HATUA TATU ZA MAISHA YA KIROHO |
YALIYOMO
0.
UTANGULIZI
1.
CHEMCHEMI NA LENGO LA MAISHA YA KIROHO
1.1. Uzima wa neema, mwanzo wa uzima wa milele
1.2. Maisha ya Kiroho na maongezi ya ndani na Mungu
1.3. Muundo wa Kiroho
1.3.1.
Maisha ya kimaumbile na yanayopita maumbile
1.3.2.
Maadili ya Kimungu
1.3.3.
Maadili ya kibinadamu
1.3.4.
Vipaji saba vya Roho Mtakatifu
1.3.5.
Neema za msaada na aina zake
1.4. Uwemo wa Utatu mtakatifu ndani mwetu kama chemchemi isiyoumbwa ya
maisha ya Kiroho
1.5. Kristo mkombozi anavyoathiri mwili wake wa fumbo
1.6. Msaada wa mama Maria
1.7. Ustawi wa uzima wa neema kwa njia ya stahili, sala na sakramenti
1.8. Ukamilifu wa Kikristo ni nini hasa?
1.9. Ukuu wa ukamilifu wa Kikristo na heri nane
1.10. Ukamilifu na ushujaa
1.11. Ukamilifu wa Kikristo na matakaso ya Kimungu
1.12. Ukamilifu na amri ya kumpenda Mungu
1.13. Ukamilifu na mashauri ya Kiinjili
1.14. Wajibu wa pekee wa mapadri na watawa wa kulenga ukamilifu
1.15. Hatua tatu za maisha ya Kiroho kadiri ya mababu na walimu wakuu
1.16. Somo la Kimungu
1.17. Uongozi wa Kiroho
2.
UTAKASO WA WANAOANZA
2.1. Hatua ya Kiroho ya wanaoanza
2.2. Fikra za kidunia na ufishaji kadiri ya Injili
2.3. Ufishaji kadiri ya mtume Paulo na sababu zinazofanya uwe wa lazima
2.4. Dhambi ambazo tuziepe: mizizi yake na matokeo yake
2.5. Kilema tawala, mdudu anayekula ndani kwa ndani
2.6. Maono ya kuratibiwa
2.7. Kujitakasa upande wa hisi
2.8. Kujitakasa upande wa ubunifu na kumbukumbu
2.9. Kujitakasa upande wa akili
2.10. Kujitakasa upande wa utashi
2.11. Kupona kiburi
2.12. Kupona uvivu wa roho
2.13. Sakramenti ya kitubio
2.14. Kushiriki misa, chemchemi ya utakatifu
2.15. Komunyo takatifu
2.16. Sala ya kuomba
2.17. Sala ya Kanisa
2.18. Sala ya moyo ya wanaoanza inavyozidi kuwa sahili
2.19. Kufikia maisha ya sala na kudumu ndani yake
2.20. Wachelewaji
3.
MWANGA WA WANAOENDELEA
3.1. Lugha ya walimu wa Kiroho ikilinganishwa na ile ya wanateolojia
3.2. Kuingia hatua ya mwanga
3.3. Wongofu wa pili kadiri ya walimu wengine
3.4. Kutakaswa upande wa hisi na kuingia hatua ya mwanga
3.5. Tufanye nini katika usiku wa hisi
3.6. Sifa kuu za hatua ya wanaoendelea
3.7. Jengo la Kiroho la wanaoendelea
3.8. Busara na maisha ya Kiroho
3.9. Haki, aina zake na kuunda utashi
3.10. Subira na upole
3.11. Usafi wa moyo, thamani na matunda yake
3.12. Unyenyekevu wa wanaoendelea
3.13. Unyenyekevu wa Neno aliyefanyika mwili na ule wa kwetu
unavyotakiwa kuwa
3.14. Roho ya ufukara
3.15. Ukuu wa utiifu
3.16. Usahili na unyofu
3.17. Roho ya imani na ustawi wake
3.18. Tumaini kwa Mungu na hakika yake
3.19. Upendo wa kulingana na matakwa ya Mungu
3.20. Upendo wa kidugu, mng'ao wa upendo wa Mungu
3.21. Ari kwa utukufu wa Mungu na kwa wokovu wa watu
3.22. Usikivu kwa Roho Mtakatifu
3.23. Upambanuzi wa roho
3.24. Sadaka ya misa na wanaoendelea
3.25. Komunyo ya wanaoendelea
3.26. Ibada ya wanaoendelea kwa bikira Maria
3.27. Kitabu cha "Kumfuasa Yesu Kristo" kinawaelekeza wote
njia ya mafumbo
3.28. Sala ya kumiminiwa
3.29. Uzushi wa Watulivu kuhusu sala ya kumiminiwa na kuhusu upendo safi
3.30. Ngazi za sala ya kumiminiwa kwa wanaoendelea
3.31. Maswala kuhusu sala ya kumiminiwa
3.32. Yaliyo mapya katika sala ya kumiminiwa
3.33. Ulinganifu na tofauti kati ya watakatifu Teresa wa Yesu na Yohane
wa Msalaba
4.
MUUNGANO WA WALIOKAMILIKA
4.1. Kuingia hatua ya muungano kupitia usiku wa roho
4.1.1.
Haja ya kutakaswa roho na utangulizi wa hatua ya muungano
4.1.2.
Ufafanuzi wa utakaso wa Kimungu wa roho
4.1.3.
Kinachosababisha roho kutakaswa
4.1.4.
Giza la mwanga mkali
4.1.5.
Miongozo kwa usiku wa roho
4.1.6.
Matokeo ya roho kutakaswa hasa upande wa maadili ya Kimungu
4.1.7.
Hatua ya waliokamilika: muungano wao na Mungu
4.1.8.
Aina mojawapo ya maisha makamilifu: njia ya utoto wa Kiroho
4.2. Ushujaa wa maadili
4.2.1.
Ushujaa wa maadili kwa jumla
4.2.2.
Imani ya kishujaa inayozama katika mafumbo
4.2.3.
Tumaini la kishujaa na kujiachilia kwa Mungu
4.2.4.
Upendo wa kishujaa
4.2.5.
Ushujaa wa maadili ya kibinadamu
4.2.6.
Upendo kwa Yesu msulubiwa na kwa Maria katika hatua ya muungano
4.3. Namna na ngazi za hatua ya muungano
4.3.1.
Maisha kamili ya kitume na sala ya kumiminiwa
4.3.2.
Maisha ya malipizi
4.3.3.
Roho Mtakatifu anavyomuathiri aliyekamilika
4.3.4.
Muungano mkavu na muungano wa kutoka nje ya nafsi
4.3.5.
Muungano unaotugeuza, utangulizi wa ule wa mbinguni
5.
NEEMA ZA PEKEE
5.1. Karama
5.2. Mafunuo na njozi
5.3. Maneno na miguso ya Kimungu
5.4. Madonda matakatifu na kudanganyika
5.5. Tofauti kati ya matukio hayo ya Kimungu na yale yatokanayo na
ugonjwa
5.6. Matukio ya Kishetani
6.
HATIMA
Mtu
akiacha kuongea na wenzake, mara anaanza kuwaza yanayomvutia zaidi. Mawazo
hayo yanatofautiana hasa kadiri ya umri na uadilifu wa watu. Kwa mtu
anayelenga ukweli na wema yanaelekea kugeuka maongezi
na Mungu, naye mwenyewe, badala ya kujipendea katika yote (yaani kujifanya
lengo la yote, ajue asijue) anamlenga Mungu katika kila jambo pamoja na
kumpenda na kuwapenda watu kwa ajili yake. Ndiyo maisha ya Kiroho.
