HATUA TATU ZA MAISHA YA KIROHO

Karama Historia Maisha na utendaji Katiba Safari ya Malezi Maktaba Pepe

 

 

 

 

 

R. GARRIGOU-LAGRANGE, O.P.

 

 

HATUA TATU ZA MAISHA YA KIROHO

 

UTANGULIZI WA UZIMA WA MBINGUNI

 

(tafsiri fupi)

 

 

 

 

YALIYOMO

 

0. UTANGULIZI

 

1. CHEMCHEMI NA LENGO LA MAISHA YA KIROHO

1.1. Uzima wa neema, mwanzo wa uzima wa milele

1.2. Maisha ya Kiroho na maongezi ya ndani na Mungu

1.3. Muundo wa Kiroho

1.3.1. Maisha ya kimaumbile na yanayopita maumbile

1.3.2. Maadili ya Kimungu

1.3.3. Maadili ya kibinadamu

1.3.4. Vipaji saba vya Roho Mtakatifu

1.3.5. Neema za msaada na aina zake

1.4. Uwemo wa Utatu mtakatifu ndani mwetu kama chemchemi isiyoumbwa ya maisha ya Kiroho

1.5. Kristo mkombozi anavyoathiri mwili wake wa fumbo

1.6. Msaada wa mama Maria

1.7. Ustawi wa uzima wa neema kwa njia ya stahili, sala na sakramenti

1.8. Ukamilifu wa Kikristo ni nini hasa?

1.9. Ukuu wa ukamilifu wa Kikristo na heri nane

1.10. Ukamilifu na ushujaa

1.11. Ukamilifu wa Kikristo na matakaso ya Kimungu

1.12. Ukamilifu na amri ya kumpenda Mungu

1.13. Ukamilifu na mashauri ya Kiinjili

1.14. Wajibu wa pekee wa mapadri na watawa wa kulenga ukamilifu

1.15. Hatua tatu za maisha ya Kiroho kadiri ya mababu na walimu wakuu

1.16. Somo la Kimungu

1.17. Uongozi wa Kiroho

 

2. UTAKASO WA WANAOANZA

2.1. Hatua ya Kiroho ya wanaoanza

2.2. Fikra za kidunia na ufishaji kadiri ya Injili

2.3. Ufishaji kadiri ya mtume Paulo na sababu zinazofanya uwe wa lazima

2.4. Dhambi ambazo tuziepe: mizizi yake na matokeo yake

2.5. Kilema tawala, mdudu anayekula ndani kwa ndani

2.6. Maono ya kuratibiwa

2.7. Kujitakasa upande wa hisi

2.8. Kujitakasa upande wa ubunifu na kumbukumbu

2.9. Kujitakasa upande wa akili

2.10. Kujitakasa upande wa utashi

2.11. Kupona kiburi

2.12. Kupona uvivu wa roho

2.13. Sakramenti ya kitubio

2.14. Kushiriki misa, chemchemi ya utakatifu

2.15. Komunyo takatifu

2.16. Sala ya kuomba

2.17. Sala ya Kanisa

2.18. Sala ya moyo ya wanaoanza inavyozidi kuwa sahili

2.19. Kufikia maisha ya sala na kudumu ndani yake

2.20. Wachelewaji

 

3. MWANGA WA WANAOENDELEA

3.1. Lugha ya walimu wa Kiroho ikilinganishwa na ile ya wanateolojia

3.2. Kuingia hatua ya mwanga

3.3. Wongofu wa pili kadiri ya walimu wengine

3.4. Kutakaswa upande wa hisi na kuingia hatua ya mwanga

3.5. Tufanye nini katika usiku wa hisi

3.6. Sifa kuu za hatua ya wanaoendelea

3.7. Jengo la Kiroho la wanaoendelea

3.8. Busara na maisha ya Kiroho

3.9. Haki, aina zake na kuunda utashi

3.10. Subira na upole

3.11. Usafi wa moyo, thamani na matunda yake

3.12. Unyenyekevu wa wanaoendelea

3.13. Unyenyekevu wa Neno aliyefanyika mwili na ule wa kwetu unavyotakiwa kuwa

3.14. Roho ya ufukara

3.15. Ukuu wa utiifu

3.16. Usahili na unyofu

3.17. Roho ya imani na ustawi wake

3.18. Tumaini kwa Mungu na hakika yake

3.19. Upendo wa kulingana na matakwa ya Mungu

3.20. Upendo wa kidugu, mng'ao wa upendo wa Mungu

3.21. Ari kwa utukufu wa Mungu na kwa wokovu wa watu

3.22. Usikivu kwa Roho Mtakatifu

3.23. Upambanuzi wa roho

3.24. Sadaka ya misa na wanaoendelea

3.25. Komunyo ya wanaoendelea

3.26. Ibada ya wanaoendelea kwa bikira Maria

3.27. Kitabu cha "Kumfuasa Yesu Kristo" kinawaelekeza wote njia ya mafumbo

3.28. Sala ya kumiminiwa

3.29. Uzushi wa Watulivu kuhusu sala ya kumiminiwa na kuhusu upendo safi

3.30. Ngazi za sala ya kumiminiwa kwa wanaoendelea

3.31. Maswala kuhusu sala ya kumiminiwa

3.32. Yaliyo mapya katika sala ya kumiminiwa

3.33. Ulinganifu na tofauti kati ya watakatifu Teresa wa Yesu na Yohane wa Msalaba

 

4. MUUNGANO WA WALIOKAMILIKA

4.1. Kuingia hatua ya muungano kupitia usiku wa roho

4.1.1. Haja ya kutakaswa roho na utangulizi wa hatua ya muungano

4.1.2. Ufafanuzi wa utakaso wa Kimungu wa roho

4.1.3. Kinachosababisha roho kutakaswa

4.1.4. Giza la mwanga mkali

4.1.5. Miongozo kwa usiku wa roho

4.1.6. Matokeo ya roho kutakaswa hasa upande wa maadili ya Kimungu

4.1.7. Hatua ya waliokamilika: muungano wao na Mungu

4.1.8. Aina mojawapo ya maisha makamilifu: njia ya utoto wa Kiroho

4.2. Ushujaa wa maadili

4.2.1. Ushujaa wa maadili kwa jumla

4.2.2. Imani ya kishujaa inayozama katika mafumbo

4.2.3. Tumaini la kishujaa na kujiachilia kwa Mungu

4.2.4. Upendo wa kishujaa

4.2.5. Ushujaa wa maadili ya kibinadamu

4.2.6. Upendo kwa Yesu msulubiwa na kwa Maria katika hatua ya muungano

4.3. Namna na ngazi za hatua ya muungano

4.3.1. Maisha kamili ya kitume na sala ya kumiminiwa

4.3.2. Maisha ya malipizi

4.3.3. Roho Mtakatifu anavyomuathiri aliyekamilika

4.3.4. Muungano mkavu na muungano wa kutoka nje ya nafsi

4.3.5. Muungano unaotugeuza, utangulizi wa ule wa mbinguni

 

5. NEEMA ZA PEKEE

5.1. Karama

5.2. Mafunuo na njozi

5.3. Maneno na miguso ya Kimungu

5.4. Madonda matakatifu na kudanganyika

5.5. Tofauti kati ya matukio hayo ya Kimungu na yale yatokanayo na ugonjwa

5.6. Matukio ya Kishetani

 

6. HATIMA

 

 

 

 

0. UTANGULIZI

 

0.1.        KITU KILICHO MUHIMU PEKE YAKE

 

Mtu akiacha kuongea na wenzake, mara anaanza kuwaza yanayomvutia zaidi. Mawazo hayo yanatofautiana hasa kadiri ya umri na uadilifu wa watu. Kwa mtu anayelenga ukweli na wema yanaelekea kugeuka maongezi na Mungu, naye mwenyewe, badala ya kujipendea katika yote (yaani kujifanya lengo la yote, ajue asijue) anamlenga Mungu katika kila jambo pamoja na kumpenda na kuwapenda watu kwa ajili yake. Ndiyo maisha ya Kiroho.

