa na Roho anayetulinganisha na Yesu katika
ushirika kamili wa Kanisa.
Safari hiyo inadai wongofu wetu wa binafsi na wa
kijumuia usikome kamwe, bali uzidi kukamilika kwa kulipokea Neno la Mungu mpaka
ndani ya moyo wetu na ya utendaji wetu, na kwa kuupokea uvuvio wa Roho Mtakatifu
kadiri tulivyojaliwa na Baba, aliye asili na lengo la maisha yoyote.
1.18.
NENO LA MUNGU
Neno la Mungu ndilo chemchemi ya kwanza ya maisha
ya Kikristo: linachochea uhusiano wa dhati na Mungu aliye hai na utekelezaji wa
matakwa yake yenye kuleta wokovu na utakatifu.
Ndiyo sababu toka mwanzo watawa waliheshimu usomaji
wake wa Kiroho, hata hekima ikaangaza maisha yao.
Uzoefu na Neno uliwapa mwanga unaohitajika kwa
utambuzi, wasilingane na mitindo ya ulimwengu.
Kwa mfano wa mwanzilishi wetu, tuitafakari hasa
Injili ili kuzingatia matendo na maneno ya Yesu, Maria na mitume.
Kutafakari Neno na mafumbo ya Kristo kunaleta ari
katika sala na utume; pia kutumia muda wetu miguuni pake ndio namna wazi ya
kumtangaza Yesu kuwa ni Bwana wetu na kuwa yu hai kati yetu.
1.19.
USHIRIKISHANO JUU YA INJILI
Kwa kuwa maisha yetu ni ya Kiinjili hasa, tutie
maanani ushirikishano wa mawazo na mang'amuzi kuhusu Injili.
Kuitafakari kijumuia kuna thamani kubwa kwa
kutufanya tuchange kwa furaha utajiri tuliochota humo ili tukue pamoja na
kusaidiana kidugu katika maisha ya Kiroho.
Tena, ushirikishano juu ya Neno unalisha imani na
tumaini, kuheshimiana na kuaminiana, kupatana na kushikamana katika sala.
Halafu zoezi hilo linatusaidia kulieneza kati ya
viungo vingine vya taifa la Mungu.
Tutafute namna za kuwafanya wote wajifunze
kushirikishana kwa unyofu.
Vilevile ugumu wa mtu fulani kushirikisha ulio na
mzizi wa kisaikolojia usiwe kisingizio cha kutomjali, bali wote wapokee toka
kwake pia yale anayotaka kuyatoa kwa maneno na matendo.
1.20.
LITURUJIA
Tuwe na hakika ya kuwa jumuia inajengwa na
liturujia, hasa ekaristi na upatanisho.
Maajabu hayo ya Mungu yanasababisha sifa, shukrani,
furaha, umoja wa mioyo, nguvu za kukabili matatizo ya kila siku na kutegemezana
katika imani.
Yesu anazidi kutuita pamoja kila siku hasa katika
ekaristi ili aseme nasi na kutuunganisha naye na kati yetu: ndio moyo wa maisha
ya Kanisa na ya utawa vilevile.
Ekaristi inafungamana na juhudi za wongofu
zinazokamilika katika kupokea mara nyingi upatanisho, ili tuwe wazi na waaminifu
katika uhusiano na Mungu.
1.21.
EKARISTI
Sisi tuliomfanya Yesu awe maana pekee ya maisha
yetu, tunavutwa kutamani tuzidi kumshiriki kwa njia ya sakramenti inayomfanya
awepo kati yetu, ya sadaka anayojitoa kwa upendo kwetu, na ya meza anayotulisha
safarini.
Kwa njia hiyo tunaitwa kuishi fumbo la Pasaka
tukiungana naye katika kujitoa kwa Baba kwa nguvu ya Roho.
Tumuabudu mara nyingi na kwa muda mrefu katika
ekaristi ili tufurahie na kutamani zaidi zawadi hiyo.
Hata tusipoweza kuhudhuria Misa kila siku, kiini
cha maisha yetu kiwe ni fumbo hilo la Bwana kuwepo hai ndani ya jumuia.
Katika kulea roho ya kijumuia tuanze daima hapo,
kwa kuwa ekaristi ikiadhimishwa au kuabudiwa na kuliwa ndipo umoja wa mioyo
unapojengwa.
1.22.
SALA YA JUMUIA
Pamoja na ekaristi, Sala ya Kanisa inatokeza wito
wetu wa kuinua daima mioyo kwa Mungu ili kumtolea sifa na maombezi.