Ni
jambo bora na la lazima kuliko elimu, sanaa, fasihi, siasa na mengineyo: wale
wasio na maisha ya Kiroho wakijihusisha na mambo hayo wanaonekana kutafuta
humo ukweli na wema, lakini utafiti wao unaathiriwa na umimi kiasi kwamba
tunapaswa kujiuliza kama utazaa matunda kwa uzima wa milele. Wengi wao
hawainuki juu ya utendaji wa kibinadamu tu na wa njenje, wala hawaishi kwa
jambo lililo bora kuliko wao, yaani kwa Mungu.
Maisha
ya Kiroho, yaani kuishi na Mungu, ndiyo kitu
pekee cha lazima kwa sababu kwa njia yake tu tunaelekea lengo letu kuu.
Tusiutenganishe wokovu na safari ya
utakatifu iliyo njia ya wokovu. Mbinguni
kutakuwa na watakatifu tu, wawe wameingia mara baada ya kufa, au wawe
wamehitaji kutakaswa toharani. Hakuna anayeingia mbinguni akiwa na doa lolote.
Ili aweze kufurahia daima uso wa Mungu, yaani kumjua na kumpenda kama mwenyewe
anavyojijua na kujipenda, ni lazima hatia yoyote hata ndogo iwe imefutwa, na
adhabu iliyostahili iwe imetimizwa au kuondolewa.
“Atafaidiwa
nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu
atatoa nini badala ya nafsi yake?” (Math. 16:26). Ikiwa tuko tayari kupoteza
vitu vingi ili kuokoa mwili, ambao kwa vyovyote utakuja kufa, kwa nini tusiwe
tayari kupoteza vyote ili kuokoa roho inayotakiwa kuishi milele? Je, binadamu
hapaswi kupenda roho kuliko mwili wake?
Hayo
tuliyoyasema ni ya kweli nyakati zote, lakini siku hizi yanahitaji kufikiriwa
zaidi, kwa sababu hakuna utulivu: wengi wamejitenga na Mungu, wakijitahidi
kupanga mbali naye maisha ya binafsi na ya jamii. Matatizo makuu yaliyowapata
daima binadamu yamepata sura mpya ya kutisha. Kwa kuwa Mungu ni mwanzo na
mwisho wa yote, mtu akitaka kutenda bila yake anajikuta vilindini mwa unyonge
mbaya kuliko utovu wa vyote. Hatimaye analazimika kutambua kuwa yote yanadai
azingatie sana swala la dini.
Mtu
asipotaka kutimiza wajibu wake kwa Mungu, aliye muumba na lengo lake kuu,
anajikuta akiabudu vingine, k.mf. sayansi au haki ya kijamii au kipeo chochote
cha kibinadamu, kwa kuwa hawezi kuishi bila ya dini. Hivyo anasogea mbali na
aliye Mkuu kabisa na kukabiliana na rundo la maswala ambayo, atake asitake,
hayana jibu lolote asiporudia swala la msingi la fungamano na Mungu.
Siku
hizi bingwa anaabudu taratibu za sayansi na kuzijali kuliko ukweli wenyewe.
Angefanya bidii hizohizo katika maisha ya Kiroho, angefikia mapema utakatifu.
Kumbe hiyo ibada ya sayansi lengo lake ni utukufu wa mtu badala ya upendo wa
Mungu. Vilevile siasa mara nyingi inajidanganya kuboresha maisha ya binadamu
kwa kukataa haki za Mungu.
Msingi
wa maswala yoyote ni swala la dini: hatuwezi kulipuuzia wala kuepa kusimama
ama upande wa Mungu ama dhidi yake. Historia ya karne ya 20 imetuonyesha hilo
waziwazi.
Mtu
akitaka kuishi bila ya Mungu, uzito wa
maisha unasogezwa kutoka upande wa dini kwenda upande mwingine. Lakini
baada ya muda analazimika kutambua kuwa yote yamevurugika.
Mali haiwezi kuwa yote ya wengi kwa wakati mmoja:
ndiyo sababu ya mashindano kati ya watu na kati ya mataifa, lengo kuu
likiwekwa katika mali. Kumbe mema ya
Kiroho yanaweza kuwa yote ya wote kwa wakati mmoja: tunaweza kuwa na
ukweli uleule, uadilifu uleule na Mungu yuleyule bila ya kunyang'anyana.
Bwana
ametuambia: “Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake, na hayo yote
mtazidishiwa” (Math. 6:33). Kukataa fundisho hilo ni kujitakia maangamizi:
"Bwana asipoijenga nyumba waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda
mji yeye aulindaye akesha bure" (Zab. 127:1).
Mtu
akijali sayansi au siasa kuliko dini, na akijitafutia utukufu badala ya
kumtafutia Mungu, maisha yatamfundisha mapema kuwa ameshika njia isiyofika
mahali. "Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu, na mtu asiyekusanya
pamoja nami hutapanya" (Math. 12:30).
Lakini
dini haiwezi kuwa jibu halisi la
maswala makuu ya leo isiposhikwa kwa dhati. Maisha ya Kiroho yanatakiwa kuwa
kweli muungano na Mungu ili dini idumu kuwa juu ya sayansi na siasa.
Lengo
ni kuwaalika watu kwenye muungano na Mungu, wakiepa hatari mbili.
Ya
kwanza ni kwamba leo kutofautisha fani kumezidi hata kufanya wengi wakose
mitazamo mipana inayohitajika ili kupima kwa busara mambo yoyote katika
uhusiano na mengine. Basi, katika maisha ya Kiroho pia kuzingatia madogomadogo
kusitusahaulishe jumla ya yote, la sivyo tutasogea mbali na hekima ya Kikristo.
Ya
pili ni kwamba vitabu vingi vya dini na vya ibada vinakosa msingi imara katika
imani na kurahisisha mno mafundisho ya Kiroho.
Maisha
ya Kiroho ni tawi la teolojia
linalohusika na utekelezaji wake katika kuongoza watu waungane kwa dhati na
Mungu likifafanua muungano huo ni nini na njia za kuufikia ni zipi. Hivyo
linafafanua taratibu za uzima wa neema kwa misingi ya teolojia likiilinganisha
na mang'amuzi ya watakatifu.
Maisha
ya Kiroho yanahitaji kuchambua mang'amuzi hayo kitaalamu, kwa kubainisha
taratibu zake kadiri ya saikolojia (k.mf. ukavu unaotakasa unavyohusiana na
muungano na Mungu). Somo hilo linakuwa la kiteolojia uchambuzi wa taratibu
hizo unapotegemea pia mafundisho ya imani. Ikiwa elimunafsia
ni ya lazima kwa maadilidini, ni ya
lazima zaidi kwa maisha ya Kiroho ambayo yanachunguza hatua zake ndani ya
mtu hadi muungano kamili.
Katika
ngazi ya chini, maadilidini yanatakiwa kuzungumzia sio tu madhambi ambayo
tuyaepe, bali pia maadili ambayo tuwe nayo na usikivu katika kumfuata Roho
Mtakatifu. Maisha ya Kiroho hayaenei kama maadilidini, lakini ni tawi la juu
yake kwa jinsi linavyolenga kufikisha hadi muungano
wa dhati na Mungu. Kwa njia yake teolojia inarudi ilipoanzia na kudumisha
umoja wake. Kwa hiyo linatakiwa kufuata mwanga
wa ufunuo wa Kimungu uliomo katika Maandiko na Mapokeo, ambao peke yake
unaweza kutujulisha uzima wa Kimungu na muungano wa roho na Mungu ambao
unapita maumbile.
Maisha
ya Kiroho yanatumia mawazo ya maadilidini, lakini kuhusiana zaidi na ustawi wa
uzima wa Kimungu rohoni. Utekelezaji wake, ambao ndio lengo la maisha ya
Kiroho kupitia uongozi wa mtu mmojammoja, una pande mbili: juhudi na mafumbo.
