Historia ya Wafransisko
|
![]() |

1.1.1. MWANZO WA MAPAMBANO
(1226-1318)
Mt. Fransisko alipokuwa hai alisongwa na kundi
la Watumishi na wasomi wa utawa wake, likisaidiwa na viongozi wa juu wa Kanisa,
ili alegeze masharti ya ufukara na kulinganisha zaidi shirika lake na yale ya
zamani. Kwa karama yake ya pekee aliweza kukabili upinzani huo wote. Juhudi yake
ya mwisho ya kuzuia shirika lisipotoke ni wasia aliouandika ili kusisitiza
msimamo wake, kudai kanuni yake isifafanuliwe, pamoja na kukataza wanashirika
wasimuombe Papa hati yoyote. Alipokufa utawa ukabaki mikononi mwa Watumishi hao,
wakiongozwa na nd. Elia Bombarone, Mkuu wa shirika miaka 1221-1227, halafu
1232-1239.
Katikati
ya hivyo vipindi vyake viwili vya uongozi, Mtumishi mkuu alikuwa nd. Yohane
Parenti. Chini yake yalizuka mabishano makali kati ya walioshikilia wasia huo na
wale waliotaka shirika lishindane na mashirika mengine. Yeye na Watumishi
wengine wakadhani utatuzi unaweza kutokea kwa viongozi wa Kanisa tu. Akipokea
ombi lao, Gregori IX (1227-1241) alitoa tamko rasmi la kwanza juu ya kanuni
(1230), akitumia mamlaka yake ya Kipapa na pia ujuzi wake wa nia ya Mt.
Fransisko (ndiye aliyemsaidia sana kutunga kanuni alipokuwa bado Kardinali, jina
lake Ugolino). Upande wa ufukara kwa jumla alitetea msimamo wa mwanzilishi (kwa
jinsi alivyomheshimu hata akamtangaza mtakatifu), ila aliulegeza kiasi, kwa
lengo la kufanikisha zaidi utume wa Ndugu Wadogo na hivyo kurekebisha Kanisa
lililokuwa na hali mbaya kiroho. Kwa ajili hiyo aliwapa hati na ruhusa nyingi za
pekee dhidi ya mamlaka ya Maaskofu na maparoko. Kuhusu wasia alitamka kuwa si
sheria inayowabana Wafransisko wasiweze kufafanua kanuni yao wala kufafanuliwa
na Kanisa, wala kuomba wala kupewa hati na fadhili za Papa. Sababu ya msingi ni
kuwa Kanisa liko juu kuliko kanuni.
Hivyo
njia ikawa wazi kuligeuza shirika la wadogo walio wote sawa, wanaohubiri toba
kwa unyenyekevu chini ya padri yeyote, liwe shirika imara la kikleri, lisilo
chini ya Maaskofu isipokuwa kwa machache. Mageuzi hayo yalisababisha kwa muda
mrefu upinzani mwingi wa Maaskofu na mapadri wanajimbo. Aliyesukuma sana shirika
kufuata njia hiyo ni nd. Elia, ambaye alimjengea Mt. Fransisko kanisa zuri sana,
halafu jirani nalo konventi kubwa mno, ili kushindana na abasia za Wabenedikto.
Alimgeuza mwanzilishi kuwa fahari ya shirika badala ya kielelezo cha kufuatwa.
Mwenye vipawa na elimu, ingawa bradha, aliathiri sana viongozi wa dini (Gregori
IX) na wa siasa (Federiko II), alistawisha misheni huko Mashariki na kukuza
nyumba za masomo, lakini pia alidhulumu vikali watetezi wa kanuni (hasa
alimuacha nd. Kaisari wa Speyer afe kwa njaa kisha kumfunga). Bila ya kutembelea
kanda za shirika, alishika uongozi wote mikononi mwake, akichagua Watumishi na
walinzi, akihamisha ndugu, akituma wawakilishi wake huko na huko kusimamia kazi
ya Watumishi, na akikataa kuitisha mkutano mkuu. Fahari zake binafsi, ushuru
aliowatoza mfululizo Watumishi (kwa ajili ya ujenzi n.k.) vilisababisha wafanye
njama dhidi yake, hadi Gregori IX akaitisha na kuendesha mkutano mkuu ambao
ulimuondoa madarakani na kutunga sheria ili kupunguza mamlaka ya Mtumishi mkuu.
Nd.