Adhimisho lake linahuisha mfululizo sala yetu kwa
kutuletea Neno kadiri ya mzunguko wa mwaka wa liturujia na linatufanya tujisikie
washiriki wa taifa la Mungu.
Sala ni zawadi ya Mungu inayotupasa tuipokee na
kuistawisha kwa bidii, mafunzo na uaminifu.
Hasa walelewa waongozwe kuthamini zaidi na zaidi
nafasi za sala ya jumuia zinazoongoza mwendo wa siku zetu, ili wazitumie zote
kwa bidii walau kuanzia zoezi, wakidumu katika uchipukizi na baadaye.
Kila ndugu apate ujuzi wa kitaaluma, wa Kiroho na
wa kichungaji kuhusu Maandiko na liturujia utakaomwezesha kulishwa navyo na
kuwasaidia waamini wengine wavumbue hazina hizo na kufaidika nazo.
Ili jumuia itimize wajibu wa kulea katika sala,
ndugu wote watoe mchango wao kwa kujenga mazingira yanayofaa, kwa kujiandaa,
kuwahi na kusali vizuri.
1.23.
SALA NA KIMYA
Sala ieleweke kuwa ni muda wa kukaa na Mungu aweze
kufanya kazi ndani mwetu na kuenea katika maisha yetu, akitufariji na kutuongoza
kati ya uchovu na mawazo ya kila aina, kusudi hatimaye tuwe wake tu.
Sala ya pamoja inazaa kadiri inavyoshikamana na ile
ya binafsi: toka mwanzo wa malezi yetu tusisitize umuhimu wa kuhusiana kwa dhati
na Baba, wa kuongea na Bwanaarusi na rafiki moyo kwa moyo, wa kuchimba
yaliyoadhimishwa katika Roho Mtakatifu, na wa kutunza kimya cha ndani na cha nje
kama nafasi ya Roho na Ukweli kutuhuisha kabisa.
Kusikia na kuitikia wito wa utakatifu kunadai kimya
hicho ambacho kimejaa uwepo wa Mungu tu, na kinatuwezesha kuelewa anapotaka na
anavyotaka kusema nasi.
Hivyo tuzoee mapema kimya na upweke: upweke wa
hiari unaelekeza kwenye kimya cha ndani, nacho kinadai kimya cha nje.
Tufurahi kuwaruhusu ndugu waliokwishaonyesha
ukomavu fulani katika maisha ya kijumuia waweze kujipatia nafasi zaidi za upweke
na sala.
Nyumba zetu ziwe tayari kupokea watu kwa ukarimu,
hasa kwa sala, lakini bila ya kuvuruga hali ya kimya, nafasi ya faragha na
mengine ya kitawa.
1.24.
SALA NA KUMSHIRIKI YESU
Tukipanda mlima wa sala pamoja na Yesu, kama
walivyofanya Petro, Yakobo na Yohane, tunafunuliwa fumbo lake katika utukufu wa
Utatu na katika ushirika wa watakatifu, tukatamani kukaa naye moja kwa moja; pia
tunaandaliwa kushuka naye kati ya watu tukabili shughuli za kila siku na
kushiriki msalaba wake bila ya kukwaza nao.
Daima watu wa sala ndio waliofanya makuu, kwa
kuelewa na kutekeleza vizuri matakwa ya Mungu.
Sala inakusudiwa kutuathiri hata kila wazo, neno na
tendo letu, katika nafasi muhimu na za kawaida vilevile, lionyeshe tunavyofanana
na Yesu katika kujitoa mhanga.
Ushirika naye utuongoze kujiunga na kila jambo
ambalo mwenyewe aliunganika nalo kwa dhati: na Baba aliyemtuma ulimwenguni, na
Roho aliyemsukuma maishani, na Kanisa alilojitoa kwa ajili yake, na binadamu
wote, hasa wenye hali ngumu zaidi ambazo alipenda kuzishiriki kama kaka yao.
Tusichoke kuhimizana ili wakati wa shughuli
tudumishe ile roho ya sala inayotakiwa iwe lengo la malimwengu yote, hivi kwamba
siku nzima na kazi zake mbalimbali zigeuke kuwa nafasi za kuungana na Bwana.
Maisha hayo ya ndani yanaleta furaha ya Kifransisko
ambayo ni nguvu ya kushinda mabaya na kuzidi kujitoa maisha yote.
1.25.
