Historia ya Wafransisko

 

Ndugu Wadogo wa Kapelekesi (Mbeya) - Piccoli Fratelli a Kapelekesi (Mbeya) - Little Brothers at Kapelekesi (Mbeya)

Home Tuujue Mtaguso Mkuu Hystoria ya utawa Historia ya Wafransisko MASWALI JUU YA MASHAURI YA KIINJILI NANI MWABUDU SANAMU rosary HATUA TATU ZA MAISHA YA KIROHO Sala ya Moyo MATAKASO KABLA YA KUAHIDI MASHAURI YA KIINJILI 

 

 

Nd. Rikardo Maria, UNWA

 

 

HISTORIA YA WAFRANSISKO

 

 

 

JEDWALI LA FAMILIA YA KIFRANSISKO

 

 

 

 

 

 

 

 

1. UTAWA WA KWANZA

 

 

1.1. NDUGU WADOGO KUPAMBANA HADI KUTENGANISHWA (1226-1517)

 

1.1.1. MWANZO WA MAPAMBANO (1226-1318)

 

Mt. Fransisko alipokuwa hai alisongwa na kundi la Watumishi na wasomi wa utawa wake, likisaidiwa na viongozi wa juu wa Kanisa, ili alegeze masharti ya ufukara na kulinganisha zaidi shirika lake na yale ya zamani. Kwa karama yake ya pekee aliweza kukabili upinzani huo wote. Juhudi yake ya mwisho ya kuzuia shirika lisipotoke ni wasia aliouandika ili kusisitiza msimamo wake, kudai kanuni yake isifafanuliwe, pamoja na kukataza wanashirika wasimuombe Papa hati yoyote. Alipokufa utawa ukabaki mikononi mwa Watumishi hao, wakiongozwa na nd. Elia Bombarone, Mkuu wa shirika miaka 1221-1227, halafu 1232-1239.

Katikati ya hivyo vipindi vyake viwili vya uongozi, Mtumishi mkuu alikuwa nd. Yohane Parenti. Chini yake yalizuka mabishano makali kati ya walioshikilia wasia huo na wale waliotaka shirika lishindane na mashirika mengine. Yeye na Watumishi wengine wakadhani utatuzi unaweza kutokea kwa viongozi wa Kanisa tu. Akipokea ombi lao, Gregori IX (1227-1241) alitoa tamko rasmi la kwanza juu ya kanuni (1230), akitumia mamlaka yake ya Kipapa na pia ujuzi wake wa nia ya Mt. Fransisko (ndiye aliyemsaidia sana kutunga kanuni alipokuwa bado Kardinali, jina lake Ugolino). Upande wa ufukara kwa jumla alitetea msimamo wa mwanzilishi (kwa jinsi alivyomheshimu hata akamtangaza mtakatifu), ila aliulegeza kiasi, kwa lengo la kufanikisha zaidi utume wa Ndugu Wadogo na hivyo kurekebisha Kanisa lililokuwa na hali mbaya kiroho. Kwa ajili hiyo aliwapa hati na ruhusa nyingi za pekee dhidi ya mamlaka ya Maaskofu na maparoko. Kuhusu wasia alitamka kuwa si sheria inayowabana Wafransisko wasiweze kufafanua kanuni yao wala kufafanuliwa na Kanisa, wala kuomba wala kupewa hati na fadhili za Papa. Sababu ya msingi ni kuwa Kanisa liko juu kuliko kanuni.

Hivyo njia ikawa wazi kuligeuza shirika la wadogo walio wote sawa, wanaohubiri toba kwa unyenyekevu chini ya padri yeyote, liwe shirika imara la kikleri, lisilo chini ya Maaskofu isipokuwa kwa machache. Mageuzi hayo yalisababisha kwa muda mrefu upinzani mwingi wa Maaskofu na mapadri wanajimbo. Aliyesukuma sana shirika kufuata njia hiyo ni nd. Elia, ambaye alimjengea Mt. Fransisko kanisa zuri sana, halafu jirani nalo konventi kubwa mno, ili kushindana na abasia za Wabenedikto. Alimgeuza mwanzilishi kuwa fahari ya shirika badala ya kielelezo cha kufuatwa. Mwenye vipawa na elimu, ingawa bradha, aliathiri sana viongozi wa dini (Gregori IX) na wa siasa (Federiko II), alistawisha misheni huko Mashariki na kukuza nyumba za masomo, lakini pia alidhulumu vikali watetezi wa kanuni (hasa alimuacha nd. Kaisari wa Speyer afe kwa njaa kisha kumfunga). Bila ya kutembelea kanda za shirika, alishika uongozi wote mikononi mwake, akichagua Watumishi na walinzi, akihamisha ndugu, akituma wawakilishi wake huko na huko kusimamia kazi ya Watumishi, na akikataa kuitisha mkutano mkuu. Fahari zake binafsi, ushuru aliowatoza mfululizo Watumishi (kwa ajili ya ujenzi n.k.) vilisababisha wafanye njama dhidi yake, hadi Gregori IX akaitisha na kuendesha mkutano mkuu ambao ulimuondoa madarakani na kutunga sheria ili kupunguza mamlaka ya Mtumishi mkuu.

Nd. Aimoni wa Faversham, Mwingereza aliyeongoza upinzani, akaja kuwa Mtumishi mkuu (1240-1244), na kulipatia shirika sura ya kudumu kufuatana na mfano wa Wadominiko upande wa muundo, utume, masomo na liturujia. Taratibu za maisha zikazidi kufuata mitindo ya kimonaki, pamoja na watawa kujitafutia visingizio vya kisheria wasibanwe nazo. Makao ya kifukara ya upwekeni yalizidi kuachwa ili wanashirika wahamie nyumba kubwa za mijini, zenye makanisa makubwa ambamo wafanye utume, wakiwanyang’anya maparoko waamini na sadaka zao. Kama alivyofanya mwenyewe huko Paris, Ndugu Wadogo wakazidi kushika nafasi kwenye vyuo vikuu na vinginevyo, na kuwa na uzito mkubwa ndani ya Kanisa, jambo lililowasogeza mbali na udogo uliowapasa. Mabradha wakanyimwa kabisa nafasi za uongozi na kukubaliwa tu kutoa huduma ndogondogo za nyumbani (bustani n.k.), wakiwaachia raia huduma duni zaidi. Kazi za mikono nje ya konventi zilikatazwa; badala yake ile ya kuombaomba ikaja kusifiwa na kushika nafasi ya kwanza upande wa uchumi. Zilipangwa pia njia za hakika za kupata mahitaji, hasa kwa nyumba za masomo.

Alipokufa, nd. Kreshensi wa Iesi alishika nafasi yake (1244-1247), akatambua hali halisi, lakini hakuweza kuirekebisha (pia kwa sababu ya uzee wake). Akiona kwamba Mt. Fransisko alikuwa bado kielelezo cha wadogo, aliagiza zikusanywe habari zote juu yake, halafu akamuagiza nd. Thoma wa Celano aandike upya maisha ya mwanzilishi. Juhudi zake kwa ajili ya kushika njia ya kati hazikuridhisha wala upande mmoja (wenzi wa Mt. Fransisko na ndugu “wa Kiroho”, yaani wenye nia ya kushika kanuni kadiri ya Roho Mtakatifu) wala upande wa pili (“jumuia”, yaani waliopenda maisha katika konventi kubwa na hali ilivyo). Inosenti IV (1243-1254) alikubali kutoa tamko la pili juu ya kanuni (1245) ili kuilegeza. Hasa alifungua milango ili Ndugu Wadogo wajipatie vitu vingi, akitamka kuwa vyote walivyonavyo, kama si vya wafadhili tena, basi ni vya Papa. Hivyo kwa kutofautisha kutumia vitu na kuvimiliki kisheria, Ndugu Wadogo waliweza kujidai fukara ingawa wanatumia vingi, eti si vya kwao! Lakini wengi hawakuridhika na ujanja huo.

Akachaguliwa M.H. Yohane wa Parma (1247-1257), mtu wa kufaa sana kwa elimu na utakatifu, aliyeongoza hasa kwa mfano wa maisha yake bora. Alikusudia kurudisha shirika katika hali ya mwanzoni kufuatana na wasia, kwa kuheshimu Maaskofu na mapadri na kukataa fadhili za Papa. Alitembelea kwa miguu kanda zote akiamsha nia ya kushika kanuni na wasia. Hivyo mkutano mkuu (1254) ulisimamisha utumiaji wa fadhili kadhaa; lakini, alivyosema M.H. Egidi wa Asizi (+1262), juhudi hizo nzuri zilikuwa zimechelewa zisiweze kurekebisha shirika lote. Wapinzani walimshtaki M.H. Yohane, akalazimika kujiuzulu. Mkutano mkuu ulitaka aendelee, lakini mwenyewe hakurudi nyuma. Hatimaye walimuomba walau amchague mwandamizi wake, naye akamtaja Mt. Bonaventura wa Bagnoregio akaenda kuishi upwekeni.

Mt. Bonaventura (1257-1274), kufuatana na tabia yake, alikubali hali ilivyo na kujitahidi kuepusha shirika na hatari za nje na za ndani alizoziona mapema. Upinzani wa Maaskofu na maparoko dhidi ya Ndugu Wadogo ulikuwa umeungwa mkono na chuo kikuu cha Paris: hapo hazikupingwa tu ruhusa kadhaa walizopewa, bali msingi wenyewe wa mtindo wao na wa Wadominiko. Baada ya Mt. Bonaventura na Mt. Thoma wa Akwino kuutetea, Papa alilaani upinzani na kusifu sana mtindo wa Kiinjili. Mwalimu huyo kuchaguliwa kuwa Mtumishi mkuu kukawa ushindi mwingine mkubwa chuoni.