Upande wa juhudi maisha ya Kiroho yanazungumzia hasa namna ya kufisha vilema na kutekeleza maadili. Upande wa mafumbo yanazungumzia hasa usikivu kwa Roho Mtakatifu, neema ya kuzama katika mafumbo ya imani, na muungano unaotokana na neema hiyo, halafu karama ambazo pengine zinaongozana nayo.
Hapa
tutaeleza yaliyo ya lazima tu, kwa kukwepa aina mbili za upotovu ambazo ni
rahisi zitupate: moja kwa kuzingatia mafundisho ya imani na kupuuzia
mang'amuzi, nyingine kwa kuzingatia mang'amuzi na kupuuzia mafundisho ya
imani.
Tunapaswa
kuzungumzia maisha ya Kiroho kwa mwanga wa teolojia kuhusu neema ya utakaso,
maadili ya kujaliwa na vipaji saba; pasipo hayo tungekusanya tu dalili za hali
za Kiroho za juu, badala ya kuelewa kanuni za msingi za ustawi wa uzima wa Kimungu ambao hauwezi kung'amuliwa kwa kuwa si wa
kimaumbile. Pia tungetia maanani mno uhaba wa watu wanaofikia muungano wa
ndani na Mungu: hapo tungedhani kuwa walio wengi hawaitwi hata kwa mbali na
kwa jumla kufikia hatua hiyo; tungesahau maneno ya Bwana yanayokumbushwa na
walimu wa Kiroho kuhusu swala hilo: “Waitwao ni wengi, bali wateule ni
wachache” (Math. 22:14).
Upande
wa pili tunapaswa kuzingatia maelezo ya watakatifu kuhusu hatua mbalimbali za
maisha ya Kiroho, tukiyaangaza kwa imani ili kutambua katika mang'amuzi yao
yapi ni ya pekee na yapi ni ya juu, lakini yanakusudiwa kuwa ya kawaida. Upande huo hatari
nyingine ni kudhani kuwa neema ya kuzama katika sala ni ya wengi,
tukiichanganya na sala nyofu ya mapenzi ambao ni utangulizi wake tu. Kufuatana
na aina hizo mbili za upotovu, kuna makosa mawili ya kuepwa katika kuongoza
watu: kuwaachisha njia ya juhudi mapema mno au baadaye mno.
Basi,
tunapaswa kuchimba ukamilifu wa Kikristo ili kuona wazi lengo ambalo Mwokozi
amewawekea watu tusilipunguze. Halafu kuchambua mang'amuzi ili tutofautishe
yaliyo ya lazima na yaliyo ya ziada. Hatimaye kujumlisha hayo mawili ili kuona
yaliyo ya lazima au ya kufaa na ya
kutamaniwa kusudi tuufikie ukamilifu, na yale ambayo ni ya
pekee tu na hayahitajiki kufikia utakatifu mkuu.
Kutokana
na shida hizo mbalimbali, kusoma maisha ya Kiroho kunadai ujuzi wa teolojia (hasa
juu ya neema, maadili ya kumiminiwa, na vipaji vya Roho Mtakatifu kuhusiana na
mafumbo makuu ya Utatu, umwilisho, ukombozi na ekaristi) pamoja na ujuzi wa
walimu wa Kiroho, hasa wale ambao Kanisa limewataja kuwa viongozi katika
maswala hayo.
Kadiri
ya mapokeo (watakatifu Thoma wa Akwino, Yohane wa Msalaba na Fransisko wa
Sales) upande wa juhudi maisha ya
Kiroho yanazungumzia hatua ya utakaso
wa wanaoanza ambao, wakijua kwamba hawatakiwi kubaki nyuma na kupooza,
wanajitahidi kutekeleza maadili, lakini kwa
namna ya kibinadamu, yaani kwa nguvu zao zikisaidiwa na neema za kawaida.
Kumbe upande wa mafumbo unaanza mara
inapozungumziwa hatua ya mwanga ambapo
wanaoendelea, wakiangazwa na Roho Mtakatifu, wanatenda tayari, mara nyingi na
waziwazi kwa vipaji vyake saba; kwa
uongozi maalumu wa huyo mlezi wa ndani wanatenda kwa namna ipitayo maumbile ambayo kabla ya hapo ilikuwa imefichika au
kujitokeza mara mojamoja tu.
Walimu
hao wameonyesha kuwa mambo yanayopatikana upande wa mafumbo ni ya juu katika njia ya kawaida ya utakatifu, ila si ya pekee hasa (kama
njozi). Ndivyo ilivyo pia kwa wale wanaoitwa kufikia utakatifu katika utendaji
mwingi (kama mt. Visenti wa Paulo).
Basi,
kujua upande wa mafumbo hakufai tu kwa uongozi wa watu wachache wanaoitwa
kufuata njia za pekee, bali kwa uongozi wa watu wote wanaolenga ukamilifu na
muungano na Mungu katika maisha ya kila siku. Ujinga wa kiongozi wa Kiroho
kuhusu mambo hayo unaweza ukazuia wale anaowaongoza: kwa kuwa hapaswi kudhani
kila huzuni ya mtu aliyechoka kiakili ni takaso la Kimungu, lakini pia hapaswi
kudhani kuwa hilo likipatikana ni huzuni ya kinafsi tu.
Kutokana
na yote tuliyoyasema, ni wazi kwamba upande
wa juhudi unalenga upande wa mafumbo. Vilevile upande wa mafumbo
usipotanguliwa na juhudi za kufaa ni uongo mtupu.
Hatimaye
ni muhimu kuzingatia kuwa tukitazama njia ya utakatifu kuanzia maumbile
yetu, mafundisho yetu yataonekana yamepita kiasi. Lakini tukitazama njia
hiyo kuanzia mafumbo yapitayo maumbile
(uwemo wa Utatu mtakatifu ndani mwetu, umwilisho ulioleta ukombozi na ekaristi)
hapo tutaiona kwa hekima, yaani kutoka juu, badala ya kupima yote kutoka chini
unavyofanya upumbavu.
Ikiwa
kweli Utatu mtakatifu unaishi ndani mwetu, ikiwa kweli Neno alifanyika mwili
akafa kwa ajili yetu, yumo katika sakramenti kuu na kila siku anajitoa kwa
ajili yetu, basi hapo watakatifu tu,
wanaoishi kwa kujua na kama kung'amua mara nyingi uwemo huo wa Mungu, na kwa
kuupenda zaidi na zaidi katika magiza na matatizo ya maishani, ndio waliopo panapotakiwa. Hapo maisha
ya muungano wa ndani na Mungu yanaonekana kuwa peke yake ya
kawaida kweli. Kabla ya kufikia maisha hayo, tuko bado kama watu
waliosinzia, wasioishi vya kutosha kwa hazina ile kuu tuliyokabidhiwa na Mungu.
Utakatifu
ni muungano wa ndani na Mungu, yaani ukamilifu wa upendo kwake na kwa jirani,
ukamilifu ambao hata hivyo upo katika njia ya kawaida, kwa sababu amri ya
upendo inayowapasa wote haina mipaka. Utakatifu huo hauhitaji elimu ya juu,
wala utendaji mwingi wa nje, bali kuishi kwa ndani na Mungu.
Utakatifu
huo ni utangulizi wa kawaida wa uzima wa
milele; utangulizi huo unafanyika duniani au toharani, mpaka roho iwe imetakata kabisa iweze kukaribishwa kwenye heri ya kumuona Mungu.
Hatimaye,
tukisema kuzama katika mafumbo ya imani ni karibu jambo la lazima kwa kufikia
utakatifu, maana yake ni kwamba kwa kawaida pasipo hilo haiwezekani kufikia
utakatifu ambao unadai kutekeleza kwa namna bora maadili ya Kimungu na vipaji
vya Roho Mtakatifu vinavyoongozana nayo. Ndiyo tutakayoonyesha katika kozi hii.