MALEZI YA SALA
Katika malezi ya sala tuelekeze:
- kuunda moyo safi unapoweza kung'aa uzuri wa Mungu;
- kutambua daima uwepo wa Mungu na matakwa yake;
- kustawisha uwezo wa kuyashangaa maajabu yake
katika uumbaji na ukombozi;
- kuzoea kusikiliza Neno la Mungu na kutumia sala
za Biblia ili kumuonja Mungu na kuingia katika historia ya wokovu;
- kushiriki kikamilifu maadhimisho ya Kanisa kadiri
ya mwaka wa liturujia ili kuishi mafumbo makuu ya ukombozi;
- kufuata vema ratiba ili kudumisha sala hata
isipojibubujikia;
- kuwa na moyo mpana ambao unasali na kuishi
ukishiriki furaha na huzuni za wote;
- kujua jinsi watu mbalimbali wa zamani na wa siku
hizi walivyong'amua fumbo la Mungu;
- kumpenda kitoto Mama wa Mungu aliyekingiwa dhambi
asili.
1.26.
UDUGU
Mang'amuzi ya dhati ya Mungu kuwa ni Baba
yalimuongoza mzee wetu Fransisko kutambua na kuishi upya udugu wake na watu wote,
hasa na wale aliojaliwa na Baba awe nao njia moja.
Tukishiriki karama yake, tuwapokee na kuwapenda
wenzetu kama zawadi ya Bwana.
Tumetumwa kushuhudia udugu wa Kikristo kwa kuwaona
wote kuwa ni wana wa Mungu tayari, au walau wanaitwa wawe hivyo, na kwa kujitoa
kwa upendo kwa kila mmojawao, hasa wale wa mwisho.
Jina la chama lina uzito mkubwa na linadai tuwe:
- wadogo wa Yesu, wenye uhusiano wa dhati naye,
aliye kaka wa wengi;
- ndugu sisi kwa sisi kwa kupendana na kufanya kazi
pamoja;
- ndugu wadogo wa kila mmoja kusudi tustawishe
udugu ndani ya Kanisa na ya jamii, tukishuhudia upendo wa Kristo kwa wote na
kuwakumbusha ukweli huu wa msingi: "Nyinyi nyote ni ndugu".
1.27.
KUIMARISHA UDUGU
Ili tuhifadhi na kuimarisha maisha ya kidugu kadiri
ya Injili:
- tujiite na kuwazoesha wote watuite "ndugu";
- tunapoeleza karama yetu ili kuchochea miito na
kuingiza utawani, tuyakazie mambo makuu ya maisha hayo (kuishi kijumuia, kuwa
wadogo wa wote n.k.) kuliko kazi au hadhi fulani (upadri n.k.);
- kwa kuwa wito wetu kimsingi ni uleule, malezi ya
utakaji na zoezi yalingane kwa wote; baadaye tu ndugu wapewe nafasi ya
kujiendeleza kadiri ya uwezo wao na ya udogo wetu;
- tutoe huduma za kutufaa zaidi kama wadogo (kutangaza
Neno, kufundisha sala, kutekeleza matendo ya huruma, kufanya kazi za mikono n.k.);
- tuwe watu wa haki na amani, tukiwasaidia wote
kuunda dhamiri zao kuhusu tunu hizo;
- tuchangie pia maendeleo halisi ya jamii kuendana
na Injili na katiba yetu ili tuwe watu wa Mungu wasio mbali na mashaka ya maisha
ya watu.
1.28.
UPENDO WA KRISTO
Kristo katika fumbo la Pasaka ndiye kielelezo cha
kudumu cha namna ya kujenga umoja, tena ndiye chemchemi na kipimo cha upendo
unaohitajika.
Ili tufaulu kuishi kidugu ni lazima Roho wake
atuwezeshe kupendana kama Yesu alivyopenda.
Akiwa ni upendo wake uliomiminwa mioyoni mwetu,
anatusukuma tupende wote kwa kubeba udhaifu wao na matatizo yao hata kujitoa
mhanga kwa ajili yao.
Hasa kuishi na ndugu ambao hawajisikii vizuri, na
hivyo wanasababisha uchungu kwa wenzao na kuvuruga maisha ya jumuia, ni fursa ya
kukomaa kiutu na Kikristo.
Safari hiyo ya ukombozi wa moyo inadai tujikane ili
tumpokee mwingine alivyo, pamoja na tofauti na mipaka yake, sifa na kasoro
vilevile, kuanzia yule aliyepewa uongozi, tusije tukamdai mno.
Moyo huo tu, ambao unatokana na upendo na kulenga
ustawi wa upendo ndani mwetu na mwa wenzetu, utatuwezesha kutegemezana,
kukosoana, kujishtaki hadharani, kukagua na kupanga maisha kwa pamoja n.k.:
namna hizo zote tuzing'amue kuanzia utakaji.