Mashambulizi ya kutisha zaidi yalitokea ndani, upande wa ndugu “wa Kiroho”. Mt. Bonaventura alijipangia kulinganisha uaminifu kwa kanuni na mabadiliko ya shirika, akionyesha hayo hayaendi kinyume cha nia ya mwanzilishi. Ili athibitishe hayo ilimpasa kuziondolea lawama msingi wowote kwa kupigania uaminifu kwa wito wa shirika. Mwenyewe alikubali bila ya wasiwasi matamko ya Mapapa juu ya kanuni kama ufafanuzi rasmi wa wachungaji wakuu wa Kanisa na wa shirika pia. Kielelezo cha Mt. Fransisko kilitakiwa kuzingatiwa na wote kwa umoja, bila ya kupishana kuhusu namna ya kukitazama. Kwa ajili hiyo alitunga kitabu rasmi cha maisha yake kilichopitishwa na mkutano mkuu hata ukaagiza maandishi yote yaliyotangulia yatekelezwe. Ndivyo shirika lilivyopotewa kwa muda mrefu na habari nyingi muhimu juu ya mwanzilishi. Kitabu alichokiandika, bila ya kusema uongo, kinaleta baadhi tu ya matendo na mafundisho ya Mt. Fransisko yaliyochaguliwa kwa makini ili kumchora kama mfano kamili wa Kristo msulubiwa na kusisitiza mang’amuzi yake bora ya kiroho, lakini kwa kuficha mambo fulanifulani kuhusu kipeo cha udogo. Aliheshimu ufukara kama sifa kuu na utukufu wa shirika, ingawa alijali mabadiliko yaliyotokea, yaani konventi kubwa mijini n.k. Kwake elimu pamoja na utume ni sehemu ya lazima ya utendaji wa Kifransisko. Kwa ajili hiyo alikubali ruhusa lilizopewa shirika, ingawa kwa udogo alipenda kupatana na Maaskofu na maparoko. Basi, chini ya uongozi wake shirika likatulia, kwa jinsi alivyoweza kulinganisha upendo kwa Mt. Fransisko na furaha kwa mabadiliko, hamu ya kuishi upwekeni muda mrefu pamoja na ndugu “wa Kiroho” na utetezi wa konventi za mijini.

Hata kwa nje shirika likazidi kuheshimiwa na kushika nafasi katika maisha ya Kanisa (utume mbalimbali, uchaguzi wa Papa, Mtaguso mkuu). Mt. Bonaventura akafa akiwa Kardinali, wakati wa Mtaguso II wa Lyons, ambao ulionyesha hatari kwa mashirika ya Ombaomba, kwa kuwa ulipitisha hati ya kuyafuta yote isipokuwa Wadominiko na Wafransisko, pamoja na Waaugustino na Wakarmeli. Lakini iliwabidi hao wapatane na wanajimbo kwa kujinyima baadhi ya ruhusa walizopewa. Hata hivyo Mapapa waliofuata wakaendelea kuwarudishia au kuwanyang’anya tena, mpaka Mtaguso wa Vienne (1311-1312) ulipofaulu kuwatungia sheria ya kudumu baada ya miaka mia ya mashindano: kwamba kuhusu maisha yao ya ndani na uongozi watawa wawe chini ya Papa moja kwa moja, ila kuhusu utume nje ya makanisa yao wawe chini ya Maaskofu na maparoko.

Mambo yakawa magumu zaidi ndani ya shirika, hata suala la ndugu “wa Kiroho” likawa zito kwa Kanisa lote. Mwelekeo wao ulianza kutia wasiwasi ulipoingiwa na unabii na mafundisho yaliyolaaniwa ya abati Yohakimu wa Fiore (+1202). Huyo aligawa historia katika nyakati tatu: ule wa Baba tangu Adamu hadi Kristo (ulioongozwa na watu wa ndoa), ule wa Mwana tangu Kristo hadi kipindi cha Yohakimu (ulioongozwa na makleri); hatimaye ule wa Roho Mtakatifu utakaoongozwa na watawa na kupindua Ukristo kwa kufuta uongozi wa Kanisa, sakramenti na sheria ili kuanzisha Kanisa la Kiroho, la furaha, upendo na uhuru kama matunda ya maisha ya kujikatalia. Shirika jipya la watu “wa Kiroho” litakuwa kielelezo cha maisha ya Kikristo. Wakati mpya utatangazwa na malaika wa mhuri wa sita, mwenye alama ya Mungu aliye hai na mleta Injili ya milele, yaani ya Kiroho. Wafransisko wengi wakachangamka na kumuona Fransisko kuwa ndiye malaika mwenye alama ya madonda matakatifu na mleta Injili ya milele, yaani kanuni yake! Ndugu Wadogo wakajiona kuwa shirika hilo jipya ambalo lilete Kanisa la Kiroho lenye kufuata ufukara. Hapo jina “ndugu wa Kiroho” likawa na maana mpya na kuwaelekeza kupinga uongozi wa Kanisa, kuanzia Mtaguso II wa Lyons, walipojiandaa kukataa maagizo waliyoambiwa watapewa kinyume cha haki.

Upinzani ukalipuka hasa baada ya Nikola III (1277-1280) kutoa hati nyingine juu ya kanuni (1279) ili kuwaondolea Ndugu Wadogo wasiwasi wowote kuhusu namna ya kuitekeleza, pamoja na kuwatetea dhidi ya maadui wa nje. Hati hiyo inafuata kabisa msimamo wa Mt. Bonaventura. Jambo muhimu zaidi ni kutofautisha matumizi ya vitu na haki ya kuvitumia: Ndugu Wadogo hawana haki ya kutumia kitu, ila wanaruhusiwa kuwa na matumizi kadiri ya ufukara na uduni. Fundisho hilo likasababisha mabishano makali mno kwa miaka mingi, kuanzia Ufaransa Kusini. Viongozi wa shirika mara walijaribu kukomesha upinzani huo, mara waliuunga mkono. Mapapa walitumia nguvu, isipokuwa Mt. Selestini V (1294), aliyetazamwa kuwa “Papa wa kimalaika” atakayeanzisha Kanisa la Kiroho. Yeye aliwaruhusu waliotaka wajitenge na jumuia na kuishi upwekeni wakifuata kanuni bila ya kujali matamko ya Kanisa. Alipojiuzulu, mwandamizi wake Bonifasi VIII (1295-1303) alimtenga kiongozi wao, nd. Anjelo Klareno (+1337), kama mzushi. Hapo wakaanza kudai ubatili wa kujiuzulu kwa Selestini V na wa kuchaguliwa Bonifasi VIII; halafu wakadai Mapapa waliotoa matamko juu ya kanuni kuwa wazushi. Kinyume na mtangulizi wake, Klemensi V (1305-1314) alipenda kusikiliza wote, halafu akatoa (1312) tamko jipya juu ya kanuni ili kuondoa wasiwasi hasa kwa kubainisha amri za kanuni na kiasi ambacho zinawabana Ndugu Wadogo. Pia akawaweka ndugu “wa Kiroho” chini ya ulinzi wake; viongozi waliowadhulumu waliondolewa, na makosa dhidi ya ufukara yalirekebishwa ili kukwepa farakano. Lakini ikawa bure: mwaka 1317 uasi ukawa wazi usijali kutengwa na Kanisa wala kuchomwa moto. Waklareno wakaendelea hivyo zaidi ya miaka mia mpaka wat. Yohane wa Capestrano na Yakobo wa Marka walipowapatanisha na Kanisa (1430 hivi), nao wakarudi chini ya Mtumishi wa shirika lote (1473).

 

1.1.2. MAREKEBISHO NA UTENGANO (1318-1517)

 

Shirika lilipitia hatari kubwa kuliko zote za historia yake liliposhindana miaka 13 na Yohane XXII (1316-1334). Kiburi kilichowapata Ndugu Wadogo katika karne yao ya kwanza, kutokana na mafanikio yao na mashindano na Maaskofu, kikafikia upeo walipopingwa na Papa pia. Kisa chake ni dhana ya kuwa Kristo na mitume hawakumiliki chochote wala binafsi wala kwa pamoja. Dhana hiyo ililaaniwa na Kanisa, kinyume cha msimamo wa shirika. Badala ya kukubali uamuzi huo, Mtumishi mkuu nd. Mikaeli wa Cesena (1316-1328) na wanashirika karibu wote wakaukataa hata kumtangaza Yohane XXII kuwa mzushi. Mfalme mkuu wa Ujerumani akalipokea shirika chini ya ulinzi wake ili apate nguvu dhidi ya Papa, hata akafanya ndugu mdogo mmojawapo atangazwe kinyume cha sheria kuwa ni Papa badala ya Yohane XXII (bado hai). Baadaye kidogo uasi ukaisha, lakini matokeo ya kwazo kubwa hivi yalichangia sana kudidimia kwa shirika.