1. CHEMCHEMI NA LENGO LA MAISHA YA KIROHO
Kwa
kuwa maisha ya Kiroho ni namna ambayo mtu mwenye bidii anaishi kwa neema
akizidi kujitambua, tutaongelea kwanza uzima
wa neema ili kuuthamini kikamilifu. Halafu tutazingatia muundo wa Kiroho
wa maadili ya kumiminiwa pamoja na vipaji vya Roho Mtakatifu, ambavyo vyote
vinatokana na neema ya utakaso katika kila mwadilifu. Hayo yote yatatuongoza
kuzungumzia uwemo wa Utatu rohoni
mwake, na athari ya kudumu ya
Bwana wetu Yesu Kristo, aliye mshenga pekee, na ya Maria
pamoja naye kwa roho hiyo.
Ndizo chemchemi za maisha ya Kiroho tunazoikuta juu sana, kuliko chemchemi za mito zinazotoka kwenye vilele vya milima mirefu. Kwa kuwa zinatoka juu, maisha ya Kiroho yanaweza kumrudia Mungu aliye juu na kuungana naye kwa ndani.
Katika
sehemu hii ya kwanza, kisha kuongelea chemchemi za maisha ya Kiroho,
tutazungumzia lengo lake, yaani ukamilifu
wa Kikristo na wajibu wa kuulenga, kila mmoja kadiri ya hali yake maishani.
Lengo ndilo la kwanza katika kupanga nia, ingawa ni la mwisho katika
utekelezaji. Ndilo tulilo na hamu nalo toka mwanzo, ingawa tunaweza kulipata
mwishoni tu. Ndiyo sababu Bwana alianza kuhubiri kwa kutuambia juu ya heri.
Maisha
ya Kiroho yanadai Mkristo awe na hali ya
neema ya utakaso, ambayo ni kinyume cha hali ya dhambi ya mauti. Kila mtu
yupo katika mojawapo kati ya hali hizo mbili, yaani ama anamuelekea Mungu kama
lengo kuu, ama amepotoka mbali naye. Hakuna anayeweza kuwa na hali ya
kimaumbile tu, kwa kuwa wote wanaitiwa lengo linalopita maumbile, yaani
kumuona Mungu uso kwa uso na hivyo kumpenda kabisa.
Ili
mtu awe na maisha ya Kiroho haitoshi awe na neema ya utakaso, kama vile mtoto
kisha kubatizwa au mtu aliyeondolewa dhambi katika kitubio. Zaidi ya hiyo,
maisha ya Kiroho yanadai vita dhidi ya yale yote yanayoweza kutuangusha
dhambini, na juhudi halisi katika kumlenga Mungu.
Tungeng'amua
kwa ndani hali ya neema, tungeona kwamba siyo tu mwanzo wa maisha matakatifu
bali pia ni mbegu ya uzima wa milele. Ni lazima tusisitize mapema jambo hilo,
tukikumbuka neno la mt. Thoma wa Akwino: “neema ya utakaso ya mmoja ni bora
kuliko mema ya kimaumbile ya ulimwengu wote”; kwa sababu neema hiyo ni mbegu
ya uzima wa milele, ambao una ubora usio na kifani kuliko uzima wa kimaumbile
wa kwetu na wa malaika.
Ndilo
linaloweza kutuonyesha vizuri kuliko yote thamani ya neema
ya utakaso, ambayo tunaipata katika ubatizo na kurudishiwa na kitubio ikiwa
tumeipoteza. Mwanzoni mwa kozi hii ni muhimu kuthamini kweli neema hiyo ambayo
Uprotestanti umeisahau, ukifuata wanafalsafa wengi wa karne ya XIV. Hatuwezi
kujua thamani ya mbegu tusipojua kinachoweza kutokana nayo. Upande wa binadamu,
tukitaka kuthamini roho ambayo imesinzia bado katika mtoto, ni lazima tujue
nguvu ya roho ya mtu aliyekomaa. Vilevile hatuwezi kuthamini neema ya utakaso
waliyonayo waadilifu, tusipozingatia ustawi wake kamili katika uzima wa milele.
Inafaa tuuzingatie kwa mwanga wa maneno ya Bwana, ambayo ni “roho, tena ni
uzima” (Yoh. 6:63) na yana ladha bora kuliko maelezo yoyote ya teolojia.
Lugha ya Injili na mtindo wa Bwana vinatuzamisha katika sala kuliko lugha ya
kitaalamu hata ikiwa na hakika ya juu. Hakuna kinacholeta wokovu kuliko
kupumua hewa safi ya vilele vile vinavyobubujika maji hai ya mafundisho ya
Kikristo.
Neno
“uzima wa milele” ni adimu katika Agano la Kale, ambamo yote yanaelekea
ujio wa Mwokozi aliyeahidiwa. Kumbe katika mahubiri ya Yesu yote yanaelekea
moja kwa moja uzima wa milele.
Tukizingatia kwa makini maneno yake tutaona jinsi uzima huo ulivyo tofauti na maisha yajayo yaliyozungumziwa na wanafalsafa bora (k.mf. Plato)
kama hali ya kimaumbile tu na isiyo ya hakika. Kumbe Mwokozi anaongea kwa
hakika juu ya uzima wa milele, bora, usio na jana, leo na kesho, unaopita
maumbile na usiopimika, kama ule wa ndani ya Mungu, kwa kuwa unashiriki
umilele wake usiobadilika.
Yesu
alifundisha kuwa “njia imesonga iendayo uzimani” (Math. 7:14) na kuwa
tukitaka kuupata ni lazima tuache dhambi na kushika “amri” za Mungu (taz.
Math. 19:17). Mara kadhaa alisema kuwa anayemwamini “yuna uzima wa milele”
(Yoh. 5:24; 6:40,47) maana yake anayemuamini kuwa ni Mwana wa Mungu kwa imani
hai, inayoambatana na upendo na utekelezaji wa amri, ameanza kuwa na uzima wa
milele. Ndivyo alivyotamka tangu mwanzo wa mahubiri yake: “Heri walio
maskini wa roho, maana ufalme wa
mbinguni ni wao... Heri wenye njaa na kiu ya haki, maana hao watashibishwa...Heri
wenye moyo safi, maana hao watamwona
Mungu” (Math. 5:3-8). Basi, uzima wa milele ni kushiba huko na kumwona
Mungu katika ufalme wake. Kwa namna ya pekee, wanaoteswa kwa sababu ya kufanya
atakavyo Mungu wanaambiwa: “Furahini na kushangilia, kwa kuwa thawabu
yenu ni kubwa mbinguni” (Math. 5:12). Yesu akajieleza zaidi tena kabla
ya mateso yake aliposema: “Baba... ulimpa Mwanao mamlaka juu ya wote wenye
mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele. Na uzima wa milele ndio huu: wakujue
wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma” (Yoh 17:1-3).
“Wapenzi,
sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua
ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana
naye, kwa maana tutamwona kama alivyo” (1Yoh. 3:2), yaani si kwa
kuzingatia mng'ao wa sifa zake katika viumbe (vile vinavyoonekana na roho za
watakatifu zinazojitokeza katika maneno na matendo yao), bali moja kwa moja jinsi alivyo. “Wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa
jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso
kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua
sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana” (1Kor. 13:12). Mtume hakusema
kuwa nitamjua ninavyojijua mpaka ndani; kwa sababu najifahamu kuliko wengine,
lakini mimi pia sielewi yote niliyonayo ndani, k.mf. siwezi kupima uzito wote
wa dhambi zangu. Mungu tu ananijua fika: siri za moyo wangu anazielewa
kikamilifu yeye tu. Mbinguni nitamjua anavyonijua, moja kwa moja, pasipo kupitia kiumbe chochote
au wazo lolote la kimaumbile, kwa sababu hakuna wazo la namna hiyo linaloweza
kumchora Mungu na ukweli wake usio na mipaka, nuru angavu ya milele. Kila wazo
la namna hiyo lina mipaka, linazingatia sifa mojawapo ya Mungu (k.mf. ukweli
au wema). Mawazo hayo mbalimbali hayatoshi kutujulisha undani wa Mungu, umoja
wake usiogawanyika kamwe. Mawazo hayo
yanahusiana na uzima wake wa ndani
kama vile rangi saba za upinde wa mvua zinavyohusiana na mwanga mweupe ambao
zinatokana nao. Hapa chini sisi ni kama watu tulioona hizo rangi saba tu na
sasa tunatamani kuona huo mwanga mweupe unaozisababisha. Kabla hatujaona umungu
wenyewe hatuwezi kuona ulinganifu wa ndani wa sifa zake, hasa huruma isiyo na
mipaka na haki isiyo na mipaka. Mawazo yetu ya kimaumbile kuhusu sifa za Mungu
ni vipande tu vya sura nzima, ambavyo vinaleta picha fulani ya Mungu
isiyopendeza vya kutosha. Tukifikiria haki yake, inaonekana ni kali mno, na
tukifikiria upendeleo wa huruma yake unaonekana ukienda kinyume cha haki.