Aimoni wa Faversham, Mwingereza aliyeongoza upinzani, akaja kuwa Mtumishi mkuu
(1240-1244), na kulipatia shirika sura ya kudumu kufuatana na mfano wa
Wadominiko upande wa muundo, utume, masomo na liturujia. Taratibu za maisha
zikazidi kufuata mitindo ya kimonaki, pamoja na watawa kujitafutia visingizio
vya kisheria wasibanwe nazo. Makao ya kifukara ya upwekeni yalizidi kuachwa ili
wanashirika wahamie nyumba kubwa za mijini, zenye makanisa makubwa ambamo
wafanye utume, wakiwanyang’anya maparoko waamini na sadaka zao. Kama
alivyofanya mwenyewe huko Paris, Ndugu Wadogo wakazidi kushika nafasi kwenye
vyuo vikuu na vinginevyo, na kuwa na uzito mkubwa ndani ya Kanisa, jambo
lililowasogeza mbali na udogo uliowapasa. Mabradha wakanyimwa kabisa nafasi za
uongozi na kukubaliwa tu kutoa huduma ndogondogo za nyumbani (bustani n.k.),
wakiwaachia raia huduma duni zaidi. Kazi za mikono nje ya konventi zilikatazwa;
badala yake ile ya kuombaomba ikaja kusifiwa na kushika nafasi ya kwanza upande
wa uchumi. Zilipangwa pia njia za hakika za kupata mahitaji, hasa kwa nyumba za
masomo.
Alipokufa,
nd. Kreshensi wa Iesi alishika nafasi yake (1244-1247), akatambua hali halisi,
lakini hakuweza kuirekebisha (pia kwa sababu ya uzee wake). Akiona
kwamba Mt. Fransisko alikuwa bado kielelezo cha wadogo, aliagiza zikusanywe
habari zote juu yake, halafu akamuagiza nd. Thoma wa Celano aandike upya maisha
ya mwanzilishi. Juhudi zake kwa ajili ya kushika njia ya kati hazikuridhisha
wala upande mmoja (wenzi wa Mt. Fransisko na ndugu “wa Kiroho”, yaani wenye
nia ya kushika kanuni kadiri ya Roho Mtakatifu) wala upande wa pili (“jumuia”,
yaani waliopenda maisha katika konventi kubwa na hali ilivyo). Inosenti IV
(1243-1254) alikubali kutoa tamko la pili juu ya kanuni (1245) ili kuilegeza.
Hasa alifungua milango ili Ndugu Wadogo wajipatie vitu vingi, akitamka kuwa
vyote walivyonavyo, kama si vya wafadhili tena, basi ni vya Papa. Hivyo kwa
kutofautisha kutumia vitu na kuvimiliki kisheria, Ndugu Wadogo waliweza kujidai
fukara ingawa wanatumia vingi, eti si vya kwao! Lakini wengi hawakuridhika na
ujanja huo.
Akachaguliwa M.H. Yohane wa Parma (1247-1257), mtu wa kufaa sana kwa
elimu na utakatifu, aliyeongoza hasa kwa mfano wa maisha yake bora. Alikusudia
kurudisha shirika katika hali ya mwanzoni kufuatana na wasia, kwa kuheshimu
Maaskofu na mapadri na kukataa fadhili za Papa. Alitembelea kwa miguu kanda zote
akiamsha nia ya kushika kanuni na wasia. Hivyo mkutano mkuu (1254) ulisimamisha
utumiaji wa fadhili kadhaa; lakini, alivyosema M.H. Egidi
wa Asizi (+1262), juhudi hizo nzuri zilikuwa zimechelewa zisiweze kurekebisha
shirika lote. Wapinzani walimshtaki M.H. Yohane, akalazimika kujiuzulu. Mkutano mkuu ulitaka aendelee, lakini mwenyewe hakurudi nyuma. Hatimaye
walimuomba walau amchague mwandamizi wake, naye akamtaja Mt. Bonaventura
wa Bagnoregio akaenda kuishi upwekeni.
Mt. Bonaventura (1257-1274), kufuatana na tabia yake,
alikubali hali ilivyo na kujitahidi kuepusha shirika na hatari za nje na za
ndani alizoziona mapema. Upinzani wa Maaskofu na maparoko dhidi ya Ndugu Wadogo
ulikuwa umeungwa mkono na chuo kikuu cha Paris: hapo hazikupingwa tu ruhusa
kadhaa walizopewa, bali msingi wenyewe wa mtindo wao na wa Wadominiko. Baada ya
Mt. Bonaventura na Mt. Thoma wa Akwino kuutetea, Papa alilaani upinzani na
kusifu sana mtindo wa Kiinjili. Mwalimu huyo kuchaguliwa kuwa Mtumishi mkuu
kukawa ushindi mwingine mkubwa chuoni.