Matukio mengine ya nje yaliyochangia ni: vita vya miaka mia (1339-1453) katika sehemu kubwa ya Ulaya; tauni (1348-1350) iliyoua thuluthi mbili za wanashirika (matokeo yake waliobaki walikusanyika katika konventi kubwa zenye hali nzuri zaidi kiuchumi, walipunguza utume na kupokea miito bila ya kuichuja); farakano la Kanisa la Magharibi (1378-1418) lililoleta fujo na utovu wa nidhamu; hatimaye kufifia kwa tunu bora za karne za kati. Upande wa ufukara uamuzi wa Yohane XXII wa kulinganisha Ndugu Wadogo na mashirika mengine ulisababisha hao wasimamie mali na kutumia pesa (hata za binafsi) kinyume cha kanuni. Kilele cha fujo kikawa miaka ya farakano la Magharibi, ambapo kwa wakati mmoja kulikuwa na Watumishi wakuu wawili au watatu, kila mmojawao akimfuata Papa wa Roma, au yule wa Avinyoni au hatimaye yule wa Pisa. Hata hivyo baadhi yao waliongoza vizuri na kuchangia amani ya Kanisa hadi ulipopatikana umoja wake na wa shirika mwaka 1418.

Pamoja na matatizo hayo yote, kuanzia mwaka 1334 baadhi ya wanashirika Italia, halafu Hispania na Ufaransa, walijiombea ruhusa ya Mtumishi mkuu au ya Papa waweze kuishi kijumuia kadiri ya kanuni, bila ya kutumia fadhili za kuilegeza. Wakati huo marekebisho ya namna hiyo yalitokea hata katika mashirika mengine, ingawa kwa kiasi kidogo zaidi. Ni kwamba kati ya Wafransisko kuna utata wa kudumu kuhusu namna ya kulinganisha kipeo asili na maisha halisi, au sehemu mbalimbali za karama ileile: katika karne ya XIV na XV utata huo ulisababisha mapambano ya kishujaa. Walioanzisha urekebisho walikuwa watawa (wengi wao mabradha wasio na elimu) wasioridhika na hali ya shirika. Wakililia hali ya mwanzoni, walilaumu maisha ya wenzao na uongozi wa Watumishi. Hao waliitikia kwa ukali wakijisingizia wanapaswa kudumisha nidhamu na kutetea haki ya walio wengi ya kutumia ruhusa za Kanisa. Kwa kawaida waanzilishi wa marekebisho hawakuwa watakatifu, bali nia yao ilichanganyikana na upungufu wa unyenyekevu na utiifu. Wakidai haki ya kufuata kanuni “Kiroho” kadiri ya sura ya 10, walikimbilia ngazi za juu kwa msaada wa wanasiasa ambao – sawa na watu wa kawaida – kila mara walipendelea urekebisho. Kisha kukubaliwa, marekebisho yakavuta miito bora: k.mf. kati ya mwaka 1402 na 1416 walijiunga na Waoservanti Bernardino wa Siena, Mt.Yohane wa Capestrano, nd. Alberto wa Sarteano na Mt. Yakobo wa Marka ambao wanaitwa “nguzo nne za Oservansya (= kushikakanuni)”. Marekebisho yote, pamoja na kusisitiza ufukara, yalijali sana kimya na sala ya moyo upwekeni. Kama tunda la maisha ya namna hiyo yalifanya pia kazi kubwa tena bora ya kuhubiri, na hivyo kurudisha ule uwiano aliokuwa nao mwanzilishi. Mwishowe haki ya kushika kanuni kiaminifu ikatambulikana na Kanisa.

Mahali pa kwanza walipokusanyika ni makao ya upwekeni ya Brogliano karibu na Asizi. Aliyestawisha zaidi kwanzia mwaka 1368 ni nd. Paolucho Trinci (+1390), bradha aliyefanywa mkurugenzi wa jumuia zilizofuata urekebisho Italia, akiwa na haki ya kupokea wanovisi na kuanzisha nyumba nyingine. Dhidi ya upinzani wa Watumishi, Mtaguso wa Konstans (1415) uliwaruhusu Waoservanti kuenea katika kanda zote za shirika, kupokea wanashirika wote watakaopenda kujiunga nao, tena kuwa na kiongozi maalumu, yaani Watunzaji wao wawe chini ya mmojawao kama makamu wa Mtumishi mkuu badala ya kubaki chini ya Watumishi wa kanda. Hata hivyo marekebisho mengine yaliyokwishaanza (Wavilyakresi, Wakoleta, Waamadei na Waklareno) hayakupenda kujiunga na Waoservanti. Wakonventuali walipinga vikali uamuzi wa Mtaguso, na juhudi za Mapapa hazikuweza kurudisha amani, kwa kuwa hao hawakukubali kurekebishwa, wala Waoservanti kukaa chini yao. Wakati majaribio mbalimbali yalipoendelea kushindikana, Oservansya ikaenea na kustawi, hadi Eugeni IV (1431-1447) alipoiruhusu kujifanyia mikutano mikuu na ya kanda ili kujichagulia viongozi (1446). Ushindi mwingine ukawa tangazo la kuwa Bernardino wa Siena, Mkuu wake wa kwanza, ni mtakatifu (1450).

Leo X (1513-1521) alifanya jaribio la mwisho alipoitisha mkutano mkuu wa wote pamoja (1517), wakiwa na viongozi wa marekebisho mengine. Wakonventuali wakakataa tena shirika lote lisifuate urekebisho wala kuongozwa na Mwoservanti. Basi, Papa akaamua kuwatenganisha moja kwa moja, na kupindua uhusiano kati yao: Waoservanti wawe na hadhi ya kuwa ndio shirika halisi (OFM), wakati waliotetea maisha yaliyofuatwa katika konventi kubwa wakakubaliwa kuendelea nayo kwa kutumia fadhili halali walizopewa, lakini kama tawi tu (OFMConv). Alimlazimisha Mtumishi mkuu wa Wakonventuali kujiuzulu na kukabidhi mhuri wa shirika kwa Waoservanti, ambao Mtumishi wao aitwe Mtumishi mkuu wa shirika lote, likiwa ni pamoja na marekebisho mengine. Wakonventuali wasishiriki tena uchaguzi wa Mtumishi mkuu, wala kiongozi wao asiitwe Mtumishi bali Mwalimu mkuu tu! Hata hivyo wasisumbuliwe kwa kutumia fadhili walizopewa na Kanisa. Waoservanti wabaki na nyumba zao, na Wakonventuali na nyumba zao, bila ya kuvuka toka upande mmoja kwenda upande mwingine.

Ingawa hakuna takwimu ya wanashirika kabla ya karne ya XVII, tunaweza kuwakadiria kutokana na idadi ya nyumba na ya wastani wa ndugu walioishi katika nyumba:

mwaka

ndugu

1226

5000

1300

40000

1400

25000

1517

50000 na zaidi (elfu 20 au 25 Wakonventuali na 30 au 32 Waoservanti)

 

1.1.3. MAISHA NDANI YA SHIRIKA (1226-1517)

 

Kujua maisha ya ndani ya shirika lolote ni muhimu kuliko kujua matukio makuu ya miundo yake. Basi, tuone jamaa ya Ndugu Wadogo ilivyoendelea kwa ndani katika karne tatu za kwanza tulizokwishaziona.

Baada ya kifo cha mwanzilishi wanashirika walizidi kumiminika mijini, katika konventi kubwa zaidi na zaidi, na zenye sura ya kimonaki zaidi na zaidi (kanisa kubwa, ukumbi wa mikutano, ua, bustani na kuta za kandokando…). Kanuni iliendelea kuzingatiwa, lakini kwa mtazamo wa kisheria, kufuatana na matamko ya Mapapa juu yake. Ufukara mkuu ukaja kuwa sifa maalumu za kujitangazia shirika bora kuliko mengine, pamoja na kujipongeza kwa kuwa na mwanzilishi aliye Kristo wa pili, mtakatifu kuliko wengine (tazama ngao ya shirika ya karne ya XV yenye msalaba iliposulibiwa pamoja mikono ya Kristo na Fransisko). Lakini utekelezaji ukawa wa kinafiki sana, k.mf. tendo la ndugu kusafiri na boi ambaye amchukulie pesa asije akazigusa mwenyewe lilihukumiwa tayari na katiba ya Narbona (1260) iliyotungwa kama kinga ya kanuni, halafu ikarekebishwa mara nyingi ili kudhibiti makosa yaliyojitokeza pamoja na kudumisha usawa katika sura ya nje ya watawa na katika matumizi ya kila siku.

Kimya kilichosisitizwa na Mt. Fransisko kama sharti la sala, kikaja kuratibiwa kwa mfano wa monasteri: kwamba kimya kikuu kiwe cha kudumu katika kanisa, maktaba, vyumba vya kulala, ua na mezani wakati wa kula. Zaidi ya hicho, kitunzwe daima na popote kimya cha Kiinjili, yaani kukwepa maneno yoyote yasiyofaa (Math. 12:36). Katiba haikuzungumzia maburudisho, lakini sikukuu zilikuwa na nafasi za kufurahia udugu (vyakula na divai, nyimbo, maigizo na michezo), ingawa ilikatazwa mara nyingi ndugu wasipite kiasi. Hatujui vitendo vya toba vya kijumuia vilipoanza; lakini mwanzoni mwa karne ya XIV Ndugu Wadogo walikuwa wakijipiga mijeledi kila siku ya Kwaresima, halafu mara tatu kwa juma nyakati nyingine. Adhabu alizozitoa mwanzilishi zikaja kuongezwa chini ya nd. Eliya hata kuratibiwa na sheria. Mapema ulifuatwa mfano wa Wadominiko wa konventi zote kuwa na magereza, ila yajali utu. Wasiojirekebisha wafukuzwe shirikani.