Tukitafakari zaidi tunakiri kuwa ndani
ya Mungu haki na huruma ni kitu kimoja, hazitofautiani kweli. Huo ni
ukweli ambao tunauungama kwa hakika, lakini hatujaona ulinganifu
wa ndani wa sifa hizo, kwa kuwa unahitaji tutazame umungu jinsi ulivyo,
moja kwa moja, pasipo kutumia mawazo yoyote ya kimaumbile.
Mtazamo
huo ndio uzima wa milele. Nani anaweza kueleza ukuu usiopimika wa furaha na
upendo vitakavyokuwemo ndani mwetu kutokana na mtazamo huo? Upendo wa Mungu
wenye nguvu na wa moja kwa moja, hivi kwamba hakutakuwa na lolote litakaloweza
kuupunguza; upendo ambao tutafurahia hasa kuwa Mungu ni Mungu, mtakatifu,
mwenye haki na huruma pasipo mipaka, na ambao tutaabudu mipango yote ya
maongozi yake iliyolenga ufunuo wa wema wake. Tutazama katika heri yake,
alivyosema Mwokozi mwenyewe: “Vema, mtumwa mwema na uaminifu; ulikuwa
mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia
katika furaha ya bwana wako” (Math. 25:21,23). Tutamuona Mungu vile
anavyojiona moja kwa moja, ingawa
hatutaweza kumaliza vilindi vya hali yake, vya upendo wake na vya uweza wake.
Pia tutampenda anavyojipenda. Vilevile tutamuona Bwana wetu Yesu Kristo. Ndiyo
heri ya milele yenyewe, mbali ya furaha ya ziada tutakayokuwa nayo kwa kuwaona
na kuwapenda Bikira Maria pamoja na watakatifu wote, hasa tuliowafahamu
duniani.
Huo
mtazamo wa moja kwa moja wa Mungu unapita uwezo wa kimaumbile wa akili yoyote
ya malaika na ya binadamu, kwa kuwa ungehitaji ulingane
na ule wa Mungu. Basi, akili ya kiumbe inaweza kupata mtazamo huo kwa
neema ya Mungu tu, ambayo ni kama kupandikiza chipukizi la mti bora katika
shina la mti mwitu ili uzae matunda mema. Malaika na binadamu hawawezi kumjua
na kumpenda Mungu kwa namna inayopita maumbile yao kabla hawajapandikiziwa neema
ya utakaso, ambayo ni kushiriki
umungu, yaani uzima wa ndani wa Mungu. Neema hiyo tu, ikipokewa rohoni
mwetu kama zawadi isiyolipika, inatuwezesha kutenda
Kimungu, yaani kumuona moja kwa moja vile anavyojiona, na kumpenda vile
anavyojipenda. Kwa maneno mengine, akili na utashi kushirikishwa umungu
kunategemea kushirikishwa umungu kwa
roho yenyewe iliyonavyo.
Neema
hiyo ikikamilika isiweze kupotezwa inaitwa utukufu,
ambao katika akili za watakatifu wa mbinguni unatia mwanga usio wa kimaumbile unaowawezesha kumwona Mungu, na katika
utashi wao unatia upendo wa kumiminiwa
unaowawezesha kumpenda Mungu hata wasiweze kuachana naye kamwe. Kwa ubatizo
sisi tumeshapokea mbegu ya uzima wa milele, kwa kupokea neema ya utakaso
inayouleta uzima huo: pamoja na neema ya utakaso tumepokea upendo wa
kumiminiwa unaokusudiwa kudumu milele. Ndivyo Mwokozi alivyomuambia mwanamke
Msamaria: “Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, ‘Nipe
maji ninywe’, ungalimwomba yeye, naye
angalikupa maji yaliyo hai… Yeyote atakayekunywa maji yale nitakayompa
mimi hataona kiu milele, bali yale maji
nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa
milele” (Yoh. 4:10,14).
“Atakayekunywa
maji hai ya neema yanayotolewa na Mwokozi hatatamani mengine, ila atatamani
kuyapokea hayohayo kwa wingi zaidi... Zaidi ya hayo, tofauti na maji ya
kawaida ambayo yanaelekea chini, yale ya Kiroho yanapanda juu. Ni maji hai
ambayo hayaachani kamwe na chemchemi yake na ambayo yanabubujikia uzima wa
milele ambao yanatustahilisha” (mt. Thoma wa Akwino). Hayo maji hai yanatoka
kwa Mungu, ndiyo sababu yanaweza kurudi juu kwake.
Siku
ya mwisho ya sikukuu ya Vibanda, Yesu alisimama hekaluni, “akapaza sauti
yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi, kama vile
Maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake” (Yoh.
7:37-38). Anayekunywa Kiroho kwa kumuamini Mwokozi, anaweza kuchota katika
chemchemi ya maji hai, siyo kwa ajili yake tu bali pia kwa ajili ya watu
wengine ili waokoke.
Yesu
alikariri: “Amwaminiye Mwana yuna uzima wa milele” (Yoh. 3:36). Sio tu
atakuwa nao baadaye, bali kwa namna fulani anao tayari, kwa kuwa uzima wa
neema ni mwanzo wa uzima wa milele, kama vile mbegu inavyohusiana na mti wake.
Kwa undani ni uzima uleule wa Kimungu,
ambao hapa chini umo ndani ya Mkristo kama mbegu na ambao huko juu utachanua
kikamilifu katika watakatifu. Ndiyo maana Bwana aliongeza: “Aulaye mwili
wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya
mwisho” (Yoh. 6:54). Ufalme wa Mungu umo ndani mwetu kama mbegu ya haradali,
kama chachu itakayoumua donge lote, kama hazina iliyositirika shambani.
Tunawezaje kujua
kama tumepokea tayari uzima huo unaokusudiwa kudumu milele? “Sisi tunajua ya
kuwa tumepita toka mautini kuingia
uzimani, kwa maana twawapenda ndugu. Yeye asiyependa, akaa katika mauti…
Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna
uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu” (1Yoh. 3:14;
5:13).
Yesu
alisema: “Amin, amin, nawaambia: Mtu akilishika neno langu, hataona mauti milele” (Yoh. 8:51). Kwa kuwa, inavyosema liturujia,
“Ee Bwana, uzima wa waamini wako hauondolewi ila unageuzwa tu”, tena
unastawi kikamilifu mbinguni tu. Hakika uzima wa neema hapa duniani ni mbegu
ya utukufu, hivi kwamba kiwango kidogo cha neema ya utakaso ni bora kuliko
mema ya kimaumbile ya ulimwengu wote na ya malaika pia, kwa sababu kinahusu
hali ya juu, yaani uzima wa ndani wa
Mungu; kwa hiyo ni bora kuliko miujiza yote na ishara nyingine za nje za
ufunuo wa Mungu.