Ni jambo bora na la lazima kuliko elimu, sanaa, fasihi, siasa na mengineyo: wale wasio na maisha ya Kiroho wakijihusisha na mambo hayo wanaonekana kutafuta humo ukweli na wema, lakini utafiti wao unaathiriwa na umimi kiasi kwamba tunapaswa kujiuliza kama utazaa matunda kwa uzima wa milele. Wengi wao hawainuki juu ya utendaji wa kibinadamu tu na wa njenje, wala hawaishi kwa jambo lililo bora kuliko wao, yaani kwa Mungu.

Maisha ya Kiroho, yaani kuishi na Mungu, ndiyo kitu pekee cha lazima kwa sababu kwa njia yake tu tunaelekea lengo letu kuu. Tusiutenganishe wokovu na safari ya utakatifu iliyo njia ya wokovu. Mbinguni kutakuwa na watakatifu tu, wawe wameingia mara baada ya kufa, au wawe wamehitaji kutakaswa toharani. Hakuna anayeingia mbinguni akiwa na doa lolote. Ili aweze kufurahia daima uso wa Mungu, yaani kumjua na kumpenda kama mwenyewe anavyojijua na kujipenda, ni lazima hatia yoyote hata ndogo iwe imefutwa, na adhabu iliyostahili iwe imetimizwa au kuondolewa.

“Atafaidiwa nini mtu akiupata ulimwengu wote, na kupata hasara ya nafsi yake? Au mtu atatoa nini badala ya nafsi yake?” (Math. 16:26). Ikiwa tuko tayari kupoteza vitu vingi ili kuokoa mwili, ambao kwa vyovyote utakuja kufa, kwa nini tusiwe tayari kupoteza vyote ili kuokoa roho inayotakiwa kuishi milele? Je, binadamu hapaswi kupenda roho kuliko mwili wake?

 

0.2.        SWALA LA MAISHA YA KIROHO SIKU HIZI

 

Hayo tuliyoyasema ni ya kweli nyakati zote, lakini siku hizi yanahitaji kufikiriwa zaidi, kwa sababu hakuna utulivu: wengi wamejitenga na Mungu, wakijitahidi kupanga mbali naye maisha ya binafsi na ya jamii. Matatizo makuu yaliyowapata daima binadamu yamepata sura mpya ya kutisha. Kwa kuwa Mungu ni mwanzo na mwisho wa yote, mtu akitaka kutenda bila yake anajikuta vilindini mwa unyonge mbaya kuliko utovu wa vyote. Hatimaye analazimika kutambua kuwa yote yanadai azingatie sana swala la dini.

Mtu asipotaka kutimiza wajibu wake kwa Mungu, aliye muumba na lengo lake kuu, anajikuta akiabudu vingine, k.mf. sayansi au haki ya kijamii au kipeo chochote cha kibinadamu, kwa kuwa hawezi kuishi bila ya dini. Hivyo anasogea mbali na aliye Mkuu kabisa na kukabiliana na rundo la maswala ambayo, atake asitake, hayana jibu lolote asiporudia swala la msingi la fungamano na Mungu.

Siku hizi bingwa anaabudu taratibu za sayansi na kuzijali kuliko ukweli wenyewe. Angefanya bidii hizohizo katika maisha ya Kiroho, angefikia mapema utakatifu. Kumbe hiyo ibada ya sayansi lengo lake ni utukufu wa mtu badala ya upendo wa Mungu. Vilevile siasa mara nyingi inajidanganya kuboresha maisha ya binadamu kwa kukataa haki za Mungu.

 

Msingi wa maswala yoyote ni swala la dini: hatuwezi kulipuuzia wala kuepa kusimama ama upande wa Mungu ama dhidi yake. Historia ya karne ya 20 imetuonyesha hilo waziwazi.

Mtu akitaka kuishi bila ya Mungu, uzito wa maisha unasogezwa kutoka upande wa dini kwenda upande mwingine. Lakini baada ya muda analazimika kutambua kuwa yote yamevurugika.

Mali haiwezi kuwa yote ya wengi kwa wakati mmoja: ndiyo sababu ya mashindano kati ya watu na kati ya mataifa, lengo kuu likiwekwa katika mali. Kumbe mema ya Kiroho yanaweza kuwa yote ya wote kwa wakati mmoja: tunaweza kuwa na ukweli uleule, uadilifu uleule na Mungu yuleyule bila ya kunyang'anyana.

Bwana ametuambia: “Utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake, na hayo yote mtazidishiwa” (Math. 6:33). Kukataa fundisho hilo ni kujitakia maangamizi: "Bwana asipoijenga nyumba waijengao wafanya kazi bure. Bwana asipoulinda mji yeye aulindaye akesha bure" (Zab. 127:1).

 

Mtu akijali sayansi au siasa kuliko dini, na akijitafutia utukufu badala ya kumtafutia Mungu, maisha yatamfundisha mapema kuwa ameshika njia isiyofika mahali. "Mtu asiye pamoja nami yu kinyume changu, na mtu asiyekusanya pamoja nami hutapanya" (Math. 12:30).

Lakini dini haiwezi kuwa jibu halisi la maswala makuu ya leo isiposhikwa kwa dhati. Maisha ya Kiroho yanatakiwa kuwa kweli muungano na Mungu ili dini idumu kuwa juu ya sayansi na siasa.

 

0.3.        LENGO LA MAANDISHI HAYA

 

Lengo ni kuwaalika watu kwenye muungano na Mungu, wakiepa hatari mbili.

Ya kwanza ni kwamba leo kutofautisha fani kumezidi hata kufanya wengi wakose mitazamo mipana inayohitajika ili kupima kwa busara mambo yoyote katika uhusiano na mengine. Basi, katika maisha ya Kiroho pia kuzingatia madogomadogo kusitusahaulishe jumla ya yote, la sivyo tutasogea mbali na hekima ya Kikristo.

Ya pili ni kwamba vitabu vingi vya dini na vya ibada vinakosa msingi imara katika imani na kurahisisha mno mafundisho ya Kiroho.

 

0.4.        SHABAHA YA FANI HII

 

Maisha ya Kiroho ni tawi la teolojia linalohusika na utekelezaji wake katika kuongoza watu waungane kwa dhati na Mungu likifafanua muungano huo ni nini na njia za kuufikia ni zipi. Hivyo linafafanua taratibu za uzima wa neema kwa misingi ya teolojia likiilinganisha na mang'amuzi ya watakatifu.

Maisha ya Kiroho yanahitaji kuchambua mang'amuzi hayo kitaalamu, kwa kubainisha taratibu zake kadiri ya saikolojia (k.mf. ukavu unaotakasa unavyohusiana na muungano na Mungu). Somo hilo linakuwa la kiteolojia uchambuzi wa taratibu hizo unapotegemea pia mafundisho ya imani. Ikiwa elimunafsia ni ya lazima kwa maadilidini, ni ya lazima zaidi kwa maisha ya Kiroho ambayo yanachunguza hatua zake ndani ya mtu hadi muungano kamili.

Katika ngazi ya chini, maadilidini yanatakiwa kuzungumzia sio tu madhambi ambayo tuyaepe, bali pia maadili ambayo tuwe nayo na usikivu katika kumfuata Roho Mtakatifu. Maisha ya Kiroho hayaenei kama maadilidini, lakini ni tawi la juu yake kwa jinsi linavyolenga kufikisha hadi muungano wa dhati na Mungu. Kwa njia yake teolojia inarudi ilipoanzia na kudumisha umoja wake. Kwa hiyo linatakiwa kufuata mwanga wa ufunuo wa Kimungu uliomo katika Maandiko na Mapokeo, ambao peke yake unaweza kutujulisha uzima wa Kimungu na muungano wa roho na Mungu ambao unapita maumbile.

Maisha ya Kiroho yanatumia mawazo ya maadilidini, lakini kuhusiana zaidi na ustawi wa uzima wa Kimungu rohoni. Utekelezaji wake, ambao ndio lengo la maisha ya Kiroho kupitia uongozi wa mtu mmojammoja, una pande mbili: juhudi na mafumbo.

Upande wa juhudi maisha ya Kiroho yanazungumzia hasa namna ya kufisha vilema na kutekeleza maadili. Upande wa mafumbo yanazungumzia hasa usikivu kwa Roho Mtakatifu, neema ya kuzama katika mafumbo ya imani, na muungano unaotokana na neema hiyo, halafu karama ambazo pengine zinaongozana nayo.

 

0.5.        TARATIBU ZA KOZI HII

 

Hapa tutaeleza yaliyo ya lazima tu, kwa kukwepa aina mbili za upotovu ambazo ni rahisi zitupate: moja kwa kuzingatia mafundisho ya imani na kupuuzia mang'amuzi, nyingine kwa kuzingatia mang'amuzi na kupuuzia mafundisho ya imani.

Tunapaswa kuzungumzia maisha ya Kiroho kwa mwanga wa teolojia kuhusu neema ya utakaso, maadili ya kujaliwa na vipaji saba; pasipo hayo tungekusanya tu dalili za hali za Kiroho za juu, badala ya kuelewa kanuni za msingi za ustawi wa uzima wa Kimungu ambao hauwezi kung'amuliwa kwa kuwa si wa kimaumbile. Pia tungetia maanani mno uhaba wa watu wanaofikia muungano wa ndani na Mungu: hapo tungedhani kuwa walio wengi hawaitwi hata kwa mbali na kwa jumla kufikia hatua hiyo; tungesahau maneno ya Bwana yanayokumbushwa na walimu wa Kiroho kuhusu swala hilo: “Waitwao ni wengi, bali wateule ni wachache” (Math. 22:14).

Upande wa pili tunapaswa kuzingatia maelezo ya watakatifu kuhusu hatua mbalimbali za maisha ya Kiroho, tukiyaangaza kwa imani ili kutambua katika mang'amuzi yao yapi ni ya pekee na yapi ni ya juu, lakini yanakusudiwa kuwa ya kawaida. Upande huo hatari nyingine ni kudhani kuwa neema ya kuzama katika sala ni ya wengi, tukiichanganya na sala nyofu ya mapenzi ambao ni utangulizi wake tu. Kufuatana na aina hizo mbili za upotovu, kuna makosa mawili ya kuepwa katika kuongoza watu: kuwaachisha njia ya juhudi mapema mno au baadaye mno.

Basi, tunapaswa kuchimba ukamilifu wa Kikristo ili kuona wazi lengo ambalo Mwokozi amewawekea watu tusilipunguze. Halafu kuchambua mang'amuzi ili tutofautishe yaliyo ya lazima na yaliyo ya ziada. Hatimaye kujumlisha hayo mawili ili kuona yaliyo ya lazima au ya kufaa na ya kutamaniwa kusudi tuufikie ukamilifu, na yale ambayo ni ya pekee tu na hayahitajiki kufikia utakatifu mkuu.

Kutokana na shida hizo mbalimbali, kusoma maisha ya Kiroho kunadai ujuzi wa teolojia (hasa juu ya neema, maadili ya kumiminiwa, na vipaji vya Roho Mtakatifu kuhusiana na mafumbo makuu ya Utatu, umwilisho, ukombozi na ekaristi) pamoja na ujuzi wa walimu wa Kiroho, hasa wale ambao Kanisa limewataja kuwa viongozi katika maswala hayo.

 

0.6.     TOFAUTI NA UHUSIANO KATI YA UPANDE WA JUHUDI NA UPANDE WA MAFUMBO

 

Kadiri ya mapokeo (watakatifu Thoma wa Akwino, Yohane wa Msalaba na Fransisko wa Sales) upande wa juhudi maisha ya Kiroho yanazungumzia hatua ya utakaso wa wanaoanza ambao, wakijua kwamba hawatakiwi kubaki nyuma na kupooza, wanajitahidi kutekeleza maadili, lakini kwa namna ya kibinadamu, yaani kwa nguvu zao zikisaidiwa na neema za kawaida. Kumbe upande wa mafumbo unaanza mara inapozungumziwa hatua ya mwanga ambapo wanaoendelea, wakiangazwa na Roho Mtakatifu, wanatenda tayari, mara nyingi na waziwazi kwa vipaji vyake saba; kwa uongozi maalumu wa huyo mlezi wa ndani wanatenda kwa namna ipitayo maumbile ambayo kabla ya hapo ilikuwa imefichika au kujitokeza mara mojamoja tu.

Walimu hao wameonyesha kuwa mambo yanayopatikana upande wa mafumbo ni ya juu katika njia ya kawaida ya utakatifu, ila si ya pekee hasa (kama njozi). Ndivyo ilivyo pia kwa wale wanaoitwa kufikia utakatifu katika utendaji mwingi (kama mt. Visenti wa Paulo).

Basi, kujua upande wa mafumbo hakufai tu kwa uongozi wa watu wachache wanaoitwa kufuata njia za pekee, bali kwa uongozi wa watu wote wanaolenga ukamilifu na muungano na Mungu katika maisha ya kila siku. Ujinga wa kiongozi wa Kiroho kuhusu mambo hayo unaweza ukazuia wale anaowaongoza: kwa kuwa hapaswi kudhani kila huzuni ya mtu aliyechoka kiakili ni takaso la Kimungu, lakini pia hapaswi kudhani kuwa hilo likipatikana ni huzuni ya kinafsi tu.

Kutokana na yote tuliyoyasema, ni wazi kwamba upande wa juhudi unalenga upande wa mafumbo. Vilevile upande wa mafumbo usipotanguliwa na juhudi za kufaa ni uongo mtupu.

Hatimaye ni muhimu kuzingatia kuwa tukitazama njia ya utakatifu kuanzia maumbile yetu, mafundisho yetu yataonekana yamepita kiasi. Lakini tukitazama njia hiyo kuanzia mafumbo yapitayo maumbile (uwemo wa Utatu mtakatifu ndani mwetu, umwilisho ulioleta ukombozi na ekaristi) hapo tutaiona kwa hekima, yaani kutoka juu, badala ya kupima yote kutoka chini unavyofanya upumbavu.

Ikiwa kweli Utatu mtakatifu unaishi ndani mwetu, ikiwa kweli Neno alifanyika mwili akafa kwa ajili yetu, yumo katika sakramenti kuu na kila siku anajitoa kwa ajili yetu, basi hapo watakatifu tu, wanaoishi kwa kujua na kama kung'amua mara nyingi uwemo huo wa Mungu, na kwa kuupenda zaidi na zaidi katika magiza na matatizo ya maishani, ndio waliopo panapotakiwa. Hapo maisha ya muungano wa ndani na Mungu yanaonekana kuwa peke yake ya kawaida kweli. Kabla ya kufikia maisha hayo, tuko bado kama watu waliosinzia, wasioishi vya kutosha kwa hazina ile kuu tuliyokabidhiwa na Mungu.

Utakatifu ni muungano wa ndani na Mungu, yaani ukamilifu wa upendo kwake na kwa jirani, ukamilifu ambao hata hivyo upo katika njia ya kawaida, kwa sababu amri ya upendo inayowapasa wote haina mipaka. Utakatifu huo hauhitaji elimu ya juu, wala utendaji mwingi wa nje, bali kuishi kwa ndani na Mungu.

 

Utakatifu huo ni utangulizi wa kawaida wa uzima wa milele; utangulizi huo unafanyika duniani au toharani, mpaka roho iwe imetakata kabisa iweze kukaribishwa kwenye heri ya kumuona Mungu.

Hatimaye, tukisema kuzama katika mafumbo ya imani ni karibu jambo la lazima kwa kufikia utakatifu, maana yake ni kwamba kwa kawaida pasipo hilo haiwezekani kufikia utakatifu ambao unadai kutekeleza kwa namna bora maadili ya Kimungu na vipaji vya Roho Mtakatifu vinavyoongozana nayo. Ndiyo tutakayoonyesha katika kozi hii.

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

 

1. CHEMCHEMI NA LENGO LA MAISHA YA KIROHO

 

 

Kwa kuwa maisha ya Kiroho ni namna ambayo mtu mwenye bidii anaishi kwa neema akizidi kujitambua, tutaongelea kwanza uzima wa neema ili kuuthamini kikamilifu. Halafu tutazingatia muundo wa Kiroho wa maadili ya kumiminiwa pamoja na vipaji vya Roho Mtakatifu, ambavyo vyote vinatokana na neema ya utakaso katika kila mwadilifu. Hayo yote yatatuongoza kuzungumzia uwemo wa Utatu rohoni mwake, na athari ya kudumu ya Bwana wetu Yesu Kristo, aliye mshenga pekee, na ya Maria pamoja naye kwa roho hiyo.

Ndizo chemchemi za maisha ya Kiroho tunazoikuta juu sana, kuliko chemchemi za mito zinazotoka kwenye vilele vya milima mirefu. Kwa kuwa zinatoka juu, maisha ya Kiroho yanaweza kumrudia Mungu aliye juu na kuungana naye kwa ndani.

Katika sehemu hii ya kwanza, kisha kuongelea chemchemi za maisha ya Kiroho, tutazungumzia lengo lake, yaani ukamilifu wa Kikristo na wajibu wa kuulenga, kila mmoja kadiri ya hali yake maishani. Lengo ndilo la kwanza katika kupanga nia, ingawa ni la mwisho katika utekelezaji. Ndilo tulilo na hamu nalo toka mwanzo, ingawa tunaweza kulipata mwishoni tu. Ndiyo sababu Bwana alianza kuhubiri kwa kutuambia juu ya heri.

 

 

 

 

1.1. UZIMA WA NEEMA, MWANZO WA UZIMA WA MILELE

 

 

Maisha ya Kiroho yanadai Mkristo awe na hali ya neema ya utakaso, ambayo ni kinyume cha hali ya dhambi ya mauti. Kila mtu yupo katika mojawapo kati ya hali hizo mbili, yaani ama anamuelekea Mungu kama lengo kuu, ama amepotoka mbali naye. Hakuna anayeweza kuwa na hali ya kimaumbile tu, kwa kuwa wote wanaitiwa lengo linalopita maumbile, yaani kumuona Mungu uso kwa uso na hivyo kumpenda kabisa.

Ili mtu awe na maisha ya Kiroho haitoshi awe na neema ya utakaso, kama vile mtoto kisha kubatizwa au mtu aliyeondolewa dhambi katika kitubio. Zaidi ya hiyo, maisha ya Kiroho yanadai vita dhidi ya yale yote yanayoweza kutuangusha dhambini, na juhudi halisi katika kumlenga Mungu.

Tungeng'amua kwa ndani hali ya neema, tungeona kwamba siyo tu mwanzo wa maisha matakatifu bali pia ni mbegu ya uzima wa milele. Ni lazima tusisitize mapema jambo hilo, tukikumbuka neno la mt. Thoma wa Akwino: “neema ya utakaso ya mmoja ni bora kuliko mema ya kimaumbile ya ulimwengu wote”; kwa sababu neema hiyo ni mbegu ya uzima wa milele, ambao una ubora usio na kifani kuliko uzima wa kimaumbile wa kwetu na wa malaika.

Ndilo linaloweza kutuonyesha vizuri kuliko yote thamani ya neema ya utakaso, ambayo tunaipata katika ubatizo na kurudishiwa na kitubio ikiwa tumeipoteza. Mwanzoni mwa kozi hii ni muhimu kuthamini kweli neema hiyo ambayo Uprotestanti umeisahau, ukifuata wanafalsafa wengi wa karne ya XIV. Hatuwezi kujua thamani ya mbegu tusipojua kinachoweza kutokana nayo. Upande wa binadamu, tukitaka kuthamini roho ambayo imesinzia bado katika mtoto, ni lazima tujue nguvu ya roho ya mtu aliyekomaa. Vilevile hatuwezi kuthamini neema ya utakaso waliyonayo waadilifu, tusipozingatia ustawi wake kamili katika uzima wa milele. Inafaa tuuzingatie kwa mwanga wa maneno ya Bwana, ambayo ni “roho, tena ni uzima” (Yoh. 6:63) na yana ladha bora kuliko maelezo yoyote ya teolojia. Lugha ya Injili na mtindo wa Bwana vinatuzamisha katika sala kuliko lugha ya kitaalamu hata ikiwa na hakika ya juu. Hakuna kinacholeta wokovu kuliko kupumua hewa safi ya vilele vile vinavyobubujika maji hai ya mafundisho ya Kikristo.

 

 

UZIMA WA MILELE AMBAO MWOKOZI AMEWAAHIDIA WENYE MAPENZI MEMA

 

Neno “uzima wa milele” ni adimu katika Agano la Kale, ambamo yote yanaelekea ujio wa Mwokozi aliyeahidiwa. Kumbe katika mahubiri ya Yesu yote yanaelekea moja kwa moja uzima wa milele. Tukizingatia kwa makini maneno yake tutaona jinsi uzima huo ulivyo tofauti na maisha yajayo yaliyozungumziwa na wanafalsafa bora (k.mf. Plato) kama hali ya kimaumbile tu na isiyo ya hakika. Kumbe Mwokozi anaongea kwa hakika juu ya uzima wa milele, bora, usio na jana, leo na kesho, unaopita maumbile na usiopimika, kama ule wa ndani ya Mungu, kwa kuwa unashiriki umilele wake usiobadilika.

Yesu alifundisha kuwa “njia imesonga iendayo uzimani” (Math. 7:14) na kuwa tukitaka kuupata ni lazima tuache dhambi na kushika “amri” za Mungu (taz. Math. 19:17). Mara kadhaa alisema kuwa anayemwamini “yuna uzima wa milele” (Yoh. 5:24; 6:40,47) maana yake anayemuamini kuwa ni Mwana wa Mungu kwa imani hai, inayoambatana na upendo na utekelezaji wa amri, ameanza kuwa na uzima wa milele. Ndivyo alivyotamka tangu mwanzo wa mahubiri yake: “Heri walio maskini wa roho, maana ufalme wa mbinguni ni wao... Heri wenye njaa na kiu ya haki, maana hao watashibishwa...Heri wenye moyo safi, maana hao watamwona Mungu” (Math. 5:3-8). Basi, uzima wa milele ni kushiba huko na kumwona Mungu katika ufalme wake. Kwa namna ya pekee, wanaoteswa kwa sababu ya kufanya atakavyo Mungu wanaambiwa: “Furahini na kushangilia, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni” (Math. 5:12). Yesu akajieleza zaidi tena kabla ya mateso yake aliposema: “Baba... ulimpa Mwanao mamlaka juu ya wote wenye mwili, ili kwamba wote uliompa awape uzima wa milele. Na uzima wa milele ndio huu: wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma” (Yoh 17:1-3).

“Wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye, kwa maana tutamwona kama alivyo” (1Yoh. 3:2), yaani si kwa kuzingatia mng'ao wa sifa zake katika viumbe (vile vinavyoonekana na roho za watakatifu zinazojitokeza katika maneno na matendo yao), bali moja kwa moja jinsi alivyo. “Wakati wa sasa tunaona kwa kioo kwa jinsi ya fumbo; wakati ule tutaona uso kwa uso; wakati wa sasa nafahamu kwa sehemu; wakati ule nitajua sana kama mimi nami ninavyojuliwa sana” (1Kor. 13:12). Mtume hakusema kuwa nitamjua ninavyojijua mpaka ndani; kwa sababu najifahamu kuliko wengine, lakini mimi pia sielewi yote niliyonayo ndani, k.mf. siwezi kupima uzito wote wa dhambi zangu. Mungu tu ananijua fika: siri za moyo wangu anazielewa kikamilifu yeye tu. Mbinguni nitamjua anavyonijua, moja kwa moja, pasipo kupitia kiumbe chochote au wazo lolote la kimaumbile, kwa sababu hakuna wazo la namna hiyo linaloweza kumchora Mungu na ukweli wake usio na mipaka, nuru angavu ya milele. Kila wazo la namna hiyo lina mipaka, linazingatia sifa mojawapo ya Mungu (k.mf. ukweli au wema). Mawazo hayo mbalimbali hayatoshi kutujulisha undani wa Mungu, umoja wake usiogawanyika kamwe. Mawazo hayo yanahusiana na uzima wake wa ndani kama vile rangi saba za upinde wa mvua zinavyohusiana na mwanga mweupe ambao zinatokana nao. Hapa chini sisi ni kama watu tulioona hizo rangi saba tu na sasa tunatamani kuona huo mwanga mweupe unaozisababisha. Kabla hatujaona umungu wenyewe hatuwezi kuona ulinganifu wa ndani wa sifa zake, hasa huruma isiyo na mipaka na haki isiyo na mipaka. Mawazo yetu ya kimaumbile kuhusu sifa za Mungu ni vipande tu vya sura nzima, ambavyo vinaleta picha fulani ya Mungu isiyopendeza vya kutosha. Tukifikiria haki yake, inaonekana ni kali mno, na tukifikiria upendeleo wa huruma yake unaonekana ukienda kinyume cha haki. Tukitafakari zaidi tunakiri kuwa ndani ya Mungu haki na huruma ni kitu kimoja, hazitofautiani kweli. Huo ni ukweli ambao tunauungama kwa hakika, lakini hatujaona ulinganifu wa ndani wa sifa hizo, kwa kuwa unahitaji tutazame umungu jinsi ulivyo, moja kwa moja, pasipo kutumia mawazo yoyote ya kimaumbile.

Mtazamo huo ndio uzima wa milele. Nani anaweza kueleza ukuu usiopimika wa furaha na upendo vitakavyokuwemo ndani mwetu kutokana na mtazamo huo? Upendo wa Mungu wenye nguvu na wa moja kwa moja, hivi kwamba hakutakuwa na lolote litakaloweza kuupunguza; upendo ambao tutafurahia hasa kuwa Mungu ni Mungu, mtakatifu, mwenye haki na huruma pasipo mipaka, na ambao tutaabudu mipango yote ya maongozi yake iliyolenga ufunuo wa wema wake. Tutazama katika heri yake, alivyosema Mwokozi mwenyewe: “Vema, mtumwa mwema na uaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako” (Math. 25:21,23). Tutamuona Mungu vile anavyojiona moja kwa moja, ingawa hatutaweza kumaliza vilindi vya hali yake, vya upendo wake na vya uweza wake. Pia tutampenda anavyojipenda. Vilevile tutamuona Bwana wetu Yesu Kristo. Ndiyo heri ya milele yenyewe, mbali ya furaha ya ziada tutakayokuwa nayo kwa kuwaona na kuwapenda Bikira Maria pamoja na watakatifu wote, hasa tuliowafahamu duniani.

 

 

MBEGU YA UZIMA WA MILELE NDANI MWETU

 

Huo mtazamo wa moja kwa moja wa Mungu unapita uwezo wa kimaumbile wa akili yoyote ya malaika na ya binadamu, kwa kuwa ungehitaji ulingane na ule wa Mungu. Basi, akili ya kiumbe inaweza kupata mtazamo huo kwa neema ya Mungu tu, ambayo ni kama kupandikiza chipukizi la mti bora katika shina la mti mwitu ili uzae matunda mema. Malaika na binadamu hawawezi kumjua na kumpenda Mungu kwa namna inayopita maumbile yao kabla hawajapandikiziwa neema ya utakaso, ambayo ni kushiriki umungu, yaani uzima wa ndani wa Mungu. Neema hiyo tu, ikipokewa rohoni mwetu kama zawadi isiyolipika, inatuwezesha kutenda Kimungu, yaani kumuona moja kwa moja vile anavyojiona, na kumpenda vile anavyojipenda. Kwa maneno mengine, akili na utashi kushirikishwa umungu kunategemea kushirikishwa umungu kwa roho yenyewe iliyonavyo.

Neema hiyo ikikamilika isiweze kupotezwa inaitwa utukufu, ambao katika akili za watakatifu wa mbinguni unatia mwanga usio wa kimaumbile unaowawezesha kumwona Mungu, na katika utashi wao unatia upendo wa kumiminiwa unaowawezesha kumpenda Mungu hata wasiweze kuachana naye kamwe. Kwa ubatizo sisi tumeshapokea mbegu ya uzima wa milele, kwa kupokea neema ya utakaso inayouleta uzima huo: pamoja na neema ya utakaso tumepokea upendo wa kumiminiwa unaokusudiwa kudumu milele. Ndivyo Mwokozi alivyomuambia mwanamke Msamaria: “Kama ungaliijua karama ya Mungu, naye ni nani akuambiaye, ‘Nipe maji ninywe’, ungalimwomba yeye, naye angalikupa maji yaliyo hai… Yeyote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele, bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele” (Yoh. 4:10,14).

“Atakayekunywa maji hai ya neema yanayotolewa na Mwokozi hatatamani mengine, ila atatamani kuyapokea hayohayo kwa wingi zaidi... Zaidi ya hayo, tofauti na maji ya kawaida ambayo yanaelekea chini, yale ya Kiroho yanapanda juu. Ni maji hai ambayo hayaachani kamwe na chemchemi yake na ambayo yanabubujikia uzima wa milele ambao yanatustahilisha” (mt. Thoma wa Akwino). Hayo maji hai yanatoka kwa Mungu, ndiyo sababu yanaweza kurudi juu kwake.

Siku ya mwisho ya sikukuu ya Vibanda, Yesu alisimama hekaluni, “akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. Aniaminiye mimi, kama vile Maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake” (Yoh. 7:37-38). Anayekunywa Kiroho kwa kumuamini Mwokozi, anaweza kuchota katika chemchemi ya maji hai, siyo kwa ajili yake tu bali pia kwa ajili ya watu wengine ili waokoke.

Yesu alikariri: “Amwaminiye Mwana yuna uzima wa milele” (Yoh. 3:36). Sio tu atakuwa nao baadaye, bali kwa namna fulani anao tayari, kwa kuwa uzima wa neema ni mwanzo wa uzima wa milele, kama vile mbegu inavyohusiana na mti wake. Kwa undani ni uzima uleule wa Kimungu, ambao hapa chini umo ndani ya Mkristo kama mbegu na ambao huko juu utachanua kikamilifu katika watakatifu. Ndiyo maana Bwana aliongeza: “Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho” (Yoh. 6:54). Ufalme wa Mungu umo ndani mwetu kama mbegu ya haradali, kama chachu itakayoumua donge lote, kama hazina iliyositirika shambani.

Tunawezaje kujua kama tumepokea tayari uzima huo unaokusudiwa kudumu milele? “Sisi tunajua ya kuwa tumepita toka mautini kuingia uzimani, kwa maana twawapenda ndugu. Yeye asiyependa, akaa katika mauti… Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu” (1Yoh. 3:14; 5:13).

Yesu alisema: “Amin, amin, nawaambia: Mtu akilishika neno langu, hataona mauti milele” (Yoh. 8:51). Kwa kuwa, inavyosema liturujia, “Ee Bwana, uzima wa waamini wako hauondolewi ila unageuzwa tu”, tena unastawi kikamilifu mbinguni tu. Hakika uzima wa neema hapa duniani ni mbegu ya utukufu, hivi kwamba kiwango kidogo cha neema ya utakaso ni bora kuliko mema ya kimaumbile ya ulimwengu wote na ya malaika pia, kwa sababu kinahusu hali ya juu, yaani uzima wa ndani wa Mungu; kwa hiyo ni bora kuliko miujiza yote na ishara nyingine za nje za ufunuo wa Mungu.

Uzima uleule unaopita maumbile, ndio unaopatikana duniani katika waadilifu na mbinguni katika watakatifu. Ni pia upendo uleule wa kumiminiwa, isipokuwa tofauti mbili. Hapa chini tunamjua Mungu si kwa kumtazama mwangani, bali katika giza la imani ya kumiminiwa. Halafu hapa chini, ingawa tunatumaini kuwa naye kikamilifu milele, tunaweza kupotewa naye kwa kosa letu.

Kuna tofauti hizo mbili zinazohusu imani na tumaini, hata hivyo ni uzima uleule na upendo uleule ambavyo vinakusudiwa kudumu milele. Kwa mwanga huo tunapaswa kuelewa maisha yetu ya Kiroho yanavyotakiwa kuwa na kustawi hapa chini yawe utangulizi wa kufaa kwa uzima wa milele. Ikiwa neema ya utakaso, maadili ya kumiminiwa na vipaji vya Roho Mtakatifu kwa mfumo wake vinaulenga uzima wa milele, je havikusudiwi kulenga pia muungano wa hali ya juu na Mungu?

 

 

JAMBO MUHIMU LITOKANALO

 

Kwa kweli neema ya utakaso na upendo, vinavyotuunganisha na Mungu katika maisha yake ya ndani, ni bora, tena sana, kuliko neema za pekee (kama vile kutabiri na kusema kwa lugha ngeni) ambazo ni ishara tu za kazi za Mungu lakini hazituunganishi naye (taz. 1Kor. 12:28-13:13). Hali ya kuzama katika mafumbo ni tunda la imani tuliyomiminiwa, ikiangazwa na vipaji vya akili na vya hekima: hivyo inatokana na neema ya utakaso, ambayo inaitwa pia “neema ya maadili na vipaji” na tunaipata wote katika ubatizo; haitokani na neema za pekee.

Kwa kuwa neema ya utakaso kwa mfumo wake inalenga uzima wa milele, inalenga pia hali ile inayohitajika ili kupata mwanga wa utukufu. Hali hiyo ni upendo kamili pamoja na hamu kubwa ya heri ya kumuona Mungu; kwa kawaida hamu hiyo inatokana na neema ya kuzama katika mafumbo. Hivyo basi kuzama huko si neema ya pekee kama ulivyo k.mf. utabiri, bali ni hali ya juu iliyopo katika njia ya kawaida ya utakatifu, ingawa ni adimu kama ulivyo adimu ukamilifu mkuu.

 

Hatimaye, kwa vile neema ya utakaso kwa mfumo wake inalenga uzima wa milele, inalenga pia kutuweka tayari kupata mwanga wa utukufu mara baada ya kufa bila ya kupitia toharani, ambako ni adhabu, maana yake kunatokana na kosa lisilotakiwa pamoja na malipizi yasiyotosha; ingekuwa kawaida kutakaswa katika maisha haya kwa kujilimbikizia stahili na kukua katika upendo, badala ya kutakaswa kisha kufa pasipo stahili yoyote. Hali iliyo tayari kupokea mwanga wa utukufu mara baada ya kifo inahitaji kwanza utakaso halisi unaolingana na ule wa roho zinazotoka toharani zenye hamu kubwa ya kumwona Mungu.

Hamu hiyo imedhihirishwa na mt. Paulo vizuri ajabu: “Katika nyumba hii twaugua, tukitamani sana kuvikwa kao letu litokalo mbinguni… twaugua, tukilemewa, si kwamba twataka kuvuliwa, bali kuvikwa… Basi yeye aliyetufanya kwa ajili ya neno lilo hilo ni Mungu, aliyetupa arabuni ya Roho” (2Kor. 5:2-5).

Tukitaka kujadili maswala ya maisha ya Kiroho jinsi inavyotakiwa, hatupaswi kusahau vilele hivyo tunavyojulishwa na Maandiko na kuelezwa na teolojia ya walimu wakuu. Hasa katika maisha ya Kiroho tunatakiwa kuzingatia watu sio walivyo tu bali wanavyokusudiwa kuwa. Tunapaswa kupumua hewa bora ya vilele vya juu, badala ya kuishia katika hali ya wastani ya binadamu. Heri watu ambao wanajaribiwa hata wanakuta hewa ya kuwafaa upande wa Mungu tu na kumtamani kwa hamu kuu.

 

 

 

 

1.2. MAISHA YA KIROHO NA MAONGEZI YA NDANI NA MUNGU

 

 

MAONGEZI YA KILA MTU NA NAFSI YAKE

 

Mtu anapoacha shughuli za nje na maongezi na wenzake na kubaki peke yake - hata kama ni katikati ya kelele za jiji - mara anaanza kuwaza kama kwa kuongea na nafsi yake. Akiwa kijana anafikiria ya kesho; akiwa mzee anafikiria ya zamani, na mang'amuzi aliyonayo sasa yanamfanya apime tofauti watu na matukio. Akiwa na umimi anafuata tamaa au kiburi na hivyo ndani yake anapata huzuni tu, ndiyo sababu anajaribu kujitoroka kwa kuzama katika mambo ya nje na anasa asahau utupu wa maisha yake yasiyo na maana. Kwa kufanya hivyo anakuja kujifahamu kwa namna fulani ya hali ya chini, na vilevile kujipenda visivyo. Sanasana anajifahamu upande wa hisi, alizo nazo sawa na wanyama; hivyo ana furaha na uchungu vya kihisi kadiri ya mabadiliko ya hali ya hewa au ya biashara yake. Anavyovitamani na anavyovichukia ni vya aina hiyohiyo, na akipingwa anakasirika kutokana na jinsi anavyojipendea.

Kumbe anajifahamu kidogo tu upande wa roho, ambayo inalingana na malaika. Hata kama anaamini ukuu wa roho (yenye akili na utashi) haishi katika ngazi hiyo: hana mang'amuzi kuhusu sehemu hiyo bora ya utu wake, wala haipendi vya kutosha. Angeijua angeona ndani yake sura ya Mungu na kuanza kujipenda kwa ajili ya Mungu, si tena kujipendea kibinafsi. Hata akionyesha mara nyingi uwezo wa kuelewa na kutenda kwa ujanja, akili yake inaelekea daima yaliyo ya chini kuliko yeye. Ingawa ameumbwa ili kumtazama Mungu, ukweli mkuu, anafuata udanganyifu hata kuutetea kwa kila njia. Maisha yasipofuata ubora wa mawazo, mawazo yatafuata uduni wa maisha: yote yanafungamana, hata misimamo mizuri aliyokuwa nayo inadhoofika zaidi na zaidi.

Hivyo maongezi ya ndani yake yanaelekea mauti na hayastahili kuitwa maisha ya Kiroho. Kujipendea kwake kunamfanya ajione kiini cha yote, na kuelekeza yote (watu na vitu) kwake; lakini hiyo haiwezekani, ndiyo sababu mara nyingi anakata tamaa na kuchukizwa, havumiliki kwake wala kwa wengine. Kwa kutaka kujipendea mwishowe anajichukia pamoja na maisha, kwa kuwa katika maisha alitamani mno yaliyo ya chini.

 

Kumbe binadamu akianza kutafuta uadilifu, hata kama hajawa na neema ya utakaso, maongezi yake na nafsi yake yanakuwa tofauti: k. mf. anazingatia yanayohitajika ili aishi kwa haki na kutegemeza familia yake. Pengine mawazo hayo yanamletea mahangaiko hata kumfanya atambue unyonge wake na haja ya kumtegemea Mungu badala ya kujiamini tu. Akiwa na dhambi ya mauti isiyo dhidi ya imani wala tumaini anaweza kuwa na maadili hayo yanayodumu ndani mwetu hata baada ya kupoteza upendo. Kama ni hivyo pengine mawazo yake yanaangazwa na imani ambayo mwanga wake unapita maumbile yetu; anaweza akawaza uzima wa milele na kuutamani, ingawa si zaidi; tena pengine anajisikia msukumo wa kwenda kanisani.

 

Hatimaye, mtu huyo akijuta na kuondolewa makosa yake, anarudishiwa neema ya utakaso na upendo kwa Mungu na kwa jirani. Kuanzia hapo, mawazo yake yanakuwa mengine. Anaanza kujipenda kitakatifu, yaani si kwa ajili yake, bali kwa ajili ya Mungu, na kuwapenda watu pia kwa ajili ya Mungu; anaanza kuelewa anavyopaswa kusamehe na kupenda maadui, na kuwatakia uzima wa milele vile anavyojitakia. Lakini mara nyingi mawazo yake yanaendelea kuchafuliwa na umimi, ubinafsi, tamaa na kiburi. Kwake makosa hayo si tena ya mauti, lakini yakitokea mara nyingi yanamfanya arudie dhambi kubwa na mauti ya roho. Hapo mtu atajaribu tena kujitoroka, kwa sababu haoni uzima ndani mwake; ndiyo maana asipojifikiria upya atazidi kujitupa mikononi mwa anasa na kiburi.

Hata hivyo maongezi ya ndani mwake yanaanza tena yasiweze kuzuiwa na chochote, wala na yeye mwenyewe. Ndani mwa roho mna haja inayodai kutimizwa. Mungu tu anaweza kufanya hivyo, kwa hiyo njia pekee ni kumuendea yeye. Roho inahitaji kuongea naye kwa sababu lengo lake kuu ni Mungu aliye hai, hata isiweze kutulia isipokuwa ndani ya Mungu.

 

 
MAONGEZI YA NDANI NA MUNGU

 

Basi, maisha ya Kiroho ni maongezi ya kila mtu na nafsi yake kuinuliwa na kugeuka sura mara yanapoanza kuwa maongezi na Mungu. Ni kwamba Roho wa Mungu anawaonyesha zaidi na zaidi watu wenye mapenzi mema yale ambayo anayataka toka kwao na yale anayotaka kuwazawadia. Lo, kama tungepokea kwa mikono miwili yale yote Mungu anayotaka kutupatia!

Maonyesho hayo hayafanyiki pasipo juhudi; tunapaswa kuokoka katika vifungo vitokanavyo na dhambi, kufisha hatua kwa hatua “utu wa zamani” na kuunda “utu wa ndani”: “Kwa maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani; lakini katika viungo vyangu naona sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu” (Rom. 7:22-23) “Utu wa ndani” ndio kilicho bora ndani mwetu, yaani akili utashi ambavyo vinapaswa kutawala mwili, ulio sawa kwa mtu na kwa mnyama.

“Kwa hiyo hatulegei; bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu wa ndani unafanywa upya siku kwa siku” (2Kor. 4:16). Nguvu za Kiroho zinafanywa upya mfululizo kwa njia ya neema tunazozipokea kila siku. “Msiambiane uongo, kwa kuwa mmevua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake; mkivaa utu mpya, unaofanywa upya upate ufahamu sawasawa na mfano wake yeye aliyeuumba” (Kol. 3:9-10). Baba “awajalieni, kwa kadiri ya utajiri wa utukufu wake, kufanywa imara kwa nguvu, kwa kazi ya Roho wake, katika utu wa ndani. Kristo akae mioyoni mwenu kwa imani mkiwa na shina na msingi katika upendo; ili mpate kufahamu pamoja na watakatifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo na kina; na kuujua upendo wake Kristo, upitao ufahamu kwa jinsi ulivyo mwingi, mpate kutimilika kwa utimilifu wote wa Mungu” (Ef. 3:16-19).

Ndiyo maisha ya Kiroho na vilindi vyake, maisha yale yanayolenga mfululizo kulitazama fumbo la Mungu na kulifanya chakula chake katika muungano naye wa ndani zaidi na zaidi. Mtume aliandika hayo kwa Wakristo wote, sio kwa mmojammoja tu. Akaongeza: “Mfanywe wapya katika roho ya nia zenu; mkavae utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli… mkaenende katika upendo, kama Kristo naye alivyowapenda ninyi; tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato”(Ef. 4:23-24; 5:2).

Kwa kuzingatia maneno hayo ya Mungu tunaweza kufafanua maisha ya Kiroho kama ifuatavyo: maisha ya Kiroho ni maisha ambayo yanapita maumbile na kutuelekeza na kutufikisha kwenye muungano na Mungu kwa njia ya kujikana na kusali kweli.

“Mafundisho ya Yesu Kristo yanapita mafundisho yoyote ya watakatifu na mtu aliye na roho yake anakuta humo mana iliyositirika. Lakini inatokea kuwa wengi, kwa kusikia Injili mara nyingi, hawaguswi inavyotakiwa, kwa sababu hawana roho yake. Mnataka kuelewa mpaka ndani na kufurahia maneno ya Yesu Kristo? Mjitahidi kulinganisha maisha yenu yote na ya kwake” (Kumfuasa Yesu Kristo, I,1:2).

Maisha hayo yana hatua ya kwanza inayotawaliwa na utakaso, ya pili inayotarajia mwanga mkubwa zaidi na zaidi, na lengo lake la mwisho ni kuungana na Mungu. Ndivyo mapokeo yote yanavyofundisha, yakithibitisha uwepo wa hatua ya kutakaswa kwa wanaoanza, hatua ya kuangazwa kwa wanaoendelea, na hatua ya kuungana na Mungu kwa waliokamilika. Hivyo maisha ya ndani ya mtu yanakuwa zaidi na zaidi maongezi na Mungu.

Kwa namna hiyo, mtu anaanza kung'amua sehemu bora ya nafsi yake na kumjua Mungu. Polepole mawazo ya nafsi yake aliyoifanya kuwa lengo la yote, yanaiachia nafasi kumbukumbu ya kudumu ya Mungu. Vivyo hivyo kujipendea kunaacha nafasi kwa upendo wa Mungu na wa watu kwa ajili yake. Maongezi ya ndani yanabadilika hata kusema: “Sisi, wenyeji wetu uko mbinguni” (Fil. 3:20).

Katika roho yenye neema ya utakaso, maisha ni hasa ya unyenyekevu, kujikana, imani, tumaini na upendo, pamoja na amani inayotakana na kuweka miguso na matakwa yote chini ya upendo wa Mungu atakayekuwa heri yetu. Basi, ili tuwe na maisha ya Kiroho haitoshi tushughulikie sana utume wala kujua sana dini. Tena hayo si ya lazima. Mtu aliyeanza tu kujikana na kusali kwa juhudi, anayo tayari maisha ya Kiroho ambayo yanatakiwa kustawi zaidi na zaidi.

Katika maongezi hayo yanayoelekea kuwa ya kudumu roho inasema kwa njia ya sala, ambayo ingekuwepo hata kama Mungu angemuumba mtu mmoja au malaika mmoja tu. Sala inaweza kuwa ya kuomba, ya kuabudu au ya kushukuru; lakini daima ni kuinua roho kwa Mungu. Naye Mungu anajibu akitukumbusha yale ambayo tuliambiwa katika Injili na yanatufaa kuitakasa nukta ya sasa hivi: “Huyo Msaidizi, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia” (Yoh. 14:26)?

Hivyo mtu anazidi kuwa mtoto wa Mungu, anatambua zaidi na zaidi kuwa Mungu ni Baba yake na anazidi kujifanya mdogo mbele yake. Anaelewa yale Yesu aliyomuambia Nikodemu, yaani kuwa ni lazima kurudi katika tumbo la Mungu ili kuzaliwa upya Kiroho kila siku zaidi, k.mf. wa Neno kuzaliwa milele. Wenye heri wa mbinguni wanabaki daima katika tumbo hilo.

Watakatifu wanafuata njia hiyo, hata maongezi kati yao na Mungu hayana mwisho. Mt. Dominiko hakuweza kusema isipokuwa juu ya Mungu au na Mungu; ndiyo sababu alikuwa amejaa daima upendo kwa watu. Maongezi hayo na Mungu yanaundwa kwa njia ya Kristo mshenga: “Ulimi hauwezi kusema, / wala maandishi kufafanua, / aliyeng'amua tu anaweza kuamini / kumpenda Yesu ni nini” (Utenzi wa Jina Takatifu la Yesu).

 

 

 

 

1.3. MUUNDO WA KIROHO

 

 

Ili tuelewe mbegu ya uzima wa milele iliyomo ndani mwetu ni nini, tunatakiwa kuzingatia jinsi neema ya utakaso inavyoleta katika akili na utashi maadili ya kumiminiwa na vipaji saba vya Roho Mtakatifu. Maadili hayo na vipaji hivyo ni kama utendaji wa muundo uleule mmoja wa Kiroho unaokusudiwa kustawi hadi tuingie mbinguni.

 

 

 

1.3.1. MAISHA YA KIMAUMBILE NA YANAYOPITA MAUMBILE

 

Kwanza tutofautishe vizuri ndani ya roho yetu yale yaliyo ya kwake kwa jinsi ilivyoumbwa, na yale ambayo ni zawadi tu ya Mungu. Hata malaika, ingawa ni roho tu, ana maumbile ya chini kuliko neema ya utakaso.

Basi, sisi binadamu tuna pande mbili tofauti: upande wa hisi na upande wa akili. Wa kwanza unalingana na wanyama, ukiwa na hisi za nje (milango ya fahamu), hisi za ndani (ubunifu na kumbukumbu) na uwezo wa kupatwa na maono mbalimbali (k.mf. pendo na chuki, hamu na hofu, furaha na huzuni, hasira).

Juu ya sehemu hiyo, katika maumbile yetu ipo nyingine inayolingana na malaika, ingawa ndani mwao ina nguvu na uzuri zaidi. Upande huo roho inapita mwili, maana yake haitegemei mwili moja kwa moja, kwa hiyo inaweza kudumu baada ya mwili kufa.

Kutokana na maumbile ya roho upande huo wa juu tuna uwezo wa akili na wa utashi. Akili inajua sio tu sifa ya viumbe zinazohisikana (rangi, sauti), bali undani wao na kweli zisizobadilika kama vile: “Hakuna kinachotokea pasipo sababu, na hasa pasipo sababu kuu, yaani Mungu”. “Tunapaswa kutenda mema na kuepa maovu”. “Timiza wajibu wako, liwalo na liwe”. Mnyama hataweza kamwe kujua kweli hizo.

Kwa kuwa akili inaweza kujua sio tu yale yanayotupendeza au yanayotufaa bali pia uadilifu (k.mf. kwamba ni “afadhali kufa kuliko kusaliti”), basi utashi unaweza kupenda huo uadilifu, kuutaka na kuutekeleza. Hivyo unapata kutawala hisi na maono alivyonavyo mnyama pia. Kwa akili na utashi mtu anafanana na malaika, ingawa katika maisha haya akili yetu, tofauti na malaika, inazitegemea hisi katika kuanza kujua mambo.

Tunavyoona katika watu kadhaa, akili na utashi vinaweza vikastawi, pasipo kufikia kujua na kupenda maisha ya ndani ya Mungu, ambayo ni ya ngazi tofauti, juu kupita maumbile ya malaika na ya binadamu. Hao wanaweza kumjua kimaumbile Mungu kwa nje, kutokana na mng'ao wa sifa zake katika viumbe, lakini haiwezi kuumbwa akili yenye nguvu ya kuyajua yaliyo ya Mungu tu: “Ni nani katika binadamu ayajuaye mambo ya binadamu ila roho ya binadamu iliyo ndani yake? Vivyo hivyo na mambo ya Mungu hakuna ayafahamuye ila Roho wa Mungu” (1Kor. 2:11).

Kumbe neema ya utakaso inatuingiza katika hiyo hali ya juu ya ukweli na uzima inayopita maumbile yoyote. Ni uzima unaopita maumbile, kwa kuwa unashiriki maisha ya ndani ya Mungu, ni hali ya Kimungu ambayo tangu sasa inatuandaa kumuona milele anavyojiona na kumpenda anavyojipenda. “Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu, mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao. Lakini Mungu ametufunulia sisi kwa Roho (1Kor. 2:9-10).

Neema ya utakaso inayotuwezesha kuanza kuishi maisha ya ndani ya Mungu, katika ngazi ya juu kuliko maumbile ya malaika, ni kama chipukizi la Kimungu lililopandikizwa ndani mwa roho ili kuinua uzima wake na kuifanya izae sio tu matunda ya kimaumbile, bali matunda yanayopita maumbile, yaani matendo yanayostahili uzima wa milele. Kupandikizwa huko kunapita miujiza inayojulikana na hisi. Kwa mfano, ufufuo unaurudishia mwili uhai wa kimaumbile, ndiyo sababu unaweza kujulikana na maumbile yetu; kumbe neema ya utakaso inaipatia roho uzima usio wa kimaumbile, ndiyo sababu hauwezi kuhakikishwa na maumbile yetu.

Tangu sasa uzima huo wa neema unachanua ndani mwetu maadili ya kumiminiwa na vipaji saba vya Roho Mtakatifu. Kama vile katika maumbile yetu roho ina uwezo wa akili na kadhalika, katika ngazi inayopita maumbile neema ya utakaso inaleta rohoni maadili na vipaji hivyo ambavyo, pamoja na mzizi unaovisababisha, ndio muundo unaopita maumbile ambao tulijaliwa katika ubatizo (na tunarudishiwa na ondoleo la dhambi ikiwa tuliupoteza).

Muundo huo wa Kiroho unaweza kuonyeshwa na jedwali ifuatayo:

 

                          MAADILI                                                             VIPAJI

                                      Upendo                                                           Hekima

YA KIMUNGU             Imani                                                   Akili

                                      Tumaini                                               Elimu

 

                                      Busara                                                Shauri

                                      Haki

                                                 (Ibada)                                                Ibada

                                                 (Toba)

                                                 (Utiifu)

YA KIBINADAMU      Nguvu                                                 Nguvu

                                                 (Subira)

                                      Kiasi                                                   Uchaji wa Mungu

                                                 (Upole)

                                                 (Unyenyekevu)

                                                 (Usafi wa moyo)

 

 

 

1.3.2. MAADILI YA KIMUNGU

 

Maadili ya Kimungu ni maadili tunayomiminiwa yanayomhusu Mungu mwenyewe aliye lengo letu kuu. Tofauti na hayo, maadili ya kibinadamu yanahusu njia za kufikia lengo hilo.

Kati ya maadili ya Kimungu, imani inatuwezesha kusadiki yale yote ambayo Mungu ametufunulia, kwa sababu ndiye ukweli wenyewe. Ni kama hisi ya Kiroho inayotuwezesha kusikia muziki safi wa Kimungu usiojulikana kwa njia nyingine yoyote, maana kuna tofauti kubwa kati ya kusoma Injili kihistoria au kitaalamu na kuiamini kama Neno la Mungu, kwa kuwa kusadiki ni tendo linalopita maumbile yetu na ya malaika, likituingiza katika ulimwengu wa juu. “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu” (Ef. 2:8). Ndiyo msingi wa kufanywa waadilifu, kwa kuwa inatujulisha lengo lipitalo maumbile tunalopaswa kulikusudia. “Ibrahimu alimwamini Mungu, ikahesabiwa kwake kuwa haki” (Mwa. 15:6; Rom. 4:3,9). “Walakini haikuandikwa kwa ajili yake tu kwamba ilihesabiwa kwake; bali na kwa ajili yetu sisi tutakaohesabiwa vivyo hivyo, sisi tunaomwamini yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu katika wafu” (Rom. 4:23-24). Sisi tutaokoka tu kwa imani hiyo ambayo ni zawadi ya Mungu. Kanisa lilitamka rasmi dhidi ya Wapelajiupande kwamba hata mwanzo wa imani ni neema. Imani hiyo inapita kabisa maumbile, siyo