Mpaka mwaka 1239 ndugu wakleri na mabradha waliishi kwa usawa alivyotaka Mt. Fransisko. Baadaye shirika likabadilika na kuwa la kikleri. Sababu ni mbalimbali: heshima kubwa ya mwanzilishi kwa mapadri, ongezeko la mapadri kwa idadi na ubora, chuki ya wengi kwa sera ya nd. Eliya aliyependelea mabradha wenzake katika uongozi. Miaka miwili tu baada ya kumuondosha, mabradha wakajikuta hawaruhusiwi tena kuwa na cheo chochote, halafu ikakatazwa wasipokewe tena shirikani, isipokuwa kwa sababu ya pekee. Pia mabradha walifungiwa kabisa mlango wa ukleri kwa kufafanua visivyo maneno ya kanuni yasemayo, “wasio na elimu wasijisumbue kusudi waipate”. Basi, baada ya katazo la kufanya kazi za mikono nje ya konventi kama zamani, sura ya bradha Mfransisko ikawa kwa karne nyingi ile ya mtu ambaye hana sauti wala kura, amekusudiwa kutoa huduma za konventini na kuombaomba, ambaye heshima yake kubwa ni kuwatumikia wanashirika mapadri. Hivyo miito ya namna hiyo haikutoka tena kwa watu wenye elimu wenye kulenga utakatifu wa Kifransisko, bali kwa watu wadogo, wasiojua kusoma, wasio na mbele wala nyuma, ambao wengi wao waliingia utawani kujitafutia tu maisha ya hakika. Hapo ilibidi wachujwe sana. Kwa njia hiyo sura ya ndani ya jamaa ilibadilika sana, kwa kuwa na matabaka yenye kazi tofauti, haki tofauti na malezi tofauti. Ila marekebisho yakajaribu kurudia hali ya mwanzoni.

Baadaye ikatokea migawanyiko mingine kati ya waliopewa na wasiopewa fadhili, yaani ruhusa za pekee. Kwanza zilitolewa kwa walimu na wanafunzi ili kustawisha masomo katika ngazi za juu, halafu katika ngazi ya kati na ya chini. Wakaja kuongezwa waliowahi kuwa na vyeo, wazee na hatimaye wahubiri. Malalamiko yakawa mengi, hasa walionyimwa walipokosa hata mahitaji yao, ingawa wagonjwa waliendelea kushughuliwa vizuri, na haki zao zilitetewa na sheria. Utaratibu wa kimonaki wa kuwapanga watawa kufuatana na muda wa kukaa utawani, uliokataliwa mwanzoni ukajipenyeza shirikani; hata katika hilo, na katika kuwapa viongozi heshima kubwa za nje, marekebisho yakarudia usahili wa mwanzoni.

Mt. Fransisko aliwazoesha wafuasi wake kuwa wazi kati yao, kuelezana habari za safari, kujishtaki kwa unyenyekevu na kuomba msamaha. Ndiyo asili ya “mkutano wa makosa” ambao uliagizwa na katiba (1260) mara moja kwa wiki, ukifuatwa na mkutano wa jumuia uliojadili masuala ya pamoja. Mpango wa mwanzilishi wa kuwatuma wafuasi wake ulimwenguni wawiliwawili uliendelea, ila kwa shabaha ya kulindana bila ya kuaminiana, badala ya kushuhudia umoja wa kidugu na kusaidiana. Malezi kwa jumla yalilenga zaidi maisha ya ndani kuliko kwenda ulimwenguni, jambo lililotarajiwa kuwa la nadra tu. Mipango ya kwanza kwa malezi iliratibiwa na katiba (1260). Walezi walisaidiwa na vitabu kadhaa, hasa “Kielelezo cha Nidhamu” cha Bernardo wa Besse (+1300 hivi) ambacho kinalenga nidhamu, adabu njema, usafi na taratibu za kimonaki kuliko mitindo ya Kifransisko. Baada ya kumaliza unovisi, watawa wapya waliendelea kulelewa walau miaka mitatu, ingawa kazi hiyo ilionekana mapema kuwa ngumu sana. Sehemu mbalimbali (hasa Wakonventuali) walianza kupokea watoto wadogo kama walivyofanya wamonaki.

Toka mwanzo kazi za Ndugu Wadogo zilikuwa tatu: sala, kazi za mikono na mahubiri; uvivu ulikuwa tishio kwa mwanzilishi na viongozi wengine. Mt. Bonaventura alipochaguliwa aliwaandikia mara wanashirika wote ili kuwaonyesha hatari hiyo kubwa, lakini alipinga kabisa watawa kufanya kazi za mikono zenye malipo. Badala yake walitafutiwa kazi nyingine mbalimbali: kusoma, kuimba Zaburi, kutoa huduma za nyumbani, kuombaomba n.k.

Mchango muhimu mmojawapo wa mashirika ya Ombaomba ni kujenga daraja kati ya liturujia ya monasteri na ya makanisa makuu na mahitaji ya kidini ya jamii yenye kubadilika. Ndugu Wadogo, wakitumia haki ya wakati huo ya kila shirika kujitengenezea liturujia yake, walistawisha kalenda na taratibu zao, pamoja na kufuata kimsingi zile za Roma. Walizifupisha kwa faida ya sala ya moyo, na kuzisogeza jirani na haja za mtu binafsi. Ingawa wapinzani walisema kufanya hivyo ni kuvuruga liturujia, Mapapa wakaja kueneza breviari ya Kifransisko katika Kanisa lote la Kilatini. Hata misale ya Kiroma iliyotumiwa na kurekebishwa na Ndugu Wadogo ikaja kuenea: taratibu nyingi za ibada, nyimbo na sikukuu mpya ziliingizwa nao kabla hazijakubaliwa kwa Kanisa lote. Kwa juhudi na mafanikio ya pekee zilistawishwa ibada kwa Ekaristi, jina la Yesu, kuzaliwa kwake na kuteseka (Njia ya Msalaba), Bikira Maria (Kukingiwa Dhambi ya Asili). Kwa ajili hiyo, nje ya ibada walitumia pia maigizo, wakisaidiwa na Utawa III. Baada ya jumuia zote kupata kanisa la kitawa ambapo iliwabidi waadhimishe Sala ya Kanisa, ibada zilizidi kuwa za fahari, hasa kwa lengo la kuwapa kazi ya kufanya ndugu wasiosoma wala kuhubiri. Kwa sababu hiyohiyo, juu ya Sala ya Kanisa vikaongezwa vipindi vingine kwa ajili ya wafu, kwa heshima ya Bikira Maria n.k. Hoja ya msingi ilikuwa kwamba walio wengi wasingefanya bidii katika sala ya binafsi. Kama kawaida, marekebisho yalirudia kusisitiza sala ya moyo na kusoma tu Zaburi, pamoja na kuadhimisha Misa pasipo fahari katika makanisa madogomadogo. Wasio mapadre walihudhuria Misa, ila ilikuwa kawaida kupokea Ekaristi kila baada ya wiki mbili. Kumbe maungamo yalikuwa mara mbili kwa juma.

Kati ya walimu wa kiroho Mt.Bonaventura alishika nafasi ya kwanza. Maandishi yake yote yalilenga maisha ya kiroho, na kuathiri sana shirika na Kanisa lote hadi leo; ndiyo sababu akatangazwa mwalimu wa Kanisa kwa jina la “mwalimu wa kiserafi”. Tukiacha waandishi wengine bora na kuzingatia waliofaulu kuyatekeleza kikamilifu maisha ya kiroho, tunakuta katika karne tatu za kwanza walifariki watakatifu 25 na wenye heri 61: ndio ushahidi bora wa jinsi kipeo cha Kifransisko kinavyofaa. Wa kwanza ni wafiadini wa Moroko (5 wa mwaka 1220, na 7 wa mwaka 1227). Kufuatana na mfano wao alijiunga na shirika Mt. Antoni wa Padua (+1231), “mwalimu wa Kiinjili” mwenye utakatifu usiosemeka kulingana na moyo wa mwanzilishi. Baada ya Mt. Bonaventura kuna askofu mwingine, Mt. Ludoviko wa Tolosa (+1297), aliyekufa kijana kama alivyotamani. Karne ya XIV, iliyojaa wamisionari na wafiadini, ina ndugu wanne kutoka nchi mbalimbali waliotangazwa watakatifu: Nikola Tavelic na wenzake waliouawa Yerusalemu (1391). Watakatifu wote sita wa karne ya XV ni Waoservanti ambao walipigania kanuni na kufanya utume mkubwa: Bernardino wa Siena (+1444), Yohane wa Capestrano (+1456) na Yakobo wa Marka (+1476) toka Italia, Petro Regalado (+1456) na Didakus wa Alkala (+1463) toka Hispania, halafuYohane wa Dukla (+1484) toka Polandi.

 

1.1.4. UTUME (1226-1517)

 

Tangu mashirika ya Wafransisko na Wadominiko yaanzishwe, Mapapa walitambua yanavyohitajika na kufaa kutegemezea Kanisa la Roma ambalo, baada ya kufikia kilele cha fahari na mamlaka wakati wa Inosenti III (1198-1216), lilianza kukabiliana na upinzani mpya wa viongozi wa siasa. Ili waweze kuwatumia watawa hao bila ya pingamizi, Mapapa walijiwekea usimamizi wao wasikae chini ya Maaskofu, wakawapendelea katika tume nyingi. Hivyo toka mwanzo Ndugu Wadogo walifanya kazi katika ofisi za Papa na kupewa vyeo mbalimbali, kinyume cha matakwa ya Mt. Fransisko aliyetaka wabaki “wadogo”. Hasa baada ya Gregori IX, Mapapa waliona ustawi wa Kanisa unastahili uzingatiwe kuliko udogo wa Kifransisko. Ingawa shirika lilijitahidi kuzuia ongezeko la vyeo, katika karne ya XIII waliishi Maaskofu Wafransisko 250, katika ile ya XIV 746, katika ile ya XV 791, na miaka 17 ya kwanza ya karne ya XVI 70. Mabalozi ya Papa jumla walikuwa zaidi ya 300, Makardinali 29, na wawili wakawa Mapapa: Nikola IV (1288-1292) na Sisto IV (1471-1484). Ndugu Wadogo walichangia sana Mitaguso mikuu yote ya karne hizo tatu: Lyons I (1245), Lyons II (1274), Vienne(1311-1312), Konstans (1414-1418), Firenze (1431-1445) na Laterano V (1512-1517). Vilevile ndugu wengine walitetea haki za Papa dhidi ya upinzani, na zaidi ya 200 walipokea hata kazi ya kuwahukumu wazushi, ingawa hiyo haikuwapendeza sana.