Mashambulizi ya kutisha zaidi yalitokea ndani, upande
wa ndugu “wa Kiroho”. Mt. Bonaventura alijipangia kulinganisha uaminifu kwa
kanuni na mabadiliko ya shirika, akionyesha hayo hayaendi kinyume cha nia ya
mwanzilishi. Ili athibitishe hayo ilimpasa kuziondolea lawama msingi wowote kwa
kupigania uaminifu kwa wito wa shirika. Mwenyewe alikubali bila ya wasiwasi
matamko ya Mapapa juu ya kanuni kama ufafanuzi rasmi wa wachungaji wakuu wa
Kanisa na wa shirika pia. Kielelezo cha Mt. Fransisko kilitakiwa kuzingatiwa na
wote kwa umoja, bila ya kupishana kuhusu namna ya kukitazama. Kwa ajili hiyo
alitunga kitabu rasmi cha maisha yake kilichopitishwa na mkutano mkuu hata
ukaagiza maandishi yote yaliyotangulia yatekelezwe. Ndivyo shirika lilivyopotewa
kwa muda mrefu na habari nyingi muhimu juu ya mwanzilishi. Kitabu alichokiandika,
bila ya kusema uongo, kinaleta baadhi tu ya matendo na mafundisho ya Mt.
Fransisko yaliyochaguliwa kwa makini ili kumchora kama mfano kamili wa Kristo
msulubiwa na kusisitiza mang’amuzi yake bora ya kiroho, lakini kwa kuficha
mambo fulanifulani kuhusu kipeo cha udogo. Aliheshimu ufukara kama sifa kuu na
utukufu wa shirika, ingawa alijali mabadiliko yaliyotokea, yaani konventi kubwa
mijini n.k. Kwake elimu pamoja na utume ni sehemu ya lazima ya utendaji wa
Kifransisko. Kwa ajili hiyo alikubali ruhusa lilizopewa shirika, ingawa kwa
udogo alipenda kupatana na Maaskofu na maparoko. Basi, chini ya uongozi wake
shirika likatulia, kwa jinsi alivyoweza kulinganisha upendo kwa Mt. Fransisko na
furaha kwa mabadiliko, hamu ya kuishi upwekeni muda mrefu pamoja na ndugu “wa
Kiroho” na utetezi wa konventi za mijini.
Hata kwa nje shirika likazidi kuheshimiwa na kushika
nafasi katika maisha ya Kanisa (utume mbalimbali, uchaguzi wa Papa, Mtaguso mkuu).
Mt. Bonaventura akafa akiwa Kardinali, wakati wa Mtaguso II wa Lyons, ambao
ulionyesha hatari kwa mashirika ya Ombaomba, kwa kuwa ulipitisha hati ya
kuyafuta yote isipokuwa Wadominiko na Wafransisko, pamoja na Waaugustino na
Wakarmeli. Lakini iliwabidi hao wapatane na wanajimbo kwa kujinyima baadhi ya
ruhusa walizopewa. Hata hivyo Mapapa waliofuata wakaendelea kuwarudishia au
kuwanyang’anya tena, mpaka Mtaguso wa Vienne (1311-1312) ulipofaulu kuwatungia
sheria ya kudumu baada ya miaka mia ya mashindano: kwamba kuhusu maisha yao ya
ndani na uongozi watawa wawe chini ya Papa moja kwa moja, ila kuhusu utume nje
ya makanisa yao wawe chini ya Maaskofu na maparoko.
Mambo
yakawa magumu zaidi ndani ya shirika, hata suala la ndugu “wa Kiroho” likawa
zito kwa Kanisa lote. Mwelekeo wao ulianza kutia wasiwasi ulipoingiwa na unabii
na mafundisho yaliyolaaniwa ya abati Yohakimu wa Fiore (+1202). Huyo aligawa
historia katika nyakati tatu: ule wa Baba tangu Adamu hadi Kristo (ulioongozwa
na watu wa ndoa), ule wa Mwana tangu Kristo hadi kipindi cha Yohakimu (ulioongozwa
na makleri); hatimaye ule wa Roho Mtakatifu utakaoongozwa na watawa na kupindua
Ukristo kwa kufuta uongozi wa Kanisa, sakramenti na sheria ili kuanzisha Kanisa
la Kiroho, la furaha, upendo na uhuru kama matunda ya maisha ya kujikatalia.
Shirika jipya la watu “wa Kiroho” litakuwa kielelezo cha maisha ya Kikristo.
Wakati mpya utatangazwa na malaika wa mhuri wa sita, mwenye alama ya Mungu aliye
hai na mleta Injili ya milele, yaani ya Kiroho. Wafransisko wengi wakachangamka
na kumuona Fransisko kuwa ndiye malaika mwenye alama ya madonda matakatifu na
mleta Injili ya milele, yaani kanuni yake! Ndugu Wadogo wakajiona kuwa shirika
hilo jipya ambalo lilete Kanisa la Kiroho lenye kufuata ufukara. Hapo jina
“ndugu wa Kiroho” likawa na maana mpya na kuwaelekeza kupinga uongozi wa
Kanisa, kuanzia Mtaguso II wa Lyons, walipojiandaa kukataa maagizo waliyoambiwa
watapewa kinyume cha haki.
Ufransisko uliathiri vilevile mwelekeo wote wa sanaa ya Magharibi. Ukiitikia vizuri matarajio yote ya kidini na ya kijamii ya kipindi cha mageuzi, ulieneza mtazamo mpya wa maisha unaojali mtu na viumbe vyote. Hivyo ulichangia sana upatikanaji wa mitindo mipya na njia mpya za kufurahia uzuri, ingawa bila ya kupotewa na imani. Fasihi ya Kifransisko inapenda kusimulia, tunavyoona katika maisha ya mwanzilishi yaliyoandikwa na wafuasi wake; uchorahi unaonyesha sura halisi ya kwake na ya wengineo; hata ujenzi unafuata njia mpya, hasa kufuatana na kielelezo cha kanisa la Mt. Fransisko huko Asizi. Hata katika ujenzi wa nyumba zao Ndugu Wadogo waliweza kuzingatia ufukara bila ya kupuuzia uzuri, kiasi kwamba upendevu wake unavutia wengi hadi leo.
1.2.
MAREKEBISHO KUENDELEA (1517-1762)
1.2.1.
MATAWI MAPYA KUCHIPUKA
Utengano
wa Waoservanti na Wakonventuali ulitatua tatizo moja, lakini haukufaulu
kuunganisha makundi yaliyorekebishwa, ingawa Papa alikuwa ameagiza itungwe mara
katiba moja kwa yote. Baadhi yalidumu kuwa na kanda zao, Waoservanti wa Italia
wakaikataa katiba hiyo wakaendelea kuirekebisha mfululizo ile maalumu ya kwao,
na kanda nyingine zilijitungia vilevile na kuzidisha tofauti shirikani.
Kilichohatarisha zaidi umoja ni utaifa uliochochewa na serikali mbalimbali kwa
faida ya siasa ya nchi zao dhidi ya nyingine. Wafalme waliingilia kwa njama na
vitisho masuala ya mikutano mikuu, sawa na walivyoingilia uchaguzi wa Papa,
lakini kila mara idadi iliwapa ushindi Wahispania, hata washindani wao (Wafaransa)
wakagoma kuhudhuria mara kadhaa.
Matatizo
mengine yalihusu maisha yenyewe, hasa ufukara. Waliolazimika kujiunga na
Waoservanti, na wale wasioacha kutumia fadhili walizokuwanazo wakiwa
Wakonventuali, walikataa kurekebishwa. Kinyume chake, wengine hawakuridhika tena
na namna OFM ilivyoshika kanuni, wakadai ruhusa ya kuishika kabisa. Ndivyo
walivyofanya watawa wa mashirika mbalimbali, kwa kuwa haja ya urekebisho
ilitambulikana na wote katika Kanisa la karne ya XV na ya XVI. Kwa namna ya
pekee Ndugu Wadogo walichochewa kufanya hivyo na sura ya X ya kanuni pamoja na
wasia. Ndiyo sababu Mt. Bonaventura aliona haja ya kuwepo makao ya upwekeni
katika kila kanda ili kuwaachia uhuru wa kuishi hivyo wale wapendao. Kumbe
Waoservanti wengi na baadhi ya viongozi wao hawakukubali kuwaachia wenye bidii
uhuru huo, kwa sababu ingekuwa sawa na kukiri kwamba wamelegea. Hivyo
wakawatenda ndugu hao kama Wakonventuali wa zamani walivyowatenda Waoservanti wa
kwanza. Walioamini urekebisho unaweza kutoka kwa viongozi wakaja kujionea
haiwezekani. Miundo iliyoanza kama urekebisho ikajikuta inajaribu kuzuia juhudi
za waliopenda urekebisho, na viongozi wa shirika lililoanza kwa kushindana na
viongozi wakawalaumu waliotaka kufanya vile wakisema eti, ni wakaidi tu! Kwa
kukosa busara na wema walisababisha waliotaka urekebisho wakafuate njia zao ili
kupata ruhusa walizozihitaji, kwa kumkimbilia Papa au viongozi wa serikali. Mara
nyingine Wakonventuali walipokea makundi hayo chini ya ulinzi wao ili kuwakomoa
Waoservanti waliokuwa wanawadharau wakijidai ndio wafuasi halisi wa Mt.
Fransisko. Ndiyo asili ya matawi mapya, hasa lile la kujitegemea la Wakapuchini.
Mwaka
1525 nd. Mateo wa Bascio alimkimbilia Klementi VII (1523-1534) ili kuruhusiwa
ashike kanuni, avae kanzu asili na kuhubiri huko na huko alivyotaka.
Alipokubaliwa, walijiunga naye ndugu wawili, Ludoviko na Rafaeli wa Fossombrone.
Mtumishi wa kanda aliwatafuta sana, lakini walilindwa vizuri na Katerina Cibo,
ndugu wa Papa. Ili kukwepa dhuluma, wakajiunga na Wakonventuali, halafu wakapewa
na Klementi VII haki ya kuwa na Mtumishi wao chini ya Mkuu wa Wakonventuali na
ya kupokea wanovisi (1528). Mapema walianza kuitwa Wakapuchini kutokana na kofia
yao kubwa. Upinzani wa Mkuu wa OFM dhidi yao haukufaulu; kinyume chake, kwa kuwa
alitaka kuzuia hata makao ya upwekeni ndani ya shirika, ndugu wengi wenye bidii
wakakata tamaa wakajiunga na Wakapuchini. Njama nyingine za kuwakomesha
zikashindikana, hivi kwamba mwaka 1535 walikuwa tayari 700. Ndipo aliposhika
uongozi wao nd. Bernardino wa Asti aliyelipa shirika jipya sura ya kiroho ya
kudumu, hasa kwa njia ya katiba iliyotungwa mwaka huo na kupitishwa mwaka
uliofuata.
Hatari
nyingine zilitokea ndani ya shirika, kwa ukaidi wa nd. Ludoviko, halafu kwa
uzushi wa mwandamizi wa nd. Bernardino. Hatimaye mambo yakatulia na tawi jipya
likazidi kustawi kiroho na kitume, ingawa Julius III (1550-1555) alikataza
Waoservanti wasihamie tena kwa Wakapuchini. Hivyo hawa wakazidi kujisikia
tofauti na Wafransisko wenzao. Mkutano mkuu wa mwaka 1552 ulionyesha kuwa juhudi
kali za awali zimeanza kutulia na kujilinganisha na maisha: shirika lilipanga
masomo na kuwa na watu maarufu upande wa elimu, utume na uongozi. Jambo muhimu
zaidi, lilimzaa mtakatifu wa kwanza, bradha Felix wa Cantalice (+1587),
kielelezo cha unyofu. Mtaguso wa Trento (1545-1563) ulisifu tawi hilo kama
urekebisho wa kufaa na wenye uaminifu kwa wito wake hata kustahili kutazamwa na
Kanisa kwa namna ya pekee. Shirika likazidi kukaza nidhamu ili kuzuia ulegevu,
likaanza kuenea ng’ambo ya milima ya Italia Kaskazini (1573). Ulipozuka
upinzani wa Wakonventuali, Kanisa lilikuwa limeshang’amua ubora wa Wakapuchini;
basi, Paulo V (1605-1621) alitamka kuwa ni Ndugu Wadogo halisi na wana wa Mt.
Fransisko sawa na matawi mengine (1608), halafu akawaondoa chini ya Mkuu wa
Wakonventuali na kuwapa Mtumishi wa kwao mwenye haki ya kuhesabiwa mwandamizi
halali wa mwanzilishi (1619). Kwa wakati huo shirika limeshazaa tena watakatifu
Serafino wa Montegranaro (+1604), bradha asiye na vipawa vingi kiutu bali mwenye
karama za ajabu, Yosefu wa Leonesa (+1612), padri Mkapuchini wa kwanza kutumwa
kwa Waturuki Waislamu halafu mhubiri bora Italia, na Mt. Laurenti wa Brindisi
(+1619), “mwalimu wa Kitume”, mtimilifu kuliko Wakapuchini wote kwa
utakatifu, elimu na utume. Wakafuata Mt. Fidelis wa Sigmaringen (+1622), wa
kwanza kutoka nje ya Italia, na wa kwanza kufia dini kati ya waliotumwa na Idara
ya Papa kwa Uenezaji wa Imani, halafu Mt. Bernardo wa Corleone (+1667), mwongofu
mwenye toba kali. Pia walipatikana wenye heri 6.
Kipindi
hicho ndicho cha ukomavu wa shirika, mitazamo ya Kiitalia ilipopanuka kwa kuenea
nje ya nchi na wanashirika waliposhika nafasi muhimu katika Kanisa. Baadaye
hakuna matukio ya maana zaidi, isipokuwa mengine ya kufaa na mengine yasiyofaa
ambayo yaliathiri shirika: idadi ya watawa na ya shughuli iliongezeka pamoja na
sifa kutoka kwa viongozi wa Kanisa na serikali, lakini zilizuka vurugu pia kama
ile ya utaifa (1636-1678). Benedikto XIV (1740-1758) aliamua mhubiri wa Papa awe
daima Mkapuchini, akasema, “Shirika la Wakapuchini linastahili yoyote yale,
kwa kuwa ndilo kielelezo pekee cha ukamilifu wa Kiinjili kilichobaki hadi
nyakati zetu”. Kweli urekebisho huo uliendelea kushika kikamilifu kanuni kwa
muda mrefu kuliko mengine yote. Nyumba ziliendelea kujengwa ilivyoagizwa toka
mwanzo, ndogo sana, nje ya miji na vijiji, zikielekeza ndugu kufuata ufukara na
unyofu hata ulimwengu ulipokazania fahari. Watakatifu wa kipindi hicho ni bradha
Krispino wa Viterbo (+1750), kielelezo cha furaha ya kiroho, Ignas wa Santhià
(+1770), padri mwenye bidii kwa wagonjwa na wakosefu, Ignas wa Lakoni (+1781),
bradha ombaomba aliyesaidia sana fukara, na Felix wa Nicosia (+1787), bradha
mtiifu ajabu, mbali ya mwenye heri 1.
Vilevile
Italia, ndugu waliojikusanya katika makao ya upwekeni kuanzia mwaka 1535 (mkutano
mkuu ulipowaruhusu ili kuzuia wengine wengi wasiwakimbilie Wakapuchini), kisha
kuongezeka waliwekwa moja kwa moja chini ya Mtumishi mkuu tu (1579), wakapewa
katiba maalumu (1595), ruhusa za pekee sana (1596), hatimaye Kiongozi mkuu na
mkutano mkuu wa kwao. Hivyo mamlaka ya Mtumishi wa OFM kwao ikawa jina tu. Kati
ya hao Wariformati katika kipindi hicho tunawakuta watakatifu mabradha watatu:
Mt. Benedikto Mwafrika (+1589), mtoto wa watumwa huko Italia, Mnegro wa kwanza
kutangazwa mtakatifu, Mt. Umile wa Bisignano (+1637), mnyenyekevu ajabu, na Mt.
Karolo wa Sezze (+1670), aliyeandika vizuri sana kuhusu maisha ya kiroho; halafu
mapadri Mt. Pasifiko wa San Severino (+1721), aliyezingatia sana maisha ya sala,
na Leonardo wa Portomaurizio (+1751), tunda bora la Kirekebisho kilichoanzia
mjini Roma karne ya XVII. Pia walipatikana wenye heri 4.
Huko
Hispania, baadhi ya wafuasi wa urekebisho wa Pekupeku, baada ya kuunganishwa na
Waoservanti (1517) walimkimbilia Mkuu wa Wakonventuali ili kukwepa vizuio vya
OFM, na mmojawao, Mt. Petro wa Alcantara (+1562) akafanywa Mkurugenzi wao
(1557). Alipokufa, Pius IV (1560-1565) akawahamisha Waalkantara chini ya
Waoservanti lakini bila ya kufuta kanda zao, katiba yao na mavazi yao maalumu.
Gregori XIII (1572-1585) akamkataza Mkuu wa OFM asiingilie masuala yao ya ndani
(1578), na Urbani VIII (1623-1644) akawaruhusu wasifuate tena katiba ya shirika
lote (1642). Jinsi sisitizo la sala na toba linavyozaa matunda imethibitishwa na
umisionari wao (Amerika na Asia Mashariki) na hasa na watakatifu 9 wa urekebisho
huo, wakiwa ni pamoja na Mt. Paskali Baylon (+1592), mwenye ibada ya pekee kwa
Ekaristi, wat. Petro Batista, Martino wa Kupaa na Fransisko Blanco, mapadri,
halafu Fransisko wa Mt. Mikaeli, Gonzalo Garcia na Filipo wa Yesu, mabradha,
ambao wote walifia dini Japani (+1597), hatimaye Mt. Yohane Yosefu wa Msalaba
(+1734), mpenda ufukara mkuu. Pia walipatikana wenye heri 22.
Huko
Ufaransa makao ya upwekeni hayakustawi sana hadi mwisho wa karne ya XVI. Mwaka
1601 walioishi huko wakapewa na Kanisa Mkurugenzi mwenye mamlaka pana sana; hapo
wakaenea haraka kwa msaada wa mfalme, hata kanda zote za Ujerumani na Uholanzi
zikajirekebisha na kujiunga nao, wakaitwa Warekoleti. Mmojawao
ni Mt. John Wall (+1679), aliyefia dini huko Uingereza.
Katika karne ya XVI na ya XVII karibu kila mkutano mkuu wa OFM ulizungumzia
katiba na kupigania umoja, ambao haukuwa rahisi kutokana na mchanganyiko wa
ndugu waliopenda fadhili za Wakonventuali na wengine waliotaka urekebisho.
Katika hali hiyo Watumishi wakuu walijitahidi kuhuisha shirika lote, lakini
wengi wao walitumwa na Mapapa kama mabalozi kwa wafalme na Maaskofu wa Ulaya, au
walipewa uaskofu wa miji muhimu. Shirika halikupendezwa kwa sababu lilikuja
kukosa uongozi imara: ndiyo maana mara kadhaa liliwadai kiapo cha kutokubali
kazi hizo au walau cha kujiuzulu Utumishi. Watakatifu waliopatikana kipindi
hicho ni: Mt. Salvatore wa Horta (+1567), bradha aliyefanya miujiza mingi ajabu
(labda milioni moja), wat. Nikolaus Pieck, Jeromu wa Weert, Teodoriko van der
Eem, Nikasi wa Heeze, Wilehadi wa Denmaki, Godefrid wa Melveren, Antoni wa Weert,
Antoni wa Hoornaert, Fransisko wa Roye, mapadri, halafu Petro wa Assche na
Korneli wa Wijk-bij-Durstede (+1572), mabradha, ambao wote walifia dini Uholanzi,
Mt. John Jones (+1588), aliyefia dini Uingereza, hatimaye Fransisko Solano
(+1610), mmisionari bora Amerika Kusini aliyezunguka kotekote kwa miaka 14,
akihubiri na kuimba. Wenye heri wa kipindi hicho ni 17.
Karne ya XVII ikawa ya utulivu na utendaji, lakini ongezeko kubwa mno la
watawa lilisababisha matatizo makubwa na ulegevu hata katika marekebisho. Pamoja
na utaifa kuzidi, matawi ya Italia yalishindana kwa maandishi makali ya kukwaza.
Makwazo mengine yalitokana na desturi ya Watumishi kadhaa kutuma watawa wasiofaa
kwenye kanda nyingine au kuwaacha nyumbani mwa marafiki au ndugu. Badala ya
juhudi za watawa kwa ajili ya kanuni kama katika karne zilizopita, sanasana
tunakuta viongozi wakijitahidi kuwalazimisha washike kanuni, lakini bidii za
namna hiyo hazikuweza kufanikiwa kwa kuwa hazikutoka moyoni mwa watawa. Hatimaye
mwaka 1676 mkutano mkuu ulikubali na kuagiza kila kanda ianzishe makao 3-4 ya
upwekeni ambapo yafanyike malezi ya watakaji na wanovisi wote: baadaye katika
mazingira hayo walistawi wat. Thomas wa Cori (+1729), mhubiri maarufu na Teofilo
wa Corte (+1740), mwanafunzi wake. Lakini katika karne ya XVIII ilionekana wazi
jinsi matazamio ya wengi yalivyolenga kupata kwa visingizio vyovyote fadhili na
nafasi za kwanzakwanza. Kupitia
mikutano mikuu upuuzi wa namna hiyo uliathiri sheria za shirika. Pia mabadiliko
mengi mno ya katiba, badala ya kusaidia nidhamu, yalizidi kuipunguza kwa
kusababisha ndugu wasiijali katiba isiyodumu.
Upande
wa Wakonventuali, utengano na Waoservanti haukuwaondolea baadhi yao wasiwasi
kuhusu utekelezaji wa kanuni, ingawa Mtaguso wa Trento ulitamka (1563) kwamba
OFM na Wakapuchini tu hawaruhusiwi kuwa na mali hata kishirika, tofauti na
Wakonventuali na mashirika mengine yote. Uhusiano na matawi yaliyokimbilia chini
ya Mkuu wao ili kufuata urekebisho ulichochea hamu ya kuwaiga. Ndivyo
walivyoanza Wakonventuali wa Urekebisho Hispania: uenezi wao ulichangia uamuzi
wa Mt. Pio V (1566-1572) wa kuunganisha na OFM Wakonventuali wote wa Hispania na
Ureno (1566-1567). Juhudi za mikutano, za Watumishi wakuu na za watawa wenyewe
zilileta nidhamu na ustawi, hasa mmojawao alipochaguliwa kuwa Papa Sisto V
(1585-1590) akaanza kuwasaidia kwa kila njia, kama vile kuunganisha chini ya
Wakonventuali marekebisho madogo yaliyokuwa yameanza Italia (1562). Ila mwaka
1669 yakaja kutawanywa, baada ya kusumbuliwa sana na Wakonventuali wa kawaida na
Wakapuchini (kuhusu sare zao zilizofanana). Kabla ya hapo mkutano mkuu ulitunga
katiba mpya kabisa (1625) ili kuondoa misimamo tofauti kuhusu kanuni: katiba
hiyo haikufuata matamko ya zamani ya Mapapa juu ya kanuni, bali ilipitisha moja
kwa moja desturi za shirika zilivyokuwa. Baada ya kuthibitishwa na Urbani VIII,
Wakonventuali wakaanza kuweka nadhiri zao kwa kutamka wazi kuwa watashika kanuni
“kadiri ya katiba ya Urbani” tu.
Baada
ya kujipatia hivyo msimamo wa kudumu, Wakonventuali wakazaa mwenye heri 1 na
watakatifu 2 waliong’aa mmoja hasa upande wa sala, mwingine upande wa utume:
Mt. Yosefu wa Copertino (+1663) na Mt. Fransisko Antonio Fasani (+1742), wote
mapadri. Pia shirika liliendelea kusifiwa upande wa elimudini likaona mtawa wake
mwingine kuwa Papa (Klementi XIV, 1769-1774) ambaye naye alilipendelea sana,
k.mf. kwa kuwahamisha Waoservanti wote wa Ufaransa chini ya Wakonventuali. Kwa
mara nyingine upendeleo huo ukazaa chuki ya wengine ilivyojitokeza kisha kufa
kwake.
Takwimu
ya jumla ya Utawa I ni kama ifuatavyo:
|
Matawi |
Mwaka
1575 hivi |
Mwaka
1700 hivi |
Mwaka
1762 hivi |
|
(Waoservanti) |
32,750 |
36,400 |
39,900 |
|
(Pekupeku) |
1,700 |
6,600 |
7,000 |
|
(Wariformati) |
500 |
13,900 |
19,000 |
|
(Warekoleti) |
50 |
9,200 |
11,000 |
|
OFM
jumla |
35,000 |
66,100 |
76,900 |
|
Wakonventuali |
12,000 |
15,200 |
21,000 |
|
Wakapuchini |
3,600 |
27,300 |
34,000 |
|
Jumla kuu |
50,600 |
108,600 |
131,900 |
Bila
ya kujali tofauti kati ya tawi na tawi, karibu 60% walikuwa mapadri, ambao nusu
ya idadi yao walikuwa wahubiri, nusu “mapadri wa Misa na sufuria” tu.
Ongezeko lilipungua kwanza kutokana na Uprotestanti kuenea na kufuta kanda
kadhaa Ulaya Kaskazini, na utawala wa Kiislamu kuenea Ulaya Mashariki Kusini,
ingawa pande nyingine zilifidia. Karne yenye ongezeko la kasi zaidi ni ile ya
XVII: ndio mwanzo wa wasiwasi na hofu kwa viongozi wa Kanisa na serikali, kwa
kuwa mashirika mengine pia yalikua. Kuanzia mwaka 1634 Mapapa walichukua hatua
kuzuia upokeaji wa wanovisi na kupunguza konventi (Italia zilifungwa 24.2%),
hata kufikiria uwezekano wa kuwapeleka watawa vijana kupigana na Waturuki ili
kuwapunguza! Lakini hatua hizo hazikufanikiwa. Kuhusu uenezi, wakati wa kufikia
kilele cha idadi ya wanashirika mgawanyo ulikuwa ifuatavyo:
|
Nchi |
OFM |
OFMConv |
OFMCap |
Jumla |
|
Italia na visiwa |
26,000 |
10,700 |
15,700 |
52,400 |
|
Hispania na makoloni |
23,000 |
0 |
3,100 |
26,100 |
|
Ufaransa |
9,500 |
5,400 |
6,100 |
21,000 |
|
Ujerumani n.k. |
9,600 |
2,600 |
8,100 |
20,300 |
|
Ureno na makoloni |
4,000 |
0 |
0 |
4,000 |
|
Dola la Waturuki |
1,700 |
800 |
300 |
2,800 |
|
Polandi na Urusi |
1,500 |
1,500 |
0 |
3,000 |
|
Uingereza na Irelandi |
1,600 |
0 |
150 |
1,750 |
1.2.2. MAISHA NDANI YA SHIRIKA
Kadiri ya hati ya utengano (1517) Mkuu wa Waoservanti tu alikubaliwa
kuitwa Mtumishi mkuu, wakati yule wa Wakonventuali alipewa jina la Mwalimu Mkuu;
vilevile viongozi wa kanda. Lakini jina hilo jipya halikuja kutumika. Mkuu wa
Wakapuchini aliitwa Makamu (wa Mkuu wa Wakonventuali aliyetakiwa kumthibitisha
baada ya kuchaguliwa). Jina la “Mtumishi mkuu wa Shirika lote” lililotumiwa
na Mkuu wa OFM lilichukiwa na kulalamikiwa na Wakonventuali na Wakapuchini, hadi
Paulo V alipotamka kuwa hao wote ni wana halisi wa Mt. Fransisko, na Wakuu wao
ni waandamizi wake halali (1619). Hata hivyo mabishano ya wazi yakaendelea
kuhusu mlolongo wa uandamizi huo, mtindo asili wa kanzu na hasa kofia yake,
mpaka Aleksanda VIII (1689-1691) alipokataza maandishi yote juu ya hayo.
Kwanza Kardinali mlinzi alikuwa mmoja kwa wote, halafu Wakapuchini wakakubaliwa kuwa na mmoja wa kwao (1564), na vilevile Wakonventuali (1580). Mara kadhaa waliingilia mno masuala ya shirika hadi kulivuruga na kusababisha Mapapa walazimike kuwazuia. Mamlaka yao ilipungua ilipoanzishwa Idara ya Papa kwa Watawa (1586). Tofauti kati ya matawi kuhusu miundo ya nd