Uzima
uleule unaopita maumbile, ndio unaopatikana duniani katika waadilifu na
mbinguni katika watakatifu. Ni pia upendo uleule wa kumiminiwa, isipokuwa
tofauti mbili. Hapa chini tunamjua Mungu si kwa kumtazama mwangani, bali
katika giza la imani ya kumiminiwa.
Halafu hapa chini, ingawa tunatumaini kuwa naye kikamilifu milele, tunaweza kupotewa
naye kwa kosa letu.
Kuna
tofauti hizo mbili zinazohusu imani na tumaini, hata hivyo ni uzima uleule na
upendo uleule ambavyo vinakusudiwa kudumu milele. Kwa mwanga huo tunapaswa
kuelewa maisha yetu ya Kiroho yanavyotakiwa kuwa na kustawi hapa chini yawe
utangulizi wa kufaa kwa uzima wa milele. Ikiwa neema ya utakaso, maadili ya
kumiminiwa na vipaji vya Roho Mtakatifu kwa mfumo wake vinaulenga uzima wa
milele, je havikusudiwi kulenga pia muungano wa hali ya juu na Mungu?
Kwa
kweli neema ya utakaso na upendo, vinavyotuunganisha na Mungu katika maisha
yake ya ndani, ni bora, tena sana, kuliko neema za pekee (kama vile kutabiri
na kusema kwa lugha ngeni) ambazo ni ishara tu za kazi za Mungu lakini
hazituunganishi naye (taz. 1Kor. 12:28-13:13). Hali ya kuzama katika mafumbo
ni tunda la imani tuliyomiminiwa, ikiangazwa na vipaji vya akili na vya hekima:
hivyo inatokana na neema ya utakaso, ambayo inaitwa pia “neema ya maadili na
vipaji” na tunaipata wote katika ubatizo; haitokani na neema za pekee.
Kwa
kuwa neema ya utakaso kwa mfumo wake
inalenga uzima wa milele, inalenga pia
hali ile inayohitajika ili kupata mwanga wa utukufu. Hali hiyo ni upendo
kamili pamoja na hamu kubwa ya heri ya
kumuona Mungu; kwa kawaida hamu hiyo inatokana na neema ya kuzama katika
mafumbo. Hivyo basi kuzama huko si neema ya pekee kama ulivyo k.mf. utabiri,
bali ni hali ya juu iliyopo katika njia
ya kawaida ya utakatifu, ingawa ni adimu kama ulivyo adimu ukamilifu mkuu.
Hatimaye,
kwa vile neema ya utakaso kwa mfumo wake inalenga uzima wa milele, inalenga
pia kutuweka tayari kupata mwanga wa utukufu mara baada ya kufa bila ya
kupitia toharani, ambako ni adhabu,
maana yake kunatokana na kosa lisilotakiwa pamoja na malipizi yasiyotosha; ingekuwa
kawaida kutakaswa katika maisha haya kwa kujilimbikizia stahili na kukua
katika upendo, badala ya kutakaswa kisha kufa pasipo
stahili yoyote. Hali iliyo tayari kupokea mwanga wa utukufu mara
baada ya kifo inahitaji kwanza utakaso halisi unaolingana na ule wa roho
zinazotoka toharani zenye hamu kubwa ya kumwona Mungu.
Hamu
hiyo imedhihirishwa na mt. Paulo vizuri ajabu: “Katika nyumba hii twaugua,
tukitamani sana kuvikwa kao letu litokalo mbinguni… twaugua, tukilemewa, si
kwamba twataka kuvuliwa, bali kuvikwa… Basi yeye aliyetufanya kwa ajili ya
neno lilo hilo ni Mungu, aliyetupa arabuni ya Roho” (2Kor. 5:2-5).
Tukitaka
kujadili maswala ya maisha ya Kiroho jinsi inavyotakiwa, hatupaswi kusahau
vilele hivyo tunavyojulishwa na Maandiko na kuelezwa na teolojia ya walimu
wakuu. Hasa katika maisha ya Kiroho tunatakiwa kuzingatia watu sio walivyo tu
bali wanavyokusudiwa kuwa. Tunapaswa kupumua hewa bora ya vilele vya juu,
badala ya kuishia katika hali ya wastani ya binadamu. Heri watu ambao
wanajaribiwa hata wanakuta hewa ya kuwafaa upande wa Mungu tu na kumtamani kwa
hamu kuu.
1.2.
MAISHA YA KIROHO NA MAONGEZI YA NDANI NA MUNGU
Mtu anapoacha shughuli za nje na maongezi na wenzake na kubaki peke yake - hata kama ni katikati ya kelele za jiji - mara anaanza kuwaza kama kwa kuongea na nafsi yake. Akiwa kijana anafikiria ya kesho; akiwa mzee anafikiria ya zamani, na mang'amuzi aliyonayo sasa yanamfanya apime tofauti watu na matukio. Akiwa na umimi anafuata tamaa au kiburi na hivyo ndani yake anapata huzuni tu, ndiyo sababu anajaribu kujitoroka kwa kuzama katika mambo ya nje na anasa asahau utupu wa maisha yake yasiyo na maana. Kwa kufanya hivyo anakuja kujifahamu kwa namna fulani ya hali ya chini, na vilevile kujipenda visivyo. Sanasana anajifahamu upande wa hisi, alizo nazo sawa na wanyama; hivyo ana furaha na uchungu vya kihisi kadiri ya mabadiliko ya hali ya hewa au ya biashara yake. Anavyovitamani na anavyovichukia ni vya aina hiyohiyo, na akipingwa anakasirika kutokana na jinsi anavyojipendea.
Kumbe
anajifahamu kidogo tu upande wa roho, ambayo inalingana na malaika. Hata kama
anaamini ukuu wa roho (yenye akili na utashi) haishi katika ngazi hiyo: hana
mang'amuzi kuhusu sehemu hiyo bora ya utu wake, wala haipendi vya kutosha.
Angeijua angeona ndani yake sura ya Mungu na kuanza kujipenda kwa ajili ya
Mungu, si tena kujipendea kibinafsi. Hata akionyesha mara nyingi uwezo wa
kuelewa na kutenda kwa ujanja, akili yake inaelekea daima yaliyo ya chini
kuliko yeye. Ingawa ameumbwa ili kumtazama Mungu, ukweli mkuu, anafuata
udanganyifu hata kuutetea kwa kila njia. Maisha yasipofuata ubora wa mawazo,
mawazo yatafuata uduni wa maisha: yote yanafungamana, hata misimamo mizuri
aliyokuwa nayo inadhoofika zaidi na zaidi.
Hivyo
maongezi ya ndani yake yanaelekea mauti na hayastahili kuitwa maisha ya Kiroho.
Kujipendea kwake kunamfanya ajione kiini cha yote, na kuelekeza yote (watu na
vitu) kwake; lakini hiyo haiwezekani, ndiyo sababu mara nyingi anakata tamaa
na kuchukizwa, havumiliki kwake wala kwa wengine. Kwa kutaka kujipendea
mwishowe anajichukia pamoja na maisha, kwa kuwa katika maisha alitamani mno
yaliyo ya chini.
Kumbe
binadamu akianza kutafuta uadilifu, hata kama hajawa na neema ya utakaso,
maongezi yake na nafsi yake yanakuwa tofauti: k. mf. anazingatia
yanayohitajika ili aishi kwa haki na kutegemeza familia yake. Pengine mawazo
hayo yanamletea mahangaiko hata kumfanya atambue unyonge wake na haja ya
kumtegemea Mungu badala ya kujiamini tu. Akiwa na dhambi ya mauti isiyo dhidi
ya imani wala tumaini anaweza kuwa na maadili hayo yanayodumu ndani mwetu hata
baada ya kupoteza upendo. Kama ni hivyo pengine mawazo yake yanaangazwa na
imani ambayo mwanga wake unapita maumbile yetu; anaweza akawaza uzima wa
milele na kuutamani, ingawa si zaidi; tena pengine anajisikia msukumo wa
kwenda kanisani.