Kazi ya kawaida zaidi ilikuwa ile ya kuhubiri. Waliokubaliwa na Watumishi wakaja kuunda tabaka la juu kuliko mapadri wa kawaida (waliosoma Misa tu) na ya mabradha. Ilipobaki kazi ya wasomi tu, ikarudia mitindo ya vyuoni na kuachana na usahili wa mwanzo alioutumia na kuutaka mwanzilishi. Mhubiri mkuu wa kwanza ulikuwa Mt. Antoni ambaye kwa miaka 10 alichangamsha Italia na Ufaransa Kusini akishinda uzushi. Pamoja na kuhubiri, wengine wametuachia kwa maandishi hotuba zao, mifano mingi na maelekezo juu ya namna ya kuhubiri.

Karne ya XV ndiyo bora kwa mahubiri ya Kifransisko, ambapo nguzo za Oservansya walitoka upwekeni wakawashirikisha wote utajiri waliojipatia katika sala. Makanisa hayakutosha kukusanya wasikilizaji; wote waliguswa na wengi wakaongoka. Kutoka Italia wakahubiri nchi mbalimbali hadi Norwe. Tunda mojawapo la utume wa Mt. Yohane wa Capestrano ni ushindi wa Wakristo juu ya Waturuki waliotishia kuvamia Ulaya yote (1456). Huko Italia mahubiri hayo yalipinga mwelekeo mpya wa kuweka pembeni Ukristo katika maisha ya kila siku na kujali ustawi wa kidunia tu. Kitubio kilifuatana na mahubiri; hasa baada ya Mapapa kuruhusu watawa kutoa huduma hiyo, ikaja kuwa mojawapo ya kazi zao kuu.

Shirika likiwa na uhusiano wa pekee na watu wadogo toka mwanzo, daima ni jepesi kutambua hali na haja zao upande wa roho na wa mwili, na kuziitikia vizuri, hata kupitia Utawa III. Kipindi hicho watu walielekea sana kujiundia makundi kadiri ya fani zao n.k. Ndugu Wadogo waliwaelekeza kufanya hivyo bila ya kusahau dini, katika jina na taratibu walivyoyapatia. Walipatanisha mara nyigi wanasiasa wa miji au vyama tofauti, walisaidia maskini na wagonjwa (hata wenye ukoma na tauni), walianzisha hospitali, walilaumu hadharani dhuluma n.k. Kwa ajili hiyo, bila ya kujali upinzani wowote, walianzisha pia benki ambazo zikopeshe pesa kwa riba ndogo sana ili kukomesha waliodai riba pasipo kiasi (hasa Wayahudi).

Kabla hatujaeleza umisionari wa Ndugu Wadogo, tuangalie juhudi zao kwa ajili ya umoja kati ya Waortodoksi na Kanisa la Roma. Kabla Kostantinopoli haujatekwa na Waturuki (1453), udhaifu wa Wagiriki upande wa siasa na jeshi uliwaelekeza kutafuta msaada wa Wakristo wa Magharibi. Hivyo zilipatikana fursa nyingi za kukaribiana na kujaribu kuungana, ambazo Mapapa kila mara waliwatumia Wafransisko na Wadominiko. Kwa namna ya pekee Mtaguso II wa Lyons, kwa juhudi hasa za Mt. Bonaventura, ulifanikiwa kutangaza umoja, ingawa baadaye ukashindikana kwa sababu mbalimbali.

Juhudi nyingine kulingana na mitazamo ya nyakati hizo zilifanywa na Ndugu Wadogo waliosambaa kotekote Mashariki na kutoa mifano bora ya maisha yao, pamoja na kutangaza kwa sauti na kwa maandishi ukweli wa Kanisa katoliki ili kuwavuta Waortodoksi mmojammoja au makundimakundi kuingia katika ushirika kamili nalo. Sehemu fulanifulani matunda yaliridhisha, lakini wengine waliuawa, hasa baada ya Waturuki kuteka Ulaya Mashariki Kusini. Nje ya eneo hilo, utume huo ulifanyika pia Urusi, Georgia, Armenia, Irani, Lebanoni, Misri hata Ethiopia.

Kazi ngumu zaidi ilifanyika kwa wasio Wakristo. Karne ya XIII ilikuwa mwanzo wa umisionari wa aina mpya, ambao unaongozwa na Mapapa kwa kutumia mashirika ya Ombaomba (yaliyofaa sana kwa utayari wa kutumwa na kwa umoja wa miundo yake), unapata wamisionari mchanganyiko kutoka nchi yoyote, unaenea katika bara lote la Asia (ambalo linakuja kujulikana na Wazungu wakati huo) na hauna faida ya uchumi. Mt.Fransisko alichochea hayo kwa mifano na mafundisho yake ambayo alisisitiza kuwa wito huo ni wa Kimungu, kwa hiyo hautakiwi kuzuiwa. Kwa mang’amuzi yake alielekeza kutoa kwanza ushuhuda wa maisha ya Kikristo, halafu tu, kadiri ya mapenzi ya Mungu, kuhubiri wazi imani. Wafuasi wake hawakufuata daima maelekezo hayo, kwa maana wengi waliwachokoza Waislamu ili kuuawa.

Katika historia ya misheni za Kifransisko, tunaona kwanza uenezi mkubwa upande wa Mashariki, halafu karne nyingine ya kufifia, halafu katika karne ya XV msukumo mpya toka kwa Waoservanti, lakini kuelekea maeneo mapana ambayo yalivumbuliwa na Wazungu miaka ya mwisho ya karne hiyo na kuhitaji Injili.

Kuanzia mwaka 1217 Wafransisko wametunza mahali patakatifu pa nchi ya Yesu, ingawa iliwabidi kuvumilia magumu mengi, dhuluma na vifodini; wengi walikufa pia kwa kuwashughulikia wenye tauni. Kuanzia mwaka 1219 wengine walitumwa Afrika Kaskazini, ambapo baadhi walifia dini. Shirika lilianza kupata Maaskofu kwa ajili ya Moroko, ingawa hawakuweza kukaa huko. Kumbe Tunisia na Libya waliruhusiwa kuwaongoa Waislamu wakachuma matunda kwa muda fulani, ingawa vipindi vingine waliweza tu kuwahudumia Wakristo wageni.

Mwaka 1241 Wamongolia, baada ya kujitwalia Asia karibu nzima, walivamia Ulaya na kufadhaisha Wakristo wote, kwa sababu hakuna aliyeamini uwezekano wa kuwashinda. Mapapa walijaribu kuwasimamisha kwa kutuma Wafransisko na Wadominiko (wa kwanza ni nd. Yohane wa Pian del Carpine) waombe masharti ya amani. Ujumbe huo uliposhindikana, walianza kupenya kama wamisionari upande wa Ulaya Mashariki, wakasambaa kwa ruhusa ya watu hao wakatili sana katika utawala wao wote. Nikola IV alimtuma (1291) nd. Yohane wa Montecorvino, mwanzilishi wa misheni za China na Askofu wa kwanza wa Beijing, mwenye majimbo sita chini yake katika ufalme mzima (hadi Urusi). Nyumba za kitawa katika eneo hilo lote likafikia kuzidi 50, baadhi zikiwa na ndugu wasiopungua 20. Inosenti VI (1352-1362) aliomba mkutano mkuu wa mwaka 1353 uongeze wamisionari alivyotaka mfalme wa Mongolia, lakini itikio likawa hafifu, kwa kuwa tauni iliyoua wamisionari wengi, iliua pia watawa wengi Ulaya. Hivyo misheni zikaendelea kwa shida tu mpaka ikaja kufa China ilipojikomboa. Pia, Ndugu Wadogo waliongoa Walitwania, taifa la mwisho la Ulaya kuingia Ukristo (karne ya XIII na XIV).

Karne ya XV ilielekeza umisionari upande mwingine, na Waoservanti waliuchangamkia kuanzia visiwa vya Kanaria vilivyopokea Ukristo haraka kwa juhudi za ndugu waliofikia kuwa 200, mmojawao Mt. Didakus wa Alkala. Kutoka huko umisionari ulienea pwani za Afrika Magharibi. Mzunguko wa Afrika hadi Ras wa Tumaini Jema (Dias, 1488) na India (Da Gama, 1497-1498), na hasa uvumbuzi wa Amerika (Columbus, 1492) ulisisimua sana umisionari kwa maeneo, miundo na mbinu mpya. Wakati ambapo uenezi wa Waturuki Waislamu ulikuja kuzuia njia za Asia, na misheni zilizokuwa chini ya utawala wao zilidumaa, Ndugu Wadogo walistawisha upeo umisionari wao Amerika na Asia Mashariki kupitia baharini (wakati huo Asia Mashariki ilikuwa chini ya Askofu wa Funchal, katika kisiwa cha Afrika Magharibi!). Upande wa miundo wafalme wa Ureno na wa Hispania walipogawana ulimwengu kwa baraka ya Aleksanda VI (1492-1503) walipewa pia usimamizi wa kazi zote za misheni, pamoja na haki ya kuchagua na kutuma wamisionari katika maeneo yao. Hivyo karne ya XVI idadi ya wamisionari OFM ilifikia 6,000, wengi wao wakitokea nchi hizo mbili, kwa sababu mataifa mengine waliweza wakabaguliwa na hata kurudishwa nyumbani.