Ikiwa ndugu atajisikia anapokewa alivyo, hapo tu
ataondoa kinga zake na hofu zinazomfunga akapokea ukosoaji na shauri na kukua
vema.
1.29.
JUMUIA NA UKOSEFU
Kwa kuwa maisha na malezi yetu yana elekeo la
kidugu, kumuingiza mtu katika utamu na ugumu wa kuishi pamoja kunafanyika katika
jumuia.
Wengi wanavutiwa nayo, lakini kudumu ndani yake
katika hali halisi ya maisha kunaweza kukawa mzigo mzito: mtu wa kawaida,
akipenda umoja, hataki kuugharimia mwenyewe kwa kuwajibika.
Kwa hiyo toka mwanzo tujulishe kwamba maisha ya
jumuia yanadai sadaka, lakini kujiangamiza kwa ajili ya wenzetu ndiyo njia ya
wokovu: Injili inataka watu ambao, sawa na chembe ya ngano, wanajua kujifia ili
udugu ustawi.
Hivyo jumuia inakuwa shule tunapojifunza kumpenda
kweli Mungu kwa kuwapenda ndugu aliowaweka karibu nasi, na binadamu wote, hasa
wanaohitaji zaidi huruma ya Mungu na mshikamano wa kidugu.
Jumuia kamili haipatikani duniani, ambapo Kanisa
lenyewe, pamoja na miundo na utakatifu wake, linajengwa juu ya udhaifu wa
binadamu.
Hata hivyo kwa msaada wa Mungu tunaweza daima
kuongoka na kujenga kwa pamoja jumuia juu ya msamaha na upendo.
Umoja tunaoulenga unategemea upatanisho: kwa hiyo
utovu wetu wa ukamilifu usitukatishe tamaa, mradi tushike upya kila siku njia
tuliyoelekezwa na Neno.
1.30.
NJIA ZA UMOJA
Umoja halisi ni zawadi ya Mungu kwa wanaosikiliza
Injili na kuishika.
Ili tupendane kama watoto wa Baba mmoja:
- tukuze hali ya kifamilia, ya furaha na ya unyofu
kati yetu;
- tuzidi kuaminiana, kuelewana, kuthaminiana;
- tuelezane shida zetu;
- tuimarishane wakati wa taabu na wa kuvunjika moyo;
- tupendane bila ya masharti;
- tutumikiane kwa ukarimu;
- tutiiane kwa upendo;
- tusihukumiane;
- tuzoee kuvumilia na kusamehe sabini mara saba;
- tukosoane kidugu tukilenga daima wongofu;
- tupambane na ugeugeu wetu na misukosuko ya
kujianzia;
- tuachane na chochote kinachoweza kuvuruga maisha
ya kidugu;
- tushirikishane kila kitu.
Pasipo juhudi hizo, umoja haupatikani.
1.31.
FUMBO LA JUMUIA
Ushuhuda wa kidugu unadhoofishwa na shughuli nyingi
mno zikituzuia tusishiriki kwa kawaida sala za pamoja, maisha ya jumuia na
huduma za nyumbani.
Basi, ratiba ya kila siku isipangwe kwa kujali
utendaji wa kitume kuliko maisha ya kidugu, bali jumuia ijipatie muda wote
unaohitajika ili kuboresha maisha hayo yasiwe ya kuhangaika hata kujichosha
bure.
Tuelewe mapema kuwa ushirika wa kidugu sio tu njia
ya kufanya vizuri kazi yetu, bali ni mahali pa kung'amua uwepo wa Yesu hai kati
yetu, tena pa kuushuhudia Utatu, yaani Baba anayetaka kuwafanya watu wote kuwa
familia moja, Mwana aliyekusanya waliotawanyika, na Roho anayewaunganisha katika
upendo.
Umoja hautegemei raha ya kulingana kwa mawazo, kwa
tabia na kwa machaguo, bali wito wa Bwana aliyetuweka wakfu namna moja ili
tuishi pamoja na kufanya utume mmoja.
Hasa mfano wa jumuia za kimataifa unaweza ukasaidia
makabila mbalimbali kushirikiana, kutajirishana na kurekebishana.
Lakini umoja kati ya watu tofauti si rahisi: unadai
nia imara upande wa wote, na utambuzi upande wa viongozi na walezi.
Juhudi za kuwatii kwa imani, za kupokeana wenyewe
kwa wenyewe na za kutatua matatizo katika jumuia mchanganyiko zinadhihirisha
kwamba tuko pamoja kwa jina la Bwana.