HATUA TATU ZA MAISHA YA KIROHO

Historia Katiba Karama Maktaba Pepe Maisha na utendaji Safari ya Malezi

 

 

 

 

 

R. GARRIGOU-LAGRANGE, O.P.

 

 

HATUA TATU ZA MAISHA YA KIROHO

 

UTANGULIZI WA UZIMA WA MBINGUNI

 

(tafsiri fupi)

 

 

 

 

YALIYOMO

 

0. UTANGULIZI

 

1. CHEMCHEMI NA LENGO LA MAISHA YA KIROHO

1.1. Uzima wa neema, mwanzo wa uzima wa milele

1.2. Maisha ya Kiroho na maongezi ya ndani na Mungu

1.3. Muundo wa Kiroho

1.3.1. Maisha ya kimaumbile na yanayopita maumbile

1.3.2. Maadili ya Kimungu

1.3.3. Maadili ya kibinadamu

1.3.4. Vipaji saba vya Roho Mtakatifu

1.3.5. Neema za msaada na aina zake

1.4. Uwemo wa Utatu mtakatifu ndani mwetu kama chemchemi isiyoumbwa ya maisha ya Kiroho

1.5. Kristo mkombozi anavyoathiri mwili wake wa fumbo

1.6. Msaada wa mama Maria

1.7. Ustawi wa uzima wa neema kwa njia ya stahili, sala na sakramenti

1.8. Ukamilifu wa Kikristo ni nini hasa?

1.9. Ukuu wa ukamilifu wa Kikristo na heri nane

1.10. Ukamilifu na ushujaa

1.11. Ukamilifu wa Kikristo na matakaso ya Kimungu

1.12. Ukamilifu na amri ya kumpenda Mungu

1.13. Ukamilifu na mashauri ya Kiinjili

1.14. Wajibu wa pekee wa mapadri na watawa wa kulenga ukamilifu

1.15. Hatua tatu za maisha ya Kiroho kadiri ya mababu na walimu wakuu

1.16. Somo la Kimungu

1.17. Uongozi wa Kiroho

 

2. UTAKASO WA WANAOANZA

2.1. Hatua ya Kiroho ya wanaoanza

2.2. Fikra za kidunia na ufishaji kadiri ya Injili

2.3. Ufishaji kadiri ya mtume Paulo na sababu zinazofanya uwe wa lazima

2.4. Dhambi ambazo tuziepe: mizizi yake na matokeo yake

2.5. Kilema tawala, mdudu anayekula ndani kwa ndani

2.6. Maono ya kuratibiwa

2.7. Kujitakasa upande wa hisi

2.8. Kujitakasa upande wa ubunifu na kumbukumbu

2.9. Kujitakasa upande wa akili

2.10. Kujitakasa upande wa utashi

2.11. Kupona kiburi

2.12. Kupona uvivu wa roho

2.13. Sakramenti ya kitubio

2.14. Kushiriki misa, chemchemi ya utakatifu

2.15. Komunyo takatifu

2.16. Sala ya kuomba

2.17. Sala ya Kanisa

2.18. Sala ya moyo ya wanaoanza inavyozidi kuwa sahili

2.19. Kufikia maisha ya sala na kudumu ndani yake

2.20. Wachelewaji

 

3. MWANGA WA WANAOENDELEA

3.1. Lugha ya walimu wa Kiroho ikilinganishwa na ile ya wanateolojia

3.2. Kuingia hatua ya mwanga

3.3. Wongofu wa pili kadiri ya walimu wengine

3.4. Kutakaswa upande wa hisi na kuingia hatua ya mwanga

3.5. Tufanye nini katika usiku wa hisi

3.6. Sifa kuu za hatua ya wanaoendelea

3.7. Jengo la Kiroho la wanaoendelea

3.8. Busara na maisha ya Kiroho

3.9. Haki, aina zake na kuunda utashi

3.10. Subira na upole

3.11. Usafi wa moyo, thamani na matunda yake

3.12. Unyenyekevu wa wanaoendelea

3.13. Unyenyekevu wa Neno aliyefanyika mwili na ule wa kwetu unavyotakiwa kuwa

3.14. Roho ya ufukara

3.15. Ukuu wa utiifu

3.16. Usahili na unyofu

3.17. Roho ya imani na ustawi wake

3.18. Tumaini kwa Mungu na hakika yake

3.19. Upendo wa kulingana na matakwa ya Mungu

3.20. Upendo wa kidugu, mng'ao wa upendo wa Mungu

3.21. Ari kwa utukufu wa Mungu na kwa wokovu wa watu

3.22. Usikivu kwa Roho Mtakatifu

3.23. Upambanuzi wa roho

3.24. Sadaka ya misa na wanaoendelea

3.25. Komunyo ya wanaoendelea

3.26. Ibada ya wanaoendelea kwa bikira Maria

3.27. Kitabu cha "Kumfuasa Yesu Kristo" kinawaelekeza wote njia ya mafumbo

3.28. Sala ya kumiminiwa

3.29. Uzushi wa Watulivu kuhusu sala ya kumiminiwa na kuhusu upendo safi

3.30. Ngazi za sala ya kumiminiwa kwa wanaoendelea

3.31. Maswala kuhusu sala ya kumiminiwa

3.32. Yaliyo mapya katika sala ya kumiminiwa

3.33. Ulinganifu na tofauti kati ya watakatifu Teresa wa Yesu na Yohane wa Msalaba

 

4. MUUNGANO WA WALIOKAMILIKA

4.1. Kuingia hatua ya muungano kupitia usiku wa roho

4.1.1. Haja ya kutakaswa roho na utangulizi wa hatua ya muungano

4.1.2. Ufafanuzi wa utakaso wa Kimungu wa roho

4.1.3. Kinachosababisha roho kutakaswa

4.1.4. Giza la mwanga mkali

4.1.5. Miongozo kwa usiku wa roho

4.1.6. Matokeo ya roho kutakaswa hasa upande wa maadili ya Kimungu

4.1.7. Hatua ya waliokamilika: muungano wao na Mungu

4.1.8. Aina mojawapo ya maisha makamilifu: njia ya utoto wa Kiroho

4.2. Ushujaa wa maadili

4.2.1. Ushujaa wa maadili kwa jumla

4.2.2. Imani ya kishujaa inayozama katika mafumbo

4.2.3. Tumaini la kishujaa na kujiachilia kwa Mungu

4.2.4. Upendo wa kishujaa

4.2.5. Ushujaa wa maadili ya kibinadamu

4.2.6. Upendo kwa Yesu msulubiwa na kwa Maria katika hatua ya muungano

4.3. Namna na ngazi za hatua ya muungano

4.3.1. Maisha kamili ya kitume na sala ya kumiminiwa

4.3.2. Maisha ya malipizi

4.3.3. Roho Mtakatifu anavyomuathiri aliyekamilika

4.3.4. Muungano mkavu na muungano wa kutoka nje ya nafsi

4.3.5. Muungano unaotugeuza, utangulizi wa ule wa mbinguni

 

5. NEEMA ZA PEKEE

5.1. Karama

5.2. Mafunuo na njozi

5.3. Maneno na miguso ya Kimungu

5.4. Madonda matakatifu na kudanganyika

5.5. Tofauti kati ya matukio hayo ya Kimungu na yale yatokanayo na ugonjwa

5.6. Matukio ya Kishetani

 

6. HATIMA

 

 

 

 

0. UTANGULIZI

 

0.1.        KITU KILICHO MUHIMU PEKE YAKE

 

Mtu akiacha kuongea na wenzake, mara anaanza kuwaza yanayomvutia zaidi. Mawazo hayo yanatofautiana hasa kadiri ya umri na uadilifu wa watu. Kwa mtu anayelenga ukweli na wema yanaelekea kugeuka maongezi na Mungu, naye mwenyewe, badala ya kujipendea katika yote (yaani kujifanya lengo la yote, ajue asijue) anamlenga Mungu katika kila jambo pamoja na kumpenda na kuwapenda watu kwa ajili yake. Ndiyo maisha ya Kiroho.

Ni jambo bora na la lazima kuliko elimu, sanaa, fasihi, siasa na mengineyo: wale wasio na maisha ya Kiroho wakijihusisha na mambo hayo wanaonekana kutafuta humo ukweli na wema, lakini utafiti wao unaathiriwa na umimi kiasi kwamba tunapaswa kujiuliza kama utazaa matunda kwa uzima wa milele. Wengi wao hawainuki juu ya utendaji wa kibinadamu tu na wa njenje, wala hawaishi kwa jambo lililo bora kuliko wao, yaani kwa Mungu.

Maisha ya Kiroho, yaani kuishi na Mungu, ndiyo kitu pekee cha lazima kwa sababu kwa njia yake tu tunaelekea lengo letu kuu. Tusiutenganishe wokovu na safari ya utakatifu iliyo njia ya wokovu. Mbinguni kutakuwa na watakatifu tu, wawe wameingia mara baada ya kufa, au wawe wamehitaji kutakaswa toharani. Hakuna anayeingia mbinguni akiwa na doa lolote. Ili aweze kufurahia daima uso wa Mungu, yaani kumjua na kumpenda kama mwenyewe anavyojijua na kujipenda, ni lazima hatia yoyote hata ndogo iwe imefutwa, na adhabu iliyostahili iwe imetimizwa au kuondolewa.

“Atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake?” (Math. 16:26). Ikiwa tuko tayari kupoteza vitu vingi ili kuokoa mwili, ambao kwa vyovyote utakuja kufa, kwa nini tusiwe tayari kupoteza vyote ili kuokoa roho inayotakiwa kuishi milele? Je, binadamu hapaswi kupenda roho kuliko mwili wake?

 

0.2.        SWALA LA MAISHA YA KIROHO SIKU HIZI

 

Hayo tuliyoyasema ni ya kweli nyakati zote, lakini siku hizi yanahitaji kufikiriwa zaidi, kwa sababu hakuna utulivu: wengi wamejitenga na Mungu, wakijitahidi kupanga mbali naye maisha ya binafsi na ya jamii. Matatizo makuu yaliyowapata daima binadamu yamepata sura mpya ya kutisha. Kwa kuwa Mungu ni mwanzo na mwisho wa yote, mtu akitaka kutenda bila yake anajikuta vilindini mwa unyonge mbaya kuliko utovu wa vyote. Hatimaye analazimika kutambua kuwa yote yanadai azingatie sana swala la dini.

Mtu asipotaka kutimiza wajibu wake kwa Mungu, aliye muumba na lengo lake kuu, anajikuta akiabudu vingine, k.mf. sayansi au haki ya kijamii au kipeo chochote cha kibinadamu, kwa kuwa hawezi kuishi bila ya dini. Hivyo anasogea mbali na aliye Mkuu kabisa na kukabiliana na rundo la maswala ambayo, atake asitake, hayana jibu lolote asiporudia swala la msingi la fungamano na Mungu.

Siku hizi bingwa anaabudu taratibu za sayansi na kuzijali kuliko ukweli wenyewe. Angefanya bidii hizohizo katika maisha ya Kiroho, angefikia mapema utakatifu. Kumbe hiyo ibada ya sayansi lengo lake ni utukufu wa mtu badala ya upendo wa Mungu. Vilevile siasa mara nyingi inajidanganya kuboresha maisha ya binadamu kwa kukataa haki za Mungu.

 

Msingi wa maswala yoyote ni swala la dini: hatuwezi kulipuuzia wala kuepa kusimama ama upande wa Mungu ama dhidi yake. Historia ya karne ya 20 imetuonyesha hilo waziwazi.

Mtu akitaka kuishi bila ya Mungu, uzito wa maisha unasogezwa kutoka upande wa dini kwenda upande mwingine. Lakini baada ya muda analazimika kutambua kuwa yote yamevurugika.

Mali haiwezi kuwa yote ya wengi kwa wakati mmoja: ndiyo sababu ya mashindano kati ya watu na kati ya mataifa, lengo kuu likiwekwa katika mali. Kumbe mema ya Kiroho yanaweza kuwa yote ya wote kwa wakati mmoja: tunaweza kuwa na ukweli uleule, uadilifu uleule na Mungu yuleyule bila ya kunyang'anyana.

Bwana ametuambia: “Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake, na hayo yote mtazidishiwa” (Math. 6:33). Kukataa fundisho hilo ni kujitakia maangamizi: "Bwana asipoijenga nyumba waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji yeye aulindaye akesha bure" (Zab. 127:1).

 

Mtu akijali sayansi au siasa kuliko dini, na akijitafutia utukufu badala ya kumtafutia Mungu, maisha yatamfundisha mapema kuwa ameshika njia isiyofika mahali. "Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu, na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya" (Math. 12:30).

Lakini dini haiwezi kuwa jibu halisi la maswala makuu ya leo isiposhikwa kwa dhati. Maisha ya Kiroho yanatakiwa kuwa kweli muungano na Mungu ili dini idumu kuwa juu ya sayansi na siasa.

 

0.3.        LENGO LA MAANDISHI HAYA

 

Lengo ni kuwaalika watu kwenye muungano na Mungu, wakiepa hatari mbili.

Ya kwanza ni kwamba leo kutofautisha fani kumezidi hata kufanya wengi wakose mitazamo mipana inayohitajika ili kupima kwa busara mambo yoyote katika uhusiano na mengine. Basi, katika maisha ya Kiroho pia kuzingatia madogomadogo kusitusahaulishe jumla ya yote, la sivyo tutasogea mbali na hekima ya Kikristo.

Ya pili ni kwamba vitabu vingi vya dini na vya ibada vinakosa msingi imara katika imani na kurahisisha mno mafundisho ya Kiroho.

 

0.4.        SHABAHA YA FANI HII

 

Maisha ya Kiroho ni tawi la teolojia linalohusika na utekelezaji wake katika kuongoza watu waungane kwa dhati na Mungu likifafanua muungano huo ni nini na njia za kuufikia ni zipi. Hivyo linafafanua taratibu za uzima wa neema kwa misingi ya teolojia likiilinganisha na mang'amuzi ya watakatifu.

Maisha ya Kiroho yanahitaji kuchambua mang'amuzi hayo kitaalamu, kwa kubainisha taratibu zake kadiri ya saikolojia (k.mf. ukavu unaotakasa unavyohusiana na muungano na Mungu). Somo hilo linakuwa la kiteolojia uchambuzi wa taratibu hizo unapotegemea pia mafundisho ya imani. Ikiwa elimunafsia ni ya lazima kwa maadilidini, ni ya lazima zaidi kwa maisha ya Kiroho ambayo yanachunguza hatua zake ndani ya mtu hadi muungano kamili.

Katika ngazi ya chini, maadilidini yanatakiwa kuzungumzia sio tu madhambi ambayo tuyaepe, bali pia maadili ambayo tuwe nayo na usikivu katika kumfuata Roho Mtakatifu. Maisha ya Kiroho hayaenei kama maadilidini, lakini ni tawi la juu yake kwa jinsi linavyolenga kufikisha hadi muungano wa dhati na Mungu. Kwa njia yake teolojia inarudi ilipoanzia na kudumisha umoja wake. Kwa hiyo linatakiwa kufuata mwanga wa ufunuo wa Kimungu uliomo katika Maandiko na Mapokeo, ambao peke yake unaweza kutujulisha uzima wa Kimungu na muungano wa roho na Mungu ambao unapita maumbile.

Maisha ya Kiroho yanatumia mawazo ya maadilidini, lakini kuhusiana zaidi na ustawi wa uzima wa Kimungu rohoni. Utekelezaji wake, ambao ndio lengo la maisha ya Kiroho kupitia uongozi wa mtu mmojammoja, una pande mbili: juhudi na mafumbo.

Upande wa juhudi maisha ya Kiroho yanazungumzia hasa namna ya kufisha vilema na kutekeleza maadili. Upande wa mafumbo yanazungumzia hasa usikivu kwa Roho Mtakatifu, neema ya kuzama katika mafumbo ya imani, na muungano unaotokana na neema hiyo, halafu karama ambazo pengine zinaongozana nayo.

 

0.5.        TARATIBU ZA KOZI HII

 

Hapa tutaeleza yaliyo ya lazima tu, kwa kukwepa aina mbili za upotovu ambazo ni rahisi zitupate: moja kwa kuzingatia mafundisho ya imani na kupuuzia mang'amuzi, nyingine kwa kuzingatia mang'amuzi na kupuuzia mafundisho ya imani.

Tunapaswa kuzungumzia maisha ya Kiroho kwa mwanga wa teolojia kuhusu neema ya utakaso, maadili ya kujaliwa na vipaji saba; pasipo hayo tungekusanya tu dalili za hali za Kiroho za juu, badala ya kuelewa kanuni za msingi za ustawi wa uzima wa Kimungu ambao hauwezi kung'amuliwa kwa kuwa si wa kimaumbile. Pia tungetia maanani mno uhaba wa watu wanaofikia muungano wa ndani na Mungu: hapo tungedhani kuwa walio wengi hawaitwi hata kwa mbali na kwa jumla kufikia hatua hiyo; tungesahau maneno ya Bwana yanayokumbushwa na walimu wa Kiroho kuhusu swala hilo: “Waitwao ni wengi, bali wateule ni wachache” (Math. 22:14).

Upande wa pili tunapaswa kuzingatia maelezo ya watakatifu kuhusu hatua mbalimbali za maisha ya Kiroho, tukiyaangaza kwa imani ili kutambua katika mang'amuzi yao yapi ni ya pekee na yapi ni ya juu, lakini yanakusudiwa kuwa ya kawaida. Upande huo hatari nyingine ni kudhani kuwa neema ya kuzama katika sala ni ya wengi, tukiichanganya na sala nyofu ya mapenzi ambao ni utangulizi wake tu. Kufuatana na aina hizo mbili za upotovu, kuna makosa mawili ya kuepwa katika kuongoza watu: kuwaachisha njia ya juhudi mapema mno au baadaye mno.

Basi, tunapaswa kuchimba ukamilifu wa Kikristo ili kuona wazi lengo ambalo Mwokozi amewawekea watu tusilipunguze. Halafu kuchambua mang'amuzi ili tutofautishe yaliyo ya lazima na yaliyo ya ziada. Hatimaye kujumlisha hayo mawili ili kuona yaliyo ya lazima au ya kufaa na ya kutamaniwa kusudi tuufikie ukamilifu, na yale ambayo ni ya pekee tu na hayahitajiki kufikia utakatifu mkuu.

Kutokana na shida hizo mbalimbali, kusoma maisha ya Kiroho kunadai ujuzi wa teolojia (hasa juu ya neema, maadili ya kumiminiwa, na vipaji vya Roho Mtakatifu kuhusiana na mafumbo makuu ya Utatu, umwilisho, ukombozi na ekaristi) pamoja na ujuzi wa walimu wa Kiroho, hasa wale ambao Kanisa limewataja kuwa viongozi katika maswala hayo.

 

0.6.     TOFAUTI NA UHUSIANO KATI YA UPANDE WA JUHUDI NA UPANDE WA MAFUMBO

 

Kadiri ya mapokeo (watakatifu Thoma wa Akwino, Yohane wa Msalaba na Fransisko wa Sales) upande wa juhudi maisha ya Kiroho yanazungumzia hatua ya utakaso wa wanaoanza ambao, wakijua kwamba hawatakiwi kubaki nyuma na kupooza, wanajitahidi kutekeleza maadili, lakini kwa namna ya kibinadamu, yaani kwa nguvu zao zikisaidiwa na neema za kawaida. Kumbe upande wa mafumbo unaanza mara inapozungumziwa hatua ya mwanga ambapo wanaoendelea, wakiangazwa na Roho Mtakatifu, wanatenda tayari, mara nyingi na waziwazi kwa vipaji vyake saba; kwa uongozi maalumu wa huyo mlezi wa ndani wanatenda kwa namna ipitayo maumbile ambayo kabla ya hapo ilikuwa imefichika au kujitokeza mara mojamoja tu.

Walimu hao wameonyesha kuwa mambo yanayopatikana upande wa mafumbo ni ya juu katika njia ya kawaida ya utakatifu, ila si ya pekee hasa (kama njozi). Ndivyo ilivyo pia kwa wale wanaoitwa kufikia utakatifu katika utendaji mwingi (kama mt. Visenti wa Paulo).

Basi, kujua upande wa mafumbo hakufai tu kwa uongozi wa watu wachache wanaoitwa kufuata njia za pekee, bali kwa uongozi wa watu wote wanaolenga ukamilifu na muungano na Mungu katika maisha ya kila siku. Ujinga wa kiongozi wa Kiroho kuhusu mambo hayo unaweza ukazuia wale anaowaongoza: kwa kuwa hapaswi kudhani kila huzuni ya mtu aliyechoka kiakili ni takaso la Kimungu, lakini pia hapaswi kudhani kuwa hilo likipatikana ni huzuni ya kinafsi tu.

Kutokana na yote tuliyoyasema, ni wazi kwamba upande wa juhudi unalenga upande wa mafumbo. Vilevile upande wa mafumbo usipotanguliwa na juhudi za kufaa ni uongo mtupu.

Hatimaye ni muhimu kuzingatia kuwa tukitazama njia ya utakatifu kuanzia maumbile yetu, mafundisho yetu yataonekana yamepita kiasi. Lakini tukitazama njia hiyo kuanzia mafumbo yapitayo maumbile (uwemo wa Utatu mtakatifu ndani mwetu, umwilisho ulioleta ukombozi na ekaristi) hapo tutaiona kwa hekima, yaani kutoka juu, badala ya kupima yote kutoka chini unavyofanya upumbavu.

Ikiwa kweli Utatu mtakatifu unaishi ndani mwetu, ikiwa kweli Neno alifanyika mwili akafa kwa ajili yetu, yumo katika sakramenti kuu na kila siku anajitoa kwa ajili yetu, basi hapo watakatifu tu, wanaoishi kwa kujua na kama kung'amua mara nyingi uwemo huo wa Mungu, na kwa kuupenda zaidi na zaidi katika magiza na matatizo ya maishani, ndio waliopo panapotakiwa. Hapo maisha ya muungano wa ndani na Mungu yanaonekana kuwa peke yake ya kawaida kweli. Kabla ya kufikia maisha hayo, tuko bado kama watu waliosinzia, wasioishi vya kutosha kwa hazina ile kuu tuliyokabidhiwa na Mungu.

Utakatifu ni muungano wa ndani na Mungu, yaani ukamilifu wa upendo kwake na kwa jirani, ukamilifu ambao hata hivyo upo katika njia ya kawaida, kwa sababu amri ya upendo inayowapasa wote haina mipaka. Utakatifu huo hauhitaji elimu ya juu, wala utendaji mwingi wa nje, bali kuishi kwa ndani na Mungu.

 

Utakatifu huo ni utangulizi wa kawaida wa uzima wa milele; utangulizi huo unafanyika duniani au toharani, mpaka roho iwe imetakata kabisa iweze kukaribishwa kwenye heri ya kumuona Mungu.

Hatimaye, tukisema kuzama katika mafumbo ya imani ni karibu jambo la lazima kwa kufikia utakatifu, maana yake ni kwamba kwa kawaida pasipo hilo haiwezekani kufikia utakatifu ambao unadai kutekeleza kwa namna bora maadili ya Kimungu na vipaji vya Roho Mtakatifu vinavyoongozana nayo. Ndiyo tutakayoonyesha katika kozi hii.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

1. CHEMCHEMI NA LENGO LA MAISHA YA KIROHO

 

 

Kwa kuwa maisha ya Kiroho ni namna ambayo mtu mwenye bidii anaishi kwa neema akizidi kujitambua, tutaongelea kwanza uzima wa neema ili kuuthamini kikamilifu. Halafu tutazingatia muundo wa Kiroho wa maadili ya kumiminiwa pamoja na vipaji vya Roho Mtakatifu, ambavyo vyote vinatokana na neema ya utakaso katika kila mwadilifu. Hayo yote yatatuongoza kuzungumzia uwemo wa Utatu rohoni mwake, na athari ya kudumu ya Bwana wetu Yesu Kristo, aliye mshenga pekee, na ya Maria pamoja naye kwa roho hiyo.

Ndizo chemchemi za maisha ya Kiroho tunazoikuta juu sana, kuliko chemchemi za mito zinazotoka kwenye vilele vya milima mirefu. Kwa kuwa zinatoka juu, maisha ya Kiroho yanaweza kumrudia Mungu aliye juu na kuungana naye kwa ndani.

Katika sehemu hii ya kwanza, kisha kuongelea chemchemi za maisha ya Kiroho, tutazungumzia lengo lake, yaani ukamilifu wa Kikristo na wajibu wa kuulenga, kila mmoja kadiri ya hali yake maishani. Lengo ndilo la kwanza katika kupanga nia, ingawa ni la mwisho katika utekelezaji. Ndilo tulilo na hamu nalo toka mwanzo, ingawa tunaweza kulipata mwishoni tu. Ndiyo sababu Bwana alianza kuhubiri kwa kutuambia juu ya heri.

 

 

 

 

1.1. UZIMA WA NEEMA, MWANZO WA UZIMA WA MILELE

 

 

Maisha ya Kiroho yanadai Mkristo awe na hali ya neema ya utakaso, ambayo ni kinyume cha hali ya dhambi ya mauti. Kila mtu yupo katika mojawapo kati ya hali hizo mbili, yaani ama anamuelekea Mungu kama lengo kuu, ama amepotoka mbali naye. Hakuna anayeweza kuwa na hali ya kimaumbile tu, kwa kuwa wote wanaitiwa lengo linalopita maumbile, yaani kumuona Mungu uso kwa uso na hivyo kumpenda kabisa.

Ili mtu awe na maisha ya Kiroho haitoshi awe na neema ya utakaso, kama vile mtoto kisha kubatizwa au mtu aliyeondolewa dhambi katika kitubio. Zaidi ya hiyo, maisha ya Kiroho yanadai vita dhidi ya yale yote yanayoweza kutuangusha dhambini, na juhudi halisi katika kumlenga Mungu.

Tungeng'amua kwa ndani hali ya neema, tungeona kwamba siyo tu mwanzo wa maisha matakatifu bali pia ni mbegu ya uzima wa milele. Ni lazima tusisitize mapema jambo hilo, tukikumbuka neno la mt. Thoma wa Akwino: “neema ya utakaso ya mmoja ni bora kuliko mema ya kimaumbile ya ulimwengu wote”; kwa sababu neema hiyo ni mbegu ya uzima wa milele, ambao una ubora usio na kifani kuliko uzima wa kimaumbile wa kwetu na wa malaika.

Ndilo linaloweza kutuonyesha vizuri kuliko yote thamani ya neema ya utakaso, ambayo tunaipata katika ubatizo na kurudishiwa na kitubio ikiwa tumeipoteza. Mwanzoni mwa kozi hii ni muhimu kuthamini kweli neema hiyo ambayo Uprotestanti umeisahau, ukifuata wanafalsafa wengi wa karne ya XIV. Hatuwezi kujua thamani ya mbegu tusipojua kinachoweza kutokana nayo. Upande wa binadamu, tukitaka kuthamini roho ambayo imesinzia bado katika mtoto, ni lazima tujue nguvu ya roho ya mtu aliyekomaa. Vilevile hatuwezi kuthamini neema ya utakaso waliyonayo waadilifu, tusipozingatia ustawi wake kamili katika uzima wa milele. Inafaa tuuzingatie kwa mwanga wa maneno ya Bwana, ambayo ni “roho, tena ni uzima” (Yoh. 6:63) na yana ladha bora kuliko maelezo yoyote ya teolojia. Lugha ya Injili na mtindo wa Bwana vinatuzamisha katika sala kuliko lugha ya kitaalamu hata ikiwa na hakika ya juu. Hakuna kinacholeta wokovu kuliko kupumua hewa safi ya vilele vile vinavyobubujika maji hai ya mafundisho ya Kikristo.

 

 

UZIMA WA MILELE AMBAO MWOKOZI AMEWAAHIDIA WENYE MAPENZI MEMA

 

Neno “uzima wa milele” ni adimu katika Agano la Kale, ambamo yote yanaelekea ujio wa Mwokozi aliyeahidiwa. Kumbe katika mahubiri ya Yesu yote yanaelekea moja kwa moja uzima wa milele. Tukizingatia kwa makini maneno yake tutaona jinsi uzima huo ulivyo tofauti na maisha yajayo yaliyozungumziwa na wanafalsafa bora (k.mf. Plato) kama hali ya kimaumbile tu na isiyo ya hakika. Kumbe Mwokozi anaongea kwa hakika juu ya uzima wa milele, bora, usio na jana, leo na kesho, unaopita maumbile na usiopimika, kama ule wa ndani ya Mungu, kwa kuwa unashiriki umilele wake usiobadilika.

Yesu alifundisha kuwa “njia imesonga iendayo uzimani” (Math. 7:14) na kuwa tukitaka kuupata ni lazima tuache dhambi na kushika “amri” za Mungu (taz. Math. 19:17). Mara kadhaa alisema kuwa anayemwamini “yuna uzima wa milele” (Yoh. 5:24; 6:40,47) maana yake anayemuamini kuwa ni Mwana wa Mungu kwa imani hai, inayoambatana na upendo na utekelezaji wa amri, ameanza kuwa na uzima wa milele. Ndivyo alivyotamka tangu mwanzo wa mahubiri yake: “Heri walio maskini wa roho, maana ufalme wa mbinguni ni wao... Heri wenye njaa na kiu ya haki, maana hao watashibishwa...Heri wenye moyo safi, maana hao watamwona Mungu” (Math. 5:3-8). Basi, uzima wa milele ni kushiba huko na kumwona Mungu katika ufalme wake. Kwa namna ya pekee, wanaoteswa kwa sababu ya kufanya atakavyo Mungu wanaambiwa: “Furahini na kushangilia, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni” (Math. 5:12). Yesu akajieleza zaidi tena kabla ya mateso yake aliposema: “Baba... ulimpa Mwanao mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele. Na uzima wa milele ndio huu: wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma” (Yoh 17:1-3).

“Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye, kwa maana tutamwona kama alivyo” (1Yoh. 3:2), yaani si kwa kuzingatia mng'ao wa sifa zake katika viumbe (vile vinavyoonekana na roho za watakatifu zinazojitokeza katika maneno na matendo yao), bali moja kwa moja jinsi alivyo. “Wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana” (1Kor. 13:12). Mtume hakusema kuwa nitamjua ninavyojijua mpaka ndani; kwa sababu najifahamu kuliko wengine, lakini mimi pia sielewi yote niliyonayo ndani, k.mf. siwezi kupima uzito wote wa dhambi zangu. Mungu tu ananijua fika: siri za moyo wangu anazielewa kikamilifu yeye tu. Mbinguni nitamjua anavyonijua, moja kwa moja, pasipo kupitia kiumbe chochote au wazo lolote la kimaumbile, kwa sababu hakuna wazo la namna hiyo linaloweza kumchora Mungu na ukweli wake usio na mipaka, nuru angavu ya milele. Kila wazo la namna hiyo lina mipaka, linazingatia sifa mojawapo ya Mungu (k.mf. ukweli au wema). Mawazo hayo mbalimbali hayatoshi kutujulisha undani wa Mungu, umoja wake usiogawanyika kamwe. Mawazo hayo yanahusiana na uzima wake wa ndani kama vile rangi saba za upinde wa mvua zinavyohusiana na mwanga mweupe ambao zinatokana nao. Hapa chini sisi ni kama watu tulioona hizo rangi saba tu na sasa tunatamani kuona huo mwanga mweupe unaozisababisha. Kabla hatujaona umungu wenyewe hatuwezi kuona ulinganifu wa ndani wa sifa zake, hasa huruma isiyo na mipaka na haki isiyo na mipaka. Mawazo yetu ya kimaumbile kuhusu sifa za Mungu ni vipande tu vya sura nzima, ambavyo vinaleta picha fulani ya Mungu isiyopendeza vya kutosha. Tukifikiria haki yake, inaonekana ni kali mno, na tukifikiria upendeleo wa huruma yake unaonekana ukienda kinyume cha haki. Tukitafakari zaidi tunakiri kuwa ndani ya Mungu haki na huruma ni kitu kimoja, hazitofautiani kweli. Huo ni ukweli ambao tunauungama kwa hakika, lakini hatujaona ulinganifu wa ndani wa sifa hizo, kwa kuwa unahitaji tutazame umungu jinsi ulivyo, moja kwa moja, pasipo kutumia mawazo yoyote ya kimaumbile.

Mtazamo huo ndio uzima wa milele. Nani anaweza kueleza ukuu usiopimika wa furaha na upendo vitakavyokuwemo ndani mwetu kutokana na mtazamo huo? Upendo wa Mungu wenye nguvu na wa moja kwa moja, hivi kwamba hakutakuwa na lolote litakaloweza kuupunguza; upendo ambao tutafurahia hasa kuwa Mungu ni Mungu, mtakatifu, mwenye haki na huruma pasipo mipaka, na ambao tutaabudu mipango yote ya maongozi yake iliyolenga ufunuo wa wema wake. Tutazama katika heri yake, alivyosema Mwokozi mwenyewe: “Vema, mtumwa mwema na uaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako” (Math. 25:21,23). Tutamuona Mungu vile anavyojiona moja kwa moja, ingawa hatutaweza kumaliza vilindi vya hali yake, vya upendo wake na vya uweza wake. Pia tutampenda anavyojipenda. Vilevile tutamuona Bwana wetu Yesu Kristo. Ndiyo heri ya milele yenyewe, mbali ya furaha ya ziada tutakayokuwa nayo kwa kuwaona na kuwapenda Bikira Maria pamoja na watakatifu wote, hasa tuliowafahamu duniani.

 

 

MBEGU YA UZIMA WA MILELE NDANI MWETU

 

Huo mtazamo wa moja kwa moja wa Mungu unapita uwezo wa kimaumbile wa akili yoyote ya malaika na ya binadamu, kwa kuwa ungehitaji ulingane na ule wa Mungu. Basi, akili ya kiumbe inaweza kupata mtazamo huo kwa neema ya Mungu tu, ambayo ni kama kupandikiza chipukizi la mti bora katika shina la mti mwitu ili uzae matunda mema. Malaika na binadamu hawawezi kumjua na kumpenda Mungu kwa namna inayopita maumbile yao kabla hawajapandikiziwa neema ya utakaso, ambayo ni kushiriki umungu, yaani uzima wa ndani wa Mungu. Neema hiyo tu, ikipokewa rohoni mwetu kama zawadi isiyolipika, inatuwezesha kutenda Kimungu, yaani kumuona moja kwa moja vile anavyojiona, na kumpenda vile anavyojipenda. Kwa maneno mengine, akili na utashi kushirikishwa umungu kunategemea kushirikishwa umungu kwa roho yenyewe iliyonavyo.

Neema hiyo ikikamilika isiweze kupotezwa inaitwa utukufu, ambao katika akili za watakatifu wa mbinguni unatia mwanga usio wa kimaumbile unaowawezesha kumwona Mungu, na katika utashi wao unatia upendo wa kumiminiwa unaowawezesha kumpenda Mungu hata wasiweze kuachana naye kamwe. Kwa ubatizo sisi tumeshapokea mbegu ya uzima wa milele, kwa kupokea neema ya utakaso inayouleta uzima huo: pamoja na neema ya utakaso tumepokea upendo wa kumiminiwa unaokusudiwa kudumu milele. Ndivyo Mwokozi alivyomuambia mwanamke Msamaria: “Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, ‘Nipe maji ninywe’, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai… Yeyote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele, bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele” (Yoh. 4:10,14).

“Atakayekunywa maji hai ya neema yanayotolewa na Mwokozi hatatamani mengine, ila atatamani kuyapokea hayohayo kwa wingi zaidi... Zaidi ya hayo, tofauti na maji ya kawaida ambayo yanaelekea chini, yale ya Kiroho yanapanda juu. Ni maji hai ambayo hayaachani kamwe na chemchemi yake na ambayo yanabubujikia uzima wa milele ambao yanatustahilisha” (mt. Thoma wa Akwino). Hayo maji hai yanatoka kwa Mungu, ndiyo sababu yanaweza kurudi juu kwake.

Siku ya mwisho ya sikukuu ya Vibanda, Yesu alisimama hekaluni, “akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi, kama vile Maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake” (Yoh. 7:37-38). Anayekunywa Kiroho kwa kumuamini Mwokozi, anaweza kuchota katika chemchemi ya maji hai, siyo kwa ajili yake tu bali pia kwa ajili ya watu wengine ili waokoke.

Yesu alikariri: “Amwaminiye Mwana yuna uzima wa milele” (Yoh. 3:36). Sio tu atakuwa nao baadaye, bali kwa namna fulani anao tayari, kwa kuwa uzima wa neema ni mwanzo wa uzima wa milele, kama vile mbegu inavyohusiana na mti wake. Kwa undani ni uzima uleule wa Kimungu, ambao hapa chini umo ndani ya Mkristo kama mbegu na ambao huko juu utachanua kikamilifu katika watakatifu. Ndiyo maana Bwana aliongeza: “Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho” (Yoh. 6:54). Ufalme wa Mungu umo ndani mwetu kama mbegu ya haradali, kama chachu itakayoumua donge lote, kama hazina iliyositirika shambani.

Tunawezaje kujua kama tumepokea tayari uzima huo unaokusudiwa kudumu milele? “Sisi tunajua ya kuwa tumepita toka mautini kuingia uzimani, kwa maana twawapenda ndugu. Yeye asiyependa, akaa katika mauti… Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu” (1Yoh. 3:14; 5:13).

Yesu alisema: “Amin, amin, nawaambia: Mtu akilishika neno langu, hataona mauti milele” (Yoh. 8:51). Kwa kuwa, inavyosema liturujia, “Ee Bwana, uzima wa waamini wako hauondolewi ila unageuzwa tu”, tena unastawi kikamilifu mbinguni tu. Hakika uzima wa neema hapa duniani ni mbegu ya utukufu, hivi kwamba kiwango kidogo cha neema ya utakaso ni bora kuliko mema ya kimaumbile ya ulimwengu wote na ya malaika pia, kwa sababu kinahusu hali ya juu, yaani uzima wa ndani wa Mungu; kwa hiyo ni bora kuliko miujiza yote na ishara nyingine za nje za ufunuo wa Mungu.

Uzima uleule unaopita maumbile, ndio unaopatikana duniani katika waadilifu na mbinguni katika watakatifu. Ni pia upendo uleule wa kumiminiwa, isipokuwa tofauti mbili. Hapa chini tunamjua Mungu si kwa kumtazama mwangani, bali katika giza la imani ya kumiminiwa. Halafu hapa chini, ingawa tunatumaini kuwa naye kikamilifu milele, tunaweza kupotewa naye kwa kosa letu.

Kuna tofauti hizo mbili zinazohusu imani na tumaini, hata hivyo ni uzima uleule na upendo uleule ambavyo vinakusudiwa kudumu milele. Kwa mwanga huo tunapaswa kuelewa maisha yetu ya Kiroho yanavyotakiwa kuwa na kustawi hapa chini yawe utangulizi wa kufaa kwa uzima wa milele. Ikiwa neema ya utakaso, maadili ya kumiminiwa na vipaji vya Roho Mtakatifu kwa mfumo wake vinaulenga uzima wa milele, je havikusudiwi kulenga pia muungano wa hali ya juu na Mungu?

 

 

JAMBO MUHIMU LITOKANALO

 

Kwa kweli neema ya utakaso na upendo, vinavyotuunganisha na Mungu katika maisha yake ya ndani, ni bora, tena sana, kuliko neema za pekee (kama vile kutabiri na kusema kwa lugha ngeni) ambazo ni ishara tu za kazi za Mungu lakini hazituunganishi naye (taz. 1Kor. 12:28-13:13). Hali ya kuzama katika mafumbo ni tunda la imani tuliyomiminiwa, ikiangazwa na vipaji vya akili na vya hekima: hivyo inatokana na neema ya utakaso, ambayo inaitwa pia “neema ya maadili na vipaji” na tunaipata wote katika ubatizo; haitokani na neema za pekee.

Kwa kuwa neema ya utakaso kwa mfumo wake inalenga uzima wa milele, inalenga pia hali ile inayohitajika ili kupata mwanga wa utukufu. Hali hiyo ni upendo kamili pamoja na hamu kubwa ya heri ya kumuona Mungu; kwa kawaida hamu hiyo inatokana na neema ya kuzama katika mafumbo. Hivyo basi kuzama huko si neema ya pekee kama ulivyo k.mf. utabiri, bali ni hali ya juu iliyopo katika njia ya kawaida ya utakatifu, ingawa ni adimu kama ulivyo adimu ukamilifu mkuu.

 

Hatimaye, kwa vile neema ya utakaso kwa mfumo wake inalenga uzima wa milele, inalenga pia kutuweka tayari kupata mwanga wa utukufu mara baada ya kufa bila ya kupitia toharani, ambako ni adhabu, maana yake kunatokana na kosa lisilotakiwa pamoja na malipizi yasiyotosha; ingekuwa kawaida kutakaswa katika maisha haya kwa kujilimbikizia stahili na kukua katika upendo, badala ya kutakaswa kisha kufa pasipo stahili yoyote. Hali iliyo tayari kupokea mwanga wa utukufu mara baada ya kifo inahitaji kwanza utakaso halisi unaolingana na ule wa roho zinazotoka toharani zenye hamu kubwa ya kumwona Mungu.

Hamu hiyo imedhihirishwa na mt. Paulo vizuri ajabu: “Katika nyumba hii twaugua, tukitamani sana kuvikwa kao letu litokalo mbinguni… twaugua, tukilemewa, si kwamba twataka kuvuliwa, bali kuvikwa… Basi yeye aliyetufanya kwa ajili ya neno lilo hilo ni Mungu, aliyetupa arabuni ya Roho” (2Kor. 5:2-5).

Tukitaka kujadili maswala ya maisha ya Kiroho jinsi inavyotakiwa, hatupaswi kusahau vilele hivyo tunavyojulishwa na Maandiko na kuelezwa na teolojia ya walimu wakuu. Hasa katika maisha ya Kiroho tunatakiwa kuzingatia watu sio walivyo tu bali wanavyokusudiwa kuwa. Tunapaswa kupumua hewa bora ya vilele vya juu, badala ya kuishia katika hali ya wastani ya binadamu. Heri watu ambao wanajaribiwa hata wanakuta hewa ya kuwafaa upande wa Mungu tu na kumtamani kwa hamu kuu.

 

 

 

 

1.2. MAISHA YA KIROHO NA MAONGEZI YA NDANI NA MUNGU

 

 

MAONGEZI YA KILA MTU NA NAFSI YAKE

 

Mtu anapoacha shughuli za nje na maongezi na wenzake na kubaki peke yake - hata kama ni katikati ya kelele za jiji - mara anaanza kuwaza kama kwa kuongea na nafsi yake. Akiwa kijana anafikiria ya kesho; akiwa mzee anafikiria ya zamani, na mang'amuzi aliyonayo sasa yanamfanya apime tofauti watu na matukio. Akiwa na umimi anafuata tamaa au kiburi na hivyo ndani yake anapata huzuni tu, ndiyo sababu anajaribu kujitoroka kwa kuzama katika mambo ya nje na anasa asahau utupu wa maisha yake yasiyo na maana. Kwa kufanya hivyo anakuja kujifahamu kwa namna fulani ya hali ya chini, na vilevile kujipenda visivyo. Sanasana anajifahamu upande wa hisi, alizo nazo sawa na wanyama; hivyo ana furaha na uchungu vya kihisi kadiri ya mabadiliko ya hali ya hewa au ya biashara yake. Anavyovitamani na anavyovichukia ni vya aina hiyohiyo, na akipingwa anakasirika kutokana na jinsi anavyojipendea.

Kumbe anajifahamu kidogo tu upande wa roho, ambayo inalingana na malaika. Hata kama anaamini ukuu wa roho (yenye akili na utashi) haishi katika ngazi hiyo: hana mang'amuzi kuhusu sehemu hiyo bora ya utu wake, wala haipendi vya kutosha. Angeijua angeona ndani yake sura ya Mungu na kuanza kujipenda kwa ajili ya Mungu, si tena kujipendea kibinafsi. Hata akionyesha mara nyingi uwezo wa kuelewa na kutenda kwa ujanja, akili yake inaelekea daima yaliyo ya chini kuliko yeye. Ingawa ameumbwa ili kumtazama Mungu, ukweli mkuu, anafuata udanganyifu hata kuutetea kwa kila njia. Maisha yasipofuata ubora wa mawazo, mawazo yatafuata uduni wa maisha: yote yanafungamana, hata misimamo mizuri aliyokuwa nayo inadhoofika zaidi na zaidi.