Ndugu Wadogo 6 wa kwanza walifika Amerika (kisiwa cha Hispaniola, leo Dominikana/Haiti) mwaka 1493 na kuanza kuwahubiria wazalendo. Wengine wakafuata mapema na kuenea kadiri vilivyovumbuliwa visiwa vingine. Kufikia mwaka 1500 walikuwa wameshabatizwa wazalendo 3,000 Hispaniola na wengi zaidi Kuba. Mwaka 1504 yaliundwa majimbo matatu na mwaka 1505 kanda ya shirika. Mwaka 1511 alitawazwa Askofu wa kwanza wa Amerika visiwani (Dominikana) na mwaka 1513 wa bara (Panama), wote wawili wakiwa Wafransisko. Ila barani hatari zikawa nyingi. Waliohamia Brazili (1503) waliuawa baada ya miaka miwili, na wengi wa waliowafuata wakauawa pia. Hata hivyo Wafransisko wakaendelea na umisionari huko, wakiwa peke yao hadi 1549.

Vilevile Ndugu Wadogo ndio wamisionari wa kwanza kufika India kwa meli (1500, baada ya kupitia Brazili); wengine wakafuata. Mabanyani waliwaua 3, lakini wengine waliongoka jumla wakabatizwa pasipo mafundisho kutokana na uhaba wa wamisionari. Safarini, wengine walihubiri kisiwani Sokotra (karibu na Somalia) na kuongoa karibu wote, hata wakageuza msikiti kuwa kanisa la Bikira Maria; lakini Waarabu wakakiteka (1510) wakaharibu kila kitu.

Uenezaji wa Injili unatimia unapopenya utamaduni wa watu. Tuone basi Ufransisko ulivyoathiri Kanisa na jamii, kuanzia elimu, fasihi na sanaa.

Mt. Fransisko hakuwa msomi, tena alihisi uchu wa elimu unavyoweza kuzuia udogo na usawa wa wafuasi wake. Lakini, akitambua njia hiyo haiepukiki, alielekeza namna ya kuifuata bila ya kudhurika. Kwake na kwetu Mt. Antoni wa Padua ndiye kielelezo, kwa jinsi alivyokuwa tayari kuweka pembeni usomi. Ndiyo sababu alimruhusu kuwafundisha ndugu teolojia huko Bologna mradi isizimishwe roho ya sala na ibada. Mwaka 1231 shirika lilikuwa na nyumba za masomo hata Paris na Oxford karibu na vyuo vikuu ili kuwaandaa walimu ambao wafundishe katika konventi muhimu zaidi za kila kanda. Ndipo walipojipatia sifa ya elimu na nafasi mpya za utume, ingawa M.H. Egidi na wengineo walizidi kulaumu Paris kwamba imeharibu shirika. Tangu karne ya XIV katika konventi karibu zote kulikuwa na vipindi vya lazima kwa wasio mabradha. Pia yalianzishwa masomo kwa waliotarajia kupata daraja. Mitindo ya kufundisha ilikuwa sawa na ile ya mashirika mengine na ya vyuo vikuu: vipindi asubuhi na jioni, mijadala, mahubiri ya walimu na ya wanafunzi vilevile.

Shirika halikuwa na mwalimu maalumu na mafundisho ya lazima, ila tabia na mazingira yake yote vilielekeza Ndugu Wadogo kuwaza namna fulani, yaani kusisitiza upendo kuliko ujuzi, na utashi kuliko akili; pia kumuona Mungu kama Wema kuliko kama Ukweli. Falsafa ya Wafransisko ilifuata ile ya Plato kumpitia Mt. Augustino (Mt. Antoni alitoka shirika lake). Kati ya walimu wa vyuo vikuu aliyeelekeza njia ni Aleksanda wa Hales (+1245), aliyemfundisha Mt. Bonaventura huko Paris. Kwa mtakatifu huyo, mwalimu ni Kristo tu, na elimu ni moja tu, ile inayotuunganisha naye, hasa Maandiko Matakatifu, ambayo peke yake yanawafaa Ndugu Wadogo. Baada yake teolojia ikabili mababu wa Kanisa na maandishi ya walimu wa teolojia. Wanafalsafa na waandishi wengine wasomwe tu kwa mpito kadiri wanavyosaidia kuelewa Biblia. Ndiyo njia ya kufikia elimu, lakini mtu akitaka hekima anapaswa kuwa na maisha matakatifu.

Oxford iliwatoa hasa: nd. Roger Bacon (+1292), mtaalamu wa mambo mengi na mwanzilishi wa mtindo wa upimaji kama msingi wa sayansi; M.H. Yohane Duns Scoto (+1308), mwalimu mwenye uchambuzi mkali, anayesifiwa kwa kuonyesha Kristo kuwa kiini cha uumbaji, na kwa kutetea sifa ya Maria kukingiwa dhambi ya asili (Wafransisko wakaendelea kuitetea hadi ikatangazwa na M.H. Pius IX, wa Utawa III, mwaka 1854, kuwa dogma); na nd. Wiliamu wa Ockham (+1347) aliyepotosha falsafa akadai eti, akili haiwezi kujua yanayopita malimwengu: msimamo wake ukaenea sana, ukampa Martin Luther silaha dhidi ya imani katoliki, ukaathiri utamaduni wa Magharibi hadi leo.

Ufransisko uliathiri vilevile mwelekeo wote wa sanaa ya Magharibi. Ukiitikia vizuri matarajio yote ya kidini na ya kijamii ya kipindi cha mageuzi, ulieneza mtazamo mpya wa maisha unaojali mtu na viumbe vyote. Hivyo ulichangia sana upatikanaji wa mitindo mipya na njia mpya za kufurahia uzuri, ingawa bila ya kupotewa na imani. Fasihi ya Kifransisko inapenda kusimulia, tunavyoona katika maisha ya mwanzilishi yaliyoandikwa na wafuasi wake; uchorahi unaonyesha sura halisi ya kwake na ya wengineo; hata ujenzi unafuata njia mpya, hasa kufuatana na kielelezo cha kanisa la Mt. Fransisko huko Asizi. Hata katika ujenzi wa nyumba zao Ndugu Wadogo waliweza kuzingatia ufukara bila ya kupuuzia uzuri, kiasi kwamba upendevu wake unavutia wengi hadi leo.

 

 

1.2. MAREKEBISHO KUENDELEA (1517-1762)

 

1.2.1. MATAWI MAPYA KUCHIPUKA

 

Utengano wa Waoservanti na Wakonventuali ulitatua tatizo moja, lakini haukufaulu kuunganisha makundi yaliyorekebishwa, ingawa Papa alikuwa ameagiza itungwe mara katiba moja kwa yote. Baadhi yalidumu kuwa na kanda zao, Waoservanti wa Italia wakaikataa katiba hiyo wakaendelea kuirekebisha mfululizo ile maalumu ya kwao, na kanda nyingine zilijitungia vilevile na kuzidisha tofauti shirikani. Kilichohatarisha zaidi umoja ni utaifa uliochochewa na serikali mbalimbali kwa faida ya siasa ya nchi zao dhidi ya nyingine. Wafalme waliingilia kwa njama na vitisho masuala ya mikutano mikuu, sawa na walivyoingilia uchaguzi wa Papa, lakini kila mara idadi iliwapa ushindi Wahispania, hata washindani wao (Wafaransa) wakagoma kuhudhuria mara kadhaa.

Matatizo mengine yalihusu maisha yenyewe, hasa ufukara. Waliolazimika kujiunga na Waoservanti, na wale wasioacha kutumia fadhili walizokuwanazo wakiwa Wakonventuali, walikataa kurekebishwa. Kinyume chake, wengine hawakuridhika tena na namna OFM ilivyoshika kanuni, wakadai ruhusa ya kuishika kabisa. Ndivyo walivyofanya watawa wa mashirika mbalimbali, kwa kuwa haja ya urekebisho ilitambulikana na wote katika Kanisa la karne ya XV na ya XVI. Kwa namna ya pekee Ndugu Wadogo walichochewa kufanya hivyo na sura ya X ya kanuni pamoja na wasia. Ndiyo sababu Mt. Bonaventura aliona haja ya kuwepo makao ya upwekeni katika kila kanda ili kuwaachia uhuru wa kuishi hivyo wale wapendao. Kumbe Waoservanti wengi na baadhi ya viongozi wao hawakukubali kuwaachia wenye bidii uhuru huo, kwa sababu ingekuwa sawa na kukiri kwamba wamelegea. Hivyo wakawatenda ndugu hao kama Wakonventuali wa zamani walivyowatenda Waoservanti wa kwanza. Walioamini urekebisho unaweza kutoka kwa viongozi wakaja kujionea haiwezekani. Miundo iliyoanza kama urekebisho ikajikuta inajaribu kuzuia juhudi za waliopenda urekebisho, na viongozi wa shirika lililoanza kwa kushindana na viongozi wakawalaumu waliotaka kufanya vile wakisema eti, ni wakaidi tu! Kwa kukosa busara na wema walisababisha waliotaka urekebisho wakafuate njia zao ili kupata ruhusa walizozihitaji, kwa kumkimbilia Papa au viongozi wa serikali. Mara nyingine Wakonventuali walipokea makundi hayo chini ya ulinzi wao ili kuwakomoa Waoservanti waliokuwa wanawadharau wakijidai ndio wafuasi halisi wa Mt. Fransisko. Ndiyo asili ya matawi mapya, hasa lile la kujitegemea la Wakapuchini.

Mwaka 1525 nd. Mateo wa Bascio alimkimbilia Klementi VII (1523-1534) ili kuruhusiwa ashike kanuni, avae kanzu asili na kuhubiri huko na huko alivyotaka. Alipokubaliwa, walijiunga naye ndugu wawili, Ludoviko na Rafaeli wa Fossombrone. Mtumishi wa kanda aliwatafuta sana, lakini walilindwa vizuri na Katerina Cibo, ndugu wa Papa. Ili kukwepa dhuluma, wakajiunga na Wakonventuali, halafu wakapewa na Klementi VII haki ya kuwa na Mtumishi wao chini ya Mkuu wa Wakonventuali na ya kupokea wanovisi (1528). Mapema walianza kuitwa Wakapuchini kutokana na kofia yao kubwa. Upinzani wa Mkuu wa OFM dhidi yao haukufaulu; kinyume chake, kwa kuwa alitaka kuzuia hata makao ya upwekeni ndani ya shirika, ndugu wengi wenye bidii wakakata tamaa wakajiunga na Wakapuchini. Njama nyingine za kuwakomesha zikashindikana, hivi kwamba mwaka 1535 walikuwa tayari 700. Ndipo aliposhika uongozi wao nd. Bernardino wa Asti aliyelipa shirika jipya sura ya kiroho ya kudumu, hasa kwa njia ya katiba iliyotungwa mwaka huo na kupitishwa mwaka uliofuata.

Hatari nyingine zilitokea ndani ya shirika, kwa ukaidi wa nd. Ludoviko, halafu kwa uzushi wa mwandamizi wa nd. Bernardino. Hatimaye mambo yakatulia na tawi jipya likazidi kustawi kiroho na kitume, ingawa Julius III (1550-1555) alikataza Waoservanti wasihamie tena kwa Wakapuchini. Hivyo hawa wakazidi kujisikia tofauti na Wafransisko wenzao. Mkutano mkuu wa mwaka 1552 ulionyesha kuwa juhudi kali za awali zimeanza kutulia na kujilinganisha na maisha: shirika lilipanga masomo na kuwa na watu maarufu upande wa elimu, utume na uongozi. Jambo muhimu zaidi, lilimzaa mtakatifu wa kwanza, bradha Felix wa Cantalice (+1587), kielelezo cha unyofu. Mtaguso wa Trento (1545-1563) ulisifu tawi hilo kama urekebisho wa kufaa na wenye uaminifu kwa wito wake hata kustahili kutazamwa na Kanisa kwa namna ya pekee. Shirika likazidi kukaza nidhamu ili kuzuia ulegevu, likaanza kuenea ng’ambo ya milima ya Italia Kaskazini (1573). Ulipozuka upinzani wa Wakonventuali, Kanisa lilikuwa limeshang’amua ubora wa Wakapuchini; basi, Paulo V (1605-1621) alitamka kuwa ni Ndugu Wadogo halisi na wana wa Mt. Fransisko sawa na matawi mengine (1608), halafu akawaondoa chini ya Mkuu wa Wakonventuali na kuwapa Mtumishi wa kwao mwenye haki ya kuhesabiwa mwandamizi halali wa mwanzilishi (1619). Kwa wakati huo shirika limeshazaa tena watakatifu Serafino wa Montegranaro (+1604), bradha asiye na vipawa vingi kiutu bali mwenye karama za ajabu, Yosefu wa Leonesa (+1612), padri Mkapuchini wa kwanza kutumwa kwa Waturuki Waislamu halafu mhubiri bora Italia, na Mt. Laurenti wa Brindisi (+1619), “mwalimu wa Kitume”, mtimilifu kuliko Wakapuchini wote kwa utakatifu, elimu na utume. Wakafuata Mt. Fidelis wa Sigmaringen (+1622), wa kwanza kutoka nje ya Italia, na wa kwanza kufia dini kati ya waliotumwa na Idara ya Papa kwa Uenezaji wa Imani, halafu Mt. Bernardo wa Corleone (+1667), mwongofu mwenye toba kali. Pia walipatikana wenye heri 6.

Kipindi hicho ndicho cha ukomavu wa shirika, mitazamo ya Kiitalia ilipopanuka kwa kuenea nje ya nchi na wanashirika waliposhika nafasi muhimu katika Kanisa. Baadaye hakuna matukio ya maana zaidi, isipokuwa mengine ya kufaa na mengine yasiyofaa ambayo yaliathiri shirika: idadi ya watawa na ya shughuli iliongezeka pamoja na sifa kutoka kwa viongozi wa Kanisa na serikali, lakini zilizuka vurugu pia kama ile ya utaifa (1636-1678). Benedikto XIV (1740-1758) aliamua mhubiri wa Papa awe daima Mkapuchini, akasema, “Shirika la Wakapuchini linastahili yoyote yale, kwa kuwa ndilo kielelezo pekee cha ukamilifu wa Kiinjili kilichobaki hadi nyakati zetu”. Kweli urekebisho huo uliendelea kushika kikamilifu kanuni kwa muda mrefu kuliko mengine yote. Nyumba ziliendelea kujengwa ilivyoagizwa toka mwanzo, ndogo sana, nje ya miji na vijiji, zikielekeza ndugu kufuata ufukara na unyofu hata ulimwengu ulipokazania fahari. Watakatifu wa kipindi hicho ni bradha Krispino wa Viterbo (+1750), kielelezo cha furaha ya kiroho, Ignas wa Santhià (+1770), padri mwenye bidii kwa wagonjwa na wakosefu, Ignas wa Lakoni (+1781), bradha ombaomba aliyesaidia sana fukara, na Felix wa Nicosia (+1787), bradha mtiifu ajabu, mbali ya mwenye heri 1.

Vilevile Italia, ndugu waliojikusanya katika makao ya upwekeni kuanzia mwaka 1535 (mkutano mkuu ulipowaruhusu ili kuzuia wengine wengi wasiwakimbilie Wakapuchini), kisha kuongezeka waliwekwa moja kwa moja chini ya Mtumishi mkuu tu (1579), wakapewa katiba maalumu (1595), ruhusa za pekee sana (1596), hatimaye Kiongozi mkuu na mkutano mkuu wa kwao. Hivyo mamlaka ya Mtumishi wa OFM kwao ikawa jina tu. Kati ya hao Wariformati katika kipindi hicho tunawakuta watakatifu mabradha watatu: Mt. Benedikto Mwafrika (+1589), mtoto wa watumwa huko Italia, Mnegro wa kwanza kutangazwa mtakatifu, Mt. Umile wa Bisignano (+1637), mnyenyekevu ajabu, na Mt. Karolo wa Sezze (+1670), aliyeandika vizuri sana kuhusu maisha ya kiroho; halafu mapadri Mt. Pasifiko wa San Severino (+1721), aliyezingatia sana maisha ya sala, na Leonardo wa Portomaurizio (+1751), tunda bora la Kirekebisho kilichoanzia mjini Roma karne ya XVII. Pia walipatikana wenye heri 4.

Huko Hispania, baadhi ya wafuasi wa urekebisho wa Pekupeku, baada ya kuunganishwa na Waoservanti (1517) walimkimbilia Mkuu wa Wakonventuali ili kukwepa vizuio vya OFM, na mmojawao, Mt. Petro wa Alcantara (+1562) akafanywa Mkurugenzi wao (1557). Alipokufa, Pius IV (1560-1565) akawahamisha Waalkantara chini ya Waoservanti lakini bila ya kufuta kanda zao, katiba yao na mavazi yao maalumu. Gregori XIII (1572-1585) akamkataza Mkuu wa OFM asiingilie masuala yao ya ndani (1578), na Urbani VIII (1623-1644) akawaruhusu wasifuate tena katiba ya shirika lote (1642). Jinsi sisitizo la sala na toba linavyozaa matunda imethibitishwa na umisionari wao (Amerika na Asia Mashariki) na hasa na watakatifu 9 wa urekebisho huo, wakiwa ni pamoja na Mt. Paskali Baylon (+1592), mwenye ibada ya pekee kwa Ekaristi, wat. Petro Batista, Martino wa Kupaa na Fransisko Blanco, mapadri, halafu Fransisko wa Mt. Mikaeli, Gonzalo Garcia na Filipo wa Yesu, mabradha, ambao wote walifia dini Japani (+1597), hatimaye Mt. Yohane Yosefu wa Msalaba (+1734), mpenda ufukara mkuu. Pia walipatikana wenye heri 22.

Huko Ufaransa makao ya upwekeni hayakustawi sana hadi mwisho wa karne ya XVI. Mwaka 1601 walioishi huko wakapewa na Kanisa Mkurugenzi mwenye mamlaka pana sana; hapo wakaenea haraka kwa msaada wa mfalme, hata kanda zote za Ujerumani na Uholanzi zikajirekebisha na kujiunga nao, wakaitwa Warekoleti. Mmojawao ni Mt. John Wall (+1679), aliyefia dini huko Uingereza.

Katika karne ya XVI na ya XVII karibu kila mkutano mkuu wa OFM ulizungumzia katiba na kupigania umoja, ambao haukuwa rahisi kutokana na mchanganyiko wa ndugu waliopenda fadhili za Wakonventuali na wengine waliotaka urekebisho. Katika hali hiyo Watumishi wakuu walijitahidi kuhuisha shirika lote, lakini wengi wao walitumwa na Mapapa kama mabalozi kwa wafalme na Maaskofu wa Ulaya, au walipewa uaskofu wa miji muhimu. Shirika halikupendezwa kwa sababu lilikuja kukosa uongozi imara: ndiyo maana mara kadhaa liliwadai kiapo cha kutokubali kazi hizo au walau cha kujiuzulu Utumishi. Watakatifu waliopatikana kipindi hicho ni: Mt. Salvatore wa Horta (+1567), bradha aliyefanya miujiza mingi ajabu (labda milioni moja), wat. Nikolaus Pieck, Jeromu wa Weert, Teodoriko van der Eem, Nikasi wa Heeze, Wilehadi wa Denmaki, Godefrid wa Melveren, Antoni wa Weert, Antoni wa Hoornaert, Fransisko wa Roye, mapadri, halafu Petro wa Assche na Korneli wa Wijk-bij-Durstede (+1572), mabradha, ambao wote walifia dini Uholanzi, Mt. John Jones (+1588), aliyefia dini Uingereza, hatimaye Fransisko Solano (+1610), mmisionari bora Amerika Kusini aliyezunguka kotekote kwa miaka 14, akihubiri na kuimba. Wenye heri wa kipindi hicho ni 17.

Karne ya XVII ikawa ya utulivu na utendaji, lakini ongezeko kubwa mno la watawa lilisababisha matatizo makubwa na ulegevu hata katika marekebisho. Pamoja na utaifa kuzidi, matawi ya Italia yalishindana kwa maandishi makali ya kukwaza. Makwazo mengine yalitokana na desturi ya Watumishi kadhaa kutuma watawa wasiofaa kwenye kanda nyingine au kuwaacha nyumbani mwa marafiki au ndugu. Badala ya juhudi za watawa kwa ajili ya kanuni kama katika karne zilizopita, sanasana tunakuta viongozi wakijitahidi kuwalazimisha washike kanuni, lakini bidii za namna hiyo hazikuweza kufanikiwa kwa kuwa hazikutoka moyoni mwa watawa. Hatimaye mwaka 1676 mkutano mkuu ulikubali na kuagiza kila kanda ianzishe makao 3-4 ya upwekeni ambapo yafanyike malezi ya watakaji na wanovisi wote: baadaye katika mazingira hayo walistawi wat. Thomas wa Cori (+1729), mhubiri maarufu na Teofilo wa Corte (+1740), mwanafunzi wake. Lakini katika karne ya XVIII ilionekana wazi jinsi matazamio ya wengi yalivyolenga kupata kwa visingizio vyovyote fadhili na nafasi za kwanzakwanza. Kupitia mikutano mikuu upuuzi wa namna hiyo uliathiri sheria za shirika. Pia mabadiliko mengi mno ya katiba, badala ya kusaidia nidhamu, yalizidi kuipunguza kwa kusababisha ndugu wasiijali katiba isiyodumu.

Upande wa Wakonventuali, utengano na Waoservanti haukuwaondolea baadhi yao wasiwasi kuhusu utekelezaji wa kanuni, ingawa Mtaguso wa Trento ulitamka (1563) kwamba OFM na Wakapuchini tu hawaruhusiwi kuwa na mali hata kishirika, tofauti na Wakonventuali na mashirika mengine yote. Uhusiano na matawi yaliyokimbilia chini ya Mkuu wao ili kufuata urekebisho ulichochea hamu ya kuwaiga. Ndivyo walivyoanza Wakonventuali wa Urekebisho Hispania: uenezi wao ulichangia uamuzi wa Mt. Pio V (1566-1572) wa kuunganisha na OFM Wakonventuali wote wa Hispania na Ureno (1566-1567). Juhudi za mikutano, za Watumishi wakuu na za watawa wenyewe zilileta nidhamu na ustawi, hasa mmojawao alipochaguliwa kuwa Papa Sisto V (1585-1590) akaanza kuwasaidia kwa kila njia, kama vile kuunganisha chini ya Wakonventuali marekebisho madogo yaliyokuwa yameanza Italia (1562). Ila mwaka 1669 yakaja kutawanywa, baada ya kusumbuliwa sana na Wakonventuali wa kawaida na Wakapuchini (kuhusu sare zao zilizofanana). Kabla ya hapo mkutano mkuu ulitunga katiba mpya kabisa (1625) ili kuondoa misimamo tofauti kuhusu kanuni: katiba hiyo haikufuata matamko ya zamani ya Mapapa juu ya kanuni, bali ilipitisha moja kwa moja desturi za shirika zilivyokuwa. Baada ya kuthibitishwa na Urbani VIII, Wakonventuali wakaanza kuweka nadhiri zao kwa kutamka wazi kuwa watashika kanuni “kadiri ya katiba ya Urbani” tu.

Baada ya kujipatia hivyo msimamo wa kudumu, Wakonventuali wakazaa mwenye heri 1 na watakatifu 2 waliong’aa mmoja hasa upande wa sala, mwingine upande wa utume: Mt. Yosefu wa Copertino (+1663) na Mt. Fransisko Antonio Fasani (+1742), wote mapadri. Pia shirika liliendelea kusifiwa upande wa elimudini likaona mtawa wake mwingine kuwa Papa (Klementi XIV, 1769-1774) ambaye naye alilipendelea sana, k.mf. kwa kuwahamisha Waoservanti wote wa Ufaransa chini ya Wakonventuali. Kwa mara nyingine upendeleo huo ukazaa chuki ya wengine ilivyojitokeza kisha kufa kwake.

Takwimu ya jumla ya Utawa I ni kama ifuatavyo:

 

Matawi

Mwaka 1575 hivi

Mwaka 1700 hivi

Mwaka 1762 hivi

   (Waoservanti)

32,750

36,400

39,900

   (Pekupeku)

1,700

6,600

7,000

   (Wariformati)

500

13,900

19,000

   (Warekoleti)

50

9,200

11,000

OFM jumla

35,000

66,100

76,900

Wakonventuali

12,000

15,200

21,000

Wakapuchini

3,600

27,300

34,000

Jumla kuu

50,600

108,600

131,900

 

Bila ya kujali tofauti kati ya tawi na tawi, karibu 60% walikuwa mapadri, ambao nusu ya idadi yao walikuwa wahubiri, nusu “mapadri wa Misa na sufuria” tu. Ongezeko lilipungua kwanza kutokana na Uprotestanti kuenea na kufuta kanda kadhaa Ulaya Kaskazini, na utawala wa Kiislamu kuenea Ulaya Mashariki Kusini, ingawa pande nyingine zilifidia. Karne yenye ongezeko la kasi zaidi ni ile ya XVII: ndio mwanzo wa wasiwasi na hofu kwa viongozi wa Kanisa na serikali, kwa kuwa mashirika mengine pia yalikua. Kuanzia mwaka 1634 Mapapa walichukua hatua kuzuia upokeaji wa wanovisi na kupunguza konventi (Italia zilifungwa 24.2%), hata kufikiria uwezekano wa kuwapeleka watawa vijana kupigana na Waturuki ili kuwapunguza! Lakini hatua hizo hazikufanikiwa. Kuhusu uenezi, wakati wa kufikia kilele cha idadi ya wanashirika mgawanyo ulikuwa ifuatavyo:

 

Nchi

OFM

OFMConv

OFMCap

Jumla

Italia na visiwa

26,000

10,700

15,700

52,400

Hispania na makoloni

23,000

0

3,100

26,100

Ufaransa

9,500

5,400

6,100

21,000

Ujerumani n.k.

9,600

2,600

8,100

20,300

Ureno na makoloni

4,000

0

0

4,000

Dola la Waturuki

1,700

800

300

2,800

Polandi na Urusi

1,500

1,500

0

3,000

Uingereza na Irelandi

1,600

0

150

1,750

1.2.2. MAISHA NDANI YA SHIRIKA

 

Kadiri ya hati ya utengano (1517) Mkuu wa Waoservanti tu alikubaliwa kuitwa Mtumishi mkuu, wakati yule wa Wakonventuali alipewa jina la Mwalimu Mkuu; vilevile viongozi wa kanda. Lakini jina hilo jipya halikuja kutumika. Mkuu wa Wakapuchini aliitwa Makamu (wa Mkuu wa Wakonventuali aliyetakiwa kumthibitisha baada ya kuchaguliwa). Jina la “Mtumishi mkuu wa Shirika lote” lililotumiwa na Mkuu wa OFM lilichukiwa na kulalamikiwa na Wakonventuali na Wakapuchini, hadi Paulo V alipotamka kuwa hao wote ni wana halisi wa Mt. Fransisko, na Wakuu wao ni waandamizi wake halali (1619). Hata hivyo mabishano ya wazi yakaendelea kuhusu mlolongo wa uandamizi huo, mtindo asili wa kanzu na hasa kofia yake, mpaka Aleksanda VIII (1689-1691) alipokataza maandishi yote juu ya hayo.

Kwanza Kardinali mlinzi alikuwa mmoja kwa wote, halafu Wakapuchini wakakubaliwa kuwa na mmoja wa kwao (1564), na vilevile Wakonventuali (1580). Mara kadhaa waliingilia mno masuala ya shirika hadi kulivuruga na kusababisha Mapapa walazimike kuwazuia. Mamlaka yao ilipungua ilipoanzishwa Idara ya Papa kwa Watawa (1586). Tofauti kati ya matawi kuhusu miundo ya nd