Hatimaye,
mtu huyo akijuta na kuondolewa makosa yake, anarudishiwa neema ya utakaso na
upendo kwa Mungu na kwa jirani. Kuanzia hapo, mawazo yake yanakuwa mengine.
Anaanza kujipenda kitakatifu, yaani si kwa ajili yake, bali kwa ajili ya Mungu, na kuwapenda watu pia kwa ajili ya Mungu;
anaanza kuelewa anavyopaswa kusamehe na kupenda maadui, na kuwatakia uzima wa
milele vile anavyojitakia. Lakini mara nyingi mawazo yake yanaendelea
kuchafuliwa na umimi, ubinafsi, tamaa na kiburi. Kwake makosa hayo si tena ya
mauti, lakini yakitokea mara nyingi yanamfanya arudie dhambi kubwa na mauti ya
roho. Hapo mtu atajaribu tena kujitoroka, kwa sababu haoni uzima ndani mwake;
ndiyo maana asipojifikiria upya atazidi kujitupa mikononi mwa anasa na kiburi.
Hata
hivyo maongezi ya ndani mwake yanaanza
tena yasiweze kuzuiwa na chochote, wala na yeye mwenyewe. Ndani mwa roho
mna haja inayodai kutimizwa. Mungu tu anaweza kufanya hivyo, kwa hiyo njia
pekee ni kumuendea yeye. Roho inahitaji
kuongea naye kwa sababu lengo lake kuu ni Mungu
aliye hai, hata isiweze kutulia isipokuwa ndani ya Mungu.
Basi,
maisha ya Kiroho ni maongezi ya kila mtu na nafsi yake kuinuliwa na kugeuka
sura mara yanapoanza kuwa maongezi na Mungu. Ni kwamba Roho wa Mungu
anawaonyesha zaidi na zaidi watu wenye mapenzi mema yale ambayo anayataka toka
kwao na yale anayotaka kuwazawadia. Lo, kama tungepokea kwa mikono miwili yale
yote Mungu anayotaka kutupatia!
Maonyesho
hayo hayafanyiki pasipo juhudi; tunapaswa kuokoka katika vifungo vitokanavyo
na dhambi, kufisha hatua kwa hatua “utu wa zamani” na kuunda “utu wa ndani”: “Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa
ndani; lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na
ile sheria ya akili zangu” (Rom. 7:22-23) “Utu wa ndani” ndio kilicho
bora ndani mwetu, yaani akili utashi ambavyo vinapaswa kutawala mwili, ulio
sawa kwa mtu na kwa mnyama.
“Kwa
hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu
wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku” (2Kor. 4:16). Nguvu za
Kiroho zinafanywa upya mfululizo kwa njia ya neema tunazozipokea kila siku.
“Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo
yake; mkivaa utu mpya, unaofanywa upya
upate ufahamu sawasawa na mfano wake
yeye aliyeuumba” (Kol. 3:9-10). Baba “awajalieni, kwa kadiri ya
utajiri wa utukufu wake, kufanywa imara
kwa nguvu, kwa kazi ya Roho wake, katika
utu wa ndani. Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo; ili mpate kufahamu pamoja
na watakatifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo na kina; na kuujua
upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate
kutimilika kwa utimilifu wote wa Mungu” (Ef. 3:16-19).
Ndiyo
maisha ya Kiroho na vilindi vyake, maisha yale yanayolenga mfululizo
kulitazama fumbo la Mungu na kulifanya chakula chake katika muungano naye wa
ndani zaidi na zaidi. Mtume aliandika hayo kwa Wakristo wote, sio kwa
mmojammoja tu. Akaongeza: “Mfanywe
wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya
Mungu katika haki na utakatifu wa kweli… mkaenende
katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi; tena akajitoa kwa
ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato”(Ef.
4:23-24; 5:2).
Kwa
kuzingatia maneno hayo ya Mungu tunaweza kufafanua maisha ya Kiroho kama
ifuatavyo: maisha ya Kiroho ni maisha
ambayo yanapita maumbile na kutuelekeza na kutufikisha kwenye muungano na
Mungu kwa njia ya kujikana na kusali kweli.
“Mafundisho
ya Yesu Kristo yanapita mafundisho yoyote ya watakatifu na mtu aliye na roho
yake anakuta humo mana iliyositirika. Lakini inatokea kuwa wengi, kwa kusikia
Injili mara nyingi, hawaguswi inavyotakiwa, kwa sababu hawana roho yake.
Mnataka kuelewa mpaka ndani na kufurahia maneno ya Yesu Kristo? Mjitahidi
kulinganisha maisha yenu yote na ya kwake” (Kumfuasa Yesu Kristo,
I,1:2).
Maisha
hayo yana hatua ya kwanza inayotawaliwa na utakaso, ya pili inayotarajia
mwanga mkubwa zaidi na zaidi, na lengo lake la mwisho ni kuungana na Mungu.
Ndivyo mapokeo yote yanavyofundisha, yakithibitisha uwepo wa hatua ya
kutakaswa kwa wanaoanza, hatua ya kuangazwa kwa wanaoendelea, na hatua ya
kuungana na Mungu kwa waliokamilika. Hivyo maisha ya ndani ya mtu yanakuwa
zaidi na zaidi maongezi na Mungu.
Kwa
namna hiyo, mtu anaanza kung'amua sehemu bora ya nafsi yake na kumjua Mungu.
Polepole mawazo ya nafsi yake aliyoifanya kuwa lengo la yote, yanaiachia
nafasi kumbukumbu ya kudumu ya Mungu. Vivyo hivyo kujipendea kunaacha nafasi
kwa upendo wa Mungu na wa watu kwa ajili yake. Maongezi ya ndani yanabadilika
hata kusema: “Sisi, wenyeji wetu uko mbinguni” (Fil. 3:20).
Katika
roho yenye neema ya utakaso, maisha ni hasa ya unyenyekevu, kujikana, imani,
tumaini na upendo, pamoja na amani inayotakana na kuweka miguso na matakwa
yote chini ya upendo wa Mungu atakayekuwa heri yetu. Basi, ili tuwe na maisha
ya Kiroho haitoshi tushughulikie sana utume wala kujua sana dini. Tena hayo si
ya lazima. Mtu aliyeanza tu kujikana na kusali kwa juhudi, anayo tayari maisha
ya Kiroho ambayo yanatakiwa kustawi zaidi na zaidi.
Katika
maongezi hayo yanayoelekea kuwa ya kudumu roho inasema kwa njia ya sala,
ambayo ingekuwepo hata kama Mungu angemuumba mtu mmoja au malaika mmoja tu.
Sala inaweza kuwa ya kuomba, ya kuabudu au ya kushukuru; lakini daima ni
kuinua roho kwa Mungu. Naye Mungu anajibu akitukumbusha yale ambayo tuliambiwa
katika Injili na yanatufaa kuitakasa nukta ya sasa hivi: “Huyo Msaidizi,
huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote,
na kuwakumbusha yote niliyowaambia” (Yoh. 14:26)?
Hivyo
mtu anazidi kuwa mtoto wa Mungu, anatambua zaidi na zaidi kuwa Mungu ni Baba
yake na anazidi kujifanya mdogo mbele yake. Anaelewa yale Yesu aliyomuambia
Nikodemu, yaani kuwa ni lazima kurudi katika tumbo la Mungu ili kuzaliwa upya
Kiroho kila siku zaidi, k.mf. wa Neno kuzaliwa milele. Wenye heri wa mbinguni
wanabaki daima katika tumbo hilo.
Watakatifu
wanafuata njia hiyo, hata maongezi kati yao na Mungu hayana mwisho. Mt.
Dominiko hakuweza kusema isipokuwa juu ya Mungu au na Mungu; ndiyo sababu
alikuwa amejaa daima upendo kwa watu. Maongezi hayo na Mungu yanaundwa kwa
njia ya Kristo mshenga: “Ulimi hauwezi kusema, / wala maandishi kufafanua, /
aliyeng'amua tu anaweza kuamini / kumpenda Yesu ni nini” (Utenzi wa Jina
Takatifu la Yesu).
1.3.
MUUNDO WA KIROHO
Ili
tuelewe mbegu ya uzima wa milele iliyomo ndani mwetu ni nini, tunatakiwa
kuzingatia jinsi neema ya utakaso inavyoleta katika akili na utashi maadili ya
kumiminiwa na vipaji saba vya Roho Mtakatifu. Maadili hayo na vipaji hivyo ni
kama utendaji wa muundo uleule mmoja wa Kiroho unaokusudiwa kustawi hadi
tuingie mbinguni.
1.3.1. MAISHA YA KIMAUMBILE NA YANAYOPITA MAUMBILE
Kwanza
tutofautishe vizuri ndani ya roho yetu yale yaliyo ya kwake kwa jinsi
ilivyoumbwa, na yale ambayo ni zawadi tu ya Mungu. Hata malaika, ingawa ni
roho tu, ana maumbile ya chini kuliko neema ya utakaso.
Basi,
sisi binadamu tuna pande mbili tofauti:
upande wa hisi na upande wa akili. Wa
kwanza unalingana na wanyama, ukiwa na hisi za nje (milango ya fahamu),
hisi za ndani (ubunifu na kumbukumbu) na uwezo wa kupatwa na maono mbalimbali
(k.mf. pendo na chuki, hamu na hofu, furaha na huzuni, hasira).
Juu
ya sehemu hiyo, katika maumbile yetu ipo
nyingine inayolingana na malaika, ingawa ndani mwao ina nguvu na uzuri
zaidi. Upande huo roho inapita mwili, maana yake haitegemei mwili moja kwa
moja, kwa hiyo inaweza kudumu baada ya mwili kufa.
Kutokana
na maumbile ya roho upande huo wa juu tuna uwezo wa akili na wa utashi. Akili
inajua sio tu sifa ya viumbe zinazohisikana (rangi, sauti), bali undani wao na
kweli zisizobadilika kama vile: “Hakuna kinachotokea pasipo sababu, na hasa
pasipo sababu kuu, yaani Mungu”. “Tunapaswa kutenda mema na kuepa maovu”.
“Timiza wajibu wako, liwalo na liwe”. Mnyama hataweza kamwe kujua kweli
hizo.
Kwa
kuwa akili inaweza kujua sio tu yale yanayotupendeza au yanayotufaa bali pia
uadilifu (k.mf. kwamba ni “afadhali kufa kuliko kusaliti”), basi utashi unaweza kupenda huo uadilifu, kuutaka na kuutekeleza. Hivyo
unapata kutawala hisi na maono alivyonavyo mnyama pia. Kwa akili na utashi mtu
anafanana na malaika, ingawa katika maisha haya akili yetu, tofauti na malaika,
inazitegemea hisi katika kuanza kujua mambo.
Tunavyoona
katika watu kadhaa, akili na utashi vinaweza vikastawi, pasipo kufikia kujua
na kupenda maisha ya ndani ya Mungu,
ambayo ni ya ngazi tofauti, juu kupita maumbile ya malaika na ya binadamu. Hao
wanaweza kumjua kimaumbile Mungu kwa nje, kutokana na mng'ao wa sifa zake
katika viumbe, lakini haiwezi kuumbwa akili yenye nguvu ya kuyajua yaliyo ya
Mungu tu: “Ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya
binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo
ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu” (1Kor. 2:11).
Kumbe
neema ya utakaso inatuingiza katika hiyo hali ya juu ya ukweli na uzima
inayopita maumbile yoyote. Ni uzima unaopita maumbile, kwa kuwa unashiriki
maisha ya ndani ya Mungu, ni hali ya Kimungu ambayo tangu sasa inatuandaa kumuona milele anavyojiona na kumpenda anavyojipenda.
“Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, wala hayakuingia
katika moyo wa mwanadamu, mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao. Lakini
Mungu ametufunulia sisi kwa Roho”
(1Kor. 2:9-10).
Neema
ya utakaso inayotuwezesha kuanza kuishi maisha ya ndani ya Mungu, katika ngazi
ya juu kuliko maumbile ya malaika, ni kama chipukizi la Kimungu
lililopandikizwa ndani mwa roho ili kuinua uzima wake na kuifanya izae sio tu
matunda ya kimaumbile, bali matunda yanayopita maumbile, yaani matendo
yanayostahili uzima wa milele. Kupandikizwa huko kunapita miujiza
inayojulikana na hisi. Kwa mfano, ufufuo unaurudishia mwili uhai wa kimaumbile,
ndiyo sababu unaweza kujulikana na maumbile yetu; kumbe neema ya utakaso
inaipatia roho uzima usio wa kimaumbile, ndiyo sababu hauwezi kuhakikishwa na
maumbile yetu.
Tangu
sasa uzima huo wa neema unachanua ndani mwetu maadili
ya kumiminiwa na vipaji saba vya Roho Mtakatifu. Kama vile katika maumbile
yetu roho ina uwezo wa akili na kadhalika, katika ngazi inayopita maumbile
neema ya utakaso inaleta rohoni maadili na vipaji hivyo ambavyo, pamoja na
mzizi unaovisababisha, ndio muundo unaopita maumbile ambao tulijaliwa katika
ubatizo (na tunarudishiwa na ondoleo la dhambi ikiwa tuliupoteza).
Muundo huo wa Kiroho unaweza
kuonyeshwa na jedwali ifuatayo:
MAADILI
VIPAJI
Upendo
Hekima
YA
KIMUNGU
Imani
Akili
Tumaini
Elimu
Busara
Shauri
Haki
(Ibada)
Ibada
(Toba)
(Utiifu)
YA
KIBINADAMU Nguvu
Nguvu
(Subira)
Kiasi
Uchaji wa Mungu
(Upole)
(Unyenyekevu)
(Usafi wa moyo)
1.3.2. MAADILI YA KIMUNGU
Maadili
ya Kimungu ni maadili tunayomiminiwa yanayomhusu Mungu mwenyewe aliye lengo
letu kuu. Tofauti na hayo, maadili ya kibinadamu yanahusu njia za kufikia
lengo hilo.
Kati ya maadili ya Kimungu, imani inatuwezesha kusadiki yale yote ambayo Mungu ametufunulia, kwa sababu ndiye ukweli wenyewe. Ni kama hisi ya Kiroho inayotuwezesha kusikia muziki safi wa Kimungu usiojulikana kwa njia nyingine yoyote, maana kuna tofauti kubwa kati ya kusoma Injili kihistoria au kitaalamu na kuiamini kama Neno la Mungu, kwa kuwa kusadiki ni tendo linalopita maumbile yetu na ya malaika, likituingiza katika ulimwengu wa juu. “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu” (Ef. 2:8). Ndiyo msingi wa kufanywa waadilifu, kwa kuwa inatujulisha lengo lipitalo maumbile tunalopaswa kulikusudia. “Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa haki” (Mwa. 15:6; Rom. 4:3,9). “Walakini haikuandikwa kwa ajili yake tu kwamba ilihesabiwa kwake; bali na kwa ajili yetu sisi tutakaohesabiwa vivyo hivyo, sisi tunaomwamini yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu katika wafu” (Rom. 4:23-24). Sisi tutaokoka tu kwa imani hiyo ambayo ni zawadi ya Mungu. Kanisa lilitamka rasmi dhidi ya Wapelajiupande kwamba hata mwanzo wa imani ni neema. Imani hiyo inapita kabisa maumbile, siyo