Hivyo maongezi ya ndani yake yanaelekea mauti na hayastahili kuitwa maisha ya Kiroho. Kujipendea kwake kunamfanya ajione kiini cha yote, na kuelekeza yote (watu na vitu) kwake; lakini hiyo haiwezekani, ndiyo sababu mara nyingi anakata tamaa na kuchukizwa, havumiliki kwake wala kwa wengine. Kwa kutaka kujipendea mwishowe anajichukia pamoja na maisha, kwa kuwa katika maisha alitamani mno yaliyo ya chini.

 

Kumbe binadamu akianza kutafuta uadilifu, hata kama hajawa na neema ya utakaso, maongezi yake na nafsi yake yanakuwa tofauti: k. mf. anazingatia yanayohitajika ili aishi kwa haki na kutegemeza familia yake. Pengine mawazo hayo yanamletea mahangaiko hata kumfanya atambue unyonge wake na haja ya kumtegemea Mungu badala ya kujiamini tu. Akiwa na dhambi ya mauti isiyo dhidi ya imani wala tumaini anaweza kuwa na maadili hayo yanayodumu ndani mwetu hata baada ya kupoteza upendo. Kama ni hivyo pengine mawazo yake yanaangazwa na imani ambayo mwanga wake unapita maumbile yetu; anaweza akawaza uzima wa milele na kuutamani, ingawa si zaidi; tena pengine anajisikia msukumo wa kwenda kanisani.

 

Hatimaye, mtu huyo akijuta na kuondolewa makosa yake, anarudishiwa neema ya utakaso na upendo kwa Mungu na kwa jirani. Kuanzia hapo, mawazo yake yanakuwa mengine. Anaanza kujipenda kitakatifu, yaani si kwa ajili yake, bali kwa ajili ya Mungu, na kuwapenda watu pia kwa ajili ya Mungu; anaanza kuelewa anavyopaswa kusamehe na kupenda maadui, na kuwatakia uzima wa milele vile anavyojitakia. Lakini mara nyingi mawazo yake yanaendelea kuchafuliwa na umimi, ubinafsi, tamaa na kiburi. Kwake makosa hayo si tena ya mauti, lakini yakitokea mara nyingi yanamfanya arudie dhambi kubwa na mauti ya roho. Hapo mtu atajaribu tena kujitoroka, kwa sababu haoni uzima ndani mwake; ndiyo maana asipojifikiria upya atazidi kujitupa mikononi mwa anasa na kiburi.

Hata hivyo maongezi ya ndani mwake yanaanza tena yasiweze kuzuiwa na chochote, wala na yeye mwenyewe. Ndani mwa roho mna haja inayodai kutimizwa. Mungu tu anaweza kufanya hivyo, kwa hiyo njia pekee ni kumuendea yeye. Roho inahitaji kuongea naye kwa sababu lengo lake kuu ni Mungu aliye hai, hata isiweze kutulia isipokuwa ndani ya Mungu.

 

 
MAONGEZI YA NDANI NA MUNGU

 

Basi, maisha ya Kiroho ni maongezi ya kila mtu na nafsi yake kuinuliwa na kugeuka sura mara yanapoanza kuwa maongezi na Mungu. Ni kwamba Roho wa Mungu anawaonyesha zaidi na zaidi watu wenye mapenzi mema yale ambayo anayataka toka kwao na yale anayotaka kuwazawadia. Lo, kama tungepokea kwa mikono miwili yale yote Mungu anayotaka kutupatia!

Maonyesho hayo hayafanyiki pasipo juhudi; tunapaswa kuokoka katika vifungo vitokanavyo na dhambi, kufisha hatua kwa hatua “utu wa zamani” na kuunda “utu wa ndani”: “Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani; lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu” (Rom. 7:22-23) “Utu wa ndani” ndio kilicho bora ndani mwetu, yaani akili utashi ambavyo vinapaswa kutawala mwili, ulio sawa kwa mtu na kwa mnyama.

“Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku” (2Kor. 4:16). Nguvu za Kiroho zinafanywa upya mfululizo kwa njia ya neema tunazozipokea kila siku. “Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake; mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba” (Kol. 3:9-10). Baba “awajalieni, kwa kadiri ya utajiri wa utukufu wake, kufanywa imara kwa nguvu, kwa kazi ya Roho wake, katika utu wa ndani. Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo; ili mpate kufahamu pamoja na watakatifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo na kina; na kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate kutimilika kwa utimilifu wote wa Mungu” (Ef. 3:16-19).

Ndiyo maisha ya Kiroho na vilindi vyake, maisha yale yanayolenga mfululizo kulitazama fumbo la Mungu na kulifanya chakula chake katika muungano naye wa ndani zaidi na zaidi. Mtume aliandika hayo kwa Wakristo wote, sio kwa mmojammoja tu. Akaongeza: “Mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli… mkaenende katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi; tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato”(Ef. 4:23-24; 5:2).

Kwa kuzingatia maneno hayo ya Mungu tunaweza kufafanua maisha ya Kiroho kama ifuatavyo: maisha ya Kiroho ni maisha ambayo yanapita maumbile na kutuelekeza na kutufikisha kwenye muungano na Mungu kwa njia ya kujikana na kusali kweli.

“Mafundisho ya Yesu Kristo yanapita mafundisho yoyote ya watakatifu na mtu aliye na roho yake anakuta humo mana iliyositirika. Lakini inatokea kuwa wengi, kwa kusikia Injili mara nyingi, hawaguswi inavyotakiwa, kwa sababu hawana roho yake. Mnataka kuelewa mpaka ndani na kufurahia maneno ya Yesu Kristo? Mjitahidi kulinganisha maisha yenu yote na ya kwake” (Kumfuasa Yesu Kristo, I,1:2).

Maisha hayo yana hatua ya kwanza inayotawaliwa na utakaso, ya pili inayotarajia mwanga mkubwa zaidi na zaidi, na lengo lake la mwisho ni kuungana na Mungu. Ndivyo mapokeo yote yanavyofundisha, yakithibitisha uwepo wa hatua ya kutakaswa kwa wanaoanza, hatua ya kuangazwa kwa wanaoendelea, na hatua ya kuungana na Mungu kwa waliokamilika. Hivyo maisha ya ndani ya mtu yanakuwa zaidi na zaidi maongezi na Mungu.

Kwa namna hiyo, mtu anaanza kung'amua sehemu bora ya nafsi yake na kumjua Mungu. Polepole mawazo ya nafsi yake aliyoifanya kuwa lengo la yote, yanaiachia nafasi kumbukumbu ya kudumu ya Mungu. Vivyo hivyo kujipendea kunaacha nafasi kwa upendo wa Mungu na wa watu kwa ajili yake. Maongezi ya ndani yanabadilika hata kusema: “Sisi, wenyeji wetu uko mbinguni” (Fil. 3:20).

Katika roho yenye neema ya utakaso, maisha ni hasa ya unyenyekevu, kujikana, imani, tumaini na upendo, pamoja na amani inayotakana na kuweka miguso na matakwa yote chini ya upendo wa Mungu atakayekuwa heri yetu. Basi, ili tuwe na maisha ya Kiroho haitoshi tushughulikie sana utume wala kujua sana dini. Tena hayo si ya lazima. Mtu aliyeanza tu kujikana na kusali kwa juhudi, anayo tayari maisha ya Kiroho ambayo yanatakiwa kustawi zaidi na zaidi.

Katika maongezi hayo yanayoelekea kuwa ya kudumu roho inasema kwa njia ya sala, ambayo ingekuwepo hata kama Mungu angemuumba mtu mmoja au malaika mmoja tu. Sala inaweza kuwa ya kuomba, ya kuabudu au ya kushukuru; lakini daima ni kuinua roho kwa Mungu. Naye Mungu anajibu akitukumbusha yale ambayo tuliambiwa katika Injili na yanatufaa kuitakasa nukta ya sasa hivi: “Huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia” (Yoh. 14:26)?

Hivyo mtu anazidi kuwa mtoto wa Mungu, anatambua zaidi na zaidi kuwa Mungu ni Baba yake na anazidi kujifanya mdogo mbele yake. Anaelewa yale Yesu aliyomuambia Nikodemu, yaani kuwa ni lazima kurudi katika tumbo la Mungu ili kuzaliwa upya Kiroho kila siku zaidi, k.mf. wa Neno kuzaliwa milele. Wenye heri wa mbinguni wanabaki daima katika tumbo hilo.

Watakatifu wanafuata njia hiyo, hata maongezi kati yao na Mungu hayana mwisho. Mt. Dominiko hakuweza kusema isipokuwa juu ya Mungu au na Mungu; ndiyo sababu alikuwa amejaa daima upendo kwa watu. Maongezi hayo na Mungu yanaundwa kwa njia ya Kristo mshenga: “Ulimi hauwezi kusema, / wala maandishi kufafanua, / aliyeng'amua tu anaweza kuamini / kumpenda Yesu ni nini” (Utenzi wa Jina Takatifu la Yesu).

 

 

 

 

1.3. MUUNDO WA KIROHO

 

 

Ili tuelewe mbegu ya uzima wa milele iliyomo ndani mwetu ni nini, tunatakiwa kuzingatia jinsi neema ya utakaso inavyoleta katika akili na utashi maadili ya kumiminiwa na vipaji saba vya Roho Mtakatifu. Maadili hayo na vipaji hivyo ni kama utendaji wa muundo uleule mmoja wa Kiroho unaokusudiwa kustawi hadi tuingie mbinguni.

 

 

 

1.3.1. MAISHA YA KIMAUMBILE NA YANAYOPITA MAUMBILE

 

Kwanza tutofautishe vizuri ndani ya roho yetu yale yaliyo ya kwake kwa jinsi ilivyoumbwa, na yale ambayo ni zawadi tu ya Mungu. Hata malaika, ingawa ni roho tu, ana maumbile ya chini kuliko neema ya utakaso.

Basi, sisi binadamu tuna pande mbili tofauti: upande wa hisi na upande wa akili. Wa kwanza unalingana na wanyama, ukiwa na hisi za nje (milango ya fahamu), hisi za ndani (ubunifu na kumbukumbu) na uwezo wa kupatwa na maono mbalimbali (k.mf. pendo na chuki, hamu na hofu, furaha na huzuni, hasira).

Juu ya sehemu hiyo, katika maumbile yetu ipo nyingine inayolingana na malaika, ingawa ndani mwao ina nguvu na uzuri zaidi. Upande huo roho inapita mwili, maana yake haitegemei mwili moja kwa moja, kwa hiyo inaweza kudumu baada ya mwili kufa.

Kutokana na maumbile ya roho upande huo wa juu tuna uwezo wa akili na wa utashi. Akili inajua sio tu sifa ya viumbe zinazohisikana (rangi, sauti), bali undani wao na kweli zisizobadilika kama vile: “Hakuna kinachotokea pasipo sababu, na hasa pasipo sababu kuu, yaani Mungu”. “Tunapaswa kutenda mema na kuepa maovu”. “Timiza wajibu wako, liwalo na liwe”. Mnyama hataweza kamwe kujua kweli hizo.

Kwa kuwa akili inaweza kujua sio tu yale yanayotupendeza au yanayotufaa bali pia uadilifu (k.mf. kwamba ni “afadhali kufa kuliko kusaliti”), basi utashi unaweza kupenda huo uadilifu, kuutaka na kuutekeleza. Hivyo unapata kutawala hisi na maono alivyonavyo mnyama pia. Kwa akili na utashi mtu anafanana na malaika, ingawa katika maisha haya akili yetu, tofauti na malaika, inazitegemea hisi katika kuanza kujua mambo.

Tunavyoona katika watu kadhaa, akili na utashi vinaweza vikastawi, pasipo kufikia kujua na kupenda maisha ya ndani ya Mungu, ambayo ni ya ngazi tofauti, juu kupita maumbile ya malaika na ya binadamu. Hao wanaweza kumjua kimaumbile Mungu kwa nje, kutokana na mng'ao wa sifa zake katika viumbe, lakini haiwezi kuumbwa akili yenye nguvu ya kuyajua yaliyo ya Mungu tu: “Ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu” (1Kor. 2:11).

Kumbe neema ya utakaso inatuingiza katika hiyo hali ya juu ya ukweli na uzima inayopita maumbile yoyote. Ni uzima unaopita maumbile, kwa kuwa unashiriki maisha ya ndani ya Mungu, ni hali ya Kimungu ambayo tangu sasa inatuandaa kumuona milele anavyojiona na kumpenda anavyojipenda. “Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu, mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao. Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho (1Kor. 2:9-10).

Neema ya utakaso inayotuwezesha kuanza kuishi maisha ya ndani ya Mungu, katika ngazi ya juu kuliko maumbile ya malaika, ni kama chipukizi la Kimungu lililopandikizwa ndani mwa roho ili kuinua uzima wake na kuifanya izae sio tu matunda ya kimaumbile, bali matunda yanayopita maumbile, yaani matendo yanayostahili uzima wa milele. Kupandikizwa huko kunapita miujiza inayojulikana na hisi. Kwa mfano, ufufuo unaurudishia mwili uhai wa kimaumbile, ndiyo sababu unaweza kujulikana na maumbile yetu; kumbe neema ya utakaso inaipatia roho uzima usio wa kimaumbile, ndiyo sababu hauwezi kuhakikishwa na maumbile yetu.

Tangu sasa uzima huo wa neema unachanua ndani mwetu maadili ya kumiminiwa na vipaji saba vya Roho Mtakatifu. Kama vile katika maumbile yetu roho ina uwezo wa akili na kadhalika, katika ngazi inayopita maumbile neema ya utakaso inaleta rohoni maadili na vipaji hivyo ambavyo, pamoja na mzizi unaovisababisha, ndio muundo unaopita maumbile ambao tulijaliwa katika ubatizo (na tunarudishiwa na ondoleo la dhambi ikiwa tuliupoteza).

Muundo huo wa Kiroho unaweza kuonyeshwa na jedwali ifuatayo:

 

                          MAADILI                                                             VIPAJI

                                      Upendo                                                           Hekima

YA KIMUNGU             Imani                                                   Akili

                                      Tumaini                                               Elimu

 

                                      Busara                                                Shauri

                                      Haki

                                                 (Ibada)                                                Ibada

                                                 (Toba)

                                                 (Utiifu)

YA KIBINADAMU      Nguvu                                                 Nguvu

                                                 (Subira)

                                      Kiasi                                                   Uchaji wa Mungu

                                                 (Upole)

                                                 (Unyenyekevu)

                                                 (Usafi wa moyo)

 

 

 

1.3.2. MAADILI YA KIMUNGU

 

Maadili ya Kimungu ni maadili tunayomiminiwa yanayomhusu Mungu mwenyewe aliye lengo letu kuu. Tofauti na hayo, maadili ya kibinadamu yanahusu njia za kufikia lengo hilo.

Kati ya maadili ya Kimungu, imani inatuwezesha kusadiki yale yote ambayo Mungu ametufunulia, kwa sababu ndiye ukweli wenyewe. Ni kama hisi ya Kiroho inayotuwezesha kusikia muziki safi wa Kimungu usiojulikana kwa njia nyingine yoyote, maana kuna tofauti kubwa kati ya kusoma Injili kihistoria au kitaalamu na kuiamini kama Neno la Mungu, kwa kuwa kusadiki ni tendo linalopita maumbile yetu na ya malaika, likituingiza katika ulimwengu wa juu. “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu” (Ef. 2:8). Ndiyo msingi wa kufanywa waadilifu, kwa kuwa inatujulisha lengo lipitalo maumbile tunalopaswa kulikusudia. “Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa haki” (Mwa. 15:6; Rom. 4:3,9). “Walakini haikuandikwa kwa ajili yake tu kwamba ilihesabiwa kwake; bali na kwa ajili yetu sisi tutakaohesabiwa vivyo hivyo, sisi tunaomwamini yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu katika wafu” (Rom. 4:23-24). Sisi tutaokoka tu kwa imani hiyo ambayo ni zawadi ya Mungu. Kanisa lilitamka rasmi dhidi ya Wapelajiupande kwamba hata mwanzo wa imani ni neema. Imani hiyo inapita kabisa maumbile, siyo tu kama muujiza unaoonekana au kama utabiri wa tukio la kawaida (k.mf. mwisho wa vita); kwa sababu imani inamhusu kwanza Mungu mwenyewe katika maisha yake ya ndani, ambaye hawezi kujulikana kimaumbile, tena kwa sababu tunasadiki kwa kutegemea mamlaka ya Mungu aliyejifunua, ambayo pia haiwezi kujulikana na maumbile. Imani inatufanya tushike kwa namna ipitayo maumbile na isiyoweza kukosa, yale ambayo Mungu ametufunulia kadiri tunavyofundishwa na Kanisa lililokabidhiwa ufunuo huo.

“Tazama, msomi fulani anachimba mafundisho ya Kikatoliki bila ya kuyakataa kwa ukaidi, bali anakariri, Heri nyinyi mlio na imani; mimi pia ninapenda kuwa nayo lakini siwezi. Anasema ukweli: anataka asiweze (bado); kwa sababu kusoma na kuwa na nia njema hakufikii daima kujua ukweli, ili ionekane wazi kuwa hakika ya akili si hakika kuu inayotegemeza mafundisho ya Kikatoliki… Kinachotokea ndani mwetu tunapoamini ni tukio la mwanga wa ndani unaopita maumbile yetu... Mwongofu atawaambia, Nilisoma, nilitafakari, nilitaka nisifike; lakini siku fulani, siwezi kusema vipi, kwenye pembe ya njia, au nyumbani karibu na moto, sijui, sikuendelea kuwa yuleyule, nimesadiki... Kilichotokea ndani mwangu katika nukta ya kupata hakika kuu ni jambo tofauti kabisa na yale yote yaliyotangulia. Muwakumbuke wanafunzi wale wawili waliokwenda Emau” (H. Lacordaire).

Imani tunayomiminiwa ni kama uwezo wa kusikia ambao unapita maumbile na kutuwezesha tusikilize sauti ya Mungu kupitia manabii na Mwanae mwenyewe, kabla hatujakaribishwa kumuona uso kwa uso. Kati ya mtu anayesoma Injili bila ya imani, na mwingine mwenye imani, tofauti ni kama ile iliyopo kati ya watu wawili wanaosikiliza muziki fulani, lakini mmojawao ana karama ya muziki, mwingine hana. Wote wanasikia noti zote, lakini yule wa kwanza tu anaelewa undani na ujumbe wa muziki ule. Vivyo hivyo mwamini tu, hata kama hajui kusoma, anashika Injili kwa namna ipitayo maumbile na kama Neno la Mungu linalopita maumbile, wakati msomi pamoja na elimu yake yote hawezi kuishika hivyo pasipo imani ya kumiminiwa. “Yeye amwaminiye Mwana wa Mungu anao huo ushuhuda ndani yake. Asiyemwamini Mungu amemfanya kuwa mwongo, kwa kuwa hakuuamini huo ushuhuda ambao Mungu amemshuhudia Mwanawe” (1Yoh. 5:10).

Miaka mia iliyopita mtu asiyejua redio angeshangaa kuambiwa siku moja ataweza kusikia muziki unaochezwa wakati huohuo katika nchi nyingine. Kwa imani ya kumiminiwa tunasikia muziki wa mbinguni. Nyimbo za muziki huo ni mafumbo ya Utatu, umwilisho, ukombozi, misa na uzima wa milele. Kwa kusikiliza hayo mtu anaongozwa zaidi na zaidi kwenye kilele kile kinachotoka muziki huo bora.

Ili aelekee kweli lengo hilo na kulifikia, mtu amepewa mabawa mawili, tumaini na upendo. Pasipo hayo anaweza kuelekea tu anapoelekezwa na akili yake; kumbe akiwa nayo anarukia anapoelekezwa na imani. Kama vile akili yetu pasipo mwanga wa imani haiwezi kujua lengo letu lipitalo maumbile, utashi wetu pia hauwezi kuelekea lengo hilo nguvu zake zisipozidishwa na kuinuliwa kwenye ngazi ya juu.

Kwa tumaini tunatamani kumpata Mungu, na kusudi tumfikie tunategemea si nguvu za maumbile yetu, bali msaada aliotuahidia. Tunamtegemea mwenyewe aliye tayari daima kusaidia wanaomuitikia.

Upendo ni kumpenda Mungu kwa namna bora zaidi, isiyojitafutia faida tu; unatufanya tumpende Mungu sio tu ili tumpate hapo baadaye, bali kwa ajili yake na kuliko tunavyojipenda, kutokana na wema wake usio na mipaka, unaopendeza kuliko fadhili zake zote. Unatufanya tumpende Mungu hasa kama rafiki aliyetangulia kutupenda. Unamuelekezea vitendo vya maadili mengine yote ukiyahuisha na kuyafanya yaweze kustahili. Ndio nguvu yetu kuu inayopita maumbile, nguvu ya upendo ambayo katika karne za dhuluma imeshinda vipingamizi vyote, hata katika viumbe dhaifu kama watakatifu Anyesi na Lusia.

Hivyo mwenye mwanga wa imani anamuelekea Mungu akiruka kwa mabawa ya tumaini na upendo. Lakini akitenda dhambi ya mauti, mara anapoteza neema ya utakaso na upendo, kwa kuwa anajitenga na Mungu akiacha kumpenda kuliko nafsi yake. Hata hivyo huruma ya Mungu inamuachia imani na tumaini (mpaka atakapotenda dhambi dhidi ya maadili hayo) awe bado na mwanga wa kumuelekezea njia na aweze bado kutegemea huruma isiyo na mipaka ili kuomba neema ya uongofu.

Kati ya maadili hayo ya Kimungu, upendo ndio la juu zaidi, nao utadumu milele pamoja na neema ya utakaso, ambapo imani na tumaini vitakoma na badala yake mtu atakuwa na Mungu akimjua waziwazi, bila ya hofu ya kupotewa naye (taz. 1Kor. 13:8,13). Ndio utendaji wa juu wa muundo wa Kiroho: maadili matatu ya Kimungu ambayo yanastawi pamoja, halafu maadili ya kibinadamu yanayoendana nayo.

 

 

 

1.3.3. MAADILI YA KIBINADAMU

 

Ili tuzielewe taratibu za muundo wa Kiroho, ni muhimu tujue vizuri maadili ya kibinadamu, yaliyo chini ya yale ya Kimungu. Jina linavyosema, ya kwanza yanapatikana kwa kurudiarudia vitendo vyake; yalijulikana na wapagani pia kwa kuwa yana lengo linalojulikana na akili.

Baadhi ya watu waliojitoa kwa Mungu hawajali vya kutosha maadili hayo katika ujana wao; kinyume chake wengine wenye umri mkubwa zaidi, kisha kutambua umuhimu wa maadili hayo hawajali tena vya kutosha maadili ya Kimungu, ambayo ni bora pasipo mfano, kwa kuwa ndiyo yanayotuunganisha na Mungu.

Basi tupande ngazi kwa ngazi kutoka uadilifu wa kimaumbile hadi ule unaopita maumbile. Tuangalie kwanza mtu mwenye dhambi ya mauti anavyoweza kuwa na maadili ya uongo, k.mf. kiasi cha mchoyo; yeye anakitekeleza si kwa kupenda uadilifu, bali kwa kupenda fedha. Vilevile akilipa madeni si kwa kutekeleza haki bali kwa kukwepa gharama za kesi.

Juu kuliko hayo maadili ya uongo, mtu mwenye dhambi ya mauti anaweza kuwa na maadili halisi ya kibinadamu aliyojipatia. Wako wengi wanaofuata kiasi ili kuishi akili inavyotaka, na kwa ajili hiyohiyo wanalipa madeni na kuwalea vizuri watoto wao.

Lakini mpaka mtu anapozidi kubaki katika dhambi ya mauti, hayo maadili halisi hayana msimamo, kwa kuwa utashi wake haumuelekei Mungu: badala ya kumpenda kupita yote, anajipenda kuliko Mungu. Ndiyo sababu ni dhaifu katika kutekeleza uadilifu, hata ule wa kibinadamu. Zaidi ya hayo, maadili halisi yanayopatikana katika mtu mwenye dhambi si imara kwa kuwa maadili mengine yanayotakiwa kuyasaidia hayapo, hivyo hayawezi kushikamana. Anayeendesha gari la kukokotwa na farasi kadhaa, anahitaji kila mmoja wao awe amezoea kazi hiyo: vilevile adili moja haliwezi kwenda bila ya lingine; yote yanahusiana na kuongozwa na busara.

Basi, ili maadili ya kibinadamu yawe imara ni lazima yashikamane, na hiyo inadai mtu asibaki katika dhambi ya mauti, bali utashi wake ulenge kweli kuishi na Mungu; ni lazima ampende kuliko nafsi yake, jambo ambalo haliwezekani pasipo neema ya utakaso na upendo.

Akipata hayo, hapo maadili yote yanaweza kushikamana na kuwa imara; nayo chini ya upendo yanakuwa chanzo cha matendo yanayostahili uzima wa milele. Maadili ya Kimungu yanatuinua na kuturekebisha kuhusu lengo lipitalo maumbile na kuhusu njia zipitazo maumbile zinazoweza kutufikisha kwenye lengo hilo kuu. Bila ya hayo, maadili ya kibinadamu hayatoshi: kuna tofauti ya dhati kati ya kiasi walichokieleza wapagani na kile cha Kikristo (k.mf. kati ya ufukara wa mwanafalsafa na ule wa Kiinjili), kwa sababu kanuni na lengo ni tofauti : cha kwanza kinataka mtu ale tu kipimo cha wastani ili kufuata akili, kutodhuru afya au kuweza kutumia akili yake vizuri. Kumbe kiasi cha Kikristo kinataka mtu ajipatie chakula ili kuishi kama mtoto wa Mungu, akielekea uzima wa milele unaopita maumbile; hivyo kinadai maisha magumu zaidi; kinadai mtu autese mwili wake “na kuutumikisha” (1Kor. 9:27), kusudi asiwe tu raia mwadilifu wa nchi yake, bali pia mwenyeji “pamoja na watakatifu” na mtu “wa nyumbani mwake Mungu” (Ef. 2:19).

Tofauti hiyohiyo ipo kati ya adili la ibada linalotakiwa kumpatia Muumba heshima anayostahili, na adili la ibada la Mkristo linalomtolea Mungu asili ya neema, sadaka ya misa ipitayo maumbile. Ni tofauti ya ngazi, hivi kwamba aina ya kwanza inaweza kustawi mfululizo kwa kurudiarudia vitendo vyake, lakini bila ya kufikia kiwango kidogo cha aina ya pili iliyoinuliwa na neema ya utakaso. Kinachoongoza maadili hayo mawili yenye jina lilelile moja ni tofauti: upande mmoja ni akili ya binadamu, upande wa pili ni imani iliyomiminwa na Mungu.

Ni malengo mawili tofauti na nia mbili tofauti, ambapo busara haijui nia zipitazo maumbile, ila ikiangaziwa na imani inakuja kuzijua kwa kujua ukuu usio na mipaka wa lengo letu, yaani kumuona Mungu uso kwa uso; hapo inakuja kujua uovu wa dhambi ya mauti, thamani ya neema ya utakaso na ya neema za msaada ambazo ziombwe kila siku, na hazina ya sakramenti zilizowekwa kwa faida yetu.

Vilevile kuna tofauti kubwa kati ya utaratibu ulioelezwa na mwanafalsafa Aristotle na unyenyekevu wa Kikristo unaozitegemea kweli za imani. Kuna tofauti kubwa kati ya ubikira wa wanawake waliokabidhiwa kuchochea daima moto wa miungu, na ule wa Mkristo aliyejiweka wakfu mwili na moyo kwa Mungu ili kumfuata Yesu kikamilifu zaidi.

Upendo unapoturekebisha tulenge uzima wa milele upitao maumbile, unarekebisha maadili pia kuhusu njia zipitazo maumbile za kufikia wokovu. Kumbe katika dhambi ya mauti mtu anajipenda kuliko Mungu na kwa umimi anaelekea kutotimiza wajibu wake wa kiutu pia.

Katika utekelezaji walioendelea Kiroho wanaongozwa zaidi na kwa namna wazi na hiyo nia ipitayo maumbile, kumbe ni nia ya kibinadamu inayozidi kuwaongoza wengine.

Maadili ya kibinadamu yanasimama katikati ya pande mbili tofauti, ambazo mmoja umezidisha na mmoja una upungufu. Kwa mfano, adili la nguvu linatufanya tusimame katikati ya woga (unaokimbia hatari bila ya sababu yenye msingi) na ushupavu (unaotaka kuvunjika kichwa bila ya sababu ya kutosha). Lakini, ebu! hiyo katikati isieleweke vibaya. Wanaopenda anasa na watu vuguvugu wanataka kusimama katikati si kwa kupenda uadilifu, bali kusudi waepe matatizo ya vilema vinavyopingana pande hizo mbili. Hao wanachanganya hiyo katikati na ule wastani ambao haupatikani katikati ya vilema viwili vinavyopingana bali katikati ya njia inayoongoza kutoka uovu kwenda uadilifu. Wastani huo unakimbia uadilifu wa juu ukijisingizia kuwa “pengine yaliyo bora yanazuia yaliyo mema”, ukiwa na maana ya kwamba, eti “mara nyingi au daima yaliyo bora yanazuia yaliyo mema”.

Kumbe hiyo katikati halisi ya uadilifu haisimami tu katikati ya vilema viwili vinavyopingana, bali juu ya hivyo kama kilele. Inainuka juu ya upotovu wa pande hizo mbili tofauti: busara halisi iko juu ya upumbavu na ujanja; ukarimu uko juu ya choyo na ubadhirifu; adili la ibada liko juu ya dharau ya dini na ushirikina.

Tena hiyo katikati ambayo ni pia kilele inaelekea kuinuka pasipo kupotoka upande mmoja wala upande mwingine kadiri uadilifu unavyokua, kwa kufuata kanuni ya juu na lengo la juu.

Hatimaye, tuzingatie kuwa Injili na walimu wa kiroho wanasisitiza baadhi ya maadili ya kibinadamu ambayo yanahusiana zaidi na Mungu na kulingana zaidi na maadili ya Kimungu, nayo ni: ibada na toba (zinazompatia Mungu heshima na malipizi anavyostahili), upole (ukiambatana na subira), usafi kamili (au ubikira) na unyenyekevu ambao ni adili la msingi kwa kuwa unashinda kiburi kilicho chanzo cha dhambi zote. Unyenyekevu ukituinamisha mbele ya Mungu unatuinua juu ya ufinyu wa moyo na juu ya kiburi na kutuelekeza kuzama katika mambo ya Mungu na kuungana naye. “Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu, kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo, nanyi mtapata raha nafsini mwenu” (Math. 11:29). Yesu tu, kwa jinsi alivyojijenga katika ukweli, aliweza kusema juu ya unyenyekevu wake pasipo kuupoteza papohapo.

Maadili ya kibinadamu na yale ya Kimungu ambayo yanayaongoza, ni utendaji wa aina mbalimbali wenye kulingana vizuri ajabu, dhambi nyepesi isipokuja kuvuruga. Ni lazima tukeshe kitu chochote kisije kikaharibu ulinganifu wa muundo huo, kama inavyotokea kwa wale ambao wanadumu katika neema ya utakaso lakini wanajali elimudunia na mafungamano na watu kuliko ustawi wa imani, tumaini na upendo wa Mungu. Halafu haiwezekani kuwa na upendo mkubwa pasipo unyenyekevu mkubwa, kama vile tawi la juu la mti linazidi kwenda juu kadiri mzizi unavyozidi kupenya ardhi.

Sehemu zote za muundo huo wa Kiroho zinakua pamoja kama vidole vitano vya mkono mmoja. Kutokana na mshikamano uliopo maadili yote yanakua pamoja na upendo, lakini hasa maadili ya Kimungu kwa kuwa yale ya kujipatia pengine yanastawi kwa kasi ndogo zaidi yasipofanyiwa mazoezi.

 

 

 

1.3.4. VIPAJI SABA VYA ROHO MTAKATIFU

 

Kusudi tujue kweli muundo wa Kiroho, haitoshi kuyajua maadili. Ni lazima tuseme pia juu ya vipaji saba vya Roho Mtakatifu, pasipo kusahau namna mbalimbali za kupata msaada wa Mungu.

 

 

USHUHUDA WA MAANDIKO MATAKATIFU

 

Ufunuo kuhusu vipaji vya Roho Mtakatifu unapatikana hasa katika dondoo la Isaya 11:2 ambalo linamhusu kwanza Masiha, halafu kwa kumshiriki yeye linawahusu waadilifu wote ambao Yesu aliahidi kuwapelekea Roho Mtakatifu. Maneno yenyewe ni haya: “Roho ya Bwana atakaa juu yake, roho ya hekima na ufahamu, roho ya shauri na uweza, roho ya maarifa na ya kumcha Bwana”. Kipaji cha ibada hakitajwi katika lugha asili ya Kiyahudi, bali katika tafsiri za Septuaginta na Vulgata, na kuanzia karne ya tatu mapokeo yanashika idadi ya vipaji saba. Halafu, Isaya 11:3 kwa Kiyahudi inataja tena “kumcha Bwana”, ambapo katika Agano la Kale “kumcha Bwana” na “ibada” ni maneno mawili yenye maana karibu ileile.

Katika kitabu cha Hekima tunasoma: “Naliomba, nikapewa ufahamu; nalimwita Mungu, nikajiliwa na roho ya Hekima. Naliichagua kuliko fimbo za enzi na viti vya enzi, wala mali sikudhani kuwa ni kitu ikilinganishwa nayo; wala sikuifananisha na kito cha thamani, mradi dhahabu yote ya nchi ni kama mchanga kidogo mbele yake, na fedha itahesabiwa kama udongo. Naliipenda kupita afya njema na uzuri wa sura, hata zaidi ya nuru nikataka kuwa nayo, kwa maana mwangaza wake haufifii kamwe. Na pamoja nayo nikajiliwa na mema yote jamii… ingawa sijajua ya kama yeye ndiye aliyeyazaa… Maana yeye amekuwa hazina kwa wanadamu isiyowaishia; nao wale waitumiao hujipatia urafiki na Mungu… na tangu kizazi hata kizazi huwaingilia roho takatifu, huwafanya wanadamu kuwa rafiki za Mungu na manabii” (Hek. 7:7-11,12,14,27).

Ufunuo wa Agano la Kale umetimilizwa na Mwokozi: “Mkinipenda, mtazishika amri zangu. Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli… anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu… huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia” (Yoh. 14:15-17,26). Yohane, akitaka kuwakinga waamini dhidi ya wazushi akaongeza: “Nanyi mmepakwa mafuta na Yeye aliye Mtakatifu… Nanyi, mafuta yale mliyoyapata kwake yanakaa ndani yenu, wala hamna haja ya mtu kuwafundisha; lakini kama mafuta yake yanavyowafundisha habari za mambo yote, tena ni kweli wala si uongo” (1Yoh. 2:20,27).

Katika Maandiko yapo pia madondoo kuhusu vipaji kimojakimoja.

 

 

MAPOKEO

 

Mababu wa Kanisa waliyafafanua mara nyingi maneno hayo ya Maandiko, na kuanzia karne ya tatu mapokeo yanatamka wazi kuwa vipaji saba vya Roho Mtakatifu vimo ndani ya waadilifu wote. “Hivyo vipaji vya Roho Mtakatifu kwetu ni kama chemchemi ya Kimungu tunapochota ujuzi hai wa amri za maisha ya Kikristo, na kwa njia ya hivyo tunaweza kujua pia kama Roho Mtakatifu anakaa ndani mwetu au la” (Katekisimu ya Mtaguso wa Trento).

Ushuhuda wa Mapokeo kuhusu vipaji saba unapatikana katika liturujia ya Pentekoste, hasa katika sekwensya “Uje Roho Mtakatifu”: “Wape waamini wako, / wenye tumaini kwako, / paji zako zote saba”. Tunaukuta vilevile katika utenzi “Uje Roho Muumbaji”: “Mtoa wa vipaji saba... / tia nuru akilini / na upendo mioyoni”.

Ushuhuda wa Mapokeo ulielezwa vizuri na Leo XIII: “Mwadilifu anayeishi kwa neema ya utakaso na kutenda kwa njia ya maadili kama kwa viungo mbalimbali (vipya), anahitaji kabisa vipaji saba, ambavyo vinaitwa kikamilifu zaidi vipaji vya Roho Mtakatifu. Kwa vipaji hivyo roho ya mtu inainuliwa na kuwezeshwa kutii kwa urahisi na mapema zaidi miangaza na misukumo ya Roho Mtakatifu. Nguvu ya vipaji hivyo ni kubwa hata kumwongoza mtu kwenye utakatifu wa hali juu; vyenyewe ni bora hivi hata vinadumu mbinguni pia, ingawa kwa kiwango cha juu zaidi. Kwa njia yake roho inaongozwa na kuhimizwa kujipatia heri za Kiinjili, ambazo ni maua yanayochanua kwa wakati wake, dalili tangulizi za heri ya milele... Kwa kuwa vipaji ni vikubwa hivyo navyo vinaonyesha wema mkuu wa Roho Mtakatifu kwetu, vinatudai tumuonyeshe heshima na utiifu mkuu kabisa. Tutafikia kwa urahisi hatua hiyo tukijitahidi zaidi na zaidi kumjua, kumpenda na kumuomba... Tunapaswa kumpenda Roho Mtakatifu kwa kuwa ni Mungu... na pia kwa kuwa ni upendo wenyewe, asili, wa milele, kwa sababu hakuna kinachopendeza kuliko upendo... Yeye atatujalia kwa wingi zawadi zake za kimbingu, hasa kwa sababu utovu wa shukrani unafunga mikono ya mfadhili, lakini moyo wa shukrani unaifungua tena... Tunapaswa kumuomba mfululizo na kwa tumaini kubwa atuangaze zaidi na zaidi na kuwasha ndani mwetu moto wa upendo wake, ili kwa kutegemea imani na upendo tutembee kwa ari kuelekea tuzo la milele, kwa kuwa ndiye amana ya urithi wetu”.

 

 

MAELEZO YA MTAKATIFU THOMA WA AKWINO

 

Mwalimu huyo wa Kanisa ametufundisha hasa matatu: 1° kwamba vipaji ni misimamo ya kudumu, lakini tofauti na maadili; 2° kwamba ni vya lazima kwa wokovu; 3° kwamba vinashikamana na upendo na kukua pamoja nao.

1° “Ili kutofautisha vipaji na maadili mbalimbali tunapaswa kufuata lugha ya Biblia inayoviita si vipaji bali roho” ili tuelewe kuwa vinapatikana ndani mwetu kwa uvuvio wa Mungu au msukumo kutoka nje na wa juu wa Roho Mtakatifu. Ni lazima tuzingatie kwamba binadamu anasukumwa na mambo mawili yanayomwongoza: moja limo ndani mwake, yaani akili, lingine liko nje, yaani Mungu. “Inaeleweka mara moja kwamba chombo kinachosukumika kinatakiwa kulingana na kinachokisukuma; na ukamilifu wa kinachosukumika ni urahisi wa kusukumwa na kinachokisukuma. Basi, kadiri hicho cha mwisho kilivyo bora, ni lazima kinachosukumwa kiwe kikamilifu zaidi ili kupokea msukumo wake. Hatimaye ni wazi kwamba maadili ya kibinadamu yanamkamilisha mtu katika kujiongoza kwa akili yake katika maisha ya ndani na ya nje. Basi inahitajika iwemo ndani mwake misukumo ya juu inayomuandaa kusukumwa Kimungu, na namna hizo kamilifu zinaitwa vipaji siyo tu kwa kuwa tunamiminiwa na Mungu, bali pia kwa sababu kwa njia yake mtu anakuja kuweza kupokea mara uvuvio wa Kimungu, alivyosema Isaya: ‘Bwana Mungu amenizibua sikio langu, wala sikuwa mkaidi, wala sikurudi nyuma’ (50:5). Ndiyo sababu wengine wanasema kuwa vipaji vinamkamilisha binadamu vikimuandaa kutenda mambo bora kuliko ya maadili”.

Hapo tunaona kuwa vipaji vya Roho Mtakatifu si matendo wala si misukumo au misaada ya kupita ya neema, bali ni misimamo ya kudumu tunayomiminiwa, inayotuweka tayari kupokea uvuvio wa Mungu, kama vile tanga zinavyowezesha chombo kwenda kwa nguvu ya upepo. Kwa utayari huo wa kupokea misukumo vinatusaidia kutenda mambo yale bora yanayoitwa heri kutokana na ukamilifu wake unaoonyesha kwamba yanategemea vipaji kuliko maadili. Mfano huo ulitolewa na Bwana mwenyewe aliliposema, “Upepo huvuma upendako, na sauti yake waisikia, lakini hujui unakotoka wala unakokwenda; kadhalika na hali yake kila mtu aliyezaliwa kwa Roho” (Yoh. 3:8). Hatujui vizuri upepo unaovuma umetokea wapi na utasikika mpaka wapi; vilevile hatujui vizuri uvuvio wa Kimungu unaanzia wapi, na utatufikishia ngazi gani ya ukamilifu tukiufuata kwa uaminifu moja kwa moja. Tusiwe kama wanamaji ambao kwa uzembe hawatweki tanga wakati wa kufaa.

Wanateolojia wengi wanamuunga mkono mt. Thoma wa Akwino anaposema kuwa vipaji vinatofautiana kweli na maadili ya kumiminiwa, kama vile wanavyotofautiana wanaoviongoza, yaani Roho Mtakatifu na akili iliyoangazwa na imani; hiyo ni miongozo na kanuni tofauti. Utendaji wa kibinadamu unatokana na kanuni ya kibinadamu, utendaji upitao maumbile unatokana na kanuni ya Kimungu, yaani uvuvio wa Roho Mtakatifu. Hata busara iliyoinuliwa na upendo inafanya kazi kwa kuzingatia mafuatano ya mawazo, tofauti na kipaji cha shauri kinachotuandaa kupokea uvuvio maalumu usioyahitaji. Kwa mfano, tukiulizwa swali linalohusu siri fulani, busara inasita kuhusu namna ya kutunza siri hiyo bila ya kusema uongo, kumbe uvuvio maalumu wa Roho Mtakatifu unaondolea wasiwasi (taz. Math. 10:19). Vilevile, imani inaambatana tu na kweli tulizofunuliwa, kumbe kipaji cha akili kinatuwezesha kuona ndani ya vilindi vyake, na kile cha hekima kinatuwezesha kuonja utamu wake. Basi vipaji vinatofautiana na maadili.

Vipaji vya Roho Mtakatifu ni vya lazima kwa wokovu wa milele. “Maana Mungu humpenda yeye tu akaaye na Hekima” (Hek. 7:28). “Miongoni mwa ndugu awatawalaye ana heshima, bali machoni pa Bwana ni wao wamchao” (YbS. 10:20). Sasa kipaji bora ni hekima, na cha mwisho ni uchaji wa Mungu.

Hata maadili ya Kimungu yanajilinganisha na namna ya kibinadamu ya akili na utashi wetu, na hivyo yanatuacha katika hali isiyotosha kwa lengo letu kuu lipitalo maumbile, ambalo tunatakiwa kulijua kwa namna iliyo hai, inayochimba na kuonja, na ambalo tunatakiwa kulilenga kwa ari zaidi.

Imani hata ikiwa kubwa inaendelea kuwa na upungufu kwa sababu tatu za msingi: 1) kwa kuwa yale inayoyaamini ni giza, nayo haiyafikii moja kwa moja, ila inayona “kwa kioo kwa jinsi ya fumbo” (1Kor. 13:12); 2) inayafikia kwa njia ya matamko rasmi mbalimbali ya Kanisa, kumbe umoja wa Mungu haugawanyiki; 3) inayafikia kinadharia, kwa kukiri na kukanusha maneno fulanifulani, kumbe Mungu aliye hai ni mwanga wa uzima ambaye anatakiwa kujulikana kama kwa mang'amuzi.

Tumaini linashiriki upungufu wa imani, na vilevile upendo, kwa kuwa imani ndiyo inayoupatia la kupenda. Zaidi tena busara ina upungufu, kwa kuwa inahitaji kufuata mawazo, kutafuta sababu za kutenda, ili kuelekeza maadili ya kibinadamu; mara nyingi inasita isijue la kufanya, ila unahitajika mwanga kutoka juu, k.mf. ili kushinda vishawishi kadhaa visivyotambulikana, au vikali na vya muda mrefu.

“Akili ya binadamu, hata baada ya kukamilishwa na maadili ya Kimungu, haiwezi kujua yale yote inayohitaji kuyajua, wala haiwezi kuepuka kila upotovu. Mungu tu aliye na ujuzi wote na uwezo wote anaweza kufidia ujinga na upumbavu wetu, ugumu wa moyo na kasoro nyingine za namna hiyo. Ni kwa ajili ya kutuondolea kasoro hizo kwamba tumejaliwa vipaji vya Roho Mtakatifu, vinavyotuwezesha kupokea vizuri uvuvio wa Kimungu”. Ndiyo maana vipaji ni vya lazima kwa wokovu wetu. “Kwa njia ya maadili ya Kimungu na ya kibinadamu, mtu hajakamilika kuhusu lengo lake kuu linalopita maumbile asihitaji daima kusukumwa na Roho Mtakatifu kutoka juu”. Kwake haja hiyo ni ya kudumu, ndio sababu vipaji ni misimamo ya kudumu tunayomiminiwa.

Sisi tunatumia vipaji kwa mfano wa adili la utiifu, ili kupokea vizuri agizo kutoka juu, na kutenda kulingana nalo, lakini hatuwezi kuwa na uvuvio huo kila tunapotaka. Upande huo vipaji vinatufanya tusiweze kutenda wenyewe, ila kwa msukumo wa Roho Mtakatifu. Hivyo ni wazi zaidi kuwa vipaji, kama vile utiifu, ni misimamo ya kudumu ya mwadilifu.

Tunaweza kuona vizuri zaidi tunavyohitaji vipaji hivyo, tukizingatia jinsi kila kimoja kinavyokamilisha akili au utashi na hisi:

                                                                                                                                KIPAJI               ADILI

                                                            ili kupenya ukweli                                akili                     imani

akili iliyoangazwa na imani                                           mambo ya Mungu  hekima             upendo

           ili kuamua kuhusu  mambo yetu           shauri                busara

Vipaji vinakamilisha                                                                           malimwengu          elimu               tumaini

 

                                                                   ili tumuabudu Mungu ipasavyo            ibada                   ibada

                       utashi na hisi                       ili tusiogope hatari                                nguvu                 nguvu

                                                                   ili tushinde tamaa mbaya                      uchaji                   kiasi

 

3° Hatimaye, kwa kuwa vipaji ni vya lazima kwa wokovu, basi vinahusiana na upendo. Roho Mtakatifu haji ndani mwetu pasipo vipaji vyake saba, vinavyoendana na upendo na kwa hiyo vinapotezwa pamoja na upendo kwa dhambi yoyote ya mauti.

Basi, vipaji ni sehemu ya muundo wa Kiroho wa neema ya utakaso; ndiyo maana hiyo inaitwa “neema ya maadili na vipaji”. Kame vile maadili ya kumiminiwa yanavyokua pamoja kwa mfano wa vidole vya mkono, vipaji pia vinakua pamoja. Hakuna mwenye kiwango kikubwa cha upendo wa Mungu, inavyotakiwa na ukamilifu, asiye na vipaji vya Roho Mtakatifu kwa kiwango hichohicho.

Tutazungumzia mbele usikivu kwa Roho Mtakatifu, lakini tangu sasa tunaona thamani ya huo muundo wa Kiroho ambao ni chanzo cha uzima wa milele: ni thamani kubwa kuliko ile ya macho, ya afya, na ya akili kwa maana mwadilifu akipotewa na akili hapotewi na hazina hiyo ambayo kifo chenyewe hakiwezi kumnyang'anya. Neema ya maaadili na vipaji ina thamani kubwa kuliko karama (za kufanya miujiza, kutabiri n.k) kwa kuwa hizo ni alama za nje tu ambazo zinaweza kuelekeza njia ya kumfikia Mungu, lakini haziwezi kutuunganisha naye inavyofanya neema ya utakaso.

Ili tuone vizuri zaidi utendaji wa muundo huo wa Kiroho, inatupasa bado tuseme juu ya neema za msaada zinazohitajika ili kutekeleza maadili na vipaji.

 

 

 

1.3.5. NEEMA ZA MSAADA NA AINA ZAKE

 

 

HAJA YA NEEMA ZA MSAADA

 

Hakuna kiumbe kinachotenda pasipo nguvu ya Mungu, aliye chanzo cha utendaji wote wa miili na wa roho: “Kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu” (Mdo 17:28). Zaidi upande wa maisha yapitayo maumbile, ili tutende kadiri ya maadili ya kumiminiwa na ya vipaji, tunahitaji msukumo wa Kimungu unaoitwa neema ya msaada.

Ni ukweli wa imani kwamba pasipo neema hiyo hatuwezi kujiandaa kuongoka, wala kudumu muda mrefu katika kutenda mema, wala hasa kudumu katika neema ya utakaso mpaka kufa. Pasipo neema ya msaada hatuwezi kuzaa tendo lolote (hata dogo) linalostahili wokovu, wala zaidi hatuwezi kuufikia ukamilifu. Kwa maana hiyo Yesu alisema, “Pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lolote”(Yoh. 15:5). “Si kwamba twatosha sisi wenyewe kufikiri neno lolote kwamba ni letu wenyewe, bali utoshelevu wetu watoka kwa Mungu” (2Kor. 3:5). “Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, kutaka kwenu na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema” (Fil. 2:13), akisukuma hiari yetu bila ya kuilazimisha. Ndiye anayetujalia kujiandaa kupokea neema ya utakaso na halafu kustahili uzima wa milele.

Ndiyo sababu tunapaswa kusali daima. Haja ya kusali inatokana na haja ya kupata neema za msaada. Mbali na neema ya kwanza tunayojaliwa bure pasipo sisi kuomba (kwa kuwa ndio chanzo chenyewe cha sala), sala ndiyo njia ya kawaida, ya hakika na ya jumla ambayo Mungu anataka tupate neema tunazozihitaji. Ndiyo sababu Bwana wetu ametusisitizia: “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea, naye atafutaye huona, naye abishaye atafunguliwa” (Mt. 7:7-8). Kuna haja hiyo hasa katika kishawishi: “Kesheni, mwombe, msije mkaingia majaribuni; roho i radhi, lakini mwili ni dhaifu” (Math. 26:41). Tunaposali tunapaswa kuamini kuwa Mungu ndiye asili ya mema yote, kwa hiyo tegemeo lolote lisilo na msingi katika sala ni la kipumbavu tu.

Mungu haagizi kamwe yasiyowezekana, bali akiagiza anatuambia tufanye tunayoyaweza, tuombe tusiyoyaweza, naye mwenyewe anatusaidia ili tuweze” (Mtaguso wa Trento), tena kwa neema ya msaada anatusaidia kusali pia. Kuna neema kadhaa tusizoweza kuzipata isipokuwa kwa kusali. Haitatosha kamwe kusisitiza jambo hilo, kwa kuwa wengi mwanzoni wamejaa mawazo ya kibinadamu tu wakidhani inawezekana kufanya lolote kwa utashi na bidii, pasipo neema za msaada. Lakini watang'amua mapema ukweli wa maneno ya Yesu na ya mt. Paulo tuliyodondoa. Basi tunapaswa kuomba neema za msaada ili tushike vizuri zaidi na zaidi amri za Mungu, hasa ile kuu ya upendo.

 
 
AINA ZA NEEMA ZA MSAADA

 

Neema za msaada zina namna nyingi tofauti ambazo inafaa kuzijua, kwa kukumbushwa wazi iwezekanavyo kweli kadhaa ambazo ni za hakika, ingawa zinatokeza fumbo mojawapo la imani ambalo kuliko mengine mengi lina mchanganyiko wa mwanga na giza kwetu.

Mara nyingi tunapewa neema ya mwanga, yaani tunaangaziwa kwa ndani; k.mf. wakati wa masomo ya misa tunaangazwa kuelewa maana yake. Hiyo inafuatwa na neema ya mvutio, yaani tunavutiwa na tendo fulani, k.mf. katika kuzingatia upendo wa Mwokozi kwetu, tunajisikia kumrudishia upendo. Neema ya msaada ya namna hiyo inatenda katika utashi na kuusukuma upendo utende, hata kujitoa kwa Mungu, tayari kupokea mateso yoyote na kufa kwa ajili yake ikiwa ni lazima. Hapo si neema ya mvutio tu, bali neema ya ushujaa ambayo mara nyingi tunaipokea pasipo kuing'amua, lakini inatuwezesha kustahimili ukavu wa roho. Kati ya neema hizo, nyingi hazitambulikani na yule anayezipokea, kwa kuwa zinapita maumbile, hivyo zinapita njia zetu za kujua mambo.

Neema ya msaada inayogusa utashi inaweza kuwa na sauti kuhusu matakwa yake kwa namna mbili: kwa kuupendekezea jambo ambalo liuvutie, na kwa kuusukuma kwa ndani. Bila ya shaka Mungu anaweza kuelekeza utashi wetu upande wa uadilifu kwa kuupendekezea jambo fulani, k.mf. ahadi ya heri ya milele, au ustawi wa upendo. Ndivyo mama anavyomvuta mtoto wake atende mema kwa kumpendekezea jambo la kuvutia au kwa kumshauri. Hata malaika mlinzi anaweza kufanya hivyo kwa kututia mawazo mazuri.

Lakini kitu ambacho Mungu tu anaweza kukifanya ni kuusukuma kwa ndani utashi wetu utende mema. Mungu yumo ndani mwetu kuliko nafsi yetu, ndiye anayedumisha roho yetu, pamoja na akili na utashi alivyoviumba; ndiyo sababu anaweza kuvisukuma kwa ndani, kadiri ya maelekeo ya kimaumbile viliyonayo, pasipo kuvilazimisha, ila kwa kuvipa nguvu mpya. Kwa mfano, mama akitaka kumfundisha mtoto kutembea anamsaidia sio tu kwa sauti huku akimuonyesha kitu ambacho akifikie, bali pia kwa mikono akimuinua. Mungu anaweza kufanya hivyo upande wa roho, akiinua utashi wetu ufikie uadilifu. Ndiye Muumba wa utashi wetu; ameupa elekeo la ndani la kulenga uadilifu, naye peke yake anaweza kuusukuma kwa ndani kadiri ya elekeo hilo. Ndivyo anavyotenda kazi ndani mwetu akitufanya tutake na kutenda. Naye atafanya hivyo kadiri tutakavyomuomba kwa ukakamavu atustawishie upendo tunaopaswa kuwa nao kwake.

Neema ya msaada inaitwa ya kutangulia ikisababisha ndani mwetu wazo jema au mguso mwema, kabla hatujafanya lolote la kusababisha kitu hicho. Tusipoikaidi Mungu anatuongezea neema ya kuchangia itakayousaidia utashi wetu kutekeleza tendo linalohitajika ili kutimiza mpango wetu mzuri.

Halafu inafaa kutambua kwamba Mungu anatusukuma, mara kutenda kufuatana na uamuzi tulioukata kwa utaratibu wa kibinadamu, mara kutenda kwa uvuvio maalumu kutoka juu, bila ya sisi kukata shauri kwa utaratibu huo wa kawaida. Mfano wa namna ya kwanza ni pale ninapoamua kwenda kusali rozari saa niliyozoea kufanya hivyo; hapo natenda kwa neema ya msaada ya kawaida inayoitwa ya kushiriki tendo kwa kuwa inashirikiana nami katika kutenda kwa namna ya kibinadamu ya kuamua. Mfano wa namna ya pili ni pale ambapo ghafla, wakati wa kazi nzito, najisikia uvuvio maalumu wa kusali kidogo, nami nafanya hivyo mara: neema hiyo inaitwa ya kutenda, kwa kuwa inatenda ndani mwangu pasipo mimi kukata shauri, ingawa sio pasipo kukubali mwenyewe kwa hiari na kwa kustahili tuzo.

Kwa namna ya kwanza Mungu anatusukuma kwa kawaida kutenda namna ya kibinadamu ya maadili. Kwa namna ya pili anatusukuma kutenda namna inayopita utu ya vipaji vya Roho Mtakatifu: hapo chombo chetu kinakwenda sio tu kwa kasia, bali kwa msukumo wa upepo, tunatendewa kuliko kutenda wenyewe. Hapo kazi yetu hasa ni kukubali ile ya Mungu, kuacha Roho Mtakatifu atuongoze, kufuata mara na kwa juhudi uvuvio wake wowote. Lakini hata tukiwa na neema ya kushiriki tendo tu, kila tendo letu linalostahili tuzo ni lote la Mungu kama asili kuu, na lote la kwetu kama asili ya pili.

 

 

UAMINIFU KWA NEEMA

 

Ni muhimu tuwe waaminifu kwa neema, tena kuwa waaminifu zaidi na zaidi kwa neema ya msaada ya sasa hivi, ili tutimize wajibu wa dakika hiyo unaotudhihirishia matakwa ya Mungu kwetu. Tukumbuke maneno ya mt. Augustino, “Aliyekuumba bila yako, hatakufanya mwadilifu bila yako” kwa kuwa ni lazima ukubali na kuzitii amri. Yeye aliongeza kuwa tunapewa msaada wa Mungu si kusudi utashi wetu usifanye chochote, bali kusudi utende kwa kustahili wokovu.

Mungu anatutolea mfululizo neema za msaada ili tutimize wajibu wa sasa hivi, kama vile hewa inavyoyafikia mapafu yetu tuweze kupumua kila sasa. Kama tunavyotakiwa kuingiza hewa inayosafisha damu, tunatakiwa pia kupokea kwa mikono miwili neema inayozifanya mpya nguvu zetu za Kiroho ili tumuelekee Mungu. Kama vile asiyepumua anakufa, vivyo hivyo roho isiyopokea neema inakufa kwa kukosa hewa yake.

“Nasi tukitenda kazi pamoja naye twawasihi msiipokee neema ya Mungu bure”(2Kor. 6:1). Tunapaswa kuiitikia na kushirikiana nayo kwa bidii. Ndio ukweli mwepesi ambao tukiutekeleza siku hadi siku unatufikisha kwenye utakatifu.

Kwa hakika Mungu ndiye wa kwanza kupiga hatua kwetu kwa neema ya kutangulia; halafu anatusaidia kuikubali. Anatuongoza katika njia zetu zote hadi saa ya kufa.

Upande wetu tunapaswa kuwa waaminifu. Namna gani? Mosi kwa kupokea kwa furaha mianga ya kwanzakwanza ya neema; halafu kwa kufuata kwa makini yale inayotuambia; hatimaye kwa kufanya juu chini kuyatekeleza, bila ya kujali gharama. Hapo tutashiriki kazi ya Mungu, na utendaji wetu utakuwa tunda la neema yake na papohapo la hiari yetu.

Neema ya kwanza inayotuangaza kwa kusababisha wazo jema ndani mwetu inatosha kufanya utashi ukubali kutenda kwa adilifu, kwa maana inatupa uwezo wa kulitenda. Lakini tukikaidi wazo hilo tunajinyima neema ya msaada ambayo ingesababisha kwa hakika tulikubali. Ukaidi unaangukia neema ya kutosha kama vile mvua ya mawe inavyonyeshea maua yanayotarajiwa kuzaa matunda mengi: maua yanaangamizwa na hivyo matunda hayatazaliwa kamwe. Neema ya hakika inatolewa kwetu katika ile ya kutosha kama tunda katika ua; ni lazima tusiangamize ua ili tupate tunda. Tusipoikaidi neema ya kutosha tutapewa ile ya hakika na kwa njia yake tutaendelea bila ya wasiwasi katika njia ya wokovu. Hivyo neema ya kutosha inatufanya tusiweze kujisingizia, na ile ya hakika haituruhusu tujivunie; kwa njia yake tunasonga mbele kwa unyenyekevu na juhudi.

Ndilo fumbo la neema ambalo mwanga wake umo katika kweli mbili, wakati giza lake limo katika namna ya kuzilinganisha. Upande mmoja Mungu haagizi kamwe yasiyowezekana (angekuwa hana haki wala huruma), bali kwa upendo anawawezesha kweli wote watimize wajibu wao. Hakuna mtu mzima anayenyimwa neema ya lazima kwa wokovu asipoikataa kwa kukaidi mwaliko wa Mungu. Upande mwingine, “kwa kuwa upendo wa Mungu kwetu ni asili ya mema yote, hakuna mtu anayeweza kuwa mwema kuliko mwingine asipopendwa zaidi na Mungu” (mt. Thoma wa Akwino). Kwa maana hiyo Yesu alisema kuhusu wateule: “Hakuna mtu awezaye kuwapokonya katika mkono wa Baba yangu” (Yoh. 10:29). “Ikiwa baadhi wanaokolewa ni kwa zawadi ya Mwokozi: ikiwa wengine wanapotea ni kwa kosa lao” (Mtaguso wa Quiercy wa mwaka 853). Kukaidi neema ni ovu linalotokana na sisi wenyewe tu. Kutoikaidi kwenyewe ni jema linalotokana na Mungu, chemchemi ya mema yote. Maneno hayo ndiyo sura mbili za fumbo lilelile; kila moja ni la hakika, kama lile la kwamba wote wanaweza kuokoka, na lile la kwamba hakuna aliye bora kuliko mwenzake isipokuwa kwa sababu amependwa zaidi na Mungu. Lakini hayo mawili yanawezaje kulingana? Hakuna kiumbe anayeweza kuona ulinganifu huo kabla haijakaribishwa kumuona Mungu mbinguni, kwa sababu ni sawa na kuona jinsi haki isiyo na mipaka, huruma isiyo na mipaka, na hiari yake kuu zinavyolingana katika ubora wa Umungu.

Tusikatae ukarimu wa Mungu ambaye ametujalia neema ya utakaso, maadili ya kumiminiwa na vipaji, tena kila siku anatuvuta kwake. Tusiridhike na maisha ya wastani na kuzaa matunda yasiyoiva, wakati Mwokozi wetu mwema alisema, “Mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele” (Yoh. 10:10) hadi kufurahia milele heri yake. Mungu ana moyo mkuu, basi tuwe nao sisi pia.

Uaminifu huo unahitajika kwanza ili kutunza uzima wa neema, na kukwepa dhambi ya mauti. Uzima huo una thamani kubwa pasipo kifani, hata Mwokozi alikabili kifo ili kuturudishia. Tungejaliwa kuona wazi mng'ao wa ajabu wa neema ya utakaso, tungejisahau. Uaminifu unahitajika pia ili tustahili na kupata ustawi wa uzima huo ndani mwetu, unaotakiwa kukua mpaka tutakapoingia mbinguni, kwa sababu tunapohiji kuelekea umilele hatuwezi kusonga mbele isipokuwa kwa kukua katika upendo wa Mungu.

Kwa hiyo tunahitaji kutakasa matendo yetu yote, hata la kawaida zaidi, tukiyatenda kwa nia safi na kwa lengo lipitalo maumbile. Tungekuwa waaminifu toka asubuhi hadi jioni, siku zetu zingejaa na kufurika matendo ya upendo kwa Mungu na kwa jirani, katika nafasi yoyote, ya furaha na ya uchungu, na kufikia jioni muungano wetu na Mungu ungekuwa wa ndani na imara zaidi. Kwa watu wowote hakuna njia rahisi na ya hakika ya kupata utakatifu kuliko ile ya kuinua kila tendo juu kuliko maumbile, kwa kumtolea Mungu pamoja na Yesu, kwa utukufu wake na kwa wokovu wa watu.

 

 

 

 

1.4. UWEMO WA UTATU MTAKATIFU NDANI MWETU

KAMA CHEMCHEMI ISIYOUMBWA YA MAISHA YA KIROHO

 

 

Sasa inafaa tuzingatie chemchemi isiyoumbwa ya maisha yetu ya Kiroho, yaani Utatu mtakatifu uliomo ndani ya waadilifu wote wa duniani, toharani na mbinguni.

 

 

USHUHUDA WA MAANDIKO MATAKATIFU

 

Maandiko yanatufundisha kuwa Mungu yumo katika viumbe vyote kwa namna fulani inayotokana na hali yake ya kutokuwa na mipaka: “Niende wapi nijiepushe na roho yako? Niende wapi niukimbie uso wako? Kama ningepanda mbinguni, Wewe uko; ningefanya kuzimu kitanda changu, Wewe uko” (Zab. 139:7-8). “Mungu aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, yeye, kwa kuwa ni Bwana wa mbingu na nchi… hawi mbali na kila mmoja wetu. Kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu” (Mdo. 17:24-28). Kwa hakika, Mungu anaona vyote, anadumisha vyote, na kukiongoza kila kiumbe kitende inavyokifaa.

Lakini Maandiko yanasema pia juu ya uwemo wa pekee wa Mungu katika waadilifu. “Mtu akinipenda, atalishika neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake” (Yoh. 14:23). Nani atakuja? Mambo yaliyoumbwa tu, kama vile neema ya utakaso, maadili ya kumiminiwa na vipaji vya Roho Mtakatifu? Hapana, watakaokuja ni walewale wanaopenda, Baba na Mwana wasiotenganika na Roho Mtakatifu, ambaye Bwana alimuahidi na kumtuma wazi kwenye Pentekoste: “Mkinipenda, mtazishika amri zangu. Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele… Ndiye Roho wa kweli… anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu…” (Yoh. 14:15-17). Hao watakuja si kwa muda, bali watafanya makao yao ndani ya mwadilifu mpaka atakapodumu katika upendo.

Maneno hayo hayakuwahusu mitume tu: “Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake” (1Yoh. 4:8). Huyo anaye Mungu moyoni mwake, lakini hasa Mungu anaye huyo ndani mwake akimdumishia sio tu uhai wa kimaumbile, bali pia ule mpya wa neema na upendo.

“Pendo la Mungu limekwisha kumiminwa katika mioyo yetu na Roho Mtakatifu tuliyepewa sisi” (Rom. 5:5). Hatukujaliwa tu upendo ulioumbwa, bali Roho Mtakatifu mwenyewe, aliye Upendo-Nafsi. Hao wamo ndani mwetu, lakini tutafananishwa nao kikamilifu kwa kupokea tu mwanga wa utukufu.

“Hamjui ya kuwa ninyi mmekuwa hekalu la Mungu, na ya kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu?... Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe” (1Kor. 3:16; 6:19). Hivyo Maandiko yanafundisha wazi kuwa Nafsi tatu za Mungu zinaishi katika waadilifu wote.

 

 

USHUHUDA WA MAPOKEO

 

Mwanzoni mwa karne ya pili, mt. Inyasi wa Antiokia aliwaita Wakristo halisi “theophoroi” (= waleta Mungu) kwa kuwa wana Mungu ndani mwao. Mt. Lusia alikiri ukweli huo mbele ya mahakimu: “Ndio, wale wote wanaoishi kwa usafi na imani ni mahekalu ya Roho Mtakatifu”. Mt. Atanasi alisema kuwa Nafsi tatu za Mungu zimo ndani mwetu. Mt. Bazili alitamka kuwa Roho Mtakatifu kwa kukaa ndani mwetu anatufanya tuwe watu wa Kiroho zaidi na kufanana na Mwana Pekee. Mt. Sirili wa Aleksandria pia alisema juu ya muungano huo wa ndani kati ya mwadilifu na Roho Mtakatifu. Upande wa Magharibi, mt. Ambrosi alifundisha kuwa tumempata katika ubatizo tena zaidi katika kipaimara. Mt. Augustino alithibitisha kwa shuhuda za mababu waliomtangulia kwamba hatupewi neema tu, bali tunajaliwa Mungu mwenyewe, yaani Roho Mtakatifu na vipaji vyake saba.

Ukweli huo uliofunuliwa unawekwa tena machoni petu na Ualimu wa Kanisa. Mtaguso wa Trento ulisema: “Anayetufanya waadilifu ni Mungu ambaye kwa huruma yake anatutakasa bure na kutufanya watakatifu, akitupaka mafuta na kututia muhuri wa Roho Mtakatifu tuliyeahidiwa ambaye ni dhamana ya urithi wetu (taz. Ef. 1:13-14)”. Leo XIII alifafanua zaidi: “Inafaa sana kukumbuka maelezo yaliyotolewa na walimu wa Kanisa kadiri ya mafundisho ya Maandiko matakatifu: Mungu yumo katika vitu vyote kwa uwezo wake, kwa sababu vyote viko chini yake; halafu kwa uwepo wake, kwa sababu vyote viko wazi mbele yake; tena kwa undani wake, kwa sababu yumo ndani ya viumbe vyote kama chanzo cha uwepo wao. Lakini katika binadamu Mungu hayumo tu kwa namna ile ambayo yumo katika vitu vyote, bali zaidi kwa kujulikana na kupendwa naye, kwa sababu maumbile yetu wenyewe yanatufanya tupende, na kutamani na kufuata yaliyo mema. Kwa neema yake Mungu anakaa katika roho adilifu kama hekaluni kwa namna ya ndani na ya pekee kabisa. Ndipo kinapotokea kile kiungo cha upendo kinachofungamanisha roho na Mungu kuliko mtu na rafiki yake mkuu na kinachoifanya imfurahie kwa ukamilifu wote. Muungano huo wa ajabu, unaoitwa uwemo ndani na unaotofautiana na hali ya wenye heri wa mbinguni kwa namna yake tu, unasababishwa kwa ukweli wote na uwemo wa Utatu mzima: ‘tutakuja kwake, na kufanya makao kwake’ (Yoh. 14:23). Hata hivyo unasemwa kuwa ni hasa kazi ya Roho Mtakatifu, kwa kuwa tunaona alama za uwezo na za hekima ya Mungu hata katika mtu mwovu, lakini mwadilifu tu anashiriki upendo, ambao ni sifa ya Roho Mtakatifu... Wingi wa mema ya kimbingu unaosababishwa na uwemo wa Roho Mtakatifu katika roho adilifu unajitokeza kwa namna mbalimbali... Kati ya zawadi hizo zimo tahadhari za siri, na mialiko ya kifumbo ambavyo roho zinajaliwa kwa njia ya Roho Mtakatifu, na ambavyo visipokuwepo hatuwezi kujitahidi katika maadili, wala kuendelea, wala kufikia wokovu wa milele”.

 

 

UFAFANUZI WA TEOLOJIA KUHUSU FUMBO HILO

 

“Mbali ya neema ya utakaso hakuna lingine linaloweza kuangaza jambo hilo, kwamba Nafsi ya Kimungu iwemo ndani mwetu kwa namna mpya... Halafu, ili tuwe nalo ni lazima tuweze kulifurahia na kulitumia. Sasa hatuwezi kufurahia Nafsi ya Kimungu isipokuwa kwa neema ya utakaso na upendo” (mt. Thoma wa Akwino).

Ni kwamba pasipo hayo Mungu hakai ndani mwetu. Haitoshi kumjua kimaumbile (kifalsafa), wala kwa imani iliyokufa (anavyomjua mwamini mwenye dhambi ya mauti). Ni lazima tumjue kwa imani hai na vipaji vya Roho Mtakatifu vinavyohusiana na upendo. Hiyo namna ya mwisho ya kumjua Mungu inampata si kama jambo la mbali lililochorwa tu kwetu, bali kama jambo lililopo, tulilonalo na ambalo tunaweza kulifurahia tangu sasa. Ili Nafsi za Kimungu zikae ndani mwetu, inatakiwa tuweze kuzifahamu kama kwa mang'amuzi ya kimapenzi, ambayo msingi wake ni upendo tuliomiminiwa unaotulinganisha na maisha ya ndani ya Mungu.

Lakini ili Utatu mtakatifu ukae ndani mwetu si lazima tumjue hivyo kila sasa; inatosha tuweze kufanya hivyo kwa njia ya neema ya maadili na vipaji. Basi uwemo wa Utatu mtakatifu unadumu katika mtu mwadilifu hata usingizini mpaka atakapodumu katika neema ya utakaso. Ila mara mojamoja inatokea kuwa Mungu anatambulikana nasi kama kiini cha roho yetu, kama uhai wa maisha yetu, alivyosema mt. Paulo: “Mlipokea roho ya kufanywa wana, ambayo kwa hiyo twalia, ‘Aba!’ yaani, ‘Baba!’ Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu” (Rom. 8:15-16). Mt. Thoma wa Akwino alifafanua: “Roho Mtakatifu anathibitishia roho yetu kwa kusababisha ndani mwetu upendo kama wa mwana kwa Baba”. Upendo huo ni ishara inayotuwezesha kuwa na hakika fulani ya kwamba tuna neema ya utakaso.

Kufuatana na mafundisho hayo, Utatu mtakatifu unakaa katika roho adilifu vizuri kuliko mwili wa Mwokozi unavyokaa katika umbo la mkate lililogeuzwa, walau kwa namna fulani. Yaani Yesu yumo kweli katika maumbo ya ekaristi, lakini hayo hayamjui wala hayampendi. Kumbe Utatu mtakatifu umo ndani ya mwadilifu kama katika hekalu hai linaloujua na kuupenda (kwa kiasi tofautitofauti). Umo katika wenye heri wa mbinguni wanaoutazama moja kwa moja, hasa katika roho takatifu ya Mwokozi ambayo Neno ameungana nayo katika Nafsi moja. Kuanzia dunia hii, katika mwanga/giza la imani, Utatu mtakatifu unakaa ndani mwetu, ingawa hatuuoni, ukitustawishia uhai zaidi na zaidi hadi saa ya kuingia katika utukufu.

Uwemo huo wa Roho Mtakatifu hautuondolei haja ya kukaribia ekaristi, kwa kuwa Utatu mtakatifu unakaa ndani ya Kristo kuliko unavyokaa ndani mwetu. Ikiwa tunafaidika na kumkaribia mtakatifu wa Mungu, jinsi gani tutafaidika tukimkaribia Mwanae!

 

 

YATOKANAYO KWA MAISHA YA KIROHO

 

Ikiwa uwemo wa Utatu mtakatifu ndani mwetu unatuwezesha kumjua Mungu kama kwa mang'amuzi, maana yake ujuzi huo si jambo la pekee (kama njozi) bali lipo katika njia ya kawaida ya utakatifu. Ujuzi huo unatokana na imani iliyoangazwa na vipaji vinavyohusiana na upendo. Kama ni hivyo, basi, kwa kawaida unatakiwa kustawi kadiri upendo unavyostawi. Tutaona kuwa sala ya kumiminiwa, ambayo ni kuchanua kwa aina hiyo ya ujuzi/mang'amuzi, inaanza katika hatua ya mwanga na kukamilika katika hatua ya muungano. Ujuzi huo wa Mungu na wa wema wake utakua pamoja na ule wa unyonge wetu.

Jambo lingine linalotokana na hayo tuliyosema ni kwamba upendo uliomo ndani mwetu unapostawi sana, nafsi za Kimungu zinakuwemo mwetu kwa undani zaidi, yaani kirafiki zaidi. Ndivyo inavyotokea k.mf. wakati wa uongofu wa pili ambao ni mwanzo wa hatua ya mwanga.

Hatimaye hao Watatu wamo ndani mwetu sio tu kusudi tuwafahamu na kuwapenda kwa namna ipitayo maumbile, bali wamo kama asili ya vitendo vinavyopita maumbile, kama Yesu alivyosema, “Baba yangu anatenda kazi hata sasa, nami ninatenda kazi” (Yoh. 5:17), hasa katika kiini cha roho.

Lakini kiutendaji ni lazima tukumbuke kwamba kwa kawaida Mungu anajitoa kwa kiumbe chake kadiri hicho kilivyo tayari kumpokea. Mtu akiwa safi zaidi, ndani mwake Nafsi za Kimungu zinakuwemo na kufanya kazi zaidi. Hapo Mungu ni wetu nasi ni wake, na tunatamani kuliko yote tuendelee katika upendo wake. “Hilo ni mojawapo kati ya mambo yanayotusukuma zaidi kuendelea Kiroho, kwa sababu linaifanya roho iwe daima na juhudi kwa maendeleo yake, iwe macho ili kuzaa mfululizo vitendo vyenye nguvu na motomoto zaidi na zaidi kuhusu maadili yote, ili kwa kukua katika neema, ustawi huo umlete upya Mungu ndani mwake… kwa ajili ya muungano wa ndani zaidi, wa kudumu zaidi na imara zaidi” (L. Chardon).

 

 

TUNA WAJIBU GANI KWA MGENI WETU WA KIMUNGU?

 

Mgeni huyo anatuambia: “Mwanangu, nipe moyo wako” (Mith. 23:26). “Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu akiisikia sauti yangu, na kuufungua mlango, nitaingia kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami” (Ufu. 3:20). Roho ya mwadilifu inafanana na mbingu, kwa sababu Utatu mtakatifu umo ndani mwake, lakini bado kuna giza, na siku fulani tu itajaliwa kuuona waziwazi ndani mwake.

Kwa kifupi wajibu wetu kwake ni kama ifuatavyo: kumfikiria mara nyingi, kwa kujiambia, “Mungu anaishi ndani mwangu”. Kumwekea wakfu siku zetu, tena kila saa, kwa kusema: “Kwa jina la Baba, na la Mwana na la Roho Mtakatifu”. Kukumbuka kwamba kwetu yeye ni chemchemi ya mwanga, ya faraja na ya nguvu. Kumuomba kadiri ya neno la Bwana: “Wewe usalipo, ingia katika chumba chako cha ndani, na ukiisha kufunga mlango wako, usali mbele za Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi” (Math. 6:6). Kumuabudu kwa kusema: “Moyo wangu wamwadhimisha Bwana, na roho yangu imemfurahia Mungu, Mwokozi wangu” (Lk. 1:46-47). Kumuamini, kumtumainia, kumpenda kwa upendo unaozidi kuwa safi, mkarimu, wenye nguvu. Kumpenda kwa kumuiga hasa katika wema: “Basi iweni na huruma, kama Baba yenu alivyo na huruma” (Lk. 6:36). “Wote wawe na umoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako, hao nao wawe ndani yetu” (Yoh. 17:21).

Hayo yote yanatufanya tuone kwamba maisha ya Kiroho upande wa mafumbo (ambapo ujuzi/mang'amuzi ya Mungu kuwemo ndani mwetu ni ya sasa hivi) kwa yenyewe si ya pekee, bali ni ukamilifu wa kawaida. Watakatifu tu, ambao wanayo kikamilifu, wapo kweli wanapotakiwa. Kabla hatujaona muungano huo wa ndani na Mungu, sisi ni kama tumesinziasinzia: bado fumbo tamu la uwemo wa Utatu mtakatifu tunalijua kijuujuu mno, kumbe ndilo uzima tele tuliokaribishwa; hatujamuabudu wala kumpenda Mungu inavyotakiwa, na mara nyingi tunahesabu kile ambacho pekee ni cha lazima kama kwamba kwetu si muhimu kuliko vyote; vilevile hatujaelewa kwa undani ukuu wa zawadi tuliyopewa katika ekaristi, wala Mwili wa fumbo wa Kristo ni nini.

Roho Mtakatifu ndiye roho ya Mwili wa fumbo ambao Yesu ndiye kichwa chake. Kama vile roho nzima imo katika mwili wote na katika kila kiungo, nayo inafanya kazi bora kichwani, vivyo hivyo Roho Mtakatifu yumo mzima katika Mwili wote wa fumbo, naye anafanya kazi bora katika roho takatifu ya Mwokozi na kwa njia yake kwetu pia. Kiini cha uhai kinachounganisha hivyo Mwili wa fumbo kina nguvu ya kuunganisha zaidi kuliko roho inavyounganisha mwili wake, na kuliko umoja wa familia au taifa fulani. Hivyo vinaunganishwa na namna fulani ya kutazama, kupima, kuhisi, kupenda, kutaka na kutenda. Roho anayeunganisha Mwili wa fumbo ana nguvu pasipo mfano, kwa kuwa ni Roho aletaye utakatifu, ni chemchemi ya maji hai yanayobubujikia uzima wa milele. Mto wa neema zote unaotokana na Roho Mtakatifu unapanda juu tena kumrudia Mungu kwa namna ya ibada, sala, stahili na sadaka. Ndiyo mambo yapitayo maumbile tunayopaswa kuyajua vizuri zaidi na zaidi. Upande wa mafumbo tu ndipo roho inapozinduka kweli, na kutambua zawadi ya Mungu ilivyo, kwa namna ile hai, ya ndani na angavu tunayohitaji ili kumrudishia kikamilifu Mungu upendo alio nao kwetu.

 

 

 

 

1.5. KRISTO MKOMBOZI ANAVYOATHIRI MWILI WAKE WA FUMBO

 

 

Tumeona jinsi Utatu mtakatifu uliomo ndani ya kila mwadilifu ulivyo chemchemi isiyoumbwa ya maisha yetu ya Kiroho. Lakini utakatifu wetu unategemea pia nguvu zinazomtoka mfululizo Kristo Mkombozi ambaye, kwa njia ya sakramenti na hata nje ya hizo, anatushirikisha neema alizotustahilia alipoishi duniani na hasa wakati wa mateso yake. Basi, tuongelee sasa nguvu hizo zinazotuletea utakatifu hasa kwa njia ya sakramenti kuu kuliko zote, yaani ekaristi.

 

 

JINSI MWOKOZI ANAVYOTUSHIRIKISHA NEEMA ALIZOTUSTAHILIA

 

Anafanya hivyo kama chombo hai kilichounganika moja kwa moja na umungu, chemchemi ya neema zote. “Kwa kuwa katika utimilifu wake sisi sote tulipokea, na neema juu ya neema” (Yoh. 1:16). Yesu mwenyewe alituambia: “Kaeni ndani yangu, nami ndani yenu. Kama vile tawi lisivyoweza kuzaa peke yake, lisipokaa ndani ya mzabibu, kadhalika nanyi, msipokaa ndani yangu. Mimi ni mzabibu, ninyi ni matawi; akaaye ndani yangu nami ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lolote… Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa. Hivyo hutukuzwa Baba yangu, kwa vile mzaavyo sana; nanyi mtakuwa wanafunzi wangu” (Yoh. 15:4-8).

Mt. Paulo alitoa mfano mwingine wa kushangaza, akisema Kristo ni kama kichwa kinachovishirikisha viungo vyote uhai wa roho; Kanisa ndilo mwili wa fumbo wa Kristo, na Wakristo ndio viungo vya mwili huo. “Ninyi mmekuwa mwili wa Kristo, na viungo kila kimoja peke yake” (1Kor. 12:27). “Tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo. Katika yeye mwili wote ukiungamanishwa na kushikanishwa kwa msaada wa kila kiungo, kwa kadiri ya utendaji wa kila sehemu mojamoja, huukuza mwili upate kujijenga wenyewe katika upendo” (Ef. 4:15-16).

Kufuatana na hayo, Mwokozi anatushirikisha nguvu hai za neema kama vile kichwa kinavyovishirikisha viungo vyake uhai ambao roho ndiyo asili yake. Ili tuelewe vizuri tunapaswa kutofautisha umungu na ubinadamu wa Yesu Kristo. Kama Neno yeye anakaa pamoja na Baba na Roho Mtakatifu katika kiini cha roho yetu akiidumishia uzima wake wa kimaumbile na ule upitao maumbile; anaiongoza kufanya yale makuu na ya ndani zaidi isiyoweza kufanya peke yake. Kuhusu ubinadamu wa Mwokozi ndio chombo kilichounganika na umungu moja kwa moja ambacho tunashirikishwa neema zote. Huo ubinadamu haukai rohoni mwetu, kwa kuwa mwili wake hauwezi kuwemo rohoni mwetu, ila uko mbinguni kwa namna ya mwili na umo katika ekaristi kwa namna ya sakramenti. Hata hivyo roho adilifu inapokea mfululizo nguvu za ubinadamu wa Yesu, kwa sababu kila neema inatolewa kwa njia yake tu. Halafu, kwa kuwa kila sasa tuna wajibu fulani wa kutimiza, ubinadamu wa Mwokozi unatushirikisha nukta baada ya nukta neema ya msaada ya sasa hivi, kama vile hewa inavyoingizwa mfululizo mapafuni.

Mungu, asili ya neema, anatumia ubinadamu wa Mwokozi ili kutujalia neema, kama vile mwanamuziki bora anavyotumia ala ili kutushirikisha aliyonayo moyoni, au kama vile mwanafalsafa bora anavyotumia ufasaha wa lugha yake ili kutokeza mawazo yake. Ubinadamu wa Mwokozi ni chombo bora, chenye kujua na kutaka kutumika, kilichounganika moja kwa moja na umungu ili kutushirikisha neema zote tunazojaliwa, ambazo zote alitustahilia msalabani.

Hivyo kwa Mwokozi vinatoka mianga yote ya akili, neema zote za mvutio, za faraja na za ushujaa, tunazozihisi na tusizozihisi. Ni nguvu ya mfululizo inayochangia kila tendo linalostahili wokovu kuliko mama bora anavyoweza kumsaidia mwanae anapomfundisha kusali. Utendaji huo wa Mwokozi unawashirikisha wasioamini mianga ya imani, na Wakristo wakosefu neema ya kujuta inayowaalika kwenye kitubio. Lakini nguvu hiyo inatumika hasa katika ekaristi, kwa kuwa sakramenti hiyo haina neema tu, bali inaye mwenyewe aliye asili ya neema, tena ni sadaka yenye thamani isiyo na mipaka. Jambo hilo linatakiwa kusisitizwa, tunapoongea juu ya chemchemi ya maisha ya Kiroho.

 

 

NGUVU YA KUTAKASA INAYOTOKA KWA MWOKOZI KATIKA EKARISTI

 

Ili tufaidike zaidi na kumshukuru Bwana ni afadhali tutumie maneno yenyewe ya Injili. Tukumbuke alivyotuahidia kwanza ekaristi kwa upendo; alivyotupatia katika karamu ya mwisho, alipoweka upadri; anavyoifanya upya kila siku katika misa; anavyotaka kubaki kati yetu kwa kudumisha uwemo wake halisi katika sakramenti; hatimaye anavyojitoa kwetu katika komunyo ya kila siku, hadi ile ya mwisho tunayotumainia kuipokea kabla hatujafa. Ukarimu huo wote wa Kimungu unatokana na upendo mmoja na kulenga ustawi wa utakatifu wetu.

Maneno aliyotuahidia ekaristi (taz. Yoh. 6:26-69) yanatuonyesha kwa namna bora hizo nguvu hai za Mwokozi zinazotakiwa kutufanyia kazi na jinsi sisi tunavyotakiwa kuzipokea. Baada ya kuzidisha mikate, alisema: “Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele, ambacho Mwana wa Adamu atawapa. Kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na Baba, yaani Mungu... Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni. Kwa maana chakula cha Mungu ni kile kishukacho kutoka mbinguni na kuupa ulimwengu uzima”. Basi wakamuambia: “Bwana, sikuzote utupe chakula hiki”. Yesu akawaambia: “Mimi ndimi chakula cha uzima... Lakini niliwaambia ya kwamba mmeniona wala hamwamini... Amin, amin, nawaambia: yeye aaminiye yuna uzima wa milele. Mimi ndimi chakula cha uzima. Baba zenu waliila mana jangwani; wakafa. Hiki ni chakula kishukacho kutoka mbinguni, kwamba mtu akile wala asife. Mimi ndimi chakula chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni; mtu akila chakula hiki, ataishi milele. Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwa ajili ya uzima wa ulimwengu... Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwa maana mwili wangu ni chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli... Maneno hayo niliyowaambia ni roho, tena ni uzima”. Kutokana na hayo, wengi wa wafuasi wake walirudi nyuma, wasiandamane naye tena. Basi, Yesu akawauliza wale kumi na wawili, “Je, ninyi nanyi mwataka kuondoka?”. Simoni Petro akamjibu, “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele”. Ahadi hiyo ya ekaristi inadokeza yale yote ambayo sakramenti hiyo inakusudiwa kuzaa ndani mwetu.

Simulizi la kuiweka linatuonyesha uzito wa ahadi hiyo: “Walipokuwa wakila, Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, ‘Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu’. Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, ‘Nyweni nyote katika hiki; kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi’” (Math. 26:26-28). Maneno ya ahadi yanaangazwa na hayo yaliyomtuza mt. Petro kwa sababu alisema kwa imani, “Wewe unayo maneno ya uzima wa milele”. Hakika Yesu karamuni alikuwa na neno lenye nguvu kuliko kawaida, neno lenye kugeuza undani wa mkate kuwa mwili wake ili abaki kati yetu kisakramenti.

Papohapo aliweka upadri ili kudumisha kisakramenti sadaka ya msalabani mpaka mwisho wa nyakati. Kwa kusema, “Fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu” (Lk. 22:19; 1Kor. 11:24-25) aliwapa mitume uwezo wa kugeuza, wa kutolea sadaka ya ekaristi inayodumisha ile ya msalabani, ili watushirikishe matunda, stahili na malipizi yake mpaka mwisho wa dunia. Kuhani mkuu ni Bwana wetu, anayeendelea kujitoa; “maana yu hai sikuzote ili awaombee” (Eb. 7:25). Anafanya hivyo hasa katika sadaka takatifu, ambayo ina thamani isiyo na mipaka, kutokana na kuhani mkuu anayeitoa, sadaka inayotolewa, na damu azizi inayomwagwa kisakramenti. Papohapo Yesu anamtolea Baba yake ibada, dua, malipizi na shukrani zetu, yaani kwa jumla matendo yote ya Mwili wake wa fumbo yanayostahili wokovu.

Upendo wa Kristo umetupatia ekaristi si mara moja tu, bali kila siku upya. Angeweza kuamua misa iadhimishwe mara moja au mbili tu kwa mwaka mahali fulani patakatifu ambapo waamini waende kutoka nchi za mbali. Kumbe kila nukta misa kadhaa zinatolewa duniani kote. Hivyo analijalia Kanisa lake neema linazozihitaji kulingana na nyakati linazoishi, tuwe na nguvu ya kukabili hatari kubwa tulizonazo.

Kristo anarudi kila siku, kweli, kati yetu, si kwa muda wa saa moja, tunapoadhimisha sadaka ya ekaristi, bali kusudi abaki nasi mfululizo katika tabenakulo kama mwenzetu hapa uhamishoni, akitungojea kwa hamu ya kutusikiliza, na kumtolea daima Baba yake ibada yenye thamani isiyo na mipaka.

Hatimaye komunyo ni utimilifu wa kujitoa zawadi. Wema kwa jinsi ulivyo unaelekea kuenea; unavutia na kujishirikisha. Hiyo ni kweli hasa kwa wema mwangavu wa Mungu na Kristo wake. Katika komunyo Mwokozi anatuvuta kwake na kujitoa kwetu, sio sote kwa jumla, bali tukitaka kwa kila mmoja wetu, tena tukiwa waaminifu kwa ndani zaidi na zaidi. Anajitoa si kusudi alingane nasi bali sisi tuzidi kulingana naye. “Mkate ule tuumegao, si ushirika wa mwili wa Kristo?” (1Kor. 10:16). Tunaupokea uhai wenyewe.

Ushirika huo unatakiwa kutuunganisha na Kristo zaidi na zaidi, ukikuza ndani mwetu unyenyekevu, imani, tumaini na hasa upendo, ili moyo wetu ulingane na ule wa Mwokozi aliyekufa kwa upendo wake kwetu. Kwa maana hiyo komunyo zetu zinatakiwa kuwa na upendo mwingi zaidi na zaidi, kwa kuwa kila mojawapo inatakiwa sio tu kutunza, bali kustawisha upendo wa Mungu ndani mwetu na hivyo kutuandaa kumpokea Bwana kesho yake kwa utashi motomoto zaidi (bila ya kujali umotomoto wa hisi ambao ni wa ziada tu: tunaweza kupokea vizuri ekaristi katika ukavu mkubwa wa hisi, kama ilivyokuwa bora sala ya Yesu bustanini). Inatakiwa kuwa kama mbio ya kumuendea Mungu ambayo izidi kuwa ya kasi: kama vile vitu vinavyozidi kuanguka kwa kasi kadiri vinavyokaribia ardhi inayovivuta, roho zinatakiwa kumwendea Mungu kwa kasi kadiri wanavyomkaribia na kuvutiwa naye.

“Ninakuabudu Mungu wangu, / unayejificha altareni. / Ninakutolea moyo wangu, / usiofahamu siri yako... / Ewe Yesu nipe pendo lako, / tumaini kwako na imani. / Umeteswa nini, Bwana mwema, / kwa kunipa mkate wa uzima? / Yesu unifiche ndani yako, / ili nilionje pendo lako. / Yesu pelikane nitazame, / na kwa damu yako nitakase. / Tone moja ndilo linatosha, / na dunia yote yaokoka. / Ndani ya mafumbo Yesu yumo. / Atafumbuliwa kwangu lini? / Nikuone, Yesu, uso wako, / nishiriki nawe heri yako” (mt. Thoma wa Akwino).

Mtu akiishi hivyo ekaristi kila siku, atafikia urafiki wa ndani naye, na kuzama zaidi na zaidi katika fumbo kuu la altare na kulionja, ikiwa ni pamoja na thamani isiyo na mipaka ya misa, chemchemi ya neema mpya daima, ambayo vizazi vyote vinatakiwa kutuliza kiu yao na kupata nguvu ya kufikia mwisho wa safari ya kuelekea uzima wa milele. Nabii Eliya alipoishiwa nguvu alizipata upya kwa kula mkate kutoka mbinguni, akatembea mpaka mlima Horebu, unaomaanisha kilele cha ukamilifu.

Katika ushirika mtakatifu Kristo anatuambia kama alivyomuambia mt. Augustino: “Ndimi mkate wa watu wa uzima... Kua, nawe utanila; lakini hutanigeuza ndani mwako, kama chakula cha mwili wako; bali wewe utageuzwa ndani mwangu”. Anayemshiriki kweli Kristo anakuja kuunganishwa naye zaidi na zaidi, hata kuishi kwa mawazo yake na kwa upendo wake; hapo anaweza kusema: “Kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida” (Fil. 1:21), kwa kuwa ni mlango wa uzima usio na mwisho.

 

 

KUZIDI KUUNGANA NA KRISTO NA UTAKATIFU

 

Mafundisho hayo kuhusu kuungana na Kristo zaidi na zaidi yana uwezo mkubwa ajabu wa kumfaidisha anayeamua kuyaishi.

Kwanza ili tufie dhambi na matokeo yake tukumbuke kwamba “tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake… ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena” (Rom. 6:4-6); “hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake” (Gal. 5:24). Ndiyo kufia dhambi kwa ubatizo na kitubio.

Halafu, kwa mwanga wa imani na uvuvio wa Roho Mtakatifu, Mkristo anatakiwa kuvaa “utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba... Basi… jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu… Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu” (Kol. 3:10-14). Ndiyo hatua ya kuangazwa ya wanaomuiga Yesu Kristo kwa kujipatia msimamo wake, roho ya mafumbo yake, ya mateso, kifo na ufufuko wake. Ndiyo njia waliyoifuata watakatifu wote, kufuatana na maneno ya mtume: “Nayahesabu mambo yote kuwa hasara kwa ajili ya uzuri usio na kiasi wa kumjua Kristo Yesu, Bwana wangu; ambaye kwa ajili yake nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo” (Fil. 3:8).

Njia hiyo inaelekeza kwenye muungano kama wa kudumu na Mwokozi: “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Yafikiri yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi. Kwa maana mlikufa, na uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu” (Kol. 3:1-3). Hapo amani ya Mwokozi itatawala roho ya mtu anayependa kumuambia, “Bwana, nipe nafsi yako, pokea nafsi yangu”. Elekeo la roho kwake linamuambia tunatamani nini, likimtolea udhaifu wetu, nia yetu njema, azimio letu la uaminifu, kiu yetu ya nafsi yake. Ndiyo hatua ya kuzama kwa upendo katika mafumbo, kama utangulizi wa heri ya kuonana na Mungu uso kwa uso mbinguni.

Wengi wanadanganyika kuwa wanaweza kufikia muungano na Mungu pasipo kumkimbilia mfululizo Bwana wetu: hao watafikia tu ujuzi wa mbali wa Mungu, sio ule mtamu unaoitwa hekima ambayo ni kama mang'amuzi ya Mungu na ya maongozi yake katika mambo yote, hata yale madogo. Tusiache kamwe kwa makusudi kuzingatia ubinadamu wa Mwokozi katika sala: kwa kuwa ndiye njia inayoelekeza kwa umungu wake. Tufikirie mara nyingi utajiri wa Kiroho wa Yesu, wa akili, utashi na hisi zake, ili tuzidi kuelewa neno lake: “Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima” (Yoh. 14:6).

 

 

 

 

1.6. MSAADA WA MAMA MARIA

 

 

Tunaposema juu ya misingi ya maisha ya Kiroho, hatuwezi kuzungumzia kazi ya Kristo mshenga juu ya mwili wake wa fumbo tusidokeze pia juu ya msaada wa mama Maria. Wapo Wakatoliki kadhaa wasioamini vya kutosha haja ya kumkimbilia Maria ili kuungana na Mwokozi kwa undani zaidi. Mt. Alois Maria Grignion de Montfort alisema juu ya “walimu wanaomjua Mama wa Mungu kinadharia tu, kwa namna kavu, tasa na baridi; wanaoogopa ibada kwa Bikira mtakatifu itatumika vibaya hivi hata kwa kumheshimu mno Mama mtakatifu Bwana atachukizwa. Wakiongelea ibada kwa Maria ni kwa kuzuia namna zake zisizofaa kuliko kwa kuihimiza”; hata tunaweza kudhani wanamuona Maria kama kizuio kwa kufikia muungano na Mungu! Akasema ni kiburi kutowajali wasaidizi tuliopatiwa na Mungu kutokana na udhaifu wetu. Muungano wa ndani na Bwana katika sala unasaidiwa na ibada halisi na kubwa kwa Maria.

Mt. Thoma wa Akwino aliandika: “Kazi ya mshenga ni kuwasogeza na kuwaunganisha wale ambao amewekwa katikati yao: kwa kuwa pande mbili zinaungana kwa njia ya mshenga. Basi, kuunganisha watu na Mungu ni kazi hasa ya Kristo, kwa kuwa ndiye aliyewapatanisha na Mungu alivyosema mt. Paulo: ‘Mungu alikuwa ndani ya Kristo, akiupatanisha ulimwengu na nafsi yake’ (2Kor. 5:19). Kwa hiyo mshenga kamili kati ya Mungu na watu ni Kristo tu, kwa sababu kwa kifo chake amawapatanisha watu na Mungu. Hata mt. Paulo aliposema: ‘mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, mwanadamu Kristo Yesu’ akaongeza, ‘ambaye alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi kwa ajili ya wote’ (1Tim. 2:5-6). Hata hivyo hakuna kinachozuia wengine wasiitwe kwa namna fulani washenga kati ya Mungu na watu kwa kuwa wanachangia muungano wa Mungu na watu kama wahudumu katika ugawaji”. Kwa maana hiyo manabii na makuhani wa Agano la Kale wanaweza kuitwa washenga; kama vile mapadri wa Agano Jipya, walio wahudumu wa mshenga halisi. Mwalimu huyo akaongeza kuwa “ni kwa ubinadamu wake kwamba Kristo ni mshenga: kwa sababu ni kama binadamu kuwa yeye yupo kati ya pande mbili: chini ya Mungu kwa maumbile, juu ya watu kwa ukuu wa neema na utukufu. Tena kama binadamu anawaunganisha watu na Mungu akiwatolea amri na zawadi za Mungu, na kutoa fidia na kusali kwa ajili yao”. Yesu alitoa fidia na kustahili kama binadamu, ambaye fidia na stahili zake zilikuwa na thamani isiyo na mipaka kutokana na nafsi yake ya Kimungu. Hapo tuna ushenga wa aina mbili, wa kushuka na wa kupanda, maana yake wa kuwapa watu mwanga na neema ya Mungu na wa kumtolea Mungu ibada na malipizi anayostahili kwa ajili ya watu. Basi, hakuna kinachozuia uwepo wa washenga washiriki chini ya Kristo. Mt. Alberto alisema juu ya ubora wa ushenga wa Maria: “Yeye hakuingizwa na Bwana kwenye huduma, bali kwenye ushirika na msaada, kadiri ya maneno, ‘nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye’ (Mwa. 2:18)”. Maria alichaguliwa na Bwana si kuwa mhudumu, bali awe mshiriki wa pekee na wa ndani wa ukombozi wa wanadamu.

Maria kama Mama wa Mungu, je, hakukusudiwa kuwa mshenga kwa wote na yote? Kuwa kati ya Mungu na watu? Kwa hakika Maria yuko chini kuliko Mungu na Kristo kwa kuwa ni kiumbe; lakini pia ameinuliwa juu kuliko watu wote kwa neema ya kuwa Mama wa Mungu, na kwa ukamilifu wa neema aliyojaliwa tangu achukuliwe mimba hali amekingiwa dhambi asili, ukamilifu ambao ukaongezeka moja kwa moja hadi kifo chake. Naye hakuchaguliwa tu awe mshenga kutokana na umama wake wa Kimungu, bali kweli alikabidhiwa na kutekeleza kazi hiyo ambayo inamfaa kwa sababu kuu mbili: 1° kwa kuwa alichangia sadaka ya msalabani kwa malipizi na stahili zake; 2° kwa kuwa haachi kutuombea, kutupatia na kutugawia neema zote tunazopokea. Ndio ushenga wa kupanda na kushuka tunaopaswa kuuzingatia ili kuufaidi kila siku zaidi.

 

 

MARIA MSHENGA KWA KUCHANGIA SADAKA YA MSALABANI

 

Maisha yake yote bikira Maria alichangia sadaka ya Mwanae hadi aliposema, “Imekwisha” (Yoh. 19:30).

Kwanza ilihitajika ridhaa yake, aliyoitoa siku ya kupashwa habari na malaika, ili fumbo la umwilisho lifanyike, kama kwamba Mungu alisubiri kibali cha binadamu kwa sauti ya Maria. Kwa njia hiyo alichangia sadaka ya msalabani kwa kutupatia kuhani na sadaka yake.

Aliichangia pia kwa kumtolea Mwanae hekaluni kama sadaka safi, mzee Simeoni alipoona kwa mwanga wa kinabii kuwa mtoto wake ndiye wokovu ulioletwa na Mungu “tayari machoni pa watu wote; nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, na kuwa utukufu wa watu wako Israeli” (Lk. 2:31-32). Maria akiwa ameangaziwa kuliko yeye, alimtoa Mwanae na kuanza kuteseka pamoja naye, akitabiriwa kwamba mtoto amewekwa “kuwa ishara itakayonenewa. Nawe mwenyewe, upanga utaingia moyoni mwako” (Lk. 2:34-35).

Hasa chini ya msalaba Maria alichangia sadaka ya Kristo, akiungana naye katika malipizi na stahili kwa undani kuliko tunavyoweza kueleza. Baadhi ya watakatifu, hasa waliotiwa madonda ya Yesu, waliungana kwa namna ya pekee na mateso na stahili za Mwokozi. Lakini hayo ni madogo yakilinganishwa na muungano wa Maria aliyemtoa Mwanae kama mwenyewe alivyojitoa. Yesu angeweza kuzuia kwa urahisi ukatili wa watesi wake usimuue, lakini alitoa kwa hiari uzima wake: “Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao na uweza wa kuutwaa tena” (Yoh. 10:18). Alijinyima haki ya kuishi, akijitoa mhanga kwa wokovu wetu. Basi, Maria alisimama “penye msalaba wake Yesu” (Yoh. 19:25), akiungana naye kwa undani katika mateso na kujitoa, “akijinyima haki zake za kimama kuhusu Mwanae kwa ajili ya wokovu wa watu wote” (Benedikto XV). Alikubali kifodini cha Kristo na kukitoa kwa ajili yetu. Kadiri ya upendo wake alihisi uchungu wa Mwanae katika mwili na katika roho. Maria alionja kuliko wote uchungu wa Mwokozi; alisikitishwa na dhambi kadiri ya upendo wake: kwa Mungu, anayechukizwa nayo; kwa Mwanae, aliyesulubiwa nayo; kwa watu ambao roho zao zinaangamizwa nayo. Upendo wa Bikira ulipita ule wa watakatifu wowote.

Alichangia sadaka ya msalabani kama malipizi kwa kumtolea Mungu kwa niaba yetu, kwa uchungu mwingi na upendo mkuu, uhai wa Mwanae mpenzi, aliyemuabudu na kumpenda kuliko nafsi yake mwenyewe. Saa hiyo Mwokozi alikuwa akilipa kwa niaba yetu, kwa matendo yake ya kibinadamu yaliyoshiriki thamani isiyo na mipaka ya nafsi yake ya Kimungu, yenye uwezo wa kufidia dhambi zote na zaidi tena. Upendo wake ulimpendeza Mungu kuliko anavyochukizwa na dhambi zote. Ndio kiini cha fumbo la ukombozi. Akiungana na Mwanae huko Kalivari, Maria alilipa kwa niaba yetu si kwa msingi wa haki yenyewe, bali wa urafiki wa ndani au upendo uliomuunganisha na Mungu. Mwanae alipokuwa akifa msalabani kama mtu aliyeshindwa na kutupwa, yeye hakuacha hata kidogo kumuamini. Ndilo tendo kuu la imani; ndilo pia tendo kuu la upendo baada ya lile la Kristo mwenyewe. Tendo hilo limemfanya Maria malkia wa mashahidi, kwa kuwa sio tu shahidi kwa ajili ya Kristo, bali pamoja naye, hivi kwamba msalaba mmoja tu uliwatosha Mwana na Mama aliyesulubiwa kwa namna fulani kutokana na upendo wake kwake. Hivyo akawa mkombozi mshiriki kwa maana alikomboa binadamu pamoja na Kristo, kwa njia yake na ndani mwake.

Kwa sababu hiyohiyo, yale yote ambayo Kristo msalabani alitustahilia kwa msingi wa haki, Maria alitustahilia kwa msingi wa upendo uliomuunganisha na Mungu. Kristo tu, akiwa ni kichwa cha binadamu wote, aliweza kustahili kwa haki tushirikishwe uhai wa Kimungu, lakini ilifaa kwamba Mungu azingatie pia stahili za Maria aliyeungana naye katika kazi ya wokovu. Mapokeo yote ya Mashariki na Magharibi yanamuita Eva mpya, Mama wa watu wote upande wa roho, kama vile Eva alivyokuwa upande wa mwili. Basi Mama wa Kiroho wa watu wote anatakiwa kuwapa uzima wa Kiroho, ingawa si kama asili yake kuu. Msingi wa mafundisho hayo ni maneno ya Yesu kufani: “alipomwona mama yake, na yule mwanafunzi aliyempenda amesimama karibu, alimwambia mama yake, ‘Mama, tazama mwanao’. Kisha akamwambia yule mwanafunzi, ‘Tazama mama yako’. Na tangu saa ile mwanafunzi yule akamchukua nyumbani kwake” (Yoh. 19:26-27). Maana yenyewe ya maneno hayo yanamhusu Yohane, lakini kwa Mungu matukio na watu wana maana nyingine pia; hapo Yohane aliwakilisha watu wote waliokombolewa na sadaka ya msalabani. Mungu anasema sio tu kwa maneno, bali pia kwa matukio na watu ambao mikononi mwake wanamaanisha yale anayoyataka. Kama vile neno la Yesu lilivyosababisha ndani ya Maria mapendo makubwa ya kimama kwa mwanafunzi mpendwa, vilevile hayo mapendo yakaenea kwa wote na kumfanya kweli mama wa Kiroho wa watu wote. Basi, ikiwa mama mwema anaweza kuwastahilia watoto wake neema nyingi kutokana na maadili yake, zaidi Maria anaweza kuwastahilia watu wote kutokana na ukamilifu wa upendo wake unaomuunganisha na Mungu, ingawa si kustahili kwa msingi wa haki.

Ndio ushenga wa kupanda wa Maria, ambao akiwa na Bwana wetu alitoa sadaka ya msalabani kwa ajili yetu; sasa tuzingatie ushenga wa kushuka ambao anatugawia zawadi za Mungu.

 

 

MARIA ANAVYOTUPATIA NA KUTUGAWIA NEEMA ZOTE

 

Akiwa ni Mama wa watu wote, Maria anashughulikia wokovu wao, akiwaombea na kuwapatia neema zile wanazojaliwa. Ndiyo sababu Kanisa linamuelekea ili kupatiwa neema za kila aina, za kimwili na za Kiroho, zikiwa ni pamoja na wongofu na kifo chema, bila ya kusahau zile zinazohitajiwa na mabikira ili kutunza ubikira wao, na wachungaji kwa ajili ya utume wao, na wafiadini ili wadumu katika kukiri imani. Kwa namna fulani hata neema za sakramenti zinagawiwa kwa njia yake, kwa kuwa alitustahilia hizo huko Kalivari akiwa ameunganika na Bwana wetu, halafu kwa sala zake anatuandaa kuzipokea vema; tena pengine anatutumia padri ili tuweze kufaidi huduma hiyo. Imani ya Kanisa inasali mfululizo atuombee “sasa na saa ya kufa kwetu”; kwa maneno hayo tunajiombea neema ya sasa hivi, ambayo ni ya pekee kwa kuwa ni tofauti kwa kila mtu na kwa kila nukta aliyonayo. Ikiwa sisi tunatamka maneno hayo bila ya kuyazingatia, Maria ni tofauti, hasinzii: anajua mahitaji yetu ya Kiroho ya kila nukta, na kutuombea na kutupatia neema zile tunazojaliwa.

Msingi wa imani hiyo umo katika Maandiko na Mapokeo. Maria aligawa neema kuanzia wakati wa maisha yake duniani. Kwa njia yake Yesu alimtakasa Yohane mtangulizi wake, akaimarisha imani ya wanafunzi kwenye arusi ya Kana. Kwa njia yake Roho Mtakatifu alimiminwa juu ya mitume, alipokuwa akisali pamoja nao. Zaidi tena, baada ya kupalizwa mbinguni, akiwa ni Mama mwenye heri ya milele, anajua mahitaji ya watoto wake aliowaacha duniani. Basi, kwa upendo wake mkuu anatuombea, na kwa uwezo wake mkuu juu ya moyo wa Mwanae anatupatia neema zote tunazojaliwa, zile zote wanazozipata wasiofanya moyo wao kuwa mgumu. Ndiyo sababu alifananishwa na mfereji unaoleta maji, pia na shingo la Mwili wa Kristo.

Tutakaposema juu ya sala ya wanaoendelea tutaongelea ibada halisi kwa bikira Maria. Lakini tangu sasa tunaona umuhimu wa kufanya mara nyingi sala ya washenga, yaani kuanza kuongea na Maria kwa tumaini kubwa ili atufikishe hadi kuungana na Mwanae kwa undani, halafu kwa njia ya Mwokozi tuinuke hata muungano na Mungu.

 

 

 

 

1.7. USTAWI WA UZIMA WA NEEMA

KWA NJIA YA STAHILI, SALA NA SAKRAMENTI

 

 

Hatuwezi kusema juu ya chemchemi ya maisha ya Kiroho bila ya kusema juu ya ustawi wa neema ya utakaso na wa upendo. Hakuna wokovu bila ya adili hilo la Kimungu, lililo kuu kuliko yote na linalotakiwa kuyaongoza na kuyahuisha mengine pia. Tena halitakiwi kubaki lilivyo, bali kukua ndani mwetu hadi siku ya kufa. Fundisho hilo linaweza tena linapaswa kuangaza maisha yote ya Kiroho, kwa kuwa ni msingi wa himizo lolote la kusonga mbele kwa unyenyekevu na moyo mkuu, kwa kutamani muungano wa ndani na Mungu, kwa kujitahidi kuupata pamoja na kuuomba. Basi, tuone kwanza kwa nini upendo unatakiwa kustawi daima, halafu jinsi unavyostawi.

 

 

KWA NINI UZIMA WA NEEMA NA UPENDO USTAWI NDANI MWETU HADI KUFA?

 

Hata katika kiwango kidogo upendo halisi (ambao tuliupokea kwa ubatizo na pengine kurudishiwa kwa upatanisho) unampenda tayari Mungu Mwokozi kuliko yote, na kwa ajili yake unampenda jirani kama mtu mwenyewe anavyojipenda. Kiwango hicho cha upendo uliomiminwa rohoni kinapita tayari bila ya kifani pendo la kimaumbile tunaloweza kuwa nalo kwa Muumba na kwa watu; hakimbagui yeyote, kwa kuwa ubaguzi huo ungekuwa dhambi ya mauti ambayo ingeufuta upendo. Lakini upendo huo wa wanaoanza uko mbali na ushindi juu ya umimi wowote. Unaendana bado na kujipendea ambako, ingawa si dhambi ya mauti, kunasababisha dhambi nyepesi nyingi na hivyo kuzuia upendo usiweze kutenda na kupamba vizuri.

Bila ya shaka, upendo huo wa kiwango cha chini unatakiwa kustawi: “Hii ndiyo dua yangu, kwamba pendo lenu lizidi kuwa jingi sana” (Fil. 1:9). “Bwana awaongeze na kuwazidisha katika upendo, ninyi kwa ninyi, na kwa watu wote, kama vile sisi nasi tulivyo kwenu; apate kuifanya imara mioyo yenu iwe bila lawama katika utakatifu mbele za Mungu, Baba yetu” (1Thes. 3:12-13). “Mwenye haki na azidi kufanya haki, na mtakatifu azidi kutakaswa” (Ufu. 22:11). “Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu” (Mith. 4:18). Ni kwamba hapa duniani Mkristo ni msafiri anayemuelekea Mungu. Anamkaribia kwa vitendo vya upendo ulio kamili zaidi na zaidi, kwa “hatua za upendo” (mt. Gregori Mkuu). Upendo unaweza na kupaswa kustawi mfululizo, la sivyo Mkristo badala ya kusafiri anasimama kabla hajafika. Lengo la njia ni kutembea, si kulala. Kila mtu anayeelekea uzima wa milele anatakiwa kukua katika upendo ili azidi kumkaribia Mungu: sio tu wanaoanza na wanaoendelea, bali hata waliokamilika. Tena hao wa mwisho wanapaswa kwenda kasi zaidi kadiri wanavyomkaribia na kuvutwa naye; nguvu ya maisha yao ya Kiroho inaongezeka zaidi na zaidi, elekeo la roho yao linainuka zaidi na zaidi; kwao hakuna machweo: mwili tu unadhoofika kwa uzee.

Juu ya hayo Bwana alisema: “Mimi nikiinuliwa juu ya nchi, nitawavuta wote kwangu” (Yoh. 12:32). “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka” (Yoh. 6:44). Mungu ndiye anayetufanya twende, na anakotuvuta ni kwake: ndiye mwanzo na mwisho wa yote, ndiye wema mkuu unaovuta upendo kwa nguvu kadiri tunavyomkaribia. Ndiyo sababu katika maisha ya watakatifu, ustawi wa upendo miaka yao ya mwisho ni mkubwa sana; ingawa wanabeba uzito wa uzee na wa udhaifu fulani upande wa hisi (k.mf. kumbukumbu) wanang’amua ukweli wa maneno ya Zaburi (103:5): “Ujana wako unarejezwa kama tai”. Maendeleo hayo ya kasi zaidi na zaidi yalikuwepo hasa katika bikira Maria, kwa kuwa ndani mwake hayakuzuiwa na chochote, tena yalikuwa ya haraka kadiri ilivyokuwa kubwa neema ya kwanza aliyojaliwa. Basi, upendo ndani mwetu unatakiwa sio tu kustawi hadi kufa, bali kustawi zaidi na zaidi, kama vile kasi ya kitu kinachoanguka inavyozidi hadi kikafika ardhini.

Ikiwa ni hivyo, upendo unastawi vipi ndani mwetu? Kwa kuwa hata katika kiwango cha chini unampenda tayari Mungu kuliko yote, na jirani kwa jumla bila ya kubagua yeyote, hauwezi kuenea zaidi: lakini unaweza kuongezewa nguvu na kutia mizizi ndani ya utashi wetu zaidi na zaidi. Upendo hauongezeki kama nafaka, yaani haukui kwa wingi, bali kwa ubora, kwa kuongezewa nguvu katika utashi, ukizidi kuuelekeza kwenye mema yapitayo maumbile na kuuepusha na maovu. Mfano wake ni elimu ya msomi ambayo haipati daima taarifa mpya, ila inazidi kuchimba na kuwa na hakika; vivyo hivyo upendo unastawi ndani mwetu, ukitufanya tuwapende kwa namna kamili na safi zaidi na zaidi Mungu kwa ajili yake mwenyewe na jirani kwa ajili ya Mungu. Tukielewa mafundisho hayo, tunaona haja ya roho kutakaswa kila uchafu na kudhihirisha jinsi maadili makuu yanavyolenga ukweli na wema wa Mungu. Basi, upendo kama joto, unastawi kwa ubora, kwa kupata nguvu zaidi na zaidi; na hiyo inafanyika kwa namna tatu: kwa stahili, kwa sala na kwa sakramenti.

 

 

USTAWI WA UPENDO KWA NJIA YA STAHILI ZETU

 

Tendo linalotokana na upendo (au adili lolote linaloongozwa na kuhuishwa na upendo) linastahili tuzo linalopita maumbile, hasa ustawi wa upendo wenyewe. Stahili hazisababishi zenyewe ustawi huo, kwa kuwa upendo si adili la kujipatia, bali ni adili la kumiminiwa. Kama vile Mungu tu anaweza kuuweka ndani mwetu (kwa kuwa ni kushiriki uzima wa ndani mwake mwenyewe), yeye tu anaweza kuustawisha: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu. Hivyo, apandaye si kitu, wala atiaye maji, bali Mungu akuzaye… ninyi ni shamba la Mungu, ni jengo la Mungu” (1Kor. 3:6-9). Yeye “atawapa mbegu za kupanda na kuzizidisha, naye atayaongeza mazao ya haki yenu” (2Kor. 9:10).

Ingawa matendo ya upendo hayawezi kusababisha ustawi wa adili hilo, yanauchangia kwa namna mbili, yaani kwa kuustahili na kwa kutuandaa kuupokea.

Stahili ni haki ya kupata tuzo; hailisababishi ila inalipata. Mwadilifu kwa matendo yake mema yanayopita maumbile anastahili upendo wake ustawi, ilivyofundishwa na Mtaguso wa Trento. Bwana kabla hajampa tuzo la mbinguni anampa hapa duniani lile la kukua katika upendo wa Kimungu. Wazushi walioitwa Watulivu walidharau tuzo la Mungu wakijidai eti, hawajitafutii faida; kumbe kadiri roho inavyojipenda, inatamani zaidi tuzo hilo: kumpenda Mungu kwa nguvu na kwa usafi mkubwa zaidi na zaidi, jambo lisilotenganika na ustawi wa maadili mengine ya kumiminiwa na wa vipaji vya Roho Mtakatifu.

Matendo ya upendo na ya maadili yanayoongozana nao, sio tu kwamba yanastahili ustawi wa upendo, bali pia yanaandaa kuupokea, kama kwa kufungua na kupanua akili na utashi ili uzima wa Kimungu uweze kuvipenya zaidi, na kwa kuvitakasa uviinue juu zaidi. Hiyo ni kweli hasa kwa matendo motomoto ya upendo. Tendo la ukarimu mkubwa la upendo wa Mungu linaathiri pengine maisha yote ya baadaye na kustahili ustawi mkubwa wa upendo, likituandaa kupokea ustawi huo. Ni kama kwamba tunainuliwa hadi ghorofa ya juu, ambapo tuna mtazamo mpya wa mambo ya Mungu na mvutio mkubwa zaidi kwa mambo hayo. Aliyekuwa na talanta mbili anaongezewa, yaani Roho Mtakatifu anakuwemo ndani mwake kwa namna mpya inayofanya kazi zaidi. Kwa kawaida Roho Mtakatifu anamsukuma mtu kulingana na kiwango cha maadili na vipaji alichonacho au kulingana na usikivu wake. Kama angemsukuma bila ya sababu atende kwa upungufu, maana yake ingekuwa amepokea bure kiwango kikubwa cha maadili na vipaji. Basi, mwadilifu asipozuia kazi ya Mungu, atapokea neema kubwa zaidi na zaidi apande kwa ukarimu kumuelekea Mungu.

Wanateolojia kadhaa wamefundisha kuwa Mungu anatukuzwa na tendo moja la upendo la talanta kumi kuliko anavyotukuzwa na vitendo kumi vya upendo vya talanta mojamoja; vilevile kuwa mwadilifu mmoja aliye mkamilifu anampendeza Mungu kuliko wengine wengi wanaobaki katika wastani. Ubora ni muhimu kuliko wingi. Ndiyo sababu ukamilifu wa Maria unapita ule wa watakatifu wote, kama vile almasi moja ina thamani kuliko vito vingine vingi.

Basi, upendo unatakiwa kustawi kwa njia ya stahili zetu hadi tutakapokufa; pamoja na adili hilo utakua pia utayari wetu wa kupokea ongezeko lingine: moyo unapanuka zaidi na zaidi na ujazo wake wa Kimungu unaongezeka: “mioyo yetu imekunjuliwa… Basi, ili mlipe kadiri ile mliyopewa… nanyi pia mkunjuliwe mioyo” (2Kor. 6:11,13).

Mara nyingi tunasahau tuko safarini kuelekea uzima wa milele, na tunajaribu kustarehe katika maisha ya hapa duniani kama kwamba yangedumu moja kwa moja. Ni kama maabiria wa treni bora ambamo wanakula na kulala kama hotelini hata wakasahau wako safarini; pengine wakiangalia dirishani wanaona mandhari ikibadilika haraka na baadhi ya wenzao wakiteremka: hapo wanajisemea kuwa wao pia watawahi kufikia mwisho wa safari. Shida ni kwamba, ingawa tunaona wengi kufa, hatupati hakika ya ndani kuwa siku fulani itakuwa zamu yetu. Basi, tuishi kwa kukazia macho mwisho wa safari, kusudi tusipoteze tena muda tuliojaliwa, bali tuujaze iwezekanavyo matendo ya kustahili uzima wa milele.

 

UZIMA WA NEEMA KUSTAWI KWA NJIA YA SALA

 

Ustawi wa upendo (pamoja na maadili mengine na vipaji vinavyoongozana nao) unapatikana si kwa njia ya stahili tu, bali kwa sala pia. Ustawi huo unaombwa na Kanisa linaposali hivi, “Ee Mungu Mwenyezi wa milele, utuzidishie imani, matumaini na mapendo” (Jumapili ya 30 ya mwaka).

Tukumbuke tofauti iliyopo kati ya kuomba na kustahili: asiye na neema ya utakaso hawezi kustahili (kwa kuwa neema hiyo ndiyo asili ya stahili yoyote ipitayo maumbile); lakini kwa neema ya msaada anaweza kuomba (k.mf. neema ya wongofu) na akiomba kwa unyenyekevu, imani na udumifu, atapata. Stahili inahusu haki ya Mungu; kumbe sala inaelekea huruma ya Mungu ambayo mara nyingi inanyanyua walioanguka na kusikiliza ombi lao lisilostahili chochote. Mtu duni kuliko wote, aliyetumbukia katika vilindi ambamo hawezi kustahili tena, anaweza kulilia huruma ya Mungu: “Kilindi chapigia kelele kilindi” (Zab. 42:7), yaani kilindi cha unyonge kinalilia kile cha huruma; mkosefu akisihi kwa moyo wote anasikilizwa, roho yake inanyanyuliwa, na Mungu anatukuzwa. Nguvu ya sala haitegemei tu neema ya utakaso iliyo ya lazima ili kustahili.

Tukishaongoka na kufanywa waadilifu, tunaweza kustawishiwa uzima wa neema kwa njia ya stahili na kwa sala pia. Hiyo ikiwa na unyenyekevu, imani na udumifu, inatupatia ustawi wa maadili ya Kimungu tunaoomba katika maombi matatu ya kwanza ya Baba Yetu. Sala ya mwadilifu, anayependa kutafakari polepole na kujilisha kwa undani maombi yake (hata kusimama pengine nusu saa kuzamia mojawapo kwa upendo), inastahili pamoja na kuomba neema: inampa haki ya kustawishiwa upendo ulioisababisha, na kwa nguvu ya ombi inapata zaidi kuliko inavyostahili. Tena, ikiwa ni motomoto kweli, inapata mara tu. Hapo tunaweza kuona matunda ya sala na jinsi inavyomvuta Mungu ajitoe kwetu kwa undani, nasi tujitoe kwake. Hapo moyo unazidi kupanuka upokee neema kwa wingi zaidi; roho inajitenga na malimwengu na kumtamani zaidi Mungu, ambaye ndani yake inakuta yale yote yanayostahili kupendwa, tena kwa ngazi ya juu. Haitatosha kamwe kuyaishi hayo katika sala ya moyo, k.mf. katika kimya kikubwa cha usiku, ambapo mtu yuko peke yake na Mungu, Muumba na Mwokozi wake. Hapo anang’amua kuwa Mungu ni mwema kupita kiasi, na sala ni mwanzo wa uzima wa milele.

Tena, kwa njia ya sala mwadilifu anaweza kupata neema kadhaa ambazo hawezi kuzistahili, hasa ile ya kudumu mpaka mwisho. Hawezi kustahili zawadi hiyo kwa kuwa ni kudumu kwa hali ya neema ambayo ni chanzo chenyewe cha stahili kisichoweza kustahiliwa. Hata hivyo neema hiyo ya kifo chema inaweza kupatikana kwa sala nyenyekevu, yenye imani, ya kila siku. Kanisa linatualika kukariri kwa bidii: “Maria mtakatifu, Mama wa Mungu, utuombee sisi wakosefu, sasa na saa ya kufa kwetu. Amina”.

Vivyo hivyo tunaweza kumuomba Mungu neema ya kumjua kwa ndani zaidi na zaidi, yaani ya kuzama katika sala, ambayo matokeo yake ni kuungana na Mungu kwa namna imara na yenye matunda mengi zaidi: “Neno moja nimelitaka kwa Bwana, nalo ndilo nitakalolitafuta: nikae nyumbani mwa Bwana siku zote za maisha yangu. Niutazame uzuri wa Bwana na kutafakari hekaluni mwake” (Zab. 27:4), yaani kuona kila siku vizuri zaidi jinsi wema wake usivyo na mipaka kwa wale ambao wanamtafuta na kumpata.

 

 

USTAWI WA UZIMA WA NEEMA KWA NJIA YA SAKRAMENTI

 

Hatimaye, upendo (pamoja na maadili mengine na vipaji saba) unastawi ndani mwetu kwa njia ya sakramenti, hasa ekaristi. Stahili na sala za mwadilifu zinapata zawadi za Mungu kulingana na imani na upendo alivyonavyo; kumbe sakramenti zinaleta neema kwa nguvu zake zenyewe katika wale wasioweka kizuio. Yaani zenyewe zinasababisha neema kwa kuwa ziliwekwa ili kutugawia stahili za Mwokozi. Zinaleta neema bila ya kutegemea sala na stahili za yule anayeziadhimisha na yule anayezipokea. Padri mwovu, na hata mtu asiye Mkristo, anaweza kuadhimisha ubatizo halisi mradi awe na nia ya kufanya Kanisa linavyofanya.

Hata hivyo sakramenti zinaleta neema kwa kiasi tofauti kulingana na juhudi za yule anayezipokea. Mtaguso wa Trento umefundisha: “Kila mmoja anapokea uadilifu kadiri Roho Mtakatifu anavyomtakia kulingana na utayari wake”. Kama vile moto unawaka wenyewe, lakini sisi tunafaidi joto lake kadiri tunavyoukaribia, upande wa roho tunafaidika na sakramenti kadiri imani yetu ilivyo hai na utashi wetu ulivyo motomoto. Kwa msingi huo Mkristo mkosefu anajipatia neema kadiri ya majuto yake wakati wa kupokea ondoleo la dhambi. “Inatokea kwamba nguvu ya majuto ya mwenye kuungama ni kubwa, sawa au pungufu kuliko kiwango cha neema alichokipoteza; hapo anapata tena neema kwa kiwango kikubwa, sawa au pungufu kuliko awali” (mt. Thoma wa Akwino). Kwa mfano, aliyekuwa na talanta tano kabla hajazipoteza kwa dhambi ya mauti, akija kuwa na majuto kama ya talanta mbili, anapata tena neema, lakini kwa kiasi kidogo kuliko awali. Kinyume chake, kwa majuto makubwa anaweza kuipata kwa kiwango kikubwa zaidi. Hilo ni muhimu kwa wale wanaokuja kuanguka wakati wa kupanda mlima; wanaweza kuinuka kwa bidii na kuendelea na safari yao kuanzia pale walipoanguka. Lakini wakiinuka kwa kuchelewa na bila ya bidii inawatokea kwamba wanajikuta chini, badala ya kuendelea tu kupanda.

Kwa msingi huohuo komunyo moja yenye bidii inafaa kuliko nyingi vuguvugu. Kadiri tunavyomkaribia Yesu katika ekaristi kwa imani hai, tumaini imara na upendo motomoto (upande wa utashi, si wa hisi) tunafaidi joto lake, yaani neema za mwanga, upendo na ushujaa za kututosha sisi hata kuwashirikisha wengine.

Kinyume chake, tunda la komunyo linaweza kuwa dogo tukikaribia meza takatifu kwa namna ambayo inatosha tu tusikufuru. Hiyo inatakiwa kutufikirisha tuking’amua kuwa hatuendelei kweli baada ya kukomunika kila siku kwa miaka kadhaa. Ingawa tunapaswa pia kuzingatia kwamba mtu akiendelea, kadiri anavyokuja kujua ukuu wa Mungu anazidi kufahamu vilevile unyonge wake mwenyewe. Inaweza kututokea kwamba, kwa kuambatana na dhambi fulani nyepesi, tunda la komunyo ya kila siku lizidi kupungua, kama kasi ya jiwe lililorushwa hewani wima ambayo inapungua zaidi na zaidi mpaka jiwe likaanguka tena ardhini. Mungu atuepushe!

Tunatakiwa tuwe na bidii nyingi kutosha itutokee kama katika maisha ya watakatifu: kwamba kila komunyo yetu iwe na upendo mkubwa na matunda mengi kuliko ile iliyotangulia. Kumbe mara nyingi uzembe na uvuguvugu yanazuia ustawi huo.

 

 

 

 

1.8. UKAMILIFU WA KIKRISTO NI NINI HASA?

 

 

Baada ya kuongelea chemchemi za maisha ya Kiroho, tunapaswa kuzingatia lengo lake: si lengo kuu tulilokwishalizungumzia tukisema kuwa maisha ya Kiroho ni mwanzo wa uzima wa milele, ila lengo lile linaloweza kufikiwa duniani, yaani ukamilifu wa Kikristo.

 

 

DHANA DANGANYIFU NA PUNGUFU KUHUSU UKAMILIFU

 

Zamani watu wasiostaarabika waliona ukamilifu wa binadamu unategemea hasa ushujaa. Wengi kati ya wanafalsafa wa Kigiriki waliona unategemea hasa hekima. Kumbe Injili inatuambia kuwa unapatikana hasa katika upendo. Tuzikumbuke kwa ufupi dhana hizo mbili za kwanza, tukitambua sura zilizonazo siku hizi. Hivyo tutaweza kuthamini zaidi ukuu wa ile ya tatu, pia kwa sababu hizo mbili zina chembe za ukweli ambazo chini ya upendo zinaweza kupata thamani kubwa.

 

Makabila yasiyostaarabika waliweka ukamilifu wa binadamu hasa katika nguvu, moyo, uhodari, tunavyoona katika hadithi zao. Pengine utaifa unaelekea kuwarudisha watu kwenye kipeo hicho, kinachotukuza mambo yaliyo magumu, ambayo yanahitaji nguvu nyingi na kuhatarisha uhai, k.mf. vitani. Ni mtazamo wa askari, mpelelezi na rubani. Umechanganyikana na kiasi kikubwa cha kiburi, na pengine cha utovu wa haki, tena hautoshi ili kumweka binadamu mahali pake mbele ya Mungu na ya jirani.

Kuna watu motomoto wanaosafisha dhana hiyo na kuihamisha upande wa roho wakimfikiria Mkristo kuwa askari wa Kristo na kujali mno kifodini. Kumbe ubora wa kifo hicho hautokani na kuwa tendo la uhodari, bali na kuwa ishara angavu ya upendo mkuu. Karne tatu za dhuluma za Kanisa la mwanzoni zilikuwa za uhodari, lakini hasa za upendo mkubwa: ndio unaotofautisha wafiadini wa Kikristo na mashujaa wa kipagani.

Kwa mtazamo unaofanana na huo kuna watu wanaoona ukamilifu umo hasa katika ugumu wa maisha (mafungo, makesha n.k.): huo unaweza kuhitajika kwa utawa unaokusudia hasa sala na sadaka ambazo ni ishara za upendo. Ila tusiufanye ugumu huo kuwa lengo wakati ni njia tu ya maendeleo. La sivyo maisha makamilifu zaidi yangekuwa yale magumu zaidi, si yale yenye lengo bora na njia za kufaa zaidi kulifikia. Maisha ya Kiroho yanahusu uadilifu kuliko ugumu. Kwanza si kila tendo gumu ni adilifu: pengine ni juhudi ya ushupavu tu. Halafu uadilifu ni mgumu mara nyingi, lakini si daima: vitendo kadhaa vya upendo vinatendeka pasipo shida, kwa msukumo mkubwa wa roho, hata hivyo vina stahili kubwa kwa kuwa vinatokana na upendo mkubwa. Je, nguvu ndio adili bora? Ndio sifa muhimu ya askari, lakini je, ndio ukamilifu wa mtu kama mtu na wa Mkristo kama Mkristo?

Jibu ni kwamba nguvu ni ya lazima kwa ukamilifu, lakini juu yake kuna haki kuhusu wengine, kuna busara inayoongoza maadili yote ya kibinadamu, na hasa kuna maadili ya Kimungu yanayomlenga Mungu moja kwa moja: imani, tumaini na upendo. Basi, hatuwezi kukubali kuwa ukamilifu wa mtu na wa Mkristo umo hasa katika nguvu. Hiyo si ukamilifu wa akili yetu kuhusu ukweli mkuu, wala si ukamilifu wa utashi wetu kuhusu wema mkuu, ila ni adili linaloshinda hofu tu ili tuzidi kufuata njia nyofu hata tukiwa kwenye shida na hatari.

 

Ikiwa ukamilifu haumo hasa katika ushujaa, je, utapatikana katika hekima? Ndivyo walivyodhani wanafalsafa wengi, wakisema binadamu anatofautiana na viumbe vilivyo chini yake kwa akili aliyonayo, kwa hiyo ukamilifu wake kama binadamu ni hasa ule wa akili yake, yaani hekima au ujuzi mkuu.

Hakika hekima inahitajika kwa ukamilifu, lakini si kweli kwamba kumjua kimawazo Mungu kunafuatwa daima na upendo kwake. Mwanafalsafa, hata kama ana akili na wazo sahihi kuhusu Mungu kama asili na lengo kuu la ulimwengu, anaweza akawa mwovu. Ukweli ni ukamilifu wa akili, lakini si ukamilifu wa mtu mzima, wala si jema pekee la binadamu.

Elimu inaweza kuwepo pasipo upendo kwa Mungu na kwa jirani, na hapo “huleta majivuno” (1Kor. 8:1). Ukamilifu wa mtaalamu kama mtaalamu si ule wa binadamu kama binadamu, wala ule wa Mkristo kama Mkristo. Tusichanganye ukamilifu wa akili na ule wa mtu mzima unaohitaji kunyosha utashi kuhusu lengo kuu. Utashi unakusudiwa kuelekezwa kwenye ustawi wa mtu mzima, sio wa akili tu. Uadilifu unadai utashi unyoshwe, tofauti na sanaa na sayansi. Hapo tu mtu anaitwa mtu mwema moja kwa moja, sio tu mchoraji mzuri, mjenzi mzuri au mganga mzuri.

Hatimaye hapa duniani kumpenda Mungu ni bora kuliko kumjua. Ujuzi unamvuta kwetu na kumlazimisha ndani ya mipaka ya mawazo yetu finyu; kumbe upendo wa Mungu unatuvuta kwake na kutufanya tupende ndani mwake hata yale tusiyoweza kuyajua sawasawa, kwa sababu tuna hakika ya kuwa maisha yake ya ndani yaliyofichika kwetu yanapendeza kupita kiasi.

Dhana ya kuwa hekima ndiyo ukamilifu inajitokeza leo katika wale wanaojali elimu kuliko yote. Hata baadhi ya Wakristo wanaelekea kudhani inawezekana kuufikia ukamilifu haraka kwa kusoma maandishi mengi ya watakatifu, bila ya kujitahidi zaidi katika utekelezaji wa maadili yao, wala kukumbuka vya kutosha kuwa sala ya kujaliwa kuzama ndani ya Mungu inatakiwa kujaa upendo upitao maumbile na kujikana.

Tutaona mbele kuwa sala hiyo sio ukamilifu hasa, bali huo umo katika kuungana na Mungu kwa upendo; ila kumtazama kwa upendo ni njia iliyounganika na lengo hilo kwa sababu kunatuandaa moja kwa moja tuungane naye. Lengo letu lisiwe hasa sala hiyo, bali Mungu mwenyewe ambaye apendwe kuliko yote.

Basi, kwa ukamilifu vinahitajika kweli ushujaa na hekima, yanahitajika pia maadili yote ya Kimungu na ya kibinadamu, pamoja na vipaji saba vya Roho Mtakatifu. Je, ukamilifu umo katika jumla ya maadili? Ndiyo, mradi jumla hiyo iwe imepangwa vizuri kama muundo hai na kati ya maadili liwepo moja lenye kuyatawala, kuyaongoza na kuyahuisha yote na kuelekeza juhudi zake zote kwenye lengo kuu. Kama ni hivyo, ukamilifu umo hasa katika adili hilo kuu ambalo mengine yote yanapaswa kulisaidia. Lenyewe ni lipi?

 

UKAMILIFU KADIRI YA INJILI ILIVYOFAFANULIWA NA MTUME PAULO

 

Bwana ametukumbusha kwa namna mbalimbali kwamba amri inayotawala amri na mashauri yote ni ile ya upendo iliyotajwa tayari katika Agano la Kale: “Mpende Bwana, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote” (Kumb. 6:5). “Umpende jirani yako kama nafsi yako. Mimi ndimi Bwana” (Law. 19:18). Ndicho kipeo kikuu kuliko ushujaa na hekima. Ndani yake mna nguvu ya aina nyingine, tena mna hekima ya kweli na ya juu zaidi.

“Kwa kuwa mmekuwa wateule wa Mungu, watakatifu wapendwao, jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana na kusameheana… Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu” (Kol. 3:12-14)”. Upendo ndio kifungo cha ukamilifu kwa kuwa ni adili bora ambalo linatuunganisha na Mungu na kudumu milele; ndio unaohuisha maadili mengine yote yawe na stahili kwa kuyalengesha kwa Mungu mpendwa kuliko yote.

Mt. Paulo alikuwa na hakika kuhusu upendo kuwa bora kuliko maadili mengine yote na vipaji vya Roho Mtakatifu na karama mbalimbali: “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao. Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi. Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu” (1Kor. 13:1-3). Pasipo upendo karama za pekee hazisaidii kitu kwa uzima wa milele. Kwa sababu nisipokuwa na upendo sitekelezi amri ya kwanza ya Mungu, silinganishi matakwa yangu na ya kwake, napotoka mbali naye, nimeshika njia isiyoelekea kwenye moyo wa Mungu. Basi, katika wokovu “kama sina upendo, si kitu mimi”, sistahili kitu ingawa ninaweza nikawasaidia wengine kuokoka kwa mahubiri na kwa miujiza.

Kwa maana hiyo, mt. Augustino alisema, “Penda, halafu tenda lolote utakalo”, nalo litakustahilisha uzima wa milele. Lakini uwe na upendo halisi, kwa sababu hakuna lililo baya kuliko upendo wa bandia (unaofumba macho usitimize wajibu wake dhidi ya maovu: huo ni udhaifu, ni ule upole wa kulaumiwa wa watu wasiomchukiza yeyote kwa kuwa wanaogopa. Au ni miguso ya kibinadamu tu inayotaka kukubaliwa na upendo halisi na kuuambukiza). Kati ya mapambano makuu ya leo, mojawapo ni lile kati ya upendo halisi na upendo wa bandia, ambao unatukumbusha Makristo wa uongo wanaozungumziwa na Injili. Uharibifu mbaya zaidi ni ule unaohusu yaliyo bora, kama vile upendo ulio adili kuu. Kwa kuwa yale yanayoonekana tu mema ni ya hatari kadiri yalivyo bora mema halisi yanayoigizwa nayo (k.mf. kipeo cha wanaotaka kuunganisha madhehebu ya Kikristo kwa kupunguza kweli za imani). Ikiwa kwa upumbavu au woga wale wanaotakiwa kuwakilisha upendo halisi wanayakubali kwa namna moja au nyingine yale yanayoficha upendo wa bandia, yanaweza kutokea mabaya yasiyopimika, makubwa kuliko yale yanayoweza kusababishwa na watesi waliojitokeza ambao ni wazi kuwa hatuwezi kushirikiana nao.

Tofauti na upendo wa bandia, ndani ya ule halisi yamo maadili yote nayo yako chini yake hivi kwamba yanaonekana kama namna na sura mbalimbali za upendo kwa Mungu na kwa jirani. “Upendo huvumilia, hufadhili; upendo hauhusudu; upendo hautakabari, haujivuni; haukosi kuwa na adabu; hautafuti mambo yake; hauoni uchungu; hauhesabu mabaya; haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli; huvumilia yote, huamini yote; hutumaini yote, hustahimili yote. Upendo haupungui neno wakati wowote; bali ukiwapo unabii utabatilika; zikiwapo lugha, zitakoma; yakiwapo maarifa, yatabatilika… Maana wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso… Basi, sasa inadumu imani, tumaini, upendo, haya matatu; na katika hayo lililo kuu ni upendo” (1Kor. 13:4-8,12-13). Imani itatoweka kwa kumuona Mungu, tumaini kwa kumpata, lakini upendo utadumu milele.

Kwa upendo huo tunakuwa hekalu la Roho Mtakatifu. Kadiri tunavyompenda Mungu tunamfahamu na kama kumng’amua kwa ujuzi upitao maumbile, jina lake hekima ya Kimungu. “Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo; ili mpate kufahamu pamoja na watakatifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo na kina; na kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate kutimilika kwa utimilifu wote wa Mungu” (Ef. 3:17-19).

Mafundisho hayohayo tumepewa na mt. Yohane: “Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake… Yeye ampendaye Mungu, ampende na ndugu yake” (1Yoh. 4:16,21). Mt. Petro aliandika vilevile: “Zaidi ya yote iweni na juhudi nyingi katika kupendana, kwa sababu upendano husitiri wingi wa dhambi” (1Pet. 4:8). Alivyosema Yesu: “Amesamehewa dhambi zake ambazo ni nyingi, kwa kuwa amependa sana” (Lk. 7:47).

Kadiri ya mafundisho hayo, ukamilifu haumo hasa katika unyenyekevu na ufukara, wala katika ibada, bali katika upendo kwa Mungu na kwa jirani unaofanya matendo ya maadili mengine yote yastahili. Ufukara sio ukamilifu, ila ni njia ya ukamilifu. Basi, njia haitafutwi kwa ajili yake, bali kwa ajili ya lengo, nayo ni bora si kulingana na ukubwa wake, bali kulingana na jinsi inavyolingana na lengo, kama vile daktari mzuri ni yule anayetoa matibabu yanayoponya, si anayeyatoa mengi zaidi. Ni vivyo hivyo kuhusu unyenyekevu unaotuinamisha mbele ya Mungu ili kupokea kwa mikono miwili msaada wake ambao utuinue hadi kwake. “Unyenyekevu ni adili la msingi kwa kuwa unaondoa kizuio kikuu, yaani kiburi, lakini umo chini ya maadili ya Kimungu yanayotuunganisha na Mungu” (mt. Thoma wa Akwino). Hata adili la ibada, linalompatia Mungu ibada inayompasa, liko chini ya maadili ya Kimungu; halistahili lisipohuishwa na upendo. Si adili la Kimungu kwa sababu halimhusu Mungu moja kwa moja, ila ibada yake. Tukisahau ukweli huo tunaweza tukazingatia liturujia kuliko Mungu mwenyewe, mifano kuliko ukweli, namna ya kusali Baba Yetu kuliko maana yake: hapo utumishi wa Mungu ungepiku upendo wake.

 

MAELEZO MENGINE YA TEOLOJIA KUHUSU UKAMILIFU

 

“Kila kiumbe ni kamili kadiri kinavyofikia lengo lake ambalo ndio ukamilifu wake wa mwisho. Sasa, lengo kuu la maisha ya binadamu ni Mungu, na upendo ndio unaotuunganisha naye, kadiri ya neno la mt. Yohane: ‘Kila mtu aishiye katika upendo, anaishi katika muungano na Mungu, na Mungu anaishi katika muungano naye’. Basi, ukamilifu wa maisha ya Kikristo umo hasa katika upendo” (mt. Thoma wa Akwino). Imani na tumaini haviwezi kuwa kiini cha ukamilifu, kwa sababu vinaweza kuwepo katika mtu ambaye kwa dhambi ya mauti amepotosha utashi wake mbali na Mungu, aliye lengo lake kuu. Vinabaki ndani mwake kama mzizi wa mti uliokatwa na ambao unaweza kuchipua tena.

Mt. Thoma akaongeza: “Ukamilifu umo hasa katika upendo kwa Mungu, halafu katika upendo kwa jirani, kwa kuwa ndio amri kuu za sheria ya Kimungu”. Hatutaweza kamwe kusisitiza mno neno la Bwana: “Amri mpya nawapa: Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi” (Yoh. 13:34-35). Ndiyo dalili kuu ya ustawi wa upendo wa Mungu mioyoni mwetu: “Yeye asemaye kwamba yumo nuruni, naye amchukia ndugu yake, yumo gizani hata sasa… Sisi tunajua ya kuwa tumepita toka mautini kuingia uzimani, kwa maana twawapenda ndugu. Yeye asiyependa, akaa katika mauti. Kila amchukiaye ndugu yake ni mwuaji; nanyi mnajua ya kuwa kila mwuaji hana uzima wa milele ukikaa ndani yake” (1Yoh. 3:14-15).

Sasa tuzingatie mambo mawili yanayotofautisha ukamilifu wa duniani na ule wa mbinguni.

 

HAPA DUNIANI “KUMPENDA MUNGU NI BORA KULIKO KUMJUA”

 

Ni lazima tusisitize neno hilo la mt. Thoma wa Akwino. Yeye alikubali kuwa akili ni bora kuliko utashi unaoongozwa nayo, kuwa ni uwezo wa kwanza wa binadamu unaomtofautisha na mnyama, kuwa mbinguni heri yetu itatokana hasa na akili kumuona Mungu uso kwa uso, kwa kuwa ndiyo njia ya kumpata milele: kuzamisha akili yetu katika vilindi vya maisha yake ya ndani yakiwa wazi tu. Hivyo Mungu atajitoa moja kwa moja kwetu, nasi tutajitoa kwake; sisi tutakuwa naye kama mali yetu, nasi tutakuwa mali yake, kwa kuwa tutamfahamu kama anavyojifahamu na anavyotufahamu. Upendo wenye heri utakuwa matokeo ya huo mtazamo wa moja kwa moja wa umungu, tena matokeo ya lazima, kwa kuwa utashi wetu utavutwa moja kwa moja na uzuri wa Mungu. Tutaona wema wake mkuu kwa namna iliyo wazi hivi hata tusiweze kutompenda; hatutaweza kuona kisingizio chochote cha kusimamisha kwa nukta moja tu tendo hilo la upendo lililo juu kuliko hiari yetu, na ambalo halitapimwa na muda, bali na umilele tulioshirikishwa, ile nukta pekee isiyokwisha kamwe ya Mungu kuwepo pasipo badiliko. Mbinguni upendo kwa Mungu na furaha ya kuwa naye kama mali yetu vitatokana kwa lazima na heri ya kumuona iliyo kiini cha heri yetu yote.

Kama ni hivyo, basi, mwalimu huyo aliwezaje kusema ukamilifu wa Kikristo hapa duniani umo hasa katika upendo ambao ni adili la utashi, badala ya kuwemo hasa katika hekima au katika sala ya kumiminiwa ambazo zinahusu akili? Jibu alilolitoa ni zito tena muhimu.

Kwa ufupi alisema kuwa kipawa fulani kinaweza kuwa bora kuliko kingine kwa maumbile yake, lakini tendo fulani la hicho cha pili linaweza kuwa bora kuliko mojawapo la hicho cha kwanza. Kwa mfano uwezo wa kuona ni bora kuliko ule wa kusikia, na kuwa kipofu ni tatizo kubwa kuliko kuwa kiziwi; lakini kusikiliza muziki bora kuna thamani kuliko kuona vitu vya kawaida. Vivyo hivyo, ingawa kwa maumbile yake akili ni bora kuliko utashi, hapa duniani kumpenda Mungu ni bora kuliko kumjua. Basi, ukamilifu unapatikana hasa katika kumpenda, hivi kwamba mtakatifu ambaye hana elimu lakini ana upendo mkubwa kwa Mungu kwa hakika ni mkamilifu kuliko mwanateolojia mkuu mwenye upendo mdogo. Jambo hilo, ambalo Wakristo wote wanalielewa kwa urahisi, tukilifikiria kwa makini linaonekana ukweli wa thamani unaoweza kuthibitishwa na madondoo mengi ya Biblia na ya walimu wa Kiroho.

Huo ubora wa upendo hapa duniani unatokana na kwamba “kazi ya akili yetu inafanyika kwa kujichorea ukweli uliojulikana, kumbe utashi wetu unavutwa na upendo kukiendea kilichopendwa jinsi kilivyo. Alivyosema mwanafalsafa, wema ulio lengo la utashi umo ndani ya vitu, kumbe ukweli umo hasa katika roho yetu” (mt. Thoma wa Akwino). Kwa hiyo tunapomjua Mungu, kwa namna fulani tunambana ndani ya mipaka ya mawazo yetu finyu ili tujichoree alivyo; kumbe tunapompenda, sisi ndio tunaovutwa naye na kuinuliwa kwake jinsi alivyo kweli. Basi, duniani na toharani upendo kwa Mungu ni bora kuliko kumjua; unahitaji kumjua kwanza, lakini unapita ujuzi huo.

Tena tokea hapa duniani upendo wetu unamfikia Mungu na kuambatana naye moja kwa moja: “Ujuzi wetu unainuka kwa Mungu kutoka kwa viumbe, kumbe upendo wetu kutoka kwa Mungu unawashukia viumbe” (mt. Thoma wa Akwino).

Hatimaye, sisi tunapenda ndani ya Mungu hata yale tusiyoyajua, kwa sababu tuna hakika ya kuwa yeye ndiye wema wenyewe. Kwa maana hiyo tunaweza kumpenda Mungu kuliko tunavyomfahamu; tena ndani mwake tunapenda zaidi yale yaliyofichika, kwa kuwa tunaamini ndiyo maisha yake ya dhati yanayopita uwezo wowote wa kujua. Basi, hapa duniani upendo kwa Mungu unashinda ujuzi unaomhusu. Hilo ni ajabu linalotuonyesha ukuu wa upendo juu ya imani na tumaini, juu ya ujuzi wowote tunaoweza kuwa nao duniani, na hata juu ya tendo la kuzama katika sala, kwa kuwa hata hilo halimpati bado Mungu jinsi alivyo, na utamu ulilonalo unatokana na upendo unaoliongoza.

Ndiyo sababu upendo ni kifungo cha ukamilifu: hakuna adili linalotuunganisha na Mungu kwa undani kuliko hili, tena maadili mengine yote yanaongozwa na kuhuishwa na kulengeshwa na upendo kwa Mungu anayependwa kuliko yote.

Tunapaswa kukariri pamoja na mapokeo yote ya Kanisa kwamba ukamilifu wa Kikristo umo hasa katika upendo wa vitendo ambao unatuunganisha kweli na Mungu katika ukavu kama katika faraja, na kuzaa kila aina ya vitendo vyema. Kwa usahihi zaidi ukamilifu haumo hasa katika adili lenyewe la upendo, bali katika utekelezaji wake ambao katika waliokamilika ni wa kudumu. Kwa sababu lengo la adili ni kutekelezwa, na ukamilifu umo katika muungano wa kudumu na Mungu. Kumbe Watulivu walikataa utendaji wowote ili wamuachie Mungu tu kutenda; hali yao ya kutotenda ilikuwa ya kujitakia kwa kujizuia, si ya kujaliwa: ilikuwa kama kusinzia tu! Hivyo walifuta juhudi na kupotosha hali za juu za kujaliwa. Kinyume chao, ni wale wanaodhani ukamilifu umo katika kuwasaidia watu, wakisahau kuwa upendo kwa Mungu ni wa juu kuliko ule kwa jirani ambao ni ishara na tunda lake tu. Hivyo wanapindua mpangilio wa upendo. Wengine tena, wanaozingatia zaidi maisha ya Kiroho, wanazidisha matendo ya sala badala ya kulenga sala sahili ya kimapenzi ambayo ni kama tendo moja tu linalodumu kwa muda fulani.

Basi upendo unatakiwa kushika nafasi ya kwanza rohoni mwetu, juu kuliko hamu ya ujuzi na ya maendeleo ya kibinadamu ya aina yoyote; hapo upendo wenyewe utazidisha nguvu zetu kwa kumtumikia Mungu na jirani.

 

 

HAPA DUNIANI UPENDO HAUWEZI KUDUMU KAMA MBINGUNI

 

Mungu tu anaweza kujipenda anavyostahili, kama vile mwenyewe tu anaweza kujifahamu kikamilifu; lakini watakatifu wa mbinguni, ingawa hawampendi anavyostahili, wanampenda kwa nguvu zao zote, kwa upendo wa kudumu moja kwa moja. Hiyo haiwezekani hapa duniani, hasa kutokana na usingizi.

Ukamilifu unaowezekana hapa duniani ni ule unaozuia yale yote yanayopinga upendo wa Mungu (yaani dhambi ya mauti) na yale yote yanayofanya upendo usimuelekee kikamilifu. Waadilifu wanaoanza maisha ya Kiroho na wale wanaoendelea wanalenga huo muungano na Mungu ambao ni maalumu wa waliokamilika. Kwao ukamilifu wa upendo unazuia sio tu dhambi ya mauti na dhambi nyepesi za makusudi, bali pia kasoro za hiari, k.mf. juhudi chache katika kumtumikia Mungu, na mazoea ya kutenda kwa namna pungufu (kulingana na talanta zao) na ya kupokea sakramenti pasipo utashi kutamani kweli. Upendo wa waliokamilika kwa jirani unaenea si kwa wote jumla tu, bali ikipatikana nafasi kwa kila mmoja wa wale ambao wana fungamano lolote nao: sio kwa marafiki tu, bali kwa wengine wowote na hata kwa maadui. Tena ndani mwao upendo huo wa kidugu una nguvu hata ya kujitolea mali na uhai kwa ajili ya watu, kwa kuwa Bwana ametuambia, “Amri yangu ndiyo hii: Mpendane, kama nilivyowapenda ninyi” (Yoh. 15:12). Ndiyo sababu mt. Paulo aliandika: “Nami kwa furaha nyingi nitatapanya, tena nitatapanywa kwa ajili ya roho zenu” (2Kor. 12:15).

Ili tufikie hatua hiyo vinahitajika: kazi kubwa juu ya nafsi zetu, mapigano halisi, moyo wa kujikana na kujikatalia hivi kwamba mapendo yetu yaache kuteremka kuelekea vitu vya dunia au ubinafsi, na badala yake yazidi kuinuka kwa Mungu kwa usafi na nguvu. Maisha ya roho yakiacha kushuka, yanapanda juu kwa Mungu. Hapa duniani roho haiwezi kubaki pale ilipo; sheria yake, kama ile ya moto, ni kupanda, si kushuka.

Hapa duniani upendo wa waliokamilika, ingawa si wa kudumu moja kwa moja kama ule wa mbinguni, unatenda karibu mfululizo na kwa namna ya ajabu: “Upendo ni jambo kubwa sana; ni jema kushinda mema yote. Upendo peke yake hugeuza mazito kuwa mepesi, hubeba magumu kwa urahisi… Upendo una hamu ya kupaa, hautaki kuzuiwa na mambo ya chini… Upendo umetoka kwa Mungu, hauwezi kutulia isipokuwa kwa Mungu peke yake mbali na viumbe vyote. Mwenye upendo huenda kama kuruka, huenda mbio kwa furaha, yu huru, hazuiliki, hutoa yote kusudi apewe yote; katika mambo yote yeye hupata yote, kwa sababu humtegemea yule aliye juu kabisa, ndiye asili panapotokea mema yote… Mara nyingi hupendo haujui kiasi, huchemka kupita kiasi chochote… Upendo hukesha unapolala, hausinzii usingizi; unapochoka haupumziki… Kama moto unaoteketea, kama mwenge unaowaka huruka juu, hupenya kila mahali” (Kumfuasa Yesu Kristo III,5:3-5).

Hayo ndiyo maisha ya watakatifu. Ndiyo wito wetu, kwa kuwa tunaitwa kuishi mbinguni, ambapo wapo watakatifu tu. Ili tufike huko tunapaswa kutakasa kila tendo la siku zetu, tukikumbuka kwamba juu ya mfululizo wa matukio ya kila siku (ya kupendeza na ya kuchukiza, yaliyotarajiwa na yasiyotarajiwa) kuna mfululizo sambamba wa neema za msaada tunazojaliwa dakika baada ya dakika ili tufaidi upeo matukio hayo. Hapo tutayaona sio tu upande wa hisi au wa akili iliyopotoshwa na umimi, bali upande wa roho kwa imani. Hapo matukio hayo yatakuwa kama mafundisho ya mambo ya Bwana, utekelezaji wa mafundisho ya Injili, na polepole kati yake na sisi yataanza maongezi ambayo karibu hayana kikomo: ndiyo maisha halisi ya Kiroho na kama mwanzo wa uzima wa milele.

 

 

 

 

1.9. UKUU WA UKAMILIFU WA KIKRISTO NA HERI NANE

 

 

Ukamilifu wa Kikristo umo hasa katika upendo unaotuunganisha na Mungu. Lakini baadhi ya wanateolojia waliwahi kujiuliza kama ukamilifu huo unadai upendo mkubwa au unaweza kupatikana pasipo kiwango kikubwa cha adili hilo. Jibu la hakika ni kwamba, kama vile utu uzima unadai nguvu za mwili nyingi kuliko za mtoto (ingawa kwa nadra watoto wenye afya wana nguvu kuliko watu wazima kadhaa), hata hali ya waliokamilika inadai upendo mkubwa kuliko ule wa wanaoanza (ingawa watakatifu kadhaa, mwanzoni mwa maisha ya Kiroho, wana upendo mkubwa kuliko baadhi ya wazee waliokamilika).

Fundisho hilo lina msingi katika mahubiri ya Mwokozi, hasa aliposema juu ya heri zinazofafanua ukuu wa ukamilifu wa Kikristo ambao Yesu anawaitia wote. Hotuba ya mlimani ni muhtasari wa mafundisho aliyoyatoa ili kutimiliza sheria ya Musa na kusahihisha ufafanuzi wake usiofaa. Heri nane zilizotangazwa mwanzoni mwa hotuba hiyo zinajumlisha vizuri ajabu kipeo cha maisha ya Kikristo zikionyesha ukuu wake wote.

Neno la kwanza la Yesu ni kuahidi heri na kuelekeza njia za kuzipata. Alianza na heri kwa sababu kila mtu kwa maumbile yake anaitamani: ndiyo lengo ambalo wote, watake wasitake, wanalitafuta katika yote. Lakini mara nyingi wanatafuta heri mahali isipokuwepo, ambapo watakuta tu mahangaiko na unyonge. Tumsikilize Bwana ambaye anatuambia heri halisi ya kudumu na lengo la maisha yetu viko wapi, tena anatupatia njia za kuvipata.

Lengo linaelekezwa na kila neno la heri, na kwa majina mbalimbali ni ile heri ya milele ambayo waadilifu wanaweza kuanza kuionja hapa duniani: ni ufalme wa Mungu, nchi ya ahadi, faraja kamili, utimilifu wa hamu zote zilizo halali na takatifu, rehema kuu, kumuona Mungu Baba yetu. Njia zinakwenda kinyume cha maelekezo ya dhana za ulimwengu, kwa kuwa lengo lenyewe ni tofauti mno.

Mpangilio wa heri nane unaanzia chini kwenda juu (kinyume na sala ya Baba Yetu ambayo kutoka kuzingatia utukufu wa Mungu inateremkia mahitaji yetu). Heri tatu za kwanza ni zile zinazopatikana katika kukwepa dhambi na kukombolewa: katika ufukara uliopokewa kwa upendo wa Mungu, katika upole na katika machozi ya majuto. Heri mbili zinazofuata ni zile za maisha ya utendaji ya Kikristo: zinahusu kiu ya haki na utekelezaji wa huruma kwa jirani. Halafu zinakuja zile za kuzama katika mafumbo ya Mungu: usafi wa moyo unaotuandaa kumuona na amani inayotokana na hekima ya kweli. Heri ya mwisho na bora kuliko zote ni ile inayoziunganisha zilizotangulia hata wakati wa kudhulumiwa kwa ajili ya haki.

 

HERI ZA UKOMBOZI KUTOKA DHAMBI

 

Hizo zinahusu hatua ya utakaso, ambayo ni maalumu kwa wanaoanza.

Wakati ulimwengu unasema kuwa heri inapatikana katika wingi wa mali, utajiri na heshima, Bwana amesema waziwazi, kwa hakika tulivu ya ukweli mkuu, “Heri walio maskini wa roho, maana ufalme wa mbinguni ni wao” (Math. 5:3). Kila heri ina viwango mbalimbali: heri walio fukara bila ya kunung’unika, kwa uvumilivu, bila ya wivu, hata wakikosa chakula, na ambao wanafanya kazi wakimtegemea Mungu tu. Heri waliobahatika zaidi, lakini hawana roho ya utajiri, fahari, kiburi, wala hawashikamani na mali. Heri zaidi walioacha vyote ili kumfuata Yesu, waliojifanya fukara kwa hiari na kuishi kweli wito huo; hao watapata mara mia hapa duniani halafu uzima wa milele. Fukara hao ni wale ambao, kwa kuvuviwa kipaji cha uchaji, wanafuata njia ambayo ni nyembamba mwanzoni, lakini baadaye inakuwa barabara kuu ya mbinguni, ambapo roho inapanuka zaidi na zaidi, wakati njia pana za ulimwengu zinaelekea maangamizi: “Ole wenu ninyi ambao mmeshiba sasa, kwa kuwa mtaona njaa” (Lk. 6:25). Kinyume chake, ufukara wenye heri unatufungulia ufalme wa Mungu, ulio bora kuliko mali yoyote, yanavyoonyesha maisha ya mt. Fransisko wa Asizi. Heri wanyenyekevu wa moyo, wasiojitwalia mema ya kimwili wala ya Kiroho, wala heshima wala upendo, na ambao hawatafuti chochote isipokuwa ufalme wa Mungu.

Wakati tamaa ya utajiri inawatenga watu na kusababisha ugomvi, mashtaka, kesi, dhuluma na hata vita kati ya mataifa, Yesu amesema, “Heri wenye upole, maana hao watairithi nchi” (Math. 5:5). Heri wasiowakasirikia ndugu zao, wasiotafuta kulipa kisasi wala kuwatawala wengine, wasiohukumu bila ya msingi, wasiomuona jirani kama adui wa kushindana naye, bali kama ndugu wa kusaidiwa, mtoto wa Baba yuleyule wa mbinguni. Kipaji cha ibada ndicho kinachotutia upole huo kwa mapendo ya kitoto hasa kwa Mungu, Baba yetu sote. Walio wapole hawashikamani mno na mtazamo wao wala hawaoni haja ya kuapa kwa chochote kile. Ili tuwe wapole hivyo, hata kwa wanaotutendea kwa ukali, tunahitaji kuungana na Yesu aliyesema, “Mjifunze kwangu, kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo” (Math. 11:29). Yeye hakuvunja “mwanzi uliopondeka” wala kuzima “utambi utokao moshi” (Math. 12:20) hata alifananishwa na “mwanakondoo apelekwaye machinjoni” asifunue “kinywa chake” (Isa. 53:7; Mdo. 8:32). Upole huo si ule usiomchukiza yeyote kwa sababu unaogopa, bali ni adili linalotegemea upendo mkubwa kwa Mungu na kwa jirani: unazidisha thamani ya huduma unayotoa, unaweza kusema lolote na kufanya mashauri yake yapokewe, na hata lawama kwa kuwa anayeambiwa anatambua kuwa vinatokana na upendo mkubwa. Heri walio wapole, maana watairithi nchi halisi ya ahadi; na tangu sasa wanajipatia kitakatifu mioyo ya wale wanaojiaminisha kwao.

Wakati ulimwengu unasema furaha imo katika anasa, Yesu amesema, “Heri wenye huzuni, maana hao watafarijika” (Math. 5:4). Tajiri alijibiwa vilevile: “Wewe uliyapokea mambo mema yako katika maisha yako, na Lazaro vivyo alipata mabaya; na sasa yeye yupo hapa anafarijiwa, na wewe unaumizwa” (Lk. 16:25). Heri yao wale ambao, kama Lazaro, wanateseka kwa subira, bila ya kufarijiwa na watu; ila Mungu anaona machozi yao. Wenye heri zaidi wanaolia juu ya dhambi zao, ambao kwa kipaji cha elimu wanang’amua kwamba dhambi ndiyo baya kubwa kuliko yote, na kwa kulia machozi wanajipatia msamaha. Hatimaye wana heri zaidi wanaolia kwa upendo wakizingatia huruma na hisani visivyo na mipaka vya mchungaji mwema aliyejitoa sadaka kwa kondoo zake. Hao wanapokea farajia isiyo na kifani kuanzia hapa duniani.

 

 

HERI ZA MAISHA YA UTENDAJI YA KIKRISTO

 

Furaha nyingine takatifu zimeandaliwa kwa mwadilifu ambaye, kisha kuopolewa katika maovu, anajitahidi kutenda mema kwa moyo wote.

Mtu mwenye shughuli nyingi anayetawaliwa na kiburi anamuita mwenye heri yule anayeishi na kutenda anavyotaka, asiyekaa chini ya wengine bali anawashinda. Kumbe Yesu amesema, “Heri wenye njaa na kiu ya haki, maana hao watashibishwa” (Math. 5:6). Maana pana ya hilo neno “haki” ni kumpatia Mungu yale anayostahili; hapo kwa upendo wake hata kiumbe anapatiwa anayostahili: kama malipo Mungu anajitoa kwetu. Ndio utaratibu kamili, katika utiifu kamili, ambao unaongozwa na upendo unaopanua moyo. Wenye heri wanaotamani haki hiyo hadi kuwa na njaa na kiu nayo. Kwa namna fulani hao watashibishwa kuanzia hapa duniani, kwa kugeuka waadilifu na watakatifu zaidi. Kiu hiyo ina heri kweli: “Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe… mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake” (Yoh. 7:37-38). Lakini ili kudumisha kiu hiyo hata hisi zikiwa zimepoa Kiroho, au katikati ya upinzani, vizuio, kukata tamaa, ni lazima tupokee kwa mikono miwili kipaji cha nguvu, ambacho kinatuzuia tusishindwe wala tusikate tamaa, na kinatutia moyo katika matatizo. “Bwana anataka tuitamani haki hiyo hivi kwamba tusishibe kamwe hapa duniani, kama vile mwenye uroho asivyoshiba kamwe… Watashiba watakapomuona Mungu milele… na tangu sasa katika mema ya Kiroho… Watu wakiwa katika dhambi, hawasikii njaa ya Kiroho, lakini wanapoacha dhambi hapo wanaisikia” (mt. Thoma wa Akwino).

Lakini njaa na kiu za haki hazitakiwi kuendana na ari chungu kuhusu wakosefu: “Heri wenye rehema, maana hao watapata rehema” (Math. 5:7). Katika maisha yetu, kama vile kwa Mungu, haki inapaswa kuungana daima na huruma. Hatuwezi kuwa wakamilifu tusipomsaidia mwenye uchungu au ugonjwa kama alivyofanya Msamaria mwema. Bwana atawalipa wanaojitolea bilauri ya maji kwa upendo wake, wanaokaribisha mezani pao fukara, walemavu na vipofu. Mkristo anapaswa kufurahia zaidi “kutoa kuliko kupokea” (Mdo. 20:35), tena kusamehe (kwa Kilatini “kutoa zaidi”) waliomchukiza, kusahau dharau na kupatana na nduguye kabla hajatolea altareni sadaka yake. Kipaji cha shauri kinatuelekeza kwenye huruma, na kutufanya tutambue mateso ya wenzetu pamoja na dawa yake, yaani pengine neno la kuwainua na kuwafariji.

Kama utendaji wetu utafuata mara nyingi maadili hayo mawili ya haki na huruma, pamoja na vipaji vinavyohusiana nayo, roho zetu zitajaa furaha takatifu tokea hapa duniani na kuwa tayari kuingizwa katika mafumbo ya Mungu.

 

 

HERI ZA KUZAMA NDANI YA MUNGU NA KUUNGANA NAYE

 

Baadhi ya wanafalsafa walidhani kuwa heri imo katika kujua ukweli, hasa ukweli mkuu, lakini hawakujali usafi wa moyo; kwa hiyo katika mambo kadhaa maisha yao yalikuwa yakipingana na mafundisho yao. Kumbe Yesu amesema, “Heri wenye moyo safi, maana hao watamwona Mungu” (Math. 5:8). Hakusema wana heri walio na akili sana pamoja na muda na njia ya kuistawisha, bali walio na moyo safi, hata kama kimaumbile akili yao ni ndogo kuliko ya wengine. Wakiwa na moyo safi watamuona Mungu: ni kama maji safi ya ziwa ambamo uangavu wa anga unarudishwa, au kama kioo cha Kiroho ambamo sura ya Mungu inaonekana. Lakini usafi halisi wa moyo unadai kujifisha kwa bidii: “Jicho lako la kuume likikukosesha, ling’oe ulitupe mbali nawe… Na mkono wako wa kuume ukikukosesha, ukate uutupe mbali nawe” (Math. 5:29-30). Tunapaswa kuangalia hasa tuwe na nia njema: si kutoa sadaka mbele ya watu ili kuonekana nao, wala kusali ili kusifiwa nao, bali kutafuta tu tumpendeze Baba wa mbinguni “aonaye sirini” (Math. 6:4,6,18). Hapo tu yatatimia maneno ya Mwalimu: “Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru” (Math. 6:22). Tokea hapa duniani Mkristo atamuona Mungu kwa namna fulani katika jirani yake, hata katika watu kadhaa ambao mwanzoni aliwaona wanampinga; atamuona katika Maandiko, katika maisha ya Kanisa, katika nafasi mbalimbali za maisha yake mwenyewe, hata katika majaribu, ambapo atajifunza maongozi ya Mungu. Ndipo sala ya kumiminiwa inapopatikana kwa msaada wa kipaji cha akili, tunapojiandaa kumuona Mungu uso kwa uso, wema wake, uzuri wake usiopimika; hapo hamu zetu zote zitatimia, nasi tutakuwa kama tumelewa na mto wa vitamu vya Kiroho.

Tangu hapa duniani huko kuzama ndani ya Mungu kunazaa matunda; kunaleta amani angavu, inavyotangaza heri ya saba: “Heri wapatanishi, maana hao wataitwa wana wa Mungu” (Math. 5:9). Heri hiyo inahusiana na kipaji cha hekima kinachotufanya tuonje mafumbo ya milele, na kuona kwa namna fulani mambo yote ndani ya Mungu. Miangaza ya Roho Mtakatifu, ambayo kipaji hicho kinatusaidia kuipokea kwa mikono miwili, inatuonyesha polepole utaratibu mzuri ajabu wa maongozi ya Mungu, pengine palepale – na hasa palepale – tulipopatwa kwanza na mshtuko mkubwa katika matukio machungu yasiyotarajiwa ambayo Mungu aliyaruhusu kwa manufaa makubwa zaidi. Haiwezekani kung’amua hivyo anavyoongoza maisha yetu bila ya kufaidi amani kubwa ambayo ni utulivu wa utaratibu. Ili tusifadhaishwe na matukio ya namna hiyo, bali tuyapokee yote mikononi mwa Mungu kama njia ya kumuendea, ni lazima kujiachilia kwa Roho Mtakatifu, anayetaka kutujalia hatua kwa hatua kutazama mambo ya Kimungu, ambako ni sharti la kuungana naye. Ndiyo sababu tumejaliwa kipaji cha hekima. Miangaza yake inatupatia amani angavu, sio tu kwa ajili yetu, bali kwa jirani pia; inatufanya wenye amani; inatusaidia kuwapa amani watu wasiotulia, kuwapenda maadui, kusema maneno ya upatanisho yanayomaliza ugomvi. Hiyo amani ambayo ulimwengu hauwezi kuitoa, ndiyo ishara ya watoto halisi wa Mungu ambao hawaachi kumfikiria Baba yao wa mbinguni. Heri hizo ni mwanzo fulani wa heri ijayo.

Hatimaye, katika heri ya nane, Bwana ameonyesha kwamba yale yote aliyoyasema yanathibitishwa hasa na majaribu yaliyovumiliwa kwa upendo: “Heri wenye kuudhiwa kwa ajili ya haki, maana ufalme wa mbinguni ni wao” (Math. 5:10). Hasa ndiyo majaribu ya mwisho yaliyo masharti ya utakatifu. Neno la kushangaza kama hilo halijasikika: halituahidii tu heri milele, bali pia wakati wa uchungu na dhuluma. Ni heri isiyo ya kimaumbile hata kidogo, haieleweki kweli isipokuwa na wale walioangazwa na Mungu. Lakini ndani yake kuna ngazi nyingi, kuanzia ile ya Mkristo anayeanza kuteseka kwa kuwa ametenda mema, ametii, ametoa mfano mzuri, hadi ile ya mfiadini. Heri hiyo inamhusu aliyeongoka anayepingwa tu katika mazingira yao; pia mtume ambaye kazi yake inazuiwa na walewale anaotaka waokoke, wasiokubali kumsamehe kwa kuwaeleza wazi kweli za Injili. Pengine makabila mazima yanapaswa kustahimili dhuluma za namna hiyo. Heri hiyo ni kamili kuliko zote kwa kuwa ni ya wale wanaofanana zaidi na Yesu aliyesulubiwa kwa ajili yetu. Kudumu wanyenyekevu, wapole na wenye huruma wakati wa dhuluma, hata kwa watesi wenyewe, na sio tu kuendelea kuwa na amani, bali kuwashirikisha wengine pia, huo ndio ukamilifu wa Kikristo. Si watakatifu wote walifia dini, lakini kwa viwango tofauti wote walidhulumiwa kwa ajili ya haki na kujua walau kidogo ule ushahidi wa moyoni uliomfanya Maria Mama wa huzuni. Yesu alisisitiza tuzo waliloahidiwa watu hao: “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni” (Math. 5:11-12). Kutokana na maneno hayo mt. Inyasi wa Antiokia na wengineo walitamani kufia dini. Ndiyo sababu wakawa “chumvi ya dunia”, “nuru ya ulimwengu” (Math. 5:13-14), na nyumba yao, iliyojengwa kwenye mwamba, sio katika mchanga, ilistahimili dhoruba zote isianguke.

 

Heri hizo ni matendo bora ya maadili yaliyokamilishwa na vipaji, hivyo zinapita juhudi zetu. Kwa maneno mengine, ukamilifu wa Kikristo unategemea mafumbo, ni mwanzo wa uzima wa milele, ambapo Mkristo atakuwa mkamilifu kama Baba, akimuona na kumpenda kama mwenyewe anavyojiona na kujipenda.

Mt. Teresa aliandika, “Vitabu kadhaa vinasema tusijali mabaya yanayosemwa juu yetu, bali tuyafurahie kuliko maneno ya sifa, tusijali sana heshima tunayopewa, tusishikamane na ukoo… na sijui mambo mangapi ya namna hiyo… Nionavyo mimi, hayo ni zawadi za Mungu tu, ni mema yanayopita maumbile”, yaani yanapita uwezo wa juhudi zetu katika kutekeleza maadili; ni matunda yanayozaliwa na usikivu mkubwa kwa Roho Mtakatifu. Mwenyewe aliandika pia, “Tukipenda heshima na tunu za kidunia, hata tukifanya sala, au afadhali niseme tukitafakari miaka na miaka, hatutaendelea kweli kamwe. Kumbe sala kamili inatukomboa kutoka kasoro hizo”. Maana yake pasipo sala ya kumiminiwa hatutaweza kamwe kuufikia ukamilifu.

Ndivyo ilivyoandikwa katika Kumfuasa Yesu Kristo: “Utakapofaulu kujidharau kabisa, uwe na hakika kwamba umepata kuonja amani yote inayowezekana hapa duniani” (III,25:3). Kwa sababu hiyohiyo, mwanafunzi anaomba kumiminiwa sala: “Mungu wangu, nahitaji sana neema kubwa zaidi, yakinipasa kufika katika hali njema, hata nisiweze kuzuiwa tena na mtu yeyote wala na kiumbe chochote… Mtu mmoja aliyekuwa na pupa ya kuruka hivi afike kwako, alisema, Nani atanipa mabawa kama ndege nipate kuruka na kufika mustarehe? Mtu asiyevunja vifungo vinavyomfunga pamoja na viumbe, hatapata nafasi ya kumfikiri Mungu na mambo yake. Ndiyo maana hatuoni watu wengi wa kuzama ndani ya Mungu, kwa kuwa wenye kujitenga kabisa na mambo mapotevu ya dunia au hata na viumbe vyote huwa wachache. Kufanya hivi hutaka neema kubwa sana, yenye kuinua roho na kuivuta hata ipae juu ya hali yake. Lakini kama mtu hapandi vile rohoni mwake kwa kujiambua na viumbe vyote akiambatana na Mungu tu, yote ayajuayo na yote awezayo hayana maana” (III,31:1-2). Ndio ustawi kamili wa muundo wa Kiroho, yaani neema ya maadili na vipaji, nao unaonyeshwa kwetu katika heri nane si kinadharia tu, bali katika utekelezaji wake.

 

 

 

 

1.10. UKAMILIFU NA USHUJAA

 

 

Ili tukamilishe tuliyoyasema kuhusu ukuu wa ukamilifu wa Kikristo, tunapaswa kuona kama wenyewe unadai upendo mkubwa pamoja na ushujaa katika maadili yote.

 

 

UKAMILIFU WA KIKRISTO UNADAI UPENDO MKUBWA

 

Kanisa linafundisha hivyo kwa kuwa ukamilifu huo unapatikana tu baada ya utekelezaji wa muda mrefu wa maadili ya kumiminiwa na ya kujipatia; kwa utekelezaji huo maadili hayo yanastawi zaidi na zaidi. Na ikiwa mwanzoni “upendo wa kiwango cha chini una uwezo wa kushinda vishawishi vyote” (mt. Thoma wa Akwino), baadaye unavishinda kweli na kuzidi kuwa na nguvu. Basi, haiwezekani kumfikiria Mkristo aliyekamilika, aliye juu kuliko wanaoanza na wanaoendelea, asiye na upendo mkubwa, ingawa kupima kiwango cha upendo kinachotakiwa ni kazi ya Mungu tu. Mfano wake ni utu uzima, ambao kwa kawaida unadai nguvu za mwili nyingi kuliko zile za ubalehe, lakini bila ya kipimo maalumu.

Fundisho hilo msingi wake mwingine ni kwamba upendo unastawi kwa nguvu kuliko kwa uenezi. Viwango vitatu vya upendo vinavyowafaa wanaoanza, wanaoendelea na waliokamilika, ni viwango vya nguvu ya adili hilo, ambalo linazidi kuzuia dhambi nyepesi za makusudi na kututenganisha na malimwengu ili tuambatane na Mungu. Hata hivyo mtu mmoja anakwepa dhambi hizo kuliko mwingine mwenye kiwango kilekile cha upendo, kwa sababu kwa wakati huo ana juhudi nyingi zaidi au halazimiki kupambana zaidi na tabia yake, uchovu na upinzani. Mt. Teresa wa Yesu alipokuwa katika nafasi zisizotazamiwa nje ya monasteri ilimtokea kutenda dhambi nyepesi nyingi zaidi, lakini pia kujipatia stahili nyingi zaidi kutokana na majaribu aliyoyashinda. Ni kama katika mtu kupanda mlima mrefu, inamtokea kuanguka kuliko mahali tambarare, lakini ana stahili ya kutenda kazi ngumu kwa kupanda.

Basi, ukamilifu unadai upendo mkubwa unaopatikana tu kwa kushinda kwanza vishawishi vingi na kujipatia stahili nyingi. Fundisho hilo limethibitishwa na mt. Yohane wa Msalaba: “Kuna watu wanaoridhika na aina yoyote ya kukusanya mawazo na ya kuongoka; wengine wanaishia katika kutekeleza maadili kwa ukamilifu mkubwa au mdogo, na kuwa waaminifu katika sala na kujinyima. Wanachokosa ni kujishusha, kuwa fukara, au kujikana na kuwa safi Kiroho… Kinyume chake wanakwepa msalaba ambao ungewalinganisha na Bwana wetu Yesu Kristo. Wanajifanya lengo ndani ya Mungu, jambo ambalo ni kinyume kabisa cha upendo… Ningependa kuweza kuwathibitishia watu wote wa Kiroho ukweli huu: kwamba njia ya Mungu haimo katika kuzidisha mawazo, mbinu na maonjo, ingawa kwa namna fulani wanaoanza wanayahitaji hayo. Lakini jambo moja tu ni la lazima kabisa, yaani kuweza kabisa kujikana kwa ndani na kwa nje, kujitoa mhanga kwa Yesu Kristo kama sadaka kamili ya kuteketezwa. Katika zoezi hilo tu tutayakuta mengine yote na mengi zaidi tena. Kumbe, tukipuuzia zoezi hilo, ambalo ni muhtasari na mzizi wa maadili, tutakuta tu vitu visivyo muhimu, na maendeleo yatakwama, hata tukiwa na mawazo na neema za kimalaika… Mtu wa Kiroho akifaulu kujiangamiza, yaani kutekeleza unyenyekevu kamili, hapo muungano wake na Mungu utatimia, nao ndio hali bora tena kuu tunayoweza kuifikia katika maisha haya”. Hali hiyo inadai upendo mkubwa, pamoja na unyenyekevu kamili: “Ukamilifu umo katika kumpenda kikamilifu Mungu na kujidharau”.

Mafundisho hayo yanalingana na yale ya mt. Thoma wa Akwino alipoeleza ukamilifu kuwa ni “hali ya wale ambao wanalenga hasa kuambatana na Mungu na kumfurahia, na ambao wanatamani kufa ili kuishi na Kristo”, wakikabili magumu kwa utukufu wa Mungu na wokovu wa watu. Basi, pasipo juhudi kubwa haiwezekani kufikia upendo mkubwa, hata kwa miaka ya kukomunika kila siku na kutenda mema yenye stahili pungufu. Kwa njia hizo tunaweza kujidumisha katika neema ya utakaso au kuinuka mapema baada ya kutenda dhambi ya mauti, lakini hatutafikia kamwe kiwango kikubwa cha upendo.

 

 

UKAMILIFU UNADAI USHUJAA KATIKA MAADILI YOTE

 

Ikiwa upendo kwa nchi yetu unatudai ushujaa ikipatwa na hatari, bila ya shaka ukamilifu wa Kikristo unadai ushujaa katika maadili, walau upande wa nia; yaani Mkristo anapaswa kuwa tayari, kwa msaada wa Mungu, kuuawa kwa ajili ya imani, kama atajikuta katika nafasi ya kulazimika kuchagua kati ya kuikana na kuteswa. Ushujaa huo wa lazima kwa wokovu unadaiwa zaidi na ukamilifu. Mkristo akiwa mwaminifu katika wajibu wowote wa kila siku, awe na hakika kuwa katika nafasi ngumu zaidi Bwana atamsaidia kulingana na ukuu wa wajibu wa dharura: “Aliye mwaminifu katika lililo dogo sana, huwa mwaminifu katika lililo kubwa pia” (Lk. 16:10). “Msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu jinsi mtakavyojibu au kusema; kwa kuwa Roho Mtakatifu atawafundisha saa ileile yawapasayo kuyasema” (Lk. 12:11-12). Tunapaswa pia kuwapenda maadui wetu na kuwasaidia wakiwa na shida kubwa.

Vipaji vya Roho Mtakatifu ni vya lazima kwa wokovu ili tupokee kwa dhati na kwa mikono miwili uvuvio wake wa pekee pale ambapo maadili hayatoshi, kutokana na nafasi kuwa ngumu zaidi. Ikiwa kila Mkristo anapaswa kukubali kifodini kuliko kuikana imani, padri aliyewekwa wakfu na Mungu awachunge watu anapaswa kuhatarisha uhai wake ili kuwaletea sakramenti wakiwa na shida kubwa nazo (k.mf. kwenda kuwaungamisha wenye tauni). Zaidi tena askofu, katika nafasi kadhaa anapaswa kutoa uhai wake kwa ajili ya kundi lake. Lakini kuwa tayari rohoni kutekeleza maadili kwa ushujaa huo ni tofauti na kuwa nayo kwa kiwango cha ushujaa.

Katika sura ijayo tutaona kuwa ukamilifu unadai Mungu atutakase hisi na roho ili kufuta kasoro za wanaoanza na za wanaoendelea. Mt. Yohane wa Msalaba alifafanua matakaso hayo yanavyowatokea wanasala wanaoitiwa ukamilifu mkuu kwa njia ya mkato; lakini mambo ya namna hiyo yanawatokea wengine pia ambao kwao matakaso hayo ya ndani yanaendana na huzuni na shida za utume. Katika majaribu hayo si kwa nadra mtu anatakiwa kushinda kishujaa vishawishi dhidi ya usafi wa moyo na subira, halafu dhidi ya imani, tumaini na upendo. Upande huo ukamilifu unadai ushujaa fulani katika maadili, ambao baadaye unaweza na kutakiwa uongezeke.

Hatimaye, upendo wa Kikristo, kwa kuwa unalenga kutulinganisha na Mwokozi aliyesulubiwa kwa ajili yetu, unatakiwa kulenga ushujaa katika maadili. Hiyo inatokana na yale tuliyoyasema kwanza: tendo la kishujaa linalompasa Mkristo yeyote, k.mf. la kukubali kuuawa kuliko kuikana imani, si chini ya lengo la upendo, yaani kumpenda Mungu kuliko yote. Kwa maumbile yake, upendo huo unampenda Mungu kuliko uhai wa mwili, kwa hiyo unapaswa kuwa tayari kutoa uhai wake unavyodaiwa na nafasi kadhaa. “Upendo wa Mungu unafanya tutende bila ya kikomo na kuvumilia bila ya kuchoka” (mt. Bernardo) hasa katika tabu za ndani na za nje ambazo watumishi wa Mungu wanapaswa kustahimili kwa utakaso wao na kwa kuchangia wokovu wa watu kwa mfano wa Mwokozi.

Mtu anaweza akapinga mafundisho hayo akisema eti, yangekuwa kweli Wakristo wanaofikia ushujaa wangekuwa wengi zaidi, kumbe ushujaa ni adimu. Mt. Thoma wa Akwino alijibu hoja ya namna hiyo kuhusu idadi ya wateule: “Jema linalolingana na hali ya kawaida ya maumbile ya kibinadamu kwa kawaida linafikiwa; lakini si hivyo kuhusu jema linalopita hiyo hali ya kawaida”. Ni adimu kudumu maisha yote katika neema ya utakaso, bila ya kutenda dhambi ya mauti baada ya ubatizo. Hata hivyo kwa mfumo wake neema ya utakaso inalenga uzima wa milele, kwa hiyo idumu milele bila ya kuangamizwa kamwe na dhambi ya mauti. Ila tumepokea hazina hiyo katika chungu ya udongo, hivyo tamaa na kiburi vinaweza kufanya tuipoteze. Wengi wanaishi kijuujuu tu, wakifuata hisi, na wachache tu wanafuata akili nyofu; hata hivyo kwa maumbile yake roho ya binadamu ina akili, nayo neema inatakiwa kuifanya iishi Kimungu kweli. Vivyo hivyo upendo ukiwa ni mbegu ya uzima wa milele, kwa mfumo wake unalenga ushujaa ili kudumu katika uaminifu kwa Mungu.

Kuhusu utakatifu mkubwa, huo unadhihirika hasa katika ulinganifu wa maadili yote, hata yale yaliyo mbalimbali zaidi. Mmoja anaweza kuelekea kimaumbile upande wa nguvu, lakini si wa upole; mwingine ni kinyume. Kwa namna fulani maumbile yanaelekea daima upande mmoja, hivi kwamba yanahitaji kukamilishwa na maadili mbalimbali. Muungano wa nguvu kubwa na upole kamili, wa upendo motomoto kwa ukweli na haki pamoja na huruma kubwa kwa waliopotoka, unathibitisha muungano wa dhati na Mungu, kwa kuwa yaliyogawanyika katika ulimwengu huwa yameunganika katika ufalme wa Mungu, na hasa ndani mwake mwenyewe. Utakatifu ni mfano mzuri wa muungano wa sifa mbalimbali za Mungu, wa haki isiyo na mipaka na huruma isiyo na mipaka ndani ya ukuu wa Umungu.

 

 

 

 

1.11. UKAMILIFU WA KIKRISTO NA MATAKASO YA KIMUNGU

 

 

Tumeshaona kuwa ukamilifu wa Kikristo umo hasa katika upendo, unaotuunganisha na Mungu na jirani kuliko adili lingine lolote. Tunatakiwa bado kusema unavyodai pia matendo ya maadili mengine na ya vipaji vya Roho Mtakatifu. Hata katika swala hilo watu walipotoka pande mbili. Watulivu waliyapuuzia mno maadili hayo na kufuta utekelezaji wa kujinyima na wa kuwatendea mema majirani. Kinyume chao, wengine walisisitiza matendo ya toba, ibada na huruma wasitambue vya kutosha ukuu wa upendo wa Mungu, na hivyo wakazingatia juhudi zao na utume wa njenje kuliko mafumbo.

 

 

MATENDO YA MAADILI YANAYODAIWA NA UKAMILIFU WA KIKRISTO

 

Ukamilifu wa Kikristo unadai matendo ya maadili mengine yaliyo ya amri na ambayo yanatakiwa kuangazwa, kuhuishwa na kustahilishwa na upendo. Tutaona kuwa amri kuu inatudai tukue zaidi na zaidi katika maadili hayo kama vile katika upendo.

Kutokana na yale tuliyokwishasema kuhusu muundo wa Kiroho, ukamilifu unadai maadili yote ya kumiminiwa na ya kujipatia, halafu vipaji saba vinavyohusiana na upendo hivi kwamba vinakuwa pamoja nao. Lakini kwa kawaida upendo wa waliokamilika unapaswa kuwa mkubwa na motomoto kuliko ule wa wanaoanza na wanaoendelea. Basi, ukamilifu unadai utekelezaji wa maadili yote na wa vipaji saba pia. Mtu hawezi kuwa mkamilifu bila ya kupenya mafumbo ya imani kwa kipaji cha akili, wala kuwa na kipaji cha hekima kwa kiwango kinacholingana na upendo (ingawa kipaji hicho kinaelekea sala hasa katika watakatifu kadhaa na utendaji zaidi katika wengine).

Upendo ndio kiungo cha ukamilifu huo wa maadili na vipaji, ambavyo kwa pamoja ni kama fungu la maua linalotolewa kwa Mungu. Basi, ukamilifu umo hasa katika upendo, ingawa unadai pia maadili mengine na vipaji saba. Vilevile na binadamu ambaye mwili ni sehemu ya utu wake, ingawa utu umo hasa katika roho inayomtofautisha na wanyama.

Neema ya utakaso na upendo wa wanaoanza havitoshi kuunda ukamilifu, mpaka vikue hadi kufikia hatua ya waliokamilika. Ili tuifikie tunahitaji kujikana, kuwa wasikivu kwa Roho Mtakatifu kwa njia ya vipaji saba, na kupokea kwa mikono miwili misalaba au matakaso yanayokusudiwa kufisha ndani mwetu umimi na kuhakikisha nafasi ya kwanza ishikwe moja kwa moja na upendo wa Mungu wenye kuangaza na kuwaka zaidi na zaidi.

 

 

MATAKASO YANAYODAIWA NA UKAMILIFU WA KIKRISTO

 

Tusisitize tangu sasa jambo hilo kufuatana na yale yaliyosemwa na mt. Paulo: “Kwa ajili yake (Kristo) nimepata hasara ya mambo yote nikiyahesabu kuwa kama mavi ili nipate Kristo; tena nionekane katika yeye… ili nimjue yeye, na uweza wa kufufuka kwake, na ushirika wa mateso yake, nikifananishwa na kufa kwake; ili nipate kwa njia yoyote kuufikia ufufuo wa wafu. Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo, kwa ajili yake, nimeshikwa na Kristo Yesu. Ndugu, sijidhanii nafsi yangu kwamba nimekwisha kushika; ila natenda neno moja tu: nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele, nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu, katika Kristo Yesu. Basi sisi tulio wakamilifu na tuwaze hayo… Lakini, hapo tulipofika na tuenende katika lilo hilo(Fil. 3:8-16). Ndio ukamilifu wa Kikristo kweli, si wa kifalsafa tu; nao tumependekezewa sisi sote tunaolishwa na Maandiko hayo hadi mwisho wa dunia.

Watu kadhaa walisema eti, mt. Thoma wa Akwino alizungumzia kidogo tu matakaso ya Kiroho. Basi, msome alivyofafanua maneno hayo kwa Wafilipi kuhusu kushiriki mateso ya Kristo walau kusudi tusipoteze misalaba yetu, tufanane naye na kuwaokoa watu pamoja naye (maana ulimwengu umejaa misalaba tasa, kama ule wa mwizi wa pili aliyesulubiwa pamoja na Yesu: njia ya kuifanya ilete faida ni kuibeba kwa uvumilivu na upendo pamoja naye). Msome pia alivyofafanua maneno ya Yesu kuhusu mzabibu wa kweli ambao Baba anausafishia kila tawi lizaalo: “Ili waadilifu wanaozaa matunda wazae kwa wingi zaidi, Mungu anapogolea ndani mwao yaliyo ya ziada; anawatakasa kwa kuwatumia tabu na kuruhusu washambuliwe na vishawishi ambavyo katikati yake wazidishe nguvu na juhudi. Hapa duniani hapana mtu safi kiasi kwamba asihitaji kutakaswa zaidi”. Ndiyo matakaso ya Kimungu yaliyokuja kuelezwa zaidi na mwalimu wa Kanisa aliyeyachimba kuliko wote, yaani mt. Yohane wa Msalaba. Katika mafundisho yake tunapata pia mwanga mkubwa ili kutofautisha hatua tatu za maisha ya Kiroho.

 

Sasa tunapaswa kuona yale yanayohitajika ili tufikie kilele cha ustawi wa kawaida wa upendo. Tunaposema kilele tusisahau neno kawaida; vilevile tunaposema kawaida tusisahau neno kilele. Mara nyingi mno tunaita “ya kawaida” yale ambayo wengi wanayafikia kweli, bila ya kujiuliza vya kutosha juu ya yale ambayo wangetakiwa kuyafikia kama wangekuwa waaminifu. Haifai kutamka eti, muungano wa karibu mfululizo na Mungu uko juu kuliko kilele cha ustawi wa kawaida wa upendo, kwa sababu tu wengi hawaufikii. Tusichanganye yanayotakiwa kuwa na yale yaliyopo maishani, la sivyo tutasema uaminifu halisi hauwezekani duniani, kwa kuwa walio wengi wanafuata faida yao (k.mf. pesa na anasa) kuliko uadilifu. Wengi wanajiongoza kwa kufuata yale yasiyo mabaya mno badala ya wajibu wao unaowadai juhudi kubwa katika mazingira ambamo yote yanawaelekeza kudidimia; wanafuata mkondo kadiri ya sera ya kujitahidi kidogo iwezekanavyo. Sio tu kwamba wanayavumilia yasiyo mabaya mno, bali wanayatenda na mara nyingi wanayaunga mkono kwa mashauri yao ili wadumishe hali yao. Wanasiasa wengi wanasema kuwa wanafanya hivyo ili kuepa mabaya makubwa zaidi ambayo wengine wangeyafanya mahali pao kama wenyewe wangepotewa na wadhifa wao kwa kutowapendeza watu. Hivyo, badala ya kuwasaidia kupanda juu tena wanawasaidia kudidimia, wakijitahidi tu kupunguza kasi ya anguko. Kuna kitu cha namna hiyo katika maisha ya Kiroho pia.

Tunapaswa kukumbuka kwamba sheria kuu ya ustawi wa kawaida wa upendo ni tofauti na ile ya maumbile yetu yaliyoanguka. Hata baada ya ubatizo hayo yanaendelea kuwa na madonda na hivyo yanatuelekeza kudidimia, kumbe neema inayotuumba upya hatua kwa hatua inatufanya tupande daima. Tunapongojea uzima wa milele, maisha yetu yanatushangaza kwa jinsi yalivyo na mwanga na giza pamoja: “Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana” (Gal. 5:16-17). Tabia mbovu inabaki hata ndani ya waliobatizwa. Upendo wa Kristo uliomo ndani mwetu haujashinda umimi wetu moja kwa moja, bali unahitaji bado kushindana nao kwa nguvu. Unahitajika utakaso mkubwa; sio tu ule tunaotakiwa kujipatia kwa kujifisha, bali ule tunaopatiwa na Mungu anapokuja kupogolea matawi ya mzabibu yazidi kuzaa.

“Ili tufikie nuru ya Kimungu na muungano kamili wa upendo na Mungu – nayasemea yanayowezekana duniani – roho inapaswa kupitia usiku wenye giza… Kwa kawaida, wateule wanapojitahidi kufikia hiyo hali ya ukamilifu wanakuta magiza makubwa, na kupaswa kuteseka katika mwili na roho hivi kwamba ujuzi wa kibinadamu hauwezi kueleza hata kidogo… Picha zake hazijulikani na mtu isipokuwa na wale waliyoyang’amua wenyewe” (mt. Yohane wa Msalaba). Tawi ambalo Mungu analisafisha si hai tu, bali anajitambua pia, na ili mtu aweze kujua huko kupogolewa ni nini anatakiwa kukupata mwenyewe. Kila mmoja anapaswa kubeba msalaba wake, lakini hajui msalaba ni nini kabla hajaubeba kwa upendo.

Bila ya tabu hatufikii kushinda kikamilifu umimi, tamaa ya anasa, uvivu, hasira, wivu, kijicho, utovu wa haki katika kuhukumu, kujipendea, kujidai kipumbavu, kujifanya lengo hata la ibada, hamu kubwa mno ya kufarijika, kiburi upande wa akili na wa roho, yale yote yanayopingana na imani na tumaini kwa Mungu, ili tumpende Bwana kikamilifu “kwa moyo wote, kwa akili yote, kwa nguvu zote, kwa roho yote” na kumpenda jirani, hata adui, tunavyojipenda. Tunahitaji kwa wingi imani, subira, ustahimilivu ili kudumu katika upendo kwa vyovyote, yanapotimia maneno ya mt. Paulo: “Naam, na wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa” (2Tim. 3:12).

Kwa hiyo mt. Yohane wa Msalaba, akielekeza njia inayofikisha kwa hakika na haraka zaidi kwenye ukamilifu wa Kikristo, alisema hatuwezi kuufikia Mungu asipotutakasa hisi – ndiyo ishara ya kuingia hatua ya mwanga – na asipotutakasa roho – kwenye kizingiti cha hatua ya muungano. Kujitakasa hakutoshi: “Mtu, hata akiwa na juhudi namna gani, hawezi kufaulu kujitakasa kikamilifu: hawezi kabisa kujiandaa kuungana na Mungu kwa upendo kamili. Ni lazima Mungu mwenyewe ashughulike na kumtakasa kwa moto ambao ni giza kwa roho… Roho zinaanza kuingia katika huo usiku wa giza Mungu mwenyewe anapowakomboa polepole kutoka hali ya wanaoanza, ambapo wanatafakari katika njia ya Kiroho, ili awaingize katika hali ya wanaoendelea, ambayo ni ile ya wanasala. Wanapaswa kupitia njia hiyo ili wawe wakamilifu, maana yake wafikie muungano wa Kimungu”.

 

Kwanza tunaachishwa faraja za kihisi, ambazo zinafaa kwa muda, lakini zinakuwa kizuio zikitafutwa kwa zenyewe. Ndiyo sababu tunahitaji kutakaswa hisi kwa ukavu na kuongozwa kwenye maisha ya Kiroho yasiyotegemea mno hisi, ubunifu na mafuatano ya mawazo. Hapo kwa vipaji vya Roho Mtakatifu, ingawa kuna giza la kusumbua, tunapata ujuzi wa kuangaziwa unaotuingiza kwa undani katika mambo ya Mungu, pengine tuyapenye kwa nukta moja kuliko kwa miezi au miaka ya kutafakari. Ili kushinda vishawishi dhidi ya usafi wa moyo au ya subira, vinavyotokea mara nyingi wakati wa usiku wa hisi, unahitajika pengine ushujaa mkubwa unaoleta faida baadaye.

Katika usiku huo hisi zinatupwa kwenye giza na ukavu kwa kutoweka kwa neema za kihisi ambazo roho ilikuwa inaziishia kwa kuzifurahia kwa umimi. Lakini katika giza hilo, akili na utashi vinaanza kuangazwa na mwanga wa uzima unaopita kutafakari kwa mafuatano ya mawazo na ambao unaelekeza kumkazia Mungu macho ya upendo katika sala. “Basi, roho imetoka, na kuanza kupenya njia ya roho wanayoifuata wale wanaoendelea, njia inayoitwa ya kuangazwa au ya kujaliwa kuzama katika sala” (mt. Yohane wa Msalaba).

Baada ya hayo yote utahitajika utakaso mwingine wa kujaliwa ili kuokoa roho kutoka kasoro za wanaoendelea ambazo “haziponyeki kadiri hao wanaoendelea wanavyodhani ni mema kamili ya Kiroho… Basi, anayetaka kusonga mbele kweli, ni lazima apitie utakaso wa usiku wa roho. Hapo tu roho itaweza kuona njia ya kufaa ya kuungana na Mungu” (mt. Yohane wa Msalaba). Utakaso huo unapatikana katika walioendelea zaidi ambao wanatamani mema lakini wanadai yafanywe nao na kwa namna yao wenyewe. Hao wanapaswa kutakaswa kila namna ya kushikilia kibinadamu akili yao na matendo yao, namna yao binafsi ya kuona, kutaka na kutenda. Utakaso huo ukivumiliwa vizuri, katikati ya vishawishi dhidi ya maadili ya Kimungu, unazidisha mara mia imani, tumaini na upendo wao.

Jaribu hilo la kutakaswa linajitokeza kwa namna tofauti katika maisha ya sala tu na katika yale ya kitume. Pia ni tofauti kadiri linavyolenga kumfikisha mtu kwenye ukamilifu mkuu kuanzia hapa duniani au linavyotokea mwishoni tu mwa maisha haya ili kumsaidia kutakaswa walau kwa kiasi fulani kabla hajafa, akijipatia hivyo stahili kwa ustawi wa upendo, badala ya kutakaswa toharani asipoweza kustahili. Hivyo dogma ya toharani inathibitisha haja ya matakaso hayo.

Hapo mchanganyiko wa mwanga na giza ni mkubwa kuliko ule wa usiku wa hisi. Roho inaonekana imekosa mianga na urahisi wa kusali na kutenda ambao ilikuwa inaufurahia mno kutokana na baki la kujipendea na kiburi. Lakini katikati ya huo usiku wa roho unaonekana mwanga mkuu zaidi; polepole, katikati ya vishawishi dhidi ya imani na tumaini, zinajitokeza sababu zenyewe za maadili ya Kimungu, ambazo ni kama nyota kuu tatu: ukweli asili wenye kufunua, huruma yenye kusaidia na wema mkuu wa Mungu. Mtu anafikia kumpenda Mungu kwa usafi mkubwa na kwa uwezo wake wote.

Tutayaeleza hayo kirefu mwanzoni mwa sehemu ya tatu na ya nne. Hapa yalihitajika tusije tukapunguza ukuu wa ustawi kamili wa kawaida wa maisha ya Kikristo. Kama tulivyokwishaona, kilele hicho kinachoweza kufikiwa duniani ni kile alichotuonyesha Bwana katika heri nane za Kiinjili: hizo, na hasa zile za mwisho, zinapita taratibu za juhudi tu na kupatikana upande wa mafumbo, kama hayo matakaso ya Kimungu.

 

 

UKAMILIFU WA KIKRISTO NA SALA YA KUMIMINIWA

 

Fundisho la kwamba ukamilifu unadai matakaso ya Kimungu ya hisi na roho lina mengi yanayotokana nalo.

Kwanza kuwa sala ya kumiminiwa, yaani kuzama katika mafumbo ya imani, imo katika njia ya kawaida ya utakatifu, kwa sababu inaanza katika ukavu wa utakaso wa hisi. Ingekuwa kosa kubwa kuchanganya sala hiyo na faraja ambazo hazifuatani nayo daima.Usemi wa kuwa mizizi ya ujuzi ni michungu lakini matunda yake ni matamu unafaa kuhusu mizizi na matunda ya sala ya kumiminiwa.

Pili, siku hizi hakuna tena mtu anayesema kuzama katika mafumbo ya imani ni karama tu, kama ile ya unabii au ile ya kusema kwa lugha ngeni. Wote wanakubaliana sala hiyo inahusiana na neema ya utakaso, yaani neema ya maadili na vipaji.

Hatimaye, tusipoweza kustahili neema ya hakika ya kuzama katika sala, maana yake si kwamba haipo katika njia ya kawaida ya utakatifu. Mwadilifu hawezi kustahili vilevile neema ya kufa katika neema ya utakaso, ingawa ni ya lazima kwa uzima wa milele. Wala hawezi kustahili neema ya hakika inayomkinga dhidi ya dhambi ya mauti adumu katika neema ya utakaso. Lakini zawadi hizo ambazo hawezi kuzistahili, anaweza kuzipata kwa sala nyenyekevu, yenye tumaini na udumifu.

Tusichanganye maswali mawili yafuatayo: “Je, sala ya kumiminiwa ipo katika njia ya kawaida ya utakatifu? Je, waadilifu wote wanaweza kuifikia, bila ya tofauti ya mazingira, malezi na uongozi?”. Kama vile isivyofaa kuchanganya haya yafuatayo: “Je, neema ya utakaso ni mbegu ya uzima wa milele? Je, kati ya wale walioipokea kwa ubatizo au kati ya waliodumu nayo miaka kadhaa, wataokoka wote au walau wengi wao?”.

Kwa nini wanasala hasa ni wachache hivi? Kwa sababu wachache tu wanajua kujitenga na viumbe. Wengine wanaweza wakawa na nia njema, lakini hawana juhudi zile zote zinazohitajika ili kufikia ukamilifu. Tena ili kuufikia ni muhimu kupata malezi mazuri na uongozi mzuri, ingawa Mungu anafidia kwa watu kadhaa wenye juhudi nyingi.

Tusisahau pia kuwa wito wa kuwa mwandani wa Mungu, kama ule wa kuishi Kikristo, unaweza kuwa wa jumla na wa mbali tu, au maalumu na wa jirani. Tena huo wa pili unaweza kuwa wa kutosha au wa hakika. Hatimaye huo wa hakika unaweza kuhusu viwango vya chini au vile vya juu vya muungano na Mungu.

Hatutakiwi kupunguza ukuu wa lengo tunalotaka kulifikia. Kuhusu njia zake, busara inapaswa kuzipendekeza kulingana na hali mbalimbali walizonazo watu, na kadiri hao walivyo kati ya wanaoanza au wanaoendelea. Hivyo vinahakikishwa ukuu wa lengo, na uongozi wa kufaa kulifikia.

 

 

 

 

1.12. UKAMILIFU NA AMRI YA KUMPENDA MUNGU

 

 

Baada ya kuona ukamilifu wa Kikristo umo hasa katika upendo, inafaa tujiulize kama ukamilifu huo ni shauri tu au amri inayowalazimisha Wakristo wote kuulenga. Ni sawa na kujiuliza maana halisi na upana wa amri ya upendo.

 

 

JE, AMRI KUU INA MIPAKA?

 

Baadhi ya watu wanadhani si lazima kuwa na upendo mkubwa ili kutimiza kikamilifu amri kuu; kwao ukamilifu haulengi amri hiyo, bali unahusika na utekelezaji wa mashauri kadhaa yaliyo juu ya amri yenyewe. Mt. Thoma wa Akwino alijibu kwa unyofu na undani kwamba wote wanapaswa kulenga ukamilifu, kila mmoja kadiri ya hali yake, ingawa hawapaswi kuwa wakamilifu tayari. Akaonyesha kuwa amri kuu inatulazimisha wote kwa jumla kulenga ukamilifu wa upendo, walau kwa kufuata njia ya kawaida, ingawa nadhiri za kitawa zinawalazimisha tu wale walioziweka waulenge kwa kufuata njia ya pekee ya wito wao. “Ukamilifu wa upendo, ambao unafanya maisha ya Kikristo yawe kamili, umo hasa katika kumpenda Mungu kwa moyo wote na jirani kama nafsi yetu. Kwa hiyo ukamilifu umo hasa katika kushika amri”, si katika kutimiza nadhiri.

Kimsingi ukamilifu wa Kikristo umo katika upendo, kwanza kwa Mungu halafu kwa jirani; tungejidanganya kama tungedhani huo upendo unaagizwa kwa kiwango fulani tu, halafu unakuwa shauri. Amri hiyo inadai wazi ukamilifu: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote, na kwa akili zako zote”. Mipaka iko wapi? Vilevile: “na jirani yako kama nafsi yako” (Lk. 10:27). Kila mmoja anajipenda iwezekanavyo, tena kwa upendo anapaswa kujitakia uzima wa milele si kwa kiwango cha chini tu, bali pasipo kujiwekea mpaka fulani, kwa sababu hatujui Mungu anataka kutufikishia wapi.

Ni hivyo kwa kuwa upendo ndio lengo la amri yoyote, na katika utashi lengo halipatikani kwa kiwango fulani tu, bali katika ukamilifu wake, tofauti na njia za kulifikia. Lengo tunalitaka au hatulitaki; hatuwezi kulitaka nusu. Daktari hawezi kutaka mgonjwa apone nusu; anapima dawa, lakini analenga afya pasipo kipimo. Basi, ukamilifu umo hasa katika amri. “Kwa nini ukamilifu huo usiagizwe kwa binadamu, ingawa hakuna anayeweza kuwa nao katika maisha haya?” (mt. Augustino). Maana yake, ukamilifu wa mbinguni unadaiwa na amri ya kumpenda Mungu si kama kitu cha kutimizwa mara moja, bali kama lengo ambalo wote wajiwekee.

Amri nyingine zilizo chini ya amri kuu, lengo lake ni kuondoa vile ambavyo vinapinga upendo na kutaka kuuangamiza; kumbe mashauri ya Kiinjili, lengo lake ni kusukumia mbali vinavyoweza vikazuia utekelezaji kamili wa upendo, ingawa haviupingi, k.mf. ndoa, shughuli za kidunia n.k. “Amri… na mashauri… vinashikwa vizuri vinapotimizwa ili kumpenda Mungu na kumpenda jirani kwa ajili ya Mungu, katika ulimwengu huu na ule ujao” (mt. Augustino). “Ndiyo sababu katika Mafundisho ya Wazee, abati Musa alisema: Mafungo, makesha, kutafakari Maandiko, kwenda uchi na kukosa vitu si ukamilifu, bali vifaa au njia za ukamilifu; huo haumo ndani ya mambo hayo, ila kwa njia yake unafikiwa kwa kasi na kwa hakika zaidi” (mt. Thoma wa Akwino). Ndiyo njia inayoelekea ukamilifu; lakini wenyewe ni kumfuata Yesu kwa upendo. Kwa maana hiyo alisema, “Ukitaka kuwa mkamilifu, enenda ukauze ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni, kisha njoo unifuate” (Math. 19:21). Tunaweza kuwa fukara kwa hiari kutokana na sababu isiyo ya kidini (k.mf. kwa kudharau utajiri kifalsafa) au kwa upendo wa Mungu; kwa vyovyote si jambo la lazima kwa ukamilifu. Huo umo hasa katika kutekeleza vizuri zaidi na zaidi amri kuu isiyo na mipaka: Wakristo wote waliopewa amri hiyo wanapaswa walau kulenga ukamilifu huo, kila mmoja kadiri ya hali yake (k.mf. ndoa au utawa), kama si kuwa nao tayari. Kwao wote kulenga upendo kamili si afadhali tu, bali ni wajibu sawa na ule wa kuelekea mbinguni, ambapo upendo wa Mungu utatawala kikamilifu, kisiwepo kitu kinachoweza tena kuupunguza.

 

 

UPENDO WA MUNGU HAUPATIKANI KATIKATI

 

Fundisho la kuwa amri kuu haina mipaka kwa jinsi ilivyotolewa linathibitishwa kwa kuzingatia kuwa lengo tunalolizungumzia hapa si la katikati (kama vile afya), bali ni lile kuu, yaani Mungu mwenyewe, aliye wema usio na mipaka. Ikiwa mgonjwa anajitakia afya pasipo kiwango, zaidi sisi tunapaswa kutamani upendo wa Mungu pasipo kiwango, kwa kuwa hatujui ni kipi ambacho Mungu anataka kutufikishia na kweli atatufikishia tukiwa waaminifu. “Binadamu hawezi kamwe kumpenda Mungu anavyotakiwa kupendwa; kama vile hatutaweza kamwe kumuamini na kumtumainia tunavyopaswa” (mt. Thoma wa Akwino). Tofauti na maadili ya kibinadamu, yale ya Kimungu, lengo lake, sababu yake na kipimo chake halisi ni Mungu mwenyewe, yaani ukweli wake na wema wake usio na mipaka. Kwa hiyo hatuwezi kumuamini mno na kumtumainia mno; hatutaweza kamwe kumpenda anavyostahili. Hivyo tunaona vizuri kuwa amri kuu haina mipaka: inawadai wote hapa duniani waulenge upendo wa Mungu ulio safi na wenye nguvu zaidi na zaidi.

Tumaini linapatikana kati ya kukata tamaa ya wokovu na kuudai kipumbavu, lakini si kwamba anayetarajia kipumbavu kuokoka anamtumainia mno Mungu, bali anabadili sababu ya kutumainia, akitumaini kile ambacho Mungu hawezi akaahidi, k.mf. msamaha pasipo majuto halisi. Vilevile kilema cha wepesi wa kuamini hakimo katika kumuamini mno, bali katika kusadiki mambo yaliyobuniwa na binadamu kama kwamba yamefunuliwa na Mungu.

Kusahau kuwa katikati adilifu ni pia kilele, na kudhani maadili ya Kimungu yamo hasa katikati sawa na maadili ya kibinadamu, ndiko sifa ya mtu wa wastani anayejisingizia kuwa na kiasi. Mtu wa namna hiyo yupo katikati ya uadilifu na uovu, tena anakaribia uovu kuliko uadilifu: “Mtu wa wastani kweli anapendezwa na kila kitu, lakini hapendezwi na chochote hata achangamke… Anachukia tamko lolote, kwa kuwa kila tamko linapinga tamko lingine tofauti. Kumbe ukijifanya kidogo rafiki na kidogo adui wa kila jambo, atakuona mwenye busara na kiasi. Mtu wa wastani anasema katika yote kuna mchanganyiko wa mema na mabaya, kwa hiyo tusiwe na msimamo mkali katika kupima mambo. Ukisisitiza ukweli kwa nguvu, mtu wa wastani atasema unajiamini mno. Mtu wa wastani anasikitika kuwa Ukristo una dogma; angependa ufundishe maadili tu; ukimuambia kuwa maadili ya Ukristo yanatokana na dogma zake kama matokeo na sababu yake, atakujibu umezidisha chumvi… Kama neno ‘kuzidisha’ lisingekuwepo, mtu wa wastani angelitunga… Kwa kawaida mtu wa wastani anaonekana mtaratibu; hawezi kuwa mnyenyekevu, la sivyo angeacha kuwa wa wastani. Mnyenyekevu anakataa uongo, hata kama ungetukuzwa na ulimwengu wote, naye anaupigia magoti ukweli… Mtu mwenye upendo hawezi kamwe kuwa wa wastani” (E. Hello).

 

 

WAJIBU WA KUSONGA MBELE KUELEKEA UZIMA WA MILELE

 

Sababu ya mwisho ya amri ya upendo kutokuwa na mipaka ni kwamba tunasafiri kuelekea uzima wa milele, nasi tunasafiri vizuri kadiri tunavyokua katika upendo wa Mungu na wa jirani. Upendo wetu unatakiwa kustawi mfululizo mpaka mwisho wa safari. Hilo si shauri tu, yaani jambo bora la hiari, bali ni agizo, linatakiwa, hivi kwamba mtu ambaye hapa duniani hataki kukua katika upendo anamchukiza Mungu. Njia ya uzima wa milele haikusudiwi kwa kusimama wala kulala, bali kwa kutembea tu. Kwa msafiri ambaye hajafikia mwisho wa lazima wa safari yake, kusonga mbele si shauri, ni sharti. Basi, tunaposafiri kumuelekea Mungu, tunasonga mbele si kimwili, bali Kiroho, kwa kukua katika upendo ambao uwe safi na wa nguvu zaidi na zaidi. Ndivyo tunavyotakiwa kuomba, na ndiyo maombi matatu ya kwanza ya Baba Yetu.

Ikiwa ni hivyo, tusipotimiza bado kikamilifu amri hiyo, je, tunaivunja? Jibu la hakika ni hapana, kwa kuwa “ili tukwepe uvunjaji huo inatosha kushika kwa namna fulani sheria ya upendo kama wanavyofanya wanaoanza” (mt. Thoma wa Akwino). Ni kweli kwamba upendo wa Mungu unaingia wote kabisa katika lengo la amri hiyo; hata ukamilifu wa mbinguni hauwekwi kando, kwa kuwa ndio lengo ambalo tulikusudie, lakini hatuivunji amri tukitimiza upendo kwa kiasi fulani. Sasa, kiwango cha chini cha kumpenda Mungu ni kutopenda chochote kuliko yeye, au kinyume chake au sawa naye; asiye na kiwango hicho hatimizi amri. Kinyume na hicho, kuna kiwango cha upendo kisichoweza kufikiwa hapa duniani, isipokuwa mbinguni, nacho ni kumpenda Mungu hivi kwamba upendo wetu umlenge kweli mfululizo. Kwa hiyo hatuvunji amri kwa sababu hatujafikia ukamilifu huo, wala hatuivunji kama hatujafikia viwango vya katikati, mradi tuwe na kiwango cha chini. Lakini tukisimama katika kiwango hicho hatutimizi kikamilifu amri kuu.

Ni kosa kudhani kuwa upendo huo tu usiokamilika ni wa lazima, na kuwa viwango vyake vya juu ni vya shauri tu. Hivyo vinaagizwa walau kama lengo, hata ikiwa si kwa sasa hivi. Ni sawa na mtoto ambaye asipokua kadiri ya taratibu za ukuaji wake, hatabaki mtoto, bali atakuwa mbilikimo. Upande wa roho pia sheria ya ukuaji ina masharti makali: ikiwa mbegu ya Kimungu tuliyotiwa kwa ubatizo haistawi, ina hatari kubwa ya kufa, ya kusongwa na magugu. Hakika katika njia ya wokovu, watu walio tofauti na vile wanavyotakiwa kuwa si wale waliozama katika mafumbo, bali ni wachelewaji na watu vuguvugu.

Yapo matatu yatokanayo na ambayo tutayafafanua hapo mbele:

Katika njia ya Mungu, asiyesonga mbele, anarudi nyuma: kwa sababu kwetu ni sheria kusonga mbele mfululizo, na asiyefanya hivyo anakuwa mchelewaji, kama garimoshi linalosimama mno kwenye stesheni lisifuate ratiba, au kama mtoto asiyekua anavyotakiwa na hivyo anakuwa mbilikimo.

2° Ustawi wa upendo unatakiwa kuwa ya kasi zaidi na zaidi kadiri tunavyomkaribia Mungu na kuvutwa naye. Ndivyo jiwe linavyoanguka kasi zaidi kadiri linavyokaribia ardhi na kuvutwa nayo.

3° Hatimaye, ikiwa ndio ukuu wa amri wa upendo, hatuwezi kuwa na wasiwasi kuhusu kuzidi kutolewa neema za msaada ili tulifikie lengo hilo, kwa sababu Mungu haagizi kamwe yasiyowezekana. Anatupenda mno, kuliko tunavyoweza kudhani. Ni juu yetu kuitikia. Baada ya kumpenda kwa moyo wote, kihisi pia, kwa mapenzi, tunapaswa kumpenda kwa akili yote, kwa upendo mtendaji, kwa nguvu zetu zote saa ya kujaribiwa inapotufikia, na hatimaye kwa roho yetu yote, iliyoachana na mahangaiko ya hisi, ili tumuabudu “katika rono na kweli” (Yoh. 4:23,24).

Fundisho hilo kwa jumla linatuonyesha kuwa haifai kutenganisha utakatifu na wokovu wa milele, kama wanavyofanya wanaosema, eti, “Mimi sitakuwa mtakatifu kamwe; kwangu inatosha niokoke”. Mtazamo huo ni kosa kubwa. Kujipatia utakatifu zaidi na zaidi ndiyo njia ya wokovu wa milele; mbinguni kutakuwa na watakatifu tu, na kwa maana hiyo wote, na kila mmojawetu, tunapaswa kulenga utakatifu.

 

 

 

 

1.13. UKAMILIFU NA MASHAURI YA KIINJILI

 

 

Tumeona kuwa waamini wote wanapaswa kulenga ukamilifu wa upendo, na kuwa hawawezi kuufikia wakiishi duniani kama kwamba ndiyo maskani yao ya milele, pasipo roho ya mashauri ya Kiinjili, yaani kutoambatana na ulimwengu. Kutokana na amri kuu huo ni wajibu wa wote, kila mmoja kadiri ya hali yake maishani. Lakini, kutokana na wito wa pekee, baadhi wana wajibu maalumu wa kulenga ukamilifu katika maisha ya pekee, kama vile padri ili awe mhudumu mwadilifu wa Bwana, na kama vile mtawa kufuatana na nadhiri au ahadi zake za kutekeleza mashauri ya ufukara, useja na utiifu. Kwanza tutazungumzia utekelezaji huo kuhusiana na ukamilifu wa Kikristo na uponyaji wa madonda yetu ya rohoni.

 

 

MASHAURI YA KIINJILI NA MADONDA YA ROHO

 

Yesu alipomualika tajiri akauze vyote ili kumfuata katika ukamilifu, “yule kijana alipolisikia neno lile, akaenda zake kwa huzuni; kwa sababu alikuwa na mali nyingi” (Math. 19:22). Utekelezaji wa vitendo wa mashauri ya Kiinjili si wajibu wala si sharti la kufikia ukamilifu tunaopaswa kuulenga; ila ni njia ya kufaa tulifikie lengo hilo kwa hakika na kasi zaidi, tusije tukasimama njiani. Ni vigumu kuwa na roho ya kutoambatana na malimwengu tusipoitekeleza kwa vitendo, tunavyoona katika huyo aliyeshindwa. Mkristo anayeishi ulimwenguni yuko katika hatari ya kuzama katika mahangaiko ya kujipatia nafasi nzuri au kuwatafutia ndugu zake, na hivyo kusahau kwamba anapaswa kuelekea nchi nyingine, na kwamba ili aifikie anahitaji sio akili kuhusu shughuli za kidunia, bali msaada wa Mungu (ambao ajiombee) na tunda la neema (yaani stahili). Pia katika maisha ya kifamilia anaelekea kukwama katika mafungamano yanayomtimizia haja ya mapendo, na hivyo kusahau wajibu wa kumpenda Mungu kuliko viumbe vyote. Mara nyingi upendo wake si mwali hai unaoinuka kwa Mungu ukihuisha mapendo mengine yote, bali ni kama makaa madogo yanayozidi kuzimika chini ya majivu: ndiyo sababu anaweza akatenda dhambi kwa urahisi, asifikirie kuwa anasaliti urafiki wa Mungu. Hatimaye yuko katika hatari ya kufuata matakwa yake na, kisha kusali kifupi, kupanga maisha yake upande wa maumbile tu, akiathiriwa na umimi, mawazo ya kibinadamu na madai ya mazingira. Hapo akili inahangaikia maswala ya kidunia na pengine michezo, halafu yakitokea matatizo makubwa yanayohitaji nguvu nyingi za Kiroho anakuja kutambua imani yake ni haba mno: kwake kweli kuu za imani hazina nguvu kiutendaji, ziko mbali angani zisiingie ndani ya roho. Anakosa imani yenye vitendo ambayo ilete nuru ya mafumbo ya wokovu katika maisha ya kila siku.

Ndizo hatari zinazomkabili Mkristo asipojitahidi kutekeleza mashauri ya Kiinjili kadiri anavyoweza. Akiteleza kwenye mteremko huo, anapotea na kuzidi kupatwa na maradhi matatu yanayopingana moja kwa moja na hayo mashauri matatu: “Kila kilichomo duniani, yaani tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia” (1Yoh. 2:16). Hayo ni madonda matatu yenye usaha yanayoziathiri roho na kuziua kwa kuzisogeza mbali na Mungu.

Madonda hayo yameenea ulimwenguni kufuatana na dhambi ya mtu wa kwanza pamoja na dhambi zetu tulizozirudiarudia. Ili tuelewe ubaya wake tunapaswa kukumbuka kuwa kwa wengi yanashika nafasi ya ule ulinganifu uliokuwepo katika hali ya uadilifu asili pande zote tatu, na ambao Mwokozi anataka kuturudishia kwa njia ya mashauri yake.

Mtu alipoumbwa kulikuwa na ulinganifu kamili kati ya Mungu na roho, kati ya roho na mwili, kati ya mwili na vitu vya nje. Kulikuwa na ulinganifu kati ya Mungu na roho, kwa sababu roho imeumbwa ili kumjua, kumpenda na kumtumikia Mungu, na kwa njia hiyo kupata uzima wa milele. Mtu wa kwanza, aliyeumbwa katika utakatifu na uadilifu, alikuwa kama mwanasala mwenye kuongea kirafiki na Mungu akijilisha hasa mambo ya Kimungu, akizingatia yote katika mwanga huo na kumtii.

Kutokana na ulinganifu huo wa juu kulikuwa na ule kati ya roho na mwili, ulioumbwa ili utumikie roho. Roho ikiwa chini ya Mungu kikamilifu iliutawala mwili wake, maono na maelekeo ya hisi yakifuata kwa makini uongozi wa akili (yenye kufuata busara na kuangazwa na imani) na msukumo wa utashi (uliohuishwa na upendo).

Hatimaye kulikuwa na ulinganifu kati ya mwili na vitu vya nje, dunia ikizaa yenyewe pasipo haja ya kulimwa kwa jasho la uso; vilevile wanyama walikuwa wakimtii mtu aliyepewa kuwatawala, au walau hawakumdhuru.

Dhambi ilivuruga ulinganifu huo wote ikiangamiza ule wa juu: mtu aliasi sheria ya Mungu, na tangu hapo roho yake inaelekea kiburi na kukariri, “Sitatii”. Imeacha kujilisha ukweli wa Kimungu ijitungie mawazo yake finyu, danganyifu, geugeu, na kujitengenezea ukweli wake yenyewe na kujiongoza kwa kuiwekea mipaka mamlaka ya Mungu, badala ya kupokea toka kwake uongozi ule ambao peke yake unafikisha kwenye uzima.

Kwa kukataa kumtii Mungu, roho imepoteza utawala wake juu ya mwili na juu ya maono yake yaliyokusudiwa kutii akili na utashi. Tena mara nyingi imejifanya mtumwa wa mwili na silika zake za kinyama: ndizo tamaa mbaya za mwili. Watu wasio na idadi wanasahau lengo lao la Kimungu na kushughulikia kutwa kucha mwili wao kama mungu wao. Maono yanaitawala roho hata isipotaka, kwa kuwa ndani yake pendo, wivu, hasira na chuki vinajitokeza vikipambana na kuipeleka huko na huko kama farasi wasiokubali lijamu wala hatamu.

Hatimaye mwili, badala ya kufaidika na vitu vya nje, umekuwa mtumwa wa vitu hivyo: unajichosha ili kuvipata kwa wingi, unajizungushia fahari ya bure kwa hasara ya maskini wenye njaa, unajiona na haja na vile vyote vinavyong’aa na kuonekana na kuthaminika: ndizo tamaa za macho. Kisha kujilimbikizia vitu, hangaiko la kuvidumisha na kuvizidisha tena linakuwa wazo kuu kwa umati wa watu ambao, kama watumwa wa shughuli hizo, hawana kamwe muda wa kusali na kusoma Injili ili kujilisha rohoni; wanajijenga hapa duniani kama kwamba wataishi hapa milele yote, wasiwazie wokovu wao.

Utumwa huo wa pande tatu, ulioshika nafasi ya ulinganifu asili pande zote tatu, ni kinyume cha utaratibu. Mwokozi alikuja kuurudisha, na kwa ajili hiyo ametupatia mashauri matatu.

 

 

MASHAURI YA KIINJILI NA KURUDIA ULINGANIFU ASILI

 

Yesu katika ubinadamu wake ndiye kielelezo cha maadili yote, mfano bora wa utakatifu wote. Utu wake uliwekwa wakfu kwa Mungu tangu achukuliwe mimba, kutokana na umoja wake na nafsi ya Neno; kwa sababu hiyo ulipokea utakatifu wa kuzaliwa nao, usioumbwa. Haiwezekani kuwaza muungano na Mungu ulio wa ndani na wa kudumu kuliko huo unaounganisha utu na umungu katika nafsi ya Neno aliyefanyika mwili. Kutokana nao utu wa Mwokozi umewekwa wakfu kwa vipawa vyake vyote na kwa matendo yake yote, hata akili yake isiweze kudanganyika, utashi wake usiweze kufanya kosa na hisi zake safi zisiweze kuvurugwa na lolote. Matendo yake yote ni ya Mungu, yanatokana na Mungu na kumuelekea Mungu; hapana pengine popote utawala wa Aliye Juu ulipotimia kikamilifu hivyo. Kwa kuwa utu wa Yesu umewekwa wakfu namna hiyo bora, ukuu wake umemtenga na roho ya ulimwengu na yale yote yaliyo maovu au yasiyo mema tu, naye akatolewa kwa ulimwengu ili kuukomboa kutoka upofu wa tamaa na kiburi.

Kwa ukuu huo wa asili, Yesu alitengana na mali, heshima, shughuli za kidunia: kielelezo cha ufukara, hakuwa na mahali “pa kujilaza kichwa chake” (Lk. 9:58). Kwa ukuu huo, Yesu hakuambatana na furaha za dunia, alikuwa huru kuhusu madai ya familia ili aiunde nyingine ya kimataifa, yaani Kanisa: hivyo ni kielelezo cha useja mtakatifu, wenye uzazi wa Kiroho usio na mipaka. Hatimaye, kwa ukuu wake upitao maumbile, Yesu hakuambatana na matakwa yake yoyote: akiwa na umri wa miaka kumi na miwili alitamka kwamba ”imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu” (Lk. 2:49), halafu “akawa mtii hata mauti, naam, mauti ya msalaba” (Fil. 2:8).

Kwa kuwa Mwokozi ametoka juu, hakuwa wa ulimwengu huu, bali alitolewa auokoe, ukuu wake wenyewe ulimtenga na yale yote yaliyo ya chini aweze kuufanyia kazi ulimwengu kutoka juu ili kazi hiyo ifike popote na ipenye zaidi, kama vile jua likifika kwenye kilele cha mzunguko wake. Kwa kuwa huru kutoka vifungo vyote vya binadamu (mali, familia na mawazo finyu), Yesu aliweza kuwashughulikia binadamu wote akiwaletea uzima wa milele. Injili yake haizeeki, ni ya kisasa daima, vile Mungu alivyo. Hivyo katika Bwana tunaona urekebisho wa ulinganifu asili pande zote tatu, urekebisho bora kuliko ukamilifu wa Adamu: “dhambi ilipozidi, neema ilikuwa nyingi zaidi” (Rom. 5:20).

Urekebisho huo unatakiwa kuendelea katika Kanisa, linalopaswa kung’aa kwa utakatifu. Sifa yake hiyo inatakiwa kuwa wa ajabu na kuonekana, sio tu mara mojamoja katika watu shujaa (k.mf. wafiadini na watakatifu waliotangazwa rasmi), bali mfululizo katika familia za kitawa ambamo idadi kubwa ya watu inafuata shule ya utakatifu na kutamka hadharani nia ya kumfuata Bwana kwa kuungana na Mungu wasiambatane na malimwengu. Lakini kuna tofauti kubwa kati ya Bwana na watu hao, hata wakiwa na juhudi za namna gani: yeye ametoka juu, hao wametoka chini, katika dhambi na udanganyifu, na wanapaswa kujitenga navyo zaidi na zaidi ili kujiweka wakfu kwa Mungu kwa ndani zaidi na zaidi.

Wale waliopokea wito huo wa pekee, Mwokozi anawapendekezea waishi sio tu kwa kufuata roho ya mashauri matatu ya Kiinjili, bali kwa kuyatekeleza kweli, akiwaahidia mara mia zaidi. Anawaalika wajitenge pande tatu ili kujiweka wakfu pande tatu na hivyo kuhakikisha ustawi wa maadili bora hadi muungano na Mungu. Katika kutumia malimwengu anawashauri wabane kwa kujinyima wasije wakavutwa kuzidisha.

Anawaalika kutekeleza ufukara, kujitenga na matumizi huru na hata umilikaji wa vitu ili kuviweka wakfu kwa Mungu visiwe tena vizuio, bali vyombo kwa safari ya kuelekea uzima wa milele. Anawaalika kuishi kwa usafi kamili, yaani kujinyima furaha za jinsia na kuuweka moyo wao wakfu kwa Mungu, usiwe tena kizuio, bali chombo ambacho upendo unakifanya kuwa cha Kimungu ili kuungana na Mungu kila siku kwa dhati na nguvu zaidi. Hatimaye anawaalika kwenye utiifu mtakatifu, kujikomboa kutoka matakwa yao yoyote, yaliyojaa ugeugeu na ukaidi, ili utashi wao usiwe tena kizuio, bali chombo ambacho upendo unazidi kukifanya cha Kimungu ili kuungana na Mungu kwa undani na nguvu kila siku zaidi.

Utekelezaji wa maadili hayo matatu na wa nadhiri zake una shida, lakini unaondoa shida nyingine nyingi. Ndege anainua mabawa, lakini ni kweli zaidi kuwa mabawa yanamuinua ndege; vilevile maadili ya kitawa na nadhiri zake vinamletea mtu wajibu wa pekee, lakini hasa vinamleta kwenye ukamilifu wa upendo kwa haraka na hakika zaidi.

Maadili ya ufukara, useja na utiifu yako chini ya adili la ibada ambalo linampa Mungu ibada inayotupasa, kwa hiyo ni kuu kuliko maadili mengine ya kibinadamu, likifuata mara yale ya Kimungu. Lenyewe linamtolea Mungu vitendo vya kitawa. Ili mtawa awe na msimamo wa kutorudi nyuma anajifunga kwa nadhiri, akiwajibika kuyatekeleza hayo matatu mpaka kufa kwa mfano wa Bwana: anajitoa pamoja naye kwa maisha mazima ya sadaka; na kwa kuwa anapaswa kutoa yote (vitu, mwili na moyo, matakwa) asijichukulie tena, jina la sadaka ya kuteketezwa linafaa kweli.

 

Sadaka hiyo itimizwe kwa dhati kila siku; hapo itatupatia mara mia zaidi. “Amin, nawaambieni: hakuna mtu aliyeacha nyumba, au ndugu waume, au ndugu wake, au mama, au baba, au watoto, au mashamba, kwa ajili yangu, na kwa ajili ya Injili, ila atapewa mara mia sasa wakati huu, nyumba, na ndugu waume, na ndugu wake, na mama, na watoto, na mashamba, pamoja na udhia; na katika ulimwengu ujao uzima wa milele” (Mk. 10:29-30). Tutaona hapo mbele kwamba: imani ndiyo uhai wa utiifu mtakatifu, na utekelezaji wa adili hilo unakuza roho ya imani; tumaini ndilo uhai wa ufukara mtakatifu, unaotufanya tuzidi kumtumaini Mungu; na upendo ndio uhai wa useja mtakatifu ambao unapotekelezwa kikamilifu unastawisha ndani mwetu upendo kwa Mungu na kwa watu kwa ajili yake.

 

 

 

 

1.14. WAJIBU WA PEKEE WA MAPADRI NA WATAWA

WA KULENGA UKAMILIFU

 

 

Baada ya kueleza wajibu wa jumla unaowapasa Wakristo wowote wa kulenga ukamilifu kutokana na amri kuu ya upendo, inafaa tuzungumzie wajibu wa pekee wa kufanya hivyo unaompasa kila padri, awe ameweka nadhiri za kitawa au sivyo. Tunatakiwa hasa kuonyesha jinsi adili la ibada linavyohitaji kuhuishwa zaidi na zaidi na upendo kwa Mungu ambao uzidi kuwa safi na wa nguvu.

 

WAJIBU HUO KWA MTAWA

 

Msingi wa wajibu huo ni nadhiri za kitawa, ambazo neema zake si za muda, bali za kudumu tukizidi kuwa waaminifu. “Kwa kusema kwa usahihi, wengine wako katika hali ya ukamilifu, sio kwa kufanya tendo la upendo kamili, bali kwa kujifunga moja kwa moja, kwa fahari fulani, kushika kile kinachoelekeza kwenye ukamilifu… Hiyo ni kweli kwa watawa na kwa maaskofu. Kwa kuwa watawa wanajifunga kwa nadhiri kujinyima malimwengu ambayo wangeweza kuyatumia kwa hiari, nao wanafanya hivyo ili kushughulikia mambo ya Mungu kwa urahisi zaidi… Vilevile maaskofu wanajifunga kushika mambo ya ukamilifu wanapokubali daraja ya uaskofu, kwa sababu mchungaji anapaswa kutoa uhai wake kwa ajili ya kondoo zake” (mt. Thoma wa Akwino).

Mtawa anatamka kuwa atalenga ukamilifu: “Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! Bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo, kwa ajili yake, nimeshikwa na Kristo Yesu” (Fil. 3:12). Hatendi kosa la unafiki kwa kutokuwa bado mkamilifu, ila analifanya asipolenga ukamilifu kwa unyofu. Kwake wajibu huo wa pekee ni mamoja na ule wa kushika nadhiri zake na kanuni aliyoahidi. Lakini wajibu huo uzingatiwe daima katika uhusiano wake na ule wa jumla unaotokana na amri kuu ya upendo; hapo utawa hautapotewa na ukuu wake kwa kutazamwa upande wa sheria tu, bali utaonekana katika upana wa maana yake ya Kiroho.

Kwa mtazamo huo unaeleweka uzito halisi wa neno la mt. Thoma wa Akwino: “Kufanya tendo kwa nadhiri kunastahili kuliko kulifanya bila ya nadhiri”. Si kwamba tuzidishe nadhiri ili kustahili zaidi, bali kwamba mtawa atekeleze nadhiri zake vizuri zaidi na zaidi, akizidi kuchimba sababu tatu alizozitoa mtakatifu huyo katika ufafanuzi wake:

Nadhiri ni tendo la adili la ibada, ambalo ni bora kuliko yale ya utiifu, ufukara na usafi wa moyo ambayo linamtolea Mungu yawe ibada.

2° Kwa nadhiri ya daima mtu anamtolea Mungu si tendo mojamoja, bali uwezo wenyewe wa kutenda, na kwa hakika ni afadhali kutoa mti na matunda yake kuliko kutoa matunda tu.

3° Kwa nadhiri utashi unaimarishwa katika kutenda mema, na kwa hakika kutenda kwa msimamo kunastahili zaidi, kama vile ni vibaya zaidi kutenda dhambi kwa utashi ulioimarika katika nia mbovu.

Tukiishi kwa roho hiyo tunaelewa kwa namna hai fundisho la kwamba, kwa kujifunga kushika mashauri matatu, zilizo kiini chenyewe cha utawa, mtu anajitenga na yale yanayoweza yakazuia mapendo yake yasimuelekee Mungu tu, halafu asipofuta uamuzi huo anajitoa kwa Bwana kama sadaka ya kuteketezwa. Hivyo hali yake ni ya kujitenga na ulimwengu na kuwekwa wakfu kwa Mungu.

Hasa mambo matatu yanaweza kuzuia mapendo yake yasimuelekee Mungu: tamaa za macho (yaani za vitu), tamaa za mwili na kiburi cha maisha (yaani kupenda kuwa huru tu). Mtawa anayakataa hayo matatu kwa nadhiri zake, kwa sababu anamtolea Mungu mali kwa ufukara, mwili na moyo kwa useja mtakatifu na matakwa yake kwa utiifu. Asipojitwalia tena chochote, tena akitekeleza vizuri zaidi na zaidi, kwa upendo mkubwa, maadili matatu yanayohusiana na nadhiri za kitawa, basi anamtolea kweli Mungu sadaka ile kamili inayostahili kuitwa ya kuteketezwa. Hapo maisha yake yanatolewa kila siku pamoja na sadaka ya misa kwa adili la ibada. Ni hivyo hasa kama mtawa anarudia mara nyingi ahadi zake kwa namna inayostahili kuliko alipozitoa kwa mara ya kwanza. Stahili zinakua ndani mwake pamoja na upendo na maadili mengine, hivyo hali yake ya kuwekwa wakfu kwa Mungu inazidi kuwa ya dhati na kamili.

Lengo la kujinyima hivyo pande tatu na kujitoa hivyo pande tatu ni kuungana na Mungu kila siku kwa ndani zaidi, kama utangulizi wa uzima wa milele. Mtawa anapaswa kuufikia muungano huo kwa kumuiga Yesu Kristo aliye “njia, na kweli, na uzima” (Yoh. 14:6). Yeye, katika ubinadamu wake, alitenganika na roho ya ulimwengu akaunganika na Mungu vizuri iwezekanavyo. Mtawa anatamka hadharani nia ya kumfuata, lakini Yesu alitoka juu, kumbe mtawa ametoka duniani, palipotawaliwa na dhambi, hivyo anapaswa kujitenga zaidi na zaidi na mambo yote ya kidunia ili kujiweka wakfu kwa Mungu kwa ndani zaidi na zaidi. Hapo ndani mwake yatatimia maneno haya: “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu, Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu. Yafikiri yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi. Kwa maana mlikufa, na uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu. Kristo atakapofunuliwa, aliye uhai wetu, ndipo na ninyi mtafunuliwa pamoja naye katika utukufu” (Kol. 3:1-4). Mt. Thoma wa Akwino alifafanua hivi: “Msionje malimwengu kwa kuwa mmefia ulimwengu; uhai wenu umefichwa pamoja na Kristo; mwenyewe amefichika kwetu, kwa kuwa yuko katika utukufu wa Mungu Baba yake, na hivyo uhai… tulionao kutoka kwake umefichika, kadiri ya maneno ya Maandiko matakatifu, Jinsi zilivyo nyingi fadhili zako ulizowawekea wakuchao; ulizowatendea wakukimbiliao mbele ya wanadamu! (Zab. 31:19). Yeye ashindaye nitampa baadhi ya ile mana iliyofichwa (Ufu. 2:17)”. Hiyo mana ya Kiroho, ambayo ile ya jangwani ilikuwa mfano wake tu, ndiyo malisho ya roho: kujaliwa kuzama katika mafumbo kwa imani hai iliyoangazwa na vipaji vya Roho Mtakatifu. Hivyo maisha ya utendaji (yaani utekelezaji wa maadili ya kibinadamu) yanaandaa kwa maisha ya sala ya kumiminiwa (yaani muungano na Mungu); kwa namna ya pekee “ubikira unalenga ustawi wa roho katika maisha ya kuzama katika sala” (mt. Thoma wa Akwino). Hivyo maisha ya kitawa yanalenga utekelezaji mkamilifu zaidi na zaidi wa amri ya upendo na undani wa muungano na Mungu.

Basi, inafaa kuzingatia daima wajibu wa pekee alionao mtawa wa kulenga ukamilifu kuhusiana na wajibu wa waamini kwa jumla unaotegemea amri kuu ya upendo. Amri hiyo inatawala mashauri ya Kiinjili, kwa kuwa hayo ni njia na vyombo tu kwa ajili ya kufikia kwa kasi na hakika zaidi ukamilifu wa upendo, yaani muungano wa dhati na Mungu unaostawisha zaidi na zaidi ule na jirani.

Hivyo, kwa mwanga wa maadili matatu ya Kimungu yanatekelezwa kikamilifu maadili matatu ya kitawa. Kati ya hayo linaundwa fungamano la ndani, hivi kwamba tumaini la heri ni kama uhai wa ufukara unaoachana na mali ya dunia ili kupata ya milele; upendo ndio uhai wa useja unaojinyima pendo la chini ili kupata upendo wa juu kabisa; imani ndiyo uhai wa utiifu unaotekeleza maagizo ya wakubwa kama kwamba yamefunuliwa na Mungu. Hivyo maisha ya kitawa yanafikisha kwenye sala ya kumiminiwa na muungano wa ndani na Mungu.

 

 

WAJIBU WA PEKEE ALIONAO PADRI WA KULENGA UKAMILIFU

 

Ikiwa bradha na sista wana wajibu wa pekee wa kulenga ukamilifu, zaidi tena anao padri, hata kama si mtawa. Utawa ni hali ya kulenga ukamilifu; maaskofu wako katika hali ya kutekeleza ukamilifu; ndiyo sababu inafaa wawe katika hatua ya muungano ya waliokamilika. Padri wa ulimwenguni anajiongezea stahili mpya akiingia utawani. Lakini kwa vyovyote anapaswa tayari alenge ukamilifu kutokana na sakramenti ya daraja na kazi zake takatifu. Wajibu huo maalumu hautofautiani na ule wa kutimiza kitakatifu majukumu mbalimbali ya kipadri. Kutokana na amri kuu anapaswa kuyatimiza vizuri zaidi na zaidi, kadiri upendo unavyostawi hadi kufa kwake.

Upadirisho unadai, sio tu hali ya neema ya utakaso na vipaji vya pekee, bali mwanzo wa ukamilifu, maisha bora kuliko yanayotakiwa kwa mtu anayeingia utawani. Kwa kuwa padri anapaswa kuwaangaza wengine, inafaa awe katika hatua ya mwanga. Tena matokeo ya upadirisho ni alama isiyofutika ambayo inamshirikisha moja kwa moja ukuhani wa Kristo, pamoja na neema ya sakramenti inayomwezesha kutimiza kazi za kipadri inavyomfaa mtumishi wa Kristo. Hiyo neema ya sakramenti inatimiliza neema ya utakaso na kumpa padri haki ya kupokea misaada inayohitajika ili atimize kitakatifu zaidi na zaidi matendo ya kipadri. Ni kama sehemu ya sura ya Kiroho ya padri, ambaye anapaswa kuelewa zaidi na zaidi ukuu na masharti ya upadri wake. Kwa hakika upadirisho ni bora kuliko nadhiri za kitawa, na wajibu maalumu wa kulenga ukamilifu unaotokana nao ni mkubwa kuliko ule unaotokana na nadhiri.

“Umekuwa padri, umepakwa mafuta ili umtolee Mungu sadaka ya misa. Fanya sasa kwa bidii, kwa uaminifu, kila wakati inapofaa. Sasa uwe na mwendo mzuri bila ya hitilafu. Usidhani kwamba u huru kuliko watu wengine, bali umefungwa kifungo cha sheria, hata imekupasa kutafuta ukamilifu mkubwa zaidi. Ni lazima padri awe mtu aliyepambwa fadhila zote, kusudi awape watu wengine mfano wa maisha mema. Mazoea yake siyo waliyozoea watu wa dunia, watu wa chini, bali yafuatana na malaika wa mbinguni; rafiki zake ndio watu watimilifu walioko duniani” (Kumfuasa Yesu Kristo, IV,5:2). Kazi za kipadri, kuhusiana na Mwokozi aliomo katika ekaristi na Mwili wake wa fumbo, zinatuonyesha kuliko upadirisho wenyewe wajibu wake wa pekee wa kulenga ukamilifu.

Padri anapoadhimisha misa ni mfano wa yule anayesema kwa niaba yake, yaani Kristo aliyejitoa kwa ajili yetu. Anapaswa kuelewa ukuu wa kazi yake na kuzidi kuungana kwa dhati na kuhani mkuu ambaye ni kafara pia. Ni unafiki, au walau ni uzembe wenye kosa, kupanda altareni bila ya nia imara ya kupanda juu katika ngazi ya upendo. Mtumishi wa Kristo anapaswa kusema kila siku kitakatifu zaidi, “Huu ndio mwili wangu… Hiki ni kikombe cha damu yangu”. Kila siku zaidi komunyo yake inatakiwa kuwa motomoto kwa utashi kuwa tayari kumtumikia Mungu, kwa sababu ekaristi inatakiwa kukuza upendo ndani mwetu, si kuutunza tu. “Kwa ukuu wa kazi ambayo padri altareni ni mtumishi wa Kristo, unadaiwa utakatifu wa ndani ulio mkubwa kuliko ule unaodaiwa na utawa” (mt. Thoma wa Akwino). Hivyo, mambo yakilingana, tendo dhidi ya utakatifu ni dhambi kubwa zaidi likitendwa na padri kuliko likitendwa na bradha. “Padri mwenye kumtolea Mungu sadaka ya misa, humsifu Mungu, huwafurahisha malaika, huthibitisha Kanisa, husaidia walio hai, hutuliza marehemu, hupewa mwenyewe neema zote” (Kumfuasa Yesu Kristo, IV,5:3). Anapaswa pia kuadhimisha Sala ya Kanisa kwa makini na ibada halisi. Sala hiyo kuu inatangulia na kufuata misa; ni wimbo wa bibi arusi wa Kristo kwa usiku na mchana, hivyo ni heshima kubwa kuhusika nao. Tusali hivyo tukizingatia nia kuu za Kanisa, kama vile kupatanisha ulimwengu kwa kueneza utawala wa Mungu.

Hatimaye padri ana wajibu wa pekee wa kulenga ukamilifu ili atimize vizuri kazi zake kwa ajili ya Mwili wa fumbo wa Kristo. “Hakuna kinachofaa zaidi kuwaongoza waamini kwenye ibada halisi kuliko mfano mwema wa padri. Macho ya watu yanamuelekea yeye, kama kioo cha ukamilifu ambao waige. Kwa hiyo, basi, anatakiwa kupanga maisha yake, sura yake ya nje, mwendo wake na, matendo yake hivi kwamba adumishe daima uzito, utaratibu na tabia ya kidini ambavyo anapaswa kuwa navyo” (Mtaguso wa Trento). Padri wa ulimwenguni halazimiki kuweka nadhiri ya ufukara, lakini anatakiwa kutoshikamana na malimwengu kwa kuwa radhi kuwapa maskini; anatakiwa pia kumtii askofu wake na kuwa kama mtumishi wa waamini, bila ya kujali matatizo na pengine masingizio anayoweza akakabiliana nayo.

Haja ya ukamilifu huo ni wazi kuhusu mahubiri, maungamo na uongozi wa Kiroho. Ili mahubiri yawe hai na kuzaa matunda, ni lazima padri aseme “yaujazayo moyo wake” (Math. 12:34). Tena mt. Thoma wa Akwino alisema yanatakiwa “kutokana na utimilifu wa sala ya kumiminiwa”, na imani hai yenye kupenya na kuonja fumbo la Kristo, thamani isiyo na kifani ya misa, ya neema ya utakaso na ya uzima wa milele. Padri anapaswa kuhubiri kama mwokozi wa roho, akifanya kazi mfululizo kwa wokovu wa wengi. Hatakiwi kuwa amepokea upadri bure. Ni vilevile kuhusu huduma ya kitubio na uongozi wa Kiroho. Padri anapaswa kuwa mtu mwangavu na motomoto, la sivyo huduma hiyo inaweza kuwa hatari kwake na kumpotosha mwenyewe, badala ya kuokoa watu. Maisha yasipopanda juu, yanateremka chini; ili yasiteremke ni lazima yapande juu kama mwali wa moto. Hasa hapa inafaa kusema: asiyesonga mbele, anarudi nyuma. Hatimaye, wanaweza wakamuelekea padri watu ambao Mungu anawadai zaidi; ni lazima wakute kwake msaada wa hakika kwa kufuata njia nyofu ya utakatifu; haifai waende mbali naye pasipo kupata chochote toka kwake.

Mh. Antoni Chevrier alikuwa akiwafundisha mapadri aliowalea wawe daima na pango, Kalivari na tabenakulo machoni mwao. Pango liwakumbushe ufukara; padri anapaswa kuwa fukara katika nyumba yake, mavazi yake na chakula chake. Anapaswa kuwa mnyenyekevu kwa Mungu na kwa watu. Kadiri alivyo hivyo anamtukuza Mungu na kumfaa jirani. Padri ni mtu asiye na kitu. Kalivari imkumbushe haja ya kujitoa sadaka, kujifisha kuhusu mwili wake, roho yake, matakwa yake, heshima yake, familia yake na ulimwengu. Anapaswa kujitoa sadaka kwa kimya, kazi, malipizi, mateso na kifo. Kadiri padri alivyokwishakufa hivyo anao uzima ndani mwake na kuwashirikisha wengine. “Padri ni msulubiwa. Kwa mfano wa Mwalimu anapaswa kwa upendo kujitoa mwili, roho, muda, mali, afya, uhai; anapaswa kutoa uhai kwa imani yake, mafundisho yake, maneno yake, sala zake, athari yake, mifano yake. Anapaswa kuwa mkate mtamu. Padri ni mtu wa kuliwa”. Tabenakulo imkumbushe upendo anaopaswa kuwa nao.

Ndicho kipeo cha upadri ambacho kila mmoja awe nacho: “Nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo” (Yoh. 13:15).

 

 

 

 

1.15. HATUA TATU ZA MAISHA YA KIROHO

KADIRI YA MABABU NA WALIMU WAKUU

 

 

Kisha kusema juu ya ukamilifu wa Kikristo, tunapaswa kuzungumzia tofauti iliyopo kati ya hatua tatu za maisha ya Kiroho; hilo ni mojawapo katika maswala makuu ya fani hiyo. Hatua hizo zinaitwa za wanaoanza, wanaoendelea na waliokamilika; au za utakaso, mwanga na muungano. Tofauti na wanateolojia kadhaa wa karne za mwishomwisho, walimu wakuu wa maisha ya Kiroho waliamini watu wowote wanaweza kutamani na kujiombea kwa unyenyekevu neema ya kuzama katika mafumbo ya imani, ambayo yote yanadhihirisha wema wa Mungu usio na mipaka. Waliona huko kuzama katika sala ni kwa lazima kwa muungano wa ndani na Mungu ulio ukamilifu wa Kikristo. Kwa msingi huo walifafanua kila hatua ya maisha ya Kiroho.

 

 

USHUHUDA WA MAANDIKO MATAKATIFU

 

Tutataja madondoo machache tu yaliyo muhimu zaidi, baada ya yale mengi tuliyokwishatoa. Katika Injili, hasa kadiri ya heri nane, tumeona ukuu wa ukamilifu wa Kikristo tusioweza kuupata tusipofisha yale yote yasiyofaa ndani mwetu, tusipobeba msalaba kwa uvumilivu, tusipomuomba Baba aliyefichika moyoni mwetu, tusipomsikiliza kwa makini Roho Mtakatifu kila anapotuangaza, ili kwa msaada wake wa pekee tuzame kwa upendo katika mafumbo ya wokovu.

Mt. Paulo aliandika yanayofaa kwa kawaida kwa hatua ya waliokamilika: “Iko hekima tusemayo kati ya wakamilifu…twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu... Mambo ambayo jicho halikuyaona, wala sikio halikuyasikia, wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu, mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao… ametufunulia sisi kwa Roho. Maana Roho huchunguza yote, hata mafumbo ya Mungu” (1Kor. 2:6-10). Ndiyo yanayotazamwa na waliokamilika wanaposali. “Kwa hiyo nampigia Baba magoti… awajalieni, kwa kadiri ya utajiri wa utukufu wake, kufanywa imara kwa nguvu, kwa kazi ya Roho wake, katika utu wa ndani. Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo; ili mpate kufahamu pamoja na watakatifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo, na kina; na kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate kutimilika kwa utimilifu wote wa Mungu” (Ef. 3:14-19). Ndiyo sifa maalumu ya hatua ya waliokamilika: kujaliwa kuzama katika fumbo la Kristo na kuungana na Mungu kutokana nako.

Katika maisha ya mitume, waliolelewa na Bwana moja kwa moja, kuna hatua tatu tofauti zinazolingana na zile za maisha ya Kiroho. Hatua ya kwanza ya maisha yao ya Kiroho, ambayo ni ile ya wanaoanza, ilichukua tangu waongoke hadi kwenye mateso ya Bwana, ambapo walipitia shida kubwa hata mt. Petro akamkana Mwalimu wake. Halafu akajuta, na ndio wongofu wake wa pili, katika ule utakaso wa Kimungu uliokuwa kama usiku wa giza na mateso. Kitu cha namna hiyo kiliwatokea mitume wengine pia walipojaliwa kughairi baada ya kukimbia. Hatua ya pili ya maisha yao ya Kiroho, ambayo ni ile ya wanaoendelea, ilichukua kuanzia Mateso hadi Pentekoste. Kipindi hicho walikuwa bado waoga, imani yao ilihitaji kuangazwa, tumaini lao lilihitaji kuimarishwa, nao upendo wao haukuwa bado na ari ile uliyopaswa kuwa nayo. Hatua hiyo ilitimia kwa kuondolewa uwepo wa kimwili wa Bwana alipopaa mbinguni. Hapo walipaswa kuendelea kwa imani tupu, wakikabili dhuluma walizotabiriwa. Hatua ya tatu iliwaanzia Pentekoste, ambayo ikawa kwao kama wongofu wa tatu, utakaso halisi wa Kimungu na mageuzo yaliyowaingiza katika maisha makamilifu. Iliangaza akili yao na kuimarisha utashi wao ili wamhubiri popote Yesu msulubiwa. Sifa maalumu ya hatua hiyo ni kuzidi kuungana kwa ndani na Mungu, kujitoa sadaka kikamilifu hadi kufia dini. Hapo mbele tutazirudia hatua zao hizo ambazo kila moja inaanza na wongofu au mageuzo ya roho. Tukizitafakari zinaangaza kweli hatua tatu za maisha ya Kiroho. Maelekezo hayo ya Maandiko yanathibitishwa na Mababu wa Kanisa.

 

 

USHUHUDA WA MAPOKEO

 

Tuone kwanza ushuhuda wa Mababu wa Mashariki.

Mt. Inyasi wa Antiokia aliandika mara nyingi juu ya uwepo wa Kiroho wa Mwokozi ndani ya waamini, akiwaita waleta-Kristo au waleta-Mungu na kuwahimiza hivi: “Tufanye tendo letu lolote kwa kuzingatia kwamba Mungu anaishi ndani mwetu; hivyo tutakuwa mahekalu yake, naye atakuwa Mungu wetu mwenye kukaa ndani mwetu”. Mwenyewe alitamani kuishi kwa kuungana na Kristo zaidi na zaidi, na kufa ili kuungana naye milele. Barua zake zimejaa ujuzi wa juu wa Kristo, imani hai yenye kupenya ambayo si tofauti na sala ya kumiminiwa na ambayo inafurika katika utendaji wa kitume wenye matunda mengi kutokana na upendo mkubwa. Lakini ili kufikia muungano huo wa dhati ni lazima kujidharau pamoja na yale yote ambayo hayafai ndani mwetu na ambayo yanafisha uzima wa Kimungu. Upande wake alitamani kusagwa na meno ya simba awe unga wa ngano wa Kristo, kama vile Yesu alivyosagwa awe mkate wetu wa ekaristi.

Mt. Irenei alisisitiza binadamu akubali kufinyangwa na Mungu kama udongo mikononi mwa mfinyanzi. Badala ya kupinga au kukwepa kazi hiyo, azidi kujionyesha mtulivu kwa Roho Mtakatifu katika sala na hivyo atafikia upimaji wa Kiroho wa mambo yote na kuishi kwa upendo wa Mungu tu.

Klementi wa Aleksandria alieleza roho inavyopanda juu kupitia hali zifuatazo: kwanza uchaji wa Mungu, halafu imani na tumaini, hatimaye upendo na hekima. Waliokamilika wana amani na kutawaliwa na upendo; wamejaliwa hekima ya siri ya Mungu, ujuzi wa dini ambao unatokana na mwanga wa Roho Mtakatifu kwa roho sikivu na kugeuza maisha yao ya ndani kwa kuwafanya marafiki wa Mungu.

Sawa naye, mwanafunzi wake Origenes alisema kuwa aliyekamilika anaishi hasa kwa upendo na kwa kawaida anapokea kwa Roho Mtakatifu hekima ya kujaliwa, ujuzi wa ndani wa fumbo la Utatu mtakatifu. Kuhusu Injili ya Yohane aliandika, “Hakuna anayeweza kuelewa maana ya Injili kama hajaegama kifuani pa Yesu wala hajapokea kutoka kwake mama Maria awe mama yake pia”. Neno ndiye anayejifunua kwa waliokamilika na kuwaunda kama alivyowaunda mitume. Mwenyewe alitofautisha wazi hatua tatu: ile ya wanaoanza, ambao ndani mwao maono yasiyofaa yanapungukiwa nguvu; ile ya wanaoendelea, ambao ndani mwao maono hayo yanaanza kuzimika kwa wingi wa neema; hatimaye ile ya waliokamilika. Alihimiza usikivu kwa Roho Mtakatifu, ambaye kwa njia yake tunaweza kumuendea Kristo na kwa njia yake tena tunapanda juu kwa Baba, katika sala ya kumiminiwa inayosaidiwa na upweke.

Didimo Kipofu alimualika kila Mkristo kuungana kikamilifu na Kristo, Bwanaarusi wa roho iliyotakata.

Mt. Bazili katika Kanuni zake alipanga maisha ya Kiroho imara yanayoandaa kwa sala ya kumiminiwa na muungano na Mungu. Kutakata zaidi na zaidi ni sharti la kuungana naye katika sala ya kumiminiwa: “Jicho la roho, kisha kuwa safi pasipo kivuli, linatazama mambo ya Mungu kwa mwanga ambao unatoka juu na kuijaza kwa wingi usiishibishe… Kisha kustahimili mapigano masumbufu sana na kufaulu kuiokoa roho – iliyoambatana sana na mwili – katika mchanganyiko wa maono, inakuwa ya kufaa kwa kuongea na Mungu… Aliyefikia hali hiyo hatakiwi tena kukubali mvuke wa maono ya kidunia uchafue na kufunika kwa ushungi macho ya roho yake na hivyo kuifanya ikose sala ya kumiminiwa ya Kiroho na ya Kimungu”.

Mt. Gregori wa Nazienzi alisema kuwa Mungu ni mwanga halisi tusioweza kuupata tusipokuwa wenyewe mwanga na kutakata ili kupanda kutoka uchaji wa Mungu kwenda hekima. Katika waandishi hao wote tunakuta majina haya matatu: utakaso, mwanga na muungano.

Mt. Gregori wa Nisa alionyesha tunavyopaswa kujitenga na viumbe na kuishi kwa Kristo ili tukaribishwe kutazama umungu na kuungana nao. Ushindi huo juu ya adui unapatikana kwa njia ya msalaba tu, na kwa kujitakasa zaidi na zaidi katika mambo yote ya hisi. Ukamilifu unaifanya roho iwe bibiarusi wa Kristo.

Hata mt. Efrem aliona kwamba sala ya kumiminiwa, tunayojaliwa kwa kuwa wasikivu kwa Roho Mtakatifu, ndiyo fadhili ya maisha makamilifu. “Tutakapokuwa tumeshinda maono yetu, na kuangamiza ndani mwetu mapenzi yoyote ya kimaumbile, na kuondoa kabisa rohoni mwetu hangaiko lolote lisilosaidia wokovu, hapo Roho Mtakatifu, kwa kuikuta roho yetu katika utulivu, na kuishirikisha akili yetu uwezo mpya, atatia mwanga mioyoni mwetu, kama inavyowashwa taa iliyo tayari kwa utambi na mafuta… Basi, kabla ya yote, tuandae roho zetu kupokea mwanga wa Kimungu, ili tustahili zawadi za Mungu”.

Kwa Dyonisi utakaso unaandaa kumjua Mungu kwa dhati; mwanga unashirikisha ujuzi huo; hatimaye utakatifu unafanya uchanue kikamilifu. Hatua ya muungano inahusu mafumbo na ni utangulizi wa uzima wa milele.

Mt. Masimo alifafanua mafundisho hayo akitofautisha hatua tatu za sala, zinazohusiana na hatua tatu za upendo. “Sala ya kawaida ni kama mkate: inawatia nguvu wanaoanza; ikiongezewa neema ya kuzama kidogo katika mafumbo, inakuwa kama mafuta tunayojipaka; hatimaye, tukizama kabisa ni kama divai tamu mno inayolevya wanaoinywa hata wakajisahau… Kuzama katika sala kunatokana na mwanga wa Roho Mtakatifu… Aliyetakata anaangazwa na kustahili kuingia ndani kabisa mwa hekalu na kufurahia muungano na Neno”. Mwenyewe alionyesha majaribu makali ambayo wanasala wanapaswa kuyapitia ili kutakaswa moja kwa moja na kuthibitishwa katika upendo wa Mungu.

Hatimaye mt. Yohane wa Damasko aliandika, “Aliyefikia kiwango cha juu kabisa cha upendo, kama kwa kutoka nje ya nafsi yake, anamvumbua Yule asiyeonekana; akiruka juu ya wingu lile la hisi linalozuia macho ya roho yasione. Akidumu katika amani, anamkazia macho Jua la Haki na kufurahia tamasha hilo asiloweza kulikinai… Kufikia kumtazama Mungu, kisha kutekeleza kwa bidii maadili, ni hazina isiyonyang’anyika kamwe”.

Basi, kadiri ya Mababu wa Mashariki, huko kuzama katika mafumbo ya Kimungu, kunakotokana na kipaji cha hekima, ni kwenye njia ya kawaida ya utakatifu. Mwanzo wake ni hatua ya wanaoendelea, halafu kunaendana kwa kawaida na upendo wa waliokamilika.

 

Mababu wa Kilatini wametuachia mafundisho hayohayo.

Mt. Augustino alitofautisha ngazi mbalimbali, akisisitiza vita dhidi ya dhambi (vilivyo kazi ngumu ya utakaso), vinavyofuatwa na mwanga kwa waliotakata, na hatimaye na muungano na Mungu. Halafu akaelekeza safari ya roho kupanda kwa Mungu kufuatana na vipaji vya Roho Mtakatifu: uchaji wa Mungu ndio kidato cha kwanza, na hekima ndiyo kilele. Kati ya hivyo viwili alibainisha vipindi viwili vya maandalizi yenye kutakasa. Alikiita kile cha mbali “maisha ya utendaji”, yaani utekelezaji wa maadili ya kibinadamu yanayohusiana na vipaji vya ibada, nguvu, elimu, shauri; halafu kile cha karibu “maisha ya sala ya kumiminiwa”, yaani utekelezaji bora wa maadili ya Kimungu na wa vipaji vya akili na hekima katika roho zilizo tulivu na sikivu kwa neema. Hapo imani ni chanzo cha kuzama katika mafumbo, na upendo motomoto unaunganisha kwa dhati roho na Mungu: ndiyo sala ya kumiminiwa.

Mt. Yohane Kasiano alionyesha kuwa hapa duniani mwisho wa maisha ya Kiroho ni kumtazama Mungu, ambako upendo kwake unatekelezwa kikamilifu. Tunapaswa kujiandaa kufikia huko kwa njia ya kusali ili tusamehewe dhambi, kutekeleza maadili na kutamani upendo wa kuwaka zaidi. Hapo sala inakuwa “yote ya moto” kutokana na “kumtazama Mungu tu na kuwaka kwa upendo motomoto… Hivyo roho katika chungu ya udongo inaanza kuonja malimbuko ya utukufu inaotumainia mbinguni”.

Mt. Gregori Mkuu alikubali kugawa maisha ya Kiroho katika ngazi tatu: mapambano na dhambi, maisha ya utendaji au utekelezaji wa maadili, na maisha ya sala ya kumiminiwa ambayo yanahitajiwa na wahubiri wa Neno la Mungu na wale wanaotaka kuufikia ukamilifu. Kwake matendo yote yanakosa ukamilifu mpaka roho ziwe zimeangazwa na sala ya kumiminiwa kutoka juu. Ndio kikomo cha juhudi, tunda la neema maalumu na utekelezaji wa kipaji cha hekima. Ni hali ya kujaliwa kuzama katika mafumbo ambayo mtu ajiandae kuipokea kwa unyenyekevu, usafi wa moyo na kukusanya mawazo karibu mfululizo. Mwenyewe alionyesha matakaso machungu ambayo “yanakausha ndani mwetu kila aina ya mapenzi ya kihisi” na kutuandaa tuzame katika sala na kuungana na Mungu, ambapo tunakuta nguvu kubwa katika majaribu na upendo motomoto.

 

 

HATUA TATU ZA MAISHA YA KIROHO NA ZILE ZA MAISHA YA KIMWILI

 

Mtakatifu Thoma wa Akwino amefananisha hatua tatu za maisha ya Kiroho na zile za maisha ya kimwili: utoto, ujana na utu uzima. Ni mfano unaostahili tuuzingatie kwa kuangalia vipindi vya mpito kati ya hatua moja na nyingine.

Inakubalika kuwa sehemu ya kwanza ya utoto inakwisha akili inapochangamka kwenye umri wa miaka saba hivi, halafu inafuata sehemu ya pili inayodumu mpaka ubalehe, kwenye miaka kumi na nne hivi. Ujana unaenea kati ya miaka hiyo na ishirini. Halafu unafuata utu uzima, ambamo tunatofautisha kipindi kinachotangulia ukomavu kamili na kile kinachoufuata kwenye miaka thelatini na tano hivi, kabla ya kuanza mteremko wa uzee.

Namna ya kuwaza inabadilika pamoja na mwili. Mtoto anafuata ubinifu na hisi; hajajua kufanya utambuzi na kupanga, na hata akili inapoanza kuchangamka inaendelea kutegemea mno hisi. Mtu anapobalehe anabadilika si kimwili tu, bali pia kinafsi, kiakili na kiadili: haridhiki tena na ubunifu, bali anaanza kutafakari maisha na haja ya kujiandaa kufanya kazi fulani. Kipindi hicho cha mpito, kinachoitwa pengine umri usio na shukrani, hakikosi matatizo; ndipo tabia adili inapoundika au inaharibika; pengine mtu anabaki nyuma, bila ya msimamo, akiwa tofauti na kawaida. Mfano huo unaangaza maisha ya Kiroho ambamo aliyeanza asipokuwa kwa wakati wake mtu anayeendelea, basi ama anaelekea maovu ama anabaki nyuma na kuwa vuguvugu, aina ya mbilikimo upande wa roho. “Kutotaka kusonga mbele ni kurudi nyuma” (mt. Bernardo), kumbe kulenga ukamilifu moja kwa moja ni kuwa nao tayari kwa namna fulani.

Ikiwa ubalehe ni kipindi kigumu upande wa mwili na wa maadili, ni kigumu vilevile kile cha uhuru wa kwanza kinachomuingiza kijana kwenye utu uzima. Akimaliza kukomaa kimwili anapaswa kuanza kushika nafasi yake katika jamii. Sawa na mwana mpotevu, wengi wanapita vibaya kipindi hicho, wakichanganya uhuru wanaoachiwa na idhini ya kutenda lolote. Kinyume chake, anayekomaa inavyotakiwa na kushika njia nzuri, anajihusisha na mambo yake binafsi, ya familia na ya jamii kwa namna bora kuliko kijana, akiyazingatia kwa upana zaidi. Inatokea karibu hivyo katika maisha ya Kiroho kwa mtu anayeendelea: namna yake ya kuwaza inainuka na kuwa ya Kiroho zaidi na zaidi; anazidi kuona vizuri mambo ya ufalme wa Mungu au maisha ya Kanisa kuhusiana na uzima wa milele.

Katika hatua tatu za maisha ya Kiroho “kuna viwango mbalimbali vya upendo kulingana na majukumu mbalimbali ambayo ustawi wa upendo unamdai mtu ayachukue. La kwanza ni kukwepa dhambi na kushinda mivuto ya tabia mbovu inayopingana na mivuto ya upendo: ndilo jukumu la wanaoanza, ambao ndani mwao upendo unatakiwa kulishwa na kutunzwa usije ukapotea. Hapo linakuja jukumu la pili: mtu anapaswa hasa kukesha na kukua katika uadilifu, jambo linalowafaa wanaoendelea ambao kazi yao hasa inalenga upendo uimarike kwa kustawi ndani mwao. Jukumu la tatu la mtu ni kujitahidi hasa kuungana na Mungu na kumfurahia: ndilo linalowafaa waliokamilika, wanaotamani kwenda zao wakae na Kristo (taz. Fil. 1:23)” (mt. Thoma wa Akwino).

Ni muhimu tuongeze kuhusu mpito kati ya hatua na hatua. Kama vile kati ya utoto na ujana kuna kipindi kigumu cha ubalehe, vilevile kuna kipindi cha namna hiyo katika kuvuka toka hatua ya utakaso ya wanaoanza kwenda hatua ya mwanga ya wanaoendelea. Hapo mtu aliyeanza kwa bidii yuko hatarini kwa kukwama katika kasoro kadhaa asizozitambua, hasa kwa kuishia kwenye faraja za kihisi katika sala; basi anaachishwa hizo ili kuingizwa katika njia ya Kiroho isiyotegemea hisi, ambapo katika ukavu anajaliwa mwanzo wa sala ya kumiminiwa ili asonge mbele.

Ndivyo alivyoeleza mt. Yohane wa Msalaba, “Usiku au utakaso wa Kimungu wa hisi unaipatia roho usafi wake ukiivua upande wa hisi na kuulinganisha na upande wa roho… Ni jambo la kawaida, linalowatokea wanaoanza walio wengi”. Hapo wanakuja kutambua kwamba, ili wakue katika upendo, wanapaswa kuwa maskini rohoni, kujinyima aina zote za upuuzi, majivuno, kiburi na ulafi wa roho. “Hayo makao ya hisi yanapopata kutulia hivyo, kwa maono kuratibiwa, tamaa mbaya kuzimwa, hamu kutulizwa na kulala usingizi katika usiku wa utakaso, ndipo roho inapoweza kutoroka iwajibike katika njia ya Kiroho. Inaanza kuwa miongoni mwa wanaoendelea, na kujikuta katika hatua inayoitwa ya mwanga. Ndipo Mungu anapolisha na kuimarisha roho kadiri anavyopenda kwa sala ya kumiminiwa, pasipo roho kuichangia kwa mafuatano ya maneno, kwa msaada wa utendaji au kushiriki kwake katika kazi hiyo” (walau kwa kawaida).

Mbele zaidi alieleza kasoro maalumu za wanaoendelea: ushamba wa kimaumbile, haja ya kujitokeza, kujiamini kipumbavu na kiburi cha chinichini. Hizo zinaonyesha wanavyohitaji utakaso wa Kimungu wa roho ili kuingia hatua ya waliokamilika. Jaribu hilo ni kipindi kigumu kama kile kinachotokea katika maisha ya kawaida, kijana anapoanza kutumia uhuru wake pengine kwa hasara yake mwenyewe.

Mt. Yohane wa Msalaba ametufafanulia sheria za juu za uzima wa neema zinazotimia kwa wale wanaosonga mbele kwa bidii wasigeuke nyuma. Tukisoma kwa makini maisha ya watumishi wa Mungu, tunaona katika matatizo yao utakaso huo wa kina wa hisi na wa roho ambao hatimaye ukaweka utu wao wote chini ya Mungu. Mtakatifu huyo alieleza vizuri kuliko wote vipindi hivyo viwili vigumu vya mpito kutoka hatua moja hadi nyingine, akiviita kwa haki matakaso ya Kimungu ya hisi na roho. Hayo yanalingana na maumbile ya binadamu (yenye sehemu mbili, yaani mwili na roho), tena na mfumo wa neema ya utakaso, mbegu ya uzima wa milele, inayotakiwa kuhuisha zaidi na zaidi vipawa vyote tulivyonavyo na kuangaza tendo letu lolote mpaka undani wa roho utakate umimi wowote (kujipendea kwa kujitambua au la) uwe kweli wa Mungu tu.

Kwa muhtasari ni kwamba katika wale wanaoanza, pamoja na kiwango cha kwanza cha upendo, yanaonekana maadili chipukizi yaani viwango vya kwanza vya upole, subira, usafi wa moyo na unyenyekevu. Kujishinda kwao kwa ndani na kwa nje kunazidi kuwaepusha na dhambi nyepesi za makusudi, au kunawaongoza kuinuka mara kutoka dhambi ya mauti ikiwa wameiangukia. Upande wa sala, wana sala ya midomo, kutafakari kwa mafuatano ya mawazo ambako kunaelekea kugeuka sala nyofu ya mapenzi. Ndani mwao vipaji vya Roho Mtakatifu vinaanza tu kujitokeza, bado vikifichikafichika: mara mojamoja wanapata miangaza yake ya pekee, lakini hawajawa tayari kufaidika nayo. Usikivu kwa Roho Mtakatifu unaendelea kuwa dhaifu; mtu anatambua zaidi utendaji wake mwenyewe na kulazimika mara nyingi kukiri umaskini wake katika kipindi kigumu cha ukavu wa hisi, utakaso mchungu wa Kimungu ambao unastahimiliwa vizuri au kiasi na unaashiria kuvukia hatua ya mwanga.

Katika wale wanaoendelea, pamoja na kiwango cha pili cha upendo, yanaonekana maadili imara, hasa upole, subira, unyenyekevu halisi zaidi unaoelekeza kuwa wema kwa jirani, na roho ya mashauri matatu ya Kiinjili. Pamoja na hayo, vipaji vya Roho Mtakatifu vinaanza kuonekana, hasa vile vitatu vya chini, yaani uchaji, elimu na ibada. Mtu ni msikivu zaidi, na kufaidika zaidi na mianga ya ndani. Hapo akijitahidi kweli, kwa kawaida inaanza sala ya kumiminiwa kwa tendo mojamoja la kuzama katika sala wakati wa kukusanya mawazo kwa hiari; halafu, akiwa mwaminifu, zinafuata polepole sala ya kujaliwa kukusanya mawazo, sala ya utulivu (mkavu au wenye faraja), ambapo ni wazi mchango wa kipaji cha ibada kinachotufanya tulie, “Aba! Yaani, Baba!” (Rom. 8:15; Gal. 4:6). Ndipo maongezi na nafsi yetu yanapogeuka kuwa kweli maongezi na Mungu. Hapo mtu, akijitahidi, anaona ndani mwake kasoro za kiburi kinachofichika, utovu wa wema kwa jirani, pengine ukali, utovu wa ari kwa wokovu wa watu wengi wanaopotea; kasoro hizo zote hakuziona mwanzoni, nazo zinahitaji utakaso mwingine wa Kimungu, ule wa roho.

Katika wale waliokamilika, pamoja na kiwango cha tatu cha upendo, ingawa wana kasoro kadhaa zisizo za hiari kabisa, tunashuhudia walivyo na maadili ya hali ya juu na pengine ya kishujaa: upole mkubwa, subira inayoyumbishwa kwa nadra tu, unyenyekevu mkuu usioogopa dharau bali unapenda kudhalilishwa, imani kubwa inayofanya waone mambo yote kutoka juu, tumaini kubwa kwa Mungu, moyo mkuu unaolenga mambo makuu ingawa yanaendana na vizuio na kushindwa, halafu kujiachilia kikamilifu katika matakwa ya Mungu ambayo hali yetu ya kesho na ya milele inayategemea. Roho ni kama inatawaliwa na Roho Mtakatifu anayeiongoza kutekeleza maadili kikamilifu zaidi. Vipaji vya akili na hekima vinaonekana kwa namna wazi na mara nyingi zaidi. Kwa kawaida ndipo inapojitokeza sala ya kumiminiwa ya muungano. Hatimaye undani wa roho umetakata, na vipawa vyote vya maumbile vipo moja kwa moja chini ya Mungu aliomo katika hekalu la ndani kama utangulizi wa heri isiyo na mwisho kamwe.

Tunaweza kuonyesha hayo maendeleo ya Kiroho kwa jedwali ifuatayo, ambayo isomwe kuanzia chini kwenda juu.

 

VIWANGO VYA UPENDO

MAADILI

VIPAJI

MATAKASO

SALA

MAKAO YA MT. TERESA

 

WALIOKAMILIKA

 

Hatua ya muungano

 

Maisha ya mafumbo

Maadili ya juu na ya kishujaa: kiwango cha 3° cha upendo, unyenyekevu kamili, imani kubwa, kujiachilia kwa Mungu, subira inayoyumbishwa kwa nadra tu.

Vipaji vya juu kuonekana vizuri na mara nyingi zaidi. Roho ni kama inatawaliwa na Roho Mtakatifu. Mtu anamuacha atende tu, lakini mwenyewe haachi kutekeleza maadili.

Utakaso wa Kimungu wa roho hasa chini ya kipaji cha akili (ambapo majaribu yanaongozana na vipaji vya nguvu na shauri vinajitokeza): kuingia hatua ya muungano.

Sala za kujaliwa ya muungano wa kawaida, ya muungano kamili (pengine kwa kutoka nje ya nafsi), ya muungano unaotugeuza, chini ya kipaji cha hekima kinachostawi (fadhili zinaongozana).

5°, 6° na 7°

 

WANAOENDE

LEA

 

Hatua ya mwanga

 

Kizingiti cha maisha ya sala hasa

Maadili imara: kiwango cha 2° cha upendo, utiifu, unyenyekevu mkubwa, roho ya mashauri ya Kiinjili.

Vipaji vya Roho Mtakatifu kuanza kuonekana, hasa vile vitatu vya chini (uchaji, elimu na ibada). Mtu anazidi kuwa msikivu na kufaidi mianga ya ndani.

Utakaso wa Kimungu wa hisi, hasa chini ya vipaji vya uchaji na elimu (majaribu yanaongozana): kuingia hatua ya mwanga.

Zinaanza sala za kumiminiwa: kuzama mara mojamoja katika mafumbo wakati wa kujikusanya kwa hiari; halafu sala ya kujaliwa kukusanya mawazo, na ya utulivu mkavu au wenye faraja. Kipaji cha ibada.

3° na 4°

 

WANAOANZA

 

Hatua ya utakaso

 

Maisha ya juhudi

Maadili chipukizi: kiwango cha 1° cha upendo, kiasi, usafi, subira, ngazi za kwanza za unyenyekevu.

Vipaji vya Roho Mtakatifu kufichikafichika: mianga ya mara mojamoja, ambayo mtu hajawa tayari kufaidika nayo. Anatambua hasa utendaji wake mwenyewe.

Utakaso wa hiari wa hisi na wa roho, yaani kujishinda kwa nje na kwa ndani.

Sala za kujipatia yaani za kujikusanya kwa hiari (sala ya midomo, tafakuri ya mafuatano ya mawazo, halafu sala ya mapenzi inayozidi kuwa sahili).

1° na 2°

 

 

 

 

1.16. SOMO LA KIMUNGU

 

 

Kati ya njia kuu za utakatifu zilizotolewa kwa wote, tunapaswa kuhesabu somo la Kiroho, hasa la Maandiko. Katika sura hii tutalizungumzia, tukionyesha misimamo inayohitajika ili kufaidika nalo.

 

 

MAANDIKO MATAKATIFU NA UZIMA WA ROHO

 

Mara nyingi udanganyifu, uzushi na uhuni vinatokana na maambukizo ya vitabu vibaya, kumbe “kusoma vitabu vitakatifu ni uzima wa roho” (mt. Ambrosi). Mt. Jeromu alisimulia jinsi alivyovutiwa na neema ya pekee asome kwa juhudi Maandiko matakatifu. Alipoanza kutawa, akipenda bado vitabu vya kipagani, alijiona katika ndoto yuko mbele ya Mungu na kuulizwa kwa ukali yeye ni nani. Alipojibu kuwa ni Mkristo, Hakimu mkuu akamjibu, “Mwongo wewe, u mfuasi wa Kikero; kwa sababu hazina yako ilipo, ndipo pia moyo wako ulipo”. Mara akaagiziwa apigwe mijeledi. “Nilipoamka nilitambua haikuwa ndoto tu, bali kweli, kwa sababu mabegani nilikuwa na alama za mapigo niliyoyapata. Kuanzia hapo nimesoma Maandiko matakatifu kwa bidii nyingi zaidi kuliko zile ambazo kwanza nilikuwa nikisoma vitabu visivyo vya dini”. Kutokana na hayo tunaelewa aliyomuandikia Eustoki: “Usingizi ukukute tu ukisoma, tena angalia sana usipatwe na usingizi juu ya kitabu tofauti na Maandiko matakatifu”.

Katika kitabu gani tutaweza kuchota uzima kuliko katika kile kilichoandikwa na Mungu? Hasa Injili, maneno ya Mwokozi na matukio ya maisha yake yanatakiwa kuwa fundisho hai ambalo tulizingatie daima. Yesu alijua namna ya kufanya mambo makuu yaeleweke kwa wote kutokana na unyofu alioutumia. Tena neno lake halibaki nadharia tu, bali linaongoza mara kwenye unyenyekevu halisi, upendo wa Mungu na wa jirani. Katika kila neno tunahisi kuwa hatafuti chochote isipokuwa utukufu wa Baba aliyemtuma na wokovu wa watu. Turudie daima hotuba ya mlimani (Math. 5-7) na maneno yaliyofuata karamu ya mwisho (Yoh. 13-17).

Tukiyasoma maneno hayo ya Kimungu kwa unyenyekevu, imani na upendo, tunakuta ndani yake neema ya pekee inayotuongoza kuiga kila siku vizuri zaidi maadili ya Mwokozi: upole wake, subira yake na upendo wake wa kishujaa kwa msalaba. Pamoja na ekaristi, ndiyo lishe halisi ya watakatifu: Neno la Mungu tuliloletewa na Mwanae pekee, Neno aliyefanyika mwili. Chini ya maneno yake limefichika wazo hai la Mungu, ambalo vipaji vya akili na hekima vinatuwezesha kulichimba na kulionja zaidi na zaidi tukiwa wasikivu.

Baada ya Injili hakuna kinachotulisha vizuri kuliko Matendo ya Mitume na Nyaraka zao. Ndiyo mafundisho ya Mwokozi yaliyotekelezwa na wafuasi wake wa kwanza, walioagizwa kutulea katika shule yake; ni mafundisho yaliyofafanuliwa kulingana na mahitaji ya waamini. Maisha ya kishujaa ya Kanisa la mwanzoni, uenezi wake kati ya matatizo makubwa, yale yote yanayoelezwa na Matendo ya Mitume ni fundisho la kumtumainia Mungu na kujiaminisha kwake. Tutaona wapi kurasa zenye undani na uhai kuliko zile za Nyaraka kuhusu nafsi na kazi za Kristo (taz. Kol. 1), uangavu wa maisha ya Kanisa na ukuu wa upendo wa Mwokozi kwake (taz. Ef. 1-3), kujaliwa uadilifu kwa njia ya kumuamini Kristo (taz. Rom. 1-11), ukuhani wa milele wa Yesu (taz. Eb. 1-9)? Halafu tukizingatia sehemu za maadili za Nyaraka, tutaona wapi mahimizo ya nguvu zaidi kwa ajili ya upendo, uwajibikaji, udumifu, subira, utakatifu, pamoja na kanuni za mwenendo kuhusu wowote – wakubwa, watu wa hali moja, wadogo – na kuhusu watu dhaifu, wakosefu, walimu wa uongo? Tutaona wapi maelezo hai zaidi kuhusu wajibu wa Wakristo wote kwa Kanisa?

Katika Agano la Kale kila Mkristo anapaswa kujua hasa Zaburi, ambazo zinadumu kuwa sala ya Kanisa.

Tukirudia kusoma mfululizo, kwa heshima na upendo, Maandiko matakatifu, tutakuta ndani yake mwanga na nguvu mpya daima. Mungu amelitia neno lake uweza usioisha, nasi tukisha kusoma vitabu vingi na kuvikinai karibu vyote, hatimaye tutairudia Injili kama utangulizi wa mwanga wa milele.

 

 

MAANDISHI YA WATAKATIFU

 

Baada ya Biblia, vitabu vya Kiroho vya watakatifu ndivyo vinavyotuangaza na kutuwasha zaidi. Ingawa havikuandikwa kwa uvuvio ule usioweza kukosea, hata hivyo vimeandikwa kwa mwanga na mpako wa Roho Mtakatifu.

Haifai kutojua vitabu bora vya watakatifu Augustino, Jeromu, Yohane Kasiano, Leo Mkuu, Benedikto, Gregori Mkuu, Bazili na Yohane Krisostomo, halafu Dyonisi na mt. Masimo Muungamadini.

Inafaa kujua yanayohusu maisha ya Kiroho katika maandishi ya watakatifu Anselmi na Bernardo, Richard wa mt. Viktori, watakatifu Alberto Mkuu, Thoma wa Akwino, Bonaventura, mh. Anjela wa Foligno Yohane Thauler, mh. Henri Suso, mt. Katerina wa Siena, Yohane Ruysbroeck, pamoja na Thomas wa Kempis anayedhaniwa kuwa mwandishi wa Kumfuasa Yesu Kristo.

Kati ya waandishi wa karne zilizofuata, inafaa kusoma vitabu vya Fransisko wa Osuna, mt. Inyasi wa Loyola, Luis wa Blois, watakatifu Teresa wa Yesu na Yohane wa Msalaba, Luis wa Granada, mt. Fransisko wa Sales, Luis Lallemant, Yohane Olier, watakatifu Visenti wa Paulo na Yohane Eudes, Yakobo B. Bossuet, mt. Luis Maria Grignion de Montfort, Petro Caussade, na mt. Alfonsi Maria wa Liguori.

Hatuwataji waandishi wa karne za mwishomwisho, ambao walio muhimu zaidi wanajulikana na wote, hasa mt. Teresa wa Mtoto Yesu.

 

 

MAISHA YA WATAKATIFU

 

Tunapaswa kuongeza juu ya usomaji wa maisha ya watakatifu, ambayo daima yanavutia na mara nyingi yanawezekana kuigwa. Vitabu vya namna hiyo vinatueleza walivyotenda, katika nafasi pengine ngumu, wanaume na wanawake wenye maumbile sawa na ya kwetu, ambao mwanzoni walikuwa na kasoro na udhaifu sawa nasi, lakini polepole neema na upendo vikaja kushinda maumbile kwa kuyaponya, kuyainua na kuyatia uzima mpya. Hasa ndani mwao tunaweza kuona maana halisi na uzito wote wa neno hili: “Neema haiangamizi maumbile (katika mema yaliyonayo), bali inayakamilisha”. Katika watakatifu, hasa kwenye hatua ya muungano, maumbile na neema vinalingana kweli.

Katika maisha yao tunapaswa kuyazingatia hasa yanayoweza kuigwa. Katika yaliyo ya pekee tuone tu ishara ya Kimungu tuliyopewa ili tutoke usingizini na kuzingatia yaliyo ya ndani na ya juu zaidi katika maisha ya Kikristo ya kawaida. Kwa mfano, mateso ya wenye madonda ya Yesu yanatukumbusha Mateso ya Mwokozi yanapaswa kuwa nini kwetu na jinsi tunavyotakiwa kusema vizuri zaidi kwenye Njia ya Msalaba, “Mama mtakatifu, fanya hivi, choma kabisa moyoni mwangu madonda ya Msulubiwa”. Neema ya pekee iliyowajalia watakatifu kadhaa kunywea katika donda la Moyo wa Yesu inatukumbusha kila Komunyo inavyopaswa kuwa motomoto na bora kuliko ile iliyotangulia. Mifano ya watakatifu kuhusu unyenyekevu, subira, tumaini, upendo usiokoma, inatuvuta kuliko mafundisho ya kinadharia tutekeleze maadili: “Mawazo hayasukumi”.

Inafaa zaidi kusoma maisha ya watakatifu yaliyoandikwa na watakatifu, kama vile yale ya mt. Fransisko wa Asizi yaliyoandikwa na mt. Bonaventura; yale ya mt. Katerina wa Siena yaliyoandikwa na kiongozi wake, mh. Raimundi wa Capua; na yale ya akina mt. Teresa yaliyoandikwa na wao wenyewe.

 

 

MISIMAMO INAYOHITAJIKA ILI KUFAIDIKA NA MASOMO HAYO

 

Sala iliyofanywa vizuri mwanzoni inatupatia neema ya msaada ya kusoma kwa imani, tukikwepa udadisi wowote usio na faida, majivuno ya akili, elekeo la kuhukumu tunayoyasoma badala ya kufaidika nayo. Imani inatuelekeza kumtafuta Mungu mwenyewe katika maandishi ya Kiroho.

Badala ya kuridhika na ujuzi peke yake, tunapaswa kuona namna ya kutekeleza wenyewe, tukiwa na hamu hai tena nyofu ya ukamilifu. Hapo, hata tukisoma yanayohusu “maadili madogomadogo” (mt. Fransisko wa Sales) tunapata faida kubwa, kwa kuwa yote yanahusiana na adili kuu la upendo. Waliosonga mbele katika njia ya ukamilifu, pengine inawafaa warudie kusoma yale yanayowafaa wanaoanza; wataona yote kwa mwanga wa juu zaidi na kushangaa yaliyofichika ndani yake; k.mf. katika mistari ya kwanza ya katekisimu ndogo inayohusu malengo ya sisi kuwepo duniani: “kumjua, kumpenda na kumtumikia Mungu ili kupata uzima wa milele”.

Vilevile inafaa wanaoanza wachungulie ukuu wa ukamilifu wa Kikristo, mradi wasidai kuruka juu kabla hawajapewa neema. Kwa kuwa lengo la kulifikia ni la mwisho katika hatua za utendaji, lakini ni la kwanza katika nia au hamu: toka mwanzo ni lazima tutake kufikia utakatifu ule unaotuwezesha kuingia mbinguni mara baada ya kufa. Hakika, toharani hakuna asiyetenda makosa aliyoweza kuyaepa.

Ikiwa wanaoanza na wanaoendelea wana hamu kubwa ya utakatifu, watakuta katika Maandiko matakatifu na katika vitabu vya watakatifu yale yanayowafaa na watafundishwa na mlezi wa ndani. Lakini ni lazima kusoma polepole, si kumeza vitabu, bali kupenyezwa na yale tunayoyasoma. Hapo masomo ya Kiroho yanageuka kuwa sala. Kwa mt. Benedikto kusoma ni kidato cha kwanza katika ngazi ifuatayo ya kupanda juu: “Lectio (kusoma), cogitatio (kufikiri), studium (kuzingatia), meditatio (kutafakari), (oratio = kusali), contemplatio (kutazama)”.

Inafaa pia turudie kusoma baada ya miaka vitabu bora vilivyokwishatusaidia. Maisha ni mafupi: turidhike kusoma na kurudia kusoma yale ambayo kweli yana mhuri wa Mungu, bila ya kupoteza muda katika masomo yasiyo na uhai wala thamani. Ni afadhali kuchimba kitabu bora kimojawapo kuliko kusoma kijuujuu vile vyote vya waandishi wa Kiroho.

Halafu tunatakiwa kusoma kwa roho ya ibada, “kwa kutafuta sio ujuzi tu, bali ladha hasa” ya mambo ya Mungu (mt. Bernardo). “Asomaye na afahamu” (Math. 24:15), akimuomba Mungu mwanga ili aelewe vema. Wanafunzi wa Emau walikuwa hawajaelewa matabiri ya manabii mpaka Bwana alipowafungua akili zao. Ndiyo sababu mt. Bernardo alisema, “Sala ikatishe somo”: hapo tu litakuwa lishe ya roho na kuelekeza kusali.

Hatimaye ni lazima tuanze mara kutekeleza tunayoyasoma: “Kila asikiaye maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba… Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga” (Math. 7:24,26). “Kwa sababu sio wale waisikiao sheria walio wenye haki mbele za Mungu, bali ni wale waitendao sheria watakaohesabiwa haki” (Rom. 2:13). “Iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu” (Yak. 1:22).

Hapo somo linazaa matunda mema: “Nyingine zilianguka penye udongo mzuri; zikamea, zikazaa moja kwa mia… ndio wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia neno, na kulishika; kisha huzaa matunda kwa kuvumilia” (Lk. 8:8,15). Ndivyo lilivyokuwa somo alilolifanya mt. Augustino aliposikia maneno haya: “Chukua na kusoma”; akafungua Nyaraka zilizokuwa mezani, akasoma: “Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu. Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo” (Rom. 13:13-14). Kuanzia hapo akaongoka, akajitenga faraghani kwa muda fulani, akajiandikisha kwa ubatizo, matunda yakawa kweli mara mia, nayo yakawafaidisha wengi hadi leo.

 

 

 

 

1.17. UONGOZI WA KIROHO

 

 

Kati ya misaada ya nje kwa utakatifu unatakiwa kuhesabiwa uongozi wa Kiroho. Kwanza tutaongea juu ya haja yake kwa jumla na kwa hatua mbalimbali za maisha ya Kiroho; halafu juu ya sifa ambazo kiongozi awe nazo, na juu ya wajibu wa yule anayeongozwa.

 

 

HAJA YA UONGOZI KWA JUMLA

 

Ingawa uongozi si wa lazima kwa utakatifu, ni njia ya kawaida ya maendeleo ya Kiroho. Bwana alipounda Kanisa lake alitaka waamini wawe chini ya papa na maaskofu upande wa nje, na chini ya waungamishi upande wa ndani, hao wakiwaelekeza njia za kutoanguka tena dhambini na za kusonga mbele katika maadili. Mt. Paulo alipoongoka, Yesu hakumfunulia mwenyewe mipango yake, bali alimtuma Damasko kwa Anania, ajue kwa njia yake yatakayompasa kuyafanya (taz. Mdo. 9:6).

“Fanya bidii sana na uangalifu mkubwa kabisa ili kumpata mtu ambaye aweze kukuongoza kwa hakika katika kazi uliyokusudia ya kuishi kitakatifu; umchague mtu anayeweza kuwaelekeza wenye mapenzi mema njia nyofu ya kumuendea Mungu… Ni kiburi kabisa kudhani huna haja na mashauri” (mt. Bazili).

“Usijifanye mwalimu wako mwenyewe, la sivyo utapotea haraka sana” (mt. Jeromu)

“Kama vile kipofu asivyoweza kushika njia nyofu asipoongozwa na mtu, hakuna anayeweza kutembea bila ya kiongozi” (mt. Augustino)

Kasiani alifundisha kwamba anayetegemea akili yake hatafikia kamwe ukamilifu wala hataweza kukwepa hila za Ibilisi; njia bora ya kushinda vishawishi vya hatari ni kuvifunua kwa kiongozi mwenye busara na neema ya kutuangazia. Kweli, mara nyingi inatosha kuvifunua kwa anayehusika ili viishe.

“Anayejifanya kiongozi wake mwenyewe anajifanya mwanafunzi wa mpumbavu… Upande wangu natamka kuwa kwangu ni rahisi zaidi na ya hakika zaidi kuwaagiza wengi kuliko kujiongoza mimi tu” (mt. Bernardo). Katika kuwaongoza wengine umimi wetu unatudanganya kidogo kuliko katika kujiongoza; na kama tungejua namna ya kutekeleza wenyewe yale tunayowaambia wengine, maendeleo yetu yangekuwa makubwa.

“Bwana wetu, ambaye pasipo yeye hatuwezi kitu, hatamjalia kamwe neema yake mtu ambaye, ingawa anaye mtu mwenye uwezo wa kumfundisha na kumuongoza, anapuuzia chombo hicho muhimu cha utakatifu, akidhani anajitosheleza na kuweza kwa nguvu zake kutafuta na kuona yanayofaa kwa wokovu wa milele… Aliye na kiongozi ambaye anamtii katika yote na kikamilifu, atalifikia lengo lake kwa urahisi na haraka sana kuliko kama akifanya peke yake, hata kama ana akili sana na vitabu vyenye hekima kuhusu mambo ya Kiroho… Kwa jumla, wale wote waliofikia ukamilifu wamefuata njia ya utiifu, isipokuwa kama kwa fadhili au neema ya pekee Mungu alimfundisha mwenyewe mtu mmojammoja asiyekuwa na wa kumuongoza” (mt. Visenti Ferrer).

Mt. Fransisko wa Sales alionyesha kuwa hatuwezi kuamua kwa haki katika kesi zetu wenyewe, kutokana na aina ya kujipendea “ya siri na isiyotambulikana ambayo tusipoona vizuri hatuwezi kuivumbua; na wale wenyewe waliopatwa nayo hawaijui wasipoonyeshwa”. Aliyekaa muda mrefu katika chumba ambacho milango na madirisha yake yamefungwa hatambui kuwa humo hewa imekuwa chafu kwa njia ya kupumua, kumbe anayeingia anatambua mara. Sisi sote tunakubali kwamba kiongozi anahitajika ili kupanda mlima mrefu; bila ya shaka anahitajika zaidi ili kupanda hadi kilele cha ukamilifu, hasa kwa sababu tunapaswa kukwepa hila za yule asiyetaka tupande.

Mt. Alfonsi aliorodhesha uongozi unahusika na nini zaidi: malipizi, namna ya kupokea sakramenti, sala, utekelezaji wa maadili na namna ya kutenda kitakatifu kazi za kila siku.

Shuhuda hizo zote na nyinginezo zinaonyesha wazi haja ya uongozi kwa jumla. Tutaelewa zaidi kwa kuzingatia hatua tatu za maisha ya Kiroho, yaani mahitaji ya wanaoanza, wanaoendelea na waliokamilika.

 

 

UONGOZI WA WANAOANZA

 

Uongozi wenye busara, imara na moyo wa kibaba unahitajiwa hasa na wanaoanza, kama unavyofanywa na walezi utawani. Baadaye haja hiyo haisikiki tena vile, isipokuwa katika vipindi vigumu yanapotokea mabadiliko na unapotakiwa uamuzi muhimu.

Wanaoanza wanahitaji kukingwa dhidi ya marudio ya makosa na dhidi ya kasoro mbili zinazopingana. Baadhi wakipokea faraja za kihisi katika sala wanazichanganya na neema za juu, na kwa kiburi wangetaka kuruka mara moja hadi kufikia muungano bila ya kupitia hatua za lazima. Hao wanahitaji kukumbushwa haja ya unyenyekevu na kusadikishwa kuwa safari ya ukamilifu ni kazi ya maisha yote: haiwezekani kuruka bila ya mabawa, na katika kujenga tunaanza na misingi. Lengo tuliloliona ni la kwanza kutamaniwa na kukusudiwa, lakini ni la mwisho kufikiwa; tena haifai kupuuzia njia duni ambazo ni za lazima ili kulifikia. Baadhi wana kiburi cha siri katika kushika maisha magumu na kujitosa mno katika malipizi hadi kuharibu afya. Baadaye, wakitaka kujitibu wanalegea na kwenda kinyume cha mara ya kwanza. Hao wanahitaji kujifunza kiasi cha Kikristo na kwamba haitoshi kuwa na maadili ya Kimungu pasipo maadili ya kibinadamu ili kutawala polepole hisi.

Uongozi unakuwa wa lazima hasa katika kipindi kirefu cha ukavu ambapo kutafakari ni kwa shida tena kuna vishawishi vikali pamoja na upinzani wa watu. Tutakavyoeleza, jaribu hilo linavusha kutoka hatua ya utakaso kwenda hatua ya mwanga mradi ziwepo dalili tatu ambazo kiongozi anatakiwa kuzitambua: 1) kutofurahia mambo ya Mungu wala ya dunia; 2) hata hivyo, kuendelea kwa kawaida kumkumbuka Mungu, kutamani ukamilifu na kuogopa kutomtumikia; 3) kushindwa kutafakari kwa mpangilio na badala yake kuvutiwa na tendo la kumtazama tu Mungu.

Katika kipindi hicho kigumu, kinachotakiwa kuwa kama wongofu wa pili, ni lazima kumsikiliza kiongozi wa kufaa ili kusonga mbele kwa bidii badala ya kubaki nyuma kama mchelewaji.

 

 

UONGOZI WA WANAOENDELEA NA WA WALIOKAMILIKA

 

Kwa kawaida uongozi wa wanaoendelea unaweza kufanyika haraka zaidi, kwa sababu anayeongozwa ameshajua zaidi maisha ya Kiroho na mara nyingi anaweza kueleza kwa neno moja anahitaji shauri kuhusu nini. Hapo kiongozi anakuwa kama shahidi wa maendeleo yake; anatakiwa kutambua kazi ya mlezi wa ndani ili awe chombo chake na kuhakikisha usikivu wa mtu kwa mianga ya Roho Mtakatifu, akipambanua ndani yake pumba na mchele, yaani kilema kikuu ambacho apambane nacho, na mvutio maalumu wa neema ambao aufuate.

Inafaa tumkimbilie kiongozi hasa wakati wa mazoezi ya Kiroho ya kila mwaka ili kumueleza kwa unyofu wote undani wa roho tusije tukajidanganya tu kwa kuangukia kiburi kilichofichika na kujiamini kipumbavu.

Kwa wanaoendelea pia kuna vipindi vigumu vinavyohitaji uongozi bora, kwa namna ya pekee wanapotakiwa kuvukia hatua ya muungano. Namna za majaribu hayo zinaweza kuwa mbalimbali, lakini kwa kawaida ni kunyimwa kwa muda mrefu faraja si za kihisi tu, bali za roho pia. Hapo vinatokea mara nyingi vishawishi dhidi ya imani, tumaini na upendo na unahitajika kwa namna ya pekee msaada wa kiongozi mwenye mwanga na mang’amuzi. Hata mtu anayeweza kuongoza wengine katika hatua hiyo hawezi kujiongoza kwa sababu “hakuna tena mapito tayari” (mt. Yohane wa Msalaba), hivyo anapaswa tu kufuata mwanga wa Roho Mtakatifu asiuchanganye na msukumo mwingine unaoweza kufanana nao.

Waliokamilika pia wanajisikia haja ya msaada huo ili kuona namna ya kulinganisha msimamo wa kujiachilia mikononi mwa Mungu na utendaji ambao Bwana anawadai, ili kutekeleza vizuri msemo huu: “kushika uaminifu na kujiachilia”. Wanajisikia haja ya kuongozwa ili kudumisha hai moyoni mwao upendo kwa msalaba pamoja na unyenyekevu mkubwa. Basi, ikiwa hao wanahitaji uongozi, zaidi tena wanauhitaji wanaoanza.

 

 

SIFA ZA KIONGOZI NA WAJIBU WA ANAYEONGOZWA

 

Kiongozi “anatakiwa kuwa amejaa upendo, elimu na busara: likikosekana mojawapo kati ya hayo matatu, kuna hatari” (mt. Fransisko wa Sales). “Ni muhimu sana kwamba kiongozi awe na mwanga: yaani awe na busara na mang’amuzi sana. Ikiwa zaidi ya hayo ni mwanateolojia pia, basi ni kamili. Lakini isipowezekana kumuona mtu mwenye sifa hizo tatu pamoja, ni afadhali awe na zile mbili za kwanza, kwa sababu katika shida kuna uwezekano wa kupata shauri la wasomi. Nionavyo mimi, hao wa mwisho, wasipojitahidi katika sala, hawafai sana kwa wanaoanza; lakini sitaki kushauri wasiwe na uhusiano nao… Elimu ni jambo kubwa… Mungu atuepushe na ibada za kijuujuu na zilizojaa upuuzi” (mt. Teresa wa Yesu).

Upendo wa kiongozi unapaswa kumfanya asijitafutie faida na aongoze mioyo kwa Mungu, si kwake mwenyewe. Y. Thauler alisema viongozi wanaojivutia watu ni kama mbwa ambao katika uwindaji wanamla mnyama badala ya kumleta kwa bwana wao; hapo huyo anawapiga